Monday, July 29, 2019

VITU VIWILI UNAVYOHITAJI ILI WATU WAKUSIKILIZE.

“There is only one excuse for a speaker's asking the attention of his audience: he must have either truth or entertainment for them.” ― Dale Carnegie
Kama unataka watu wakusikilize unapoongea, unapaswa kuwa na moja au vyote kati ya vitu hivi viwili; ukweli au burudani.
Watu wanapenda kusikiliza ukweli, ukweli ambao unawawezesha kufanya maamuzi sahihi na kupiga hatua kwenye maisha yao, ukweli unaowafanya waone wapi walikuwa wanakosea na hatua sahihi za kuchukua ni zipi. Unapokuwa na ukweli, watu wanakusikiliza, hasa pale unapokuwa na ushahidi wa ukweli huo. Japokuwa wakati mwingine ukweli huwa unaumiza na watu wengi kuukataa, lakini unapousimamia unapata watu wa kukusikiliza. Hii ndiyo inayosababisha tunawasikiliza waalimu, washauri, au viongozi mbalimbali, ambao tunajua wana ukweli ambao tunauhitaji.
Watu wanapenda burudani, watu wanapenda kusahau changamoto zao za maisha kwa muda na kucheka kidogo. Na hapa ndipo wasanii na wachekeshaji wanapopata nafasi ya kuwafikia wengine kupitia sanaa zao. Watu watamsikiliza mtu kama wanaburudika kwa kumsikiliza.
Hivyo rafiki, kama unataka kuwa mnenaji mzuri, kazana kuweka vitu hivi viwili kwenye unenaji wako, ukweli na burudani. Kila unapopata nafasi ya kuongea mbele ya wengine, jua ni ukweli gani ambao unataka watu hao wajue, labda kuhusu wewe, kuhusu mada unayozungumzia au kuhusu bidhaa au huduma unayotaka kuwauzia. Ukweli huu uwafanye waondoke na kitu ambacho hawakuwa wanakijua awali na wawe na hatua za kuchukua ambazo hawakuwa wanachukua awali. Pia waburudishe watu kupitia unenaji wako, kuwa na hadithi, mifano au visa ambavyo vinaufukisha ukweli huo kwa njia ambayo inawaburudisha watu. Unahitaji kuwa na maandalizi ya mifano au hadithi utakazotumia kwenye unenaji wako, ambavyo vitafikisha ukweli na kuwaburudisha watu pia.
Zingatia vitu hivyo viwili katika unenaji, ukweli na burudani na watu watapenda kukusikiliza kila wakati bila ya kuchoka.

No comments:

Post a Comment