Friday, January 17, 2020

HATUA O4 ZA KUPATA UHURU WA MUDA , FEDHA NA ENEO ILI KUWA NA MAISHA YA MAFANIKIO

Kupata uhuru kamili kwenye maisha ni mtego ambao wengi wamekuwa wananasa.
Chukua mfano huu, mtu aliyeajiriwa anafanya kazi kwa juhudi, ili atoe thamani zaidi na hilo lipelekee yeye kulipwa zaidi. Kwa juhudi anazoweka, mwajiri wake anaona anastahili kulipwa zaidi, hivyo anampandisha cheo na kumwongezea mshahara. Lakini cheo anachopandishwa kinakuja na majukumu zaidi, hivyo licha ya kipato kuongezeka, mtu huyo anazidi kukosa muda na hivyo anakosa uhuru na maisha yake.
Kadhalika kwenye biashara, mtu anaanza biashara ndogo, ambayo inampa muda mwingi wa kufanya mambo yake, biashara inakua, wateja wanaongezeka na faida inaongezeka pia, lakini hilo linamtaka atumie muda zaidi kwenye biashara. Wingi wa wateja unakuja na changamoto nyingi za wateja hao ambazo zinampa kazi zaidi. Hivyo licha ya biashara kukua na kipato kuongezeka, uhuru unazidi kupungua kwa sababu muda wa kufanya mambo mengine kwenye maisha yake unakuwa haupo.
Tusipokuwa makini, tutakuwa tunakimbiza uhuru kama kipepeo ambacho kinakimbilia maua mazuri, kila wakati utaona nikipiga hatua hii nitakuwa huru na unaishia kukosa uhuru zaidi.
Ili kuweza kupata uhuru kamili wa maisha yetu, ambao unajumuisha uhuru wa muda, uhuru wa fedha na uhuru a eneo, kuna hatua nne za kuchukua.
Hatua hizi nne tumeshirikishwa na Tim Ferriss kwenye kitabu chake cha THE 4-HOUR WORK WEEK.
Hapa nakwenda kukushirikisha hatua hizo nne kwa ufupi,
Karibu kwenye hatua nne za kuchukua ili kupata uhuru kamili wa maisha yako.
HATUA YA KWANZA NI D  (DEFINITION)
Hapa unabadili sheria na kanuni zote za mchezo wa kazi au biashara na kujiwekea utaratibu wako mpya ambao utautumia kuendesha maisha ya tofauti kwako kwenye eneo la kazi.
Baadhi ya mambo ya kubadili ni kutokusubiri mpaka uzeeke ndiyo upate mapumziko kupitia kustaafu, badala yake tengeneza mapumziko mafupi kwenye maisha yako ya sasa.
Pia jua maana halisi ya mafanikio kwako, unajipimaje kwamba umefanikiwa, na siyo kujilinganisha na wengine au kuiga yale ambayo wengine wanafanya.
Kwa kifupi, jua hasa kile unachokitaka na jinsi ambavyo utakipata kwa namna ambayo ni bora kwako.
HATUA YA PILI NI E  (ELIMINATION)
Hapa unakwenda kufuta mambo yote yasiyo muhimu na ambayo yanachukua muda wakoi mwingi, hivyo kubaki na machache muhimu ambayo yanachukua muda wako mchache. Hapa ndipo unapokwenda kupunguza sana muda wako wa kazi na kupata uhuru wa kwanza ambao ni MUDA.
Kuna sheria mbili ambazo Tim ametushirikisha kwenye hatua hii;
Sheria ya kwanza ni ya Pareto (80/20) ambayo inasema asilimia 80 ya matokeo inatokana na asilimia 20 ya juhudi, hivyo kuna mambo machache yanayoleta matokeo makubwa na tunapaswa kufanya hayo tu.
Sheria ya pili ni ya Parkinson, ambayo inasema jukumu huwa linameza muda ambao limepangiwa, hivyo tunapaswa kujiwekea muda mdogo wa kukamilisha majukumu yetu ili tuache kupoteza muda.
Kwenye uchambuzi wa kitabu hili utajifunza vizuri jinsi ya kutumia sheria hizi kwa pamoja ili ziwe na manufaa kwako.
HATUA YA TATU NI A (AUTOMATION)
Hapa unatengeneza mpango wa kulipwa hata kama wewe haupo, unajenga misingi ya kuiwezesha biashara au kazi yako kujiendesha yenyewe hata kama wewe haupo na wewe kupokea fedha. Kupitia hatua hii, unapata uhuru wa pili ambao ni FEDHA.
Kikwazo cha kwanza kwenye uhuru wako ni wewe mwenyewe. Umeshajiweka sana kwenye kile unachofanya kiasi kwamba hakiwezi kwenda bila ya wewe kuwepo na ndiyo maana kila hatua unayopiga unazidi kupoteza uhuru wako.
Unapaswa kuweka mfumo unaoiwezesha kazi au biashara yako kujiendesha yenyewe hata kama wewe haupo.
HATUA YA NNE NI L (LIBERATION)
Hapa unapata uhuru kamili wa maisha yako, kwa kuweza kuwa eneo lolote duniani huku kazi au biashara yako ikiendelea kujiendesha yenyewe na fedha zikiingia. Hapa unapata uhuru wa tatu ambao ni wa ENEO.
Baada ya kuamua mafanikio yana maana gani kwako, kuachana na yasiyo muhimu na kutengeneza mfumo wa biashara yako kwenda hata kama haupo, sasa unakuwa huru na maisha yako, na unaweza kuchagua kuwa eneo lolote kwa wakati wowote unaotaka wewe. Na huu ndiyo uhuru kamili ambao wengi hawapati nafasi ya kuufikia kwenye maisha yao. Lakini wewe unaweza kuufikia kama utafanyia kazi maarifa haya uliyoyapata.
Kwa pamoja, hatua hizi nne zinatupa neno DEAL, ambapo ni kutengeneza mpango mpya, kufuta yasiyo muhimu, kuiwezesha kazi kwenda bila wewe kuwepo na kuwa huru kusafiri kwenda popote.
Katika utekelezaji wa hatua hizi nne, Tim anashauri waliojiajiri kutumia mtiririko huo wa DEAL, lakini walioajiriwa kutumia mtiririko wa DELA, yaani kwa waajiriwa, kabla hajaweza kutengeneza njia ya kazi yake kwenda bila ya yeye kuwepo, anapaswa kutengeneza kwanza uhuru wa kutokuwepo kwenye kazi.

JINSI YA KUPATA MUDA WA KUTOSHA KUENDESHA BIASHARA UKIWA KATIKA AJIRA ( KAZI )-----COACH MWL. JAPHET MASATU

Sunday, January 12, 2020

ACHANA NA ULIMBUKENI WA KUFANYA KILA AINA YA FURSA MPYA UNAYOKUTANA NAYO , UTALIA -----COACH MWL JAPHET MASATU

Kuna wakati kila mtu alikuwa anakimbizana na fursa mpya ya ufugaji wa kware, ikaja ufugaji wa sungura, ikaja pesa za kidijitaji (cryptocurrency), ikaja forex. Hapo bado kuna vingine ambavyo huwa vinakuja na kupoteza, kama biashara za mtandao, kilimo na ufugaji na kadhalika.
Iko hivi rafiki, biashara huwa hazitofautiani sana, bali tamaa za watu ndiyo zinatofautiana. Hakuna biashara ambayo ni nzuri zaidi ya nyingine, bali uzuri wa biashara unategemea ni nani anayeifanya.
Msingi wa kwanza wa kufanikiwa kwenye biashara yoyote ile, ni kuwa tayari kujituma zaidi kwenye biashara hiyo zaidi ya wengine, kuijua kwa undani kuliko wengine. Na hili linakuwa rahisi kama mtu ataipenda biashara ambayo anaifanya, hapo atajituma zaidi na atapenda kuifuatilia kwa karibu na hivyo kuijua zaidi.
Ili kuachana na umalaya wa fursa mpya, zingatia haya yafuatayo;
( 1 ). Anza na kusudi kuu la maisha yako.
Kabla hujaamua ni biashara au kazi gani ufanye, jua lipi kusudi la maisha yako. Unapaswa kujua ni kitu gani uko hapa duniani kukifanya. Na hili utalijua kupitia vitu unavyopenda kufanya au vitu unavyovijali sana. Hata vipaji ulivyonavyo vinaashiria kusudi lako.
Kwa kulijua kusudi la maisha yako, hapo unaweza kuangalia ni biashara au kazi gani inayoendana na kusudi hilo, na hivyo ukiifanya, utakuwa kwenye nafasi nzuri ya kufanikiwa kuliko ukifanya kitu kingine.
( 2 ). Jiwekee maono makubwa.
Baada ya kujua kusudi, unapaswa kujiwekea maono, kwamba miaka kadhaa ijayo unajiona uko wapi. Jiwekee maono makubwa ya maisha yao, kwamba unajiona ukiwa wapi, ili maisha yako yawe na maana, unajiona ukifanya nini kila siku, maisha yako yakiwaje.
Ukishakuwa na maono, ni rahisi kuchagua biashara zipi zinazokufikisha kwenye maono hayo. Hutakimbilia kujaribu kila aina ya biashara, kwa sababu tayari unajua wapi unapotaka kufika.
( 3 ). Weka malengo ya kufikia maono yako.
Maono ni picha ya mbali, kitakachokufikisha kwenye picha hiyo ni malengo na mipango ambayo unakuwa umejiwekea. Hivyo unapaswa kuweka malengo ya kukufikisha kwenye maono uliyonayo.
Malengo yanapaswa kuwa ya muda mfupi, miezi, mwaka, mpaka miaka 2 na ya muda mrefu, miaka mitano, 10, 20 na kuendelea. Unapoweka malengo, unachagua kwa uhakika unatakaje kufika kwenye maono uliyonayo. Hivyo hata biashara utakazochagua, utaanza na malengo uliyojiwekea.
( 4 ). Komaa na malengo yako na mchakato wa kuyafikia.
Ukishakuwa na malengo, sasa hiyo ndiyo ramani yako, usihangaike na kitu kingine chochote. Wewe komaa na malengo uliyojiwekea na mchakato wa kuyafikia. Unapokutana na fursa mpya jiulize je hii ipo kwenye malengo yangu, kama haipo achana nayo na rudi kwenye malengo yako.
Malengo yanakupa wewe nidhamu ya kusimamia kitu kimoja mpaka kitimie, kwa sababu kuna muda uliojiwekea. Unahangaika na fursa mpya kila siku kwa sababu hakuna malengo unayofanyia kazi, hivyo chochote kipya kinachokuja huwezi kukikataa.
( 5 ). Acha tamaa na kutaka mafanikio ya haraka.
Rafiki, nina habari ambazo siyo njema sana kwako, hakuna mafanikio rahisi, ya haraka na yasiyohitaji kazi. Huo ni uongo ambao umewanasa wengi wenye tamaa na kuishia kutapeliwa. Jua kabisa kwamba kila biashara inahitaji kazi, muda, ujuzi na uvumilivu mkubwa. Haijalishi watu wanakuambia inalipa kiasi gani, usidanganyike, jua hakuna mafanikio bila ya uwekezaji mkubwa wa kazi, nguvu, muda na maumivu.
Hivyo mtu anapokuja kwako na fursa mpya, akikuambia hii inalipa sana, muulize ni gharama gani unapaswa kulipa kwa upande wa kazi, muda, ujuzi, nguvu na hata maumivu. Kama atakuambia hii ni rahisi, huhitaji hata kufanya kazi, kimbia haraka, unaingizwa kwenye utapeli.
( 6 ).Usisikilize maneno, angalia matokeo.
Mtu anapokuja kwako na kukuambia fursa fulani inalipa sana na unapaswa kuifanya, mwambie akuoneshe jinsi ambavyo yeye inamlipa. Kama ni fedha akuoneshe hizo fedha alizonazo ambazo amepata kwenye fursa hiyo mpya. Kadhalika kama ni mali pia akuoneshe.
Wengi wanaotangaza fursa mpya na wanazosema zinalipa, wao wenyewe zinakuwa hazijawalipa, ila wanakushawishi wewe uingie ili wanufaike kupitia wewe. Mfano mtu anayekuambia kware ni fursa inayolipa, unakuta yeye ndiye anayekuuzia mayai au kware wenyewe, hivyo ananufaika kupitia wewe kuhamasika na fursa.
Chunga sana, unapoambiwa kuna fursa mpya, mara nyingi wewe ndiye unayekuwa fursa yenyewe.
( 7 ). Rudi kwenye msingi mkuu wa biashara ambao ni thamani.
Rafiki, msingi mkuu wa biashara ni huu; mabadilishano ya fedha kwa thamani. Yaani kuna mtu mmoja ana fedha na ana uhitaji, halafu kuna mtu mwingine anaweza kutimiza uhitaji wake na anahitaji fedha, hapo sasa ndipo biashara inapofanyika. Kama hakuna thamani ambayo mtu anaihitaji, hakuna biashara.
Hivyo kwa kila fursa mpya unayokutana nayo, jiulize ni thamani gani ambayo utatoa kwa watu wenye uhitaji na kisha wewe ukapata fedha. Ukianza na biashara ya Forex ambayo imeulizwa hapa, jiulize kwa watu unaowafahamu wewe, forex inaongeza thamani gani kwao kiasi kwamba watakuwa tayari kukulipa wewe fedha. Utapata jibu ni hakuna.
Kadhalika kwenye vitu unavyoambiwa ni fursa kama ufugaji wa kware au sungura, jiulize wewe mwenyewe na wale wanaokuzunguka, ni lini umewahi kutafuta sana nyama ya sungura kwa sababu unaipenda sana? Jibu ni hakuna, lakini anakuja mtu anakuambia hii ni dili, na wewe unakubali!
Kama unaambiwa kitu ni fursa, lakini wewe mwenyewe hujawahi kuwa na uhitaji nacho, na hata wale wanaokuzunguka hawana uhitaji nacho, jua wewe ndiye fursa rafiki yangu, na kaa mbali.
Rudi kwenye msingi mkuu wa biashara, angalia kile ambacho tayari kina uhitaji. Badala ya kukimbizana na kware au sungura, fanya ufugaji wa kuku, kuku amekuwa kitoweo kwa kila mtu tangu enzi na enzi, huhitaji kumfundisha mtu faida za kula kuku au mayai ndiyo akuelewe na kununua. Ukiwa na kuku au mayai mazuri, kwa bei ambayo watu wanaweza kuimudu, una biashara.
Rafiki, watu wengi wanayumbishwa na fursa mpya kwa sababu hawana msimamo kwenye maisha yao, hawajui wanataka nini na hawajajipanga ni kwa namna gani watakipata, ndiyo maana kila kipya kinachokuja wanaona ndiyo tumaini lao. Ondoka kwenye hali hiyo sasa na jua nini hasa unataka kwenye maisha yako, jinsi gani utakipata na kisha kuwa na msimamo katika kuchukua hatua. Kila la kheri.
Nakutakia utekelezaji mwema wa yale ambayo umejifunza,
Rafiki na Kocha wako
Mwl    Japhet   Masatu

HATUA 04 ZA KUJIJENGEA TABIA YA KUJISOMEA VITABU VIZURI

Rafiki yangu mpendwa,

Huwa tunajenga tabia, halafu tabia zinatujenga, chochote ambacho unafanya sasa, ni tabia ambayo umejijengea siku za nyuma.

Mafanikio au kushindwa kwako ni matokeo ya tabia zako. Kama ukiwa na tabia bora utafanikiwa na ukiwa na tabia mbovu utashindwa.

Moja ya tabia muhimu unazopaswa kujijengea ili uweze kufanikiwa ni tabia ya kujisomea, ambayo itakupa maarifa bora na utakapoyatumia utaweza kupiga hatua zaidi.

Wengi wamekuwa wanasema wangependa sana kusoma vitabu, lakini hawana muda wa kufanya hivyo. Na mimi nimekuwa nawaambia siyo kweli kwamba hawapati muda, ila tu hawajaamua kusoma vitabu.

Hebu niambie unapataje muda wa kula milo mitatu kila siku, kuoga, kufuatilia habari na hata kulala? Ni kwa sababu vitu hivyo umevipa kipaumbele na vimeshakuwa tabia kwako.

Kadhalika kwenye usomaji, ukiupa kipaumbele na kujenga tabia, utakuwa msomaji mzuri sana.

Kwa upande wa kipaumbele hilo lifanye kwa kujiwekea ratiba nzuri, kila siku tenga muda wa kujisomea, unaweza kuanza na nusu saa au saa moja na pia unaweza kwenda mpaka masaa mawili na zaidi.

Kwa upande wa kuijenga tabia ya kujisomea, hapa tunakwenda kujifunza hatua nne za kutumia kujenga tabia hii. Karibu ujifunze na uchukue hatua na utaweza kuwa msomaji mzuri na kunufaika na maarifa unayoyapata.

( 1 ).TENGENEZA MWONEKANO.
Sisi binadamu huwa tunafanya kile ambacho tunakiona, kile tusichokiona huwa hatuhangaiki nacho, huwa hata hakipati nafasi kwenye fikra zetu.

Hivyo ili mipango ya kusoma ipate nafasi kwenye fikra zetu, lazima tutengeneze mwonekano wa yale yanayohusiana na kusoma.

Kitu cha kwanza kufanya ni kuwa na kitabu popote pale unapokuwepo, na usikiweke kwenye begi lako, bali kishike mkononi. Kwa kuwa umebeba kitabu, ni rahisi kukifungua na kusoma kurasa chache pale unapopata muda, kuliko ukiwa huna kitabu.

Unafikiri kwa nini unashika simu yako muda mwingi? Ni kwa sababu uko nayo. Ukikaa kwenye foleni kidogo tu unatoa simu na kuangalia, sasa badili hilo kwa kuwa na kitabu.

Najua kuna vitabu vya nakala tete, lakini katika kujijengea tabia ya kusoma, kuwa na nakala ngumu na tembea nayo popote.

Njia nyingine ya kutengeneza mwonekano ni kuwa na maktaba ndogo nyumbani kwako. Kama nyumbani kwako una tv, basi pia unapaswa kuwa na vitabu, na viweke pembeni ya tv yako. Kwa kuiona tv ambayo inakuvutia kuangalia, pembeni yake utaviona vitabu ambavyo vitakukumbusha lengo lako la kusoma zaidi.

Je umekuwa unatumia simu ukiwa kitandani? Kama jibu ni ndiyo, basi ni kwa sababu unaenda na simu hiyo kitandani. Hapa pia kuna fursa ya kutumia mwonekano kusoma zaidi. Badala ya kwenda kitandani na simu, wewe nenda na kitabu. Soma kurasa chache kabla ya kulala. Na hata wale ambao usingizi unawasumbua, ukienda na kitabu kitandani utapata usingizi haraka sana.

Tengeneza mwonekano ambao unakufanya ukione kitabu kila wakati na hilo litakusukuma kusoma zaidi.

( 2). TENGENEZA MVUTO.
Huwa tunafanya kile ambacho kinatuvutia kufanya, hivyo kwenye kujenga tabia ya kusoma vitabu, ufanye usomaji kuwa na mvuto kwako.

Zipo njia mbalimbali unazoweza kuzitumia kutengeneza mvuto kwenye usomaji.

Anza kwa kuweka kusoma kama kigezo cha wewe kufanya kile ambacho unapenda kufanya. Mfano kama unapenda sana kuangalia tv, basi weka lengo kwamba utaweza kuangalia tv kama tu utakuwa umesoma kurasa 5 za kitabu. Hili linafanya usomaji uwe na mvuto kwako, kwa sababu unakupeleka kufanya kile unachopenda kufanya.

Njia nyingine unayoweza kutumia kutengeneza mvuto kwenye usomaji ni kujiunga na watu ambao ni wasomaji. Unapowaona wengine wanasoma, na wewe unasukumwa kusoma pia. Unapoona wengine wameshirikisha vitabu walivyosoma, na wewe unapata mvuto wa kusoma ili ushirikishe pia.

Tumia kila fursa unayoipata kuufanya usomaji uwe na mvuto kwake, kiwe kitu ambacho unapendelea kukifanya kabla ya kufanya vitu vingine.

( 3 ). UFANYE USOMAJI KUWA RAHISI.
Kitu chochote ambacho kina mlolongo mrefu huwa hatukipendi, na hivyo hatukifanyi. Kitu chochote ambacho kinahitaji nguvu au kinaumiza huwa tunakwepa kukifanya.

Hivyo ili kujijengea tabia ya kusoma vitabu, rahisisha usomaji wako, ufanye usomaji kuwa rahisi, kwa kupunguza milolongo na kuondoa kazi au maumivu kwenye usomaji.

Punguza milolongo kwa kujiwekea masharti machache, kwamba ukipata muda ambao ni kuanzia dakika 5 na kuendelea, basi utafungua kitabu na kusoma, na hapo kitabu umekibeba muda wote. Usijiambie ni mpaka uwe umekaa, uwe na vitu gani ndiyo usome, wewe jiambie unapopata muda utafungua kitabu na kusoma, kisha fanya hivyo.

Ondoa ugumu kwenye usomaji kwa kuyafanya mazingira kuwa rahisi kusoma. Kama umetenga ratiba ya kusoma kwa umakini, basi hakikisha unakuwa kwenye mazingira ambayo yanachochea hilo. Kuwa eneo tulivu na simu yako iwe kwenye ukimya. Ukipata dakika 10 za kusoma eneo ambalo husumbuliwi, utajifunza mengi kuliko saa nzima ya kusoma eneo ambalo unasumbuliwa na kukatishwa mara kwa mara.

Tumia teknolojia kurahisisha usomaji wako. Kama unasoma nakala tete, unaweza kuboresha zaidi usomaji wako kupitia programu mbalimbali. Mfano kuweka lengo la kufikia kurasa fulani, kukumbushwa kuhusu mpango wako wa kusoma na hata kuchukua kumbukumbu kwa urahisi wakati wa kusoma.

Angalia ni vitu gani vinakupa ugumu kwenye kusoma sasa, kisha ondoa ugumu huo na utaweza kujijengea tabia nzuri ya usomaji.

SOMA; Kama Unataka Kufanikiwa 2020 Achana Na Malengo Na Kazana Na Kitu Hiki Kimoja.

( 4 ). PATA UFAHARI KUPITIA USOMAJI WAKO.
Sisi binadamu huwa tunafanya kile ambacho kinatupa raha, na kuepuka kile ambacho kinatupa maumivu. Hivyo ili uendelee kufanya kitu, lazima kiwe kinakupa raha.

Na hivyo ndivyo ilivyo kwenye usomaji, hakikisha usomaji wako unakupa raha na hapo utasukumwa kusoma zaidi. Zipo njia mbalimbali za kupata raha kupitia usomaji.

Washirikishe wengine kile ambacho umejifunza. Unaposoma kitabu, chagua mambo yasiyopungua kumi ambayo unaweza kuwaambia watu umejifunza kwenye kitabu hicho. Washirikishe kwenye maongezi, kwa maandishi na njia nyinginezo.

Weka orodha ya vitabu ulivyosoma na washirikishe wengine. Nafikiri utakuwa umeona jinsi ambavyo mwisho wa mwaka kila mtu anaorodhesha vitabu alivyosoma, na jinsi watu wanavyowasifia kwa kuweza kusoma vitabu hivyo vingi. Litumie hili kwa manufaa yako pia, na usisubiri mpaka mwaka uishe, wewe unaweza kufanya kila siku, kila wiki, kila mwezi na kadhalika. Cha kufanya, piga picha kitabu unachosoma kisha weka kwenye mitandao unayotumia na waambie watu unasoma kitabu hicho. Watajitokeza watu wa kukusifia na hilo litakufanya ujisikie vizuri. Pia kila wiki au mwezi unaweza kuorodhesha vitabu ulivyosoma na watu wanavyokusifia au kujadili kunakufanya ujisikie vizuri na uendelee kusoma zaidi.

Njia nyingine ya kujisikia vizuri kwenye usomaji ni kutoa nukuu na mifano kutoka kwenye vitabu unavyosoma wakati wa maongezi. Unapokuwa unaongea na wengine au kujadiliana mtandaoni na kwingineko, jenga hoja zako kwa mifano na nukuu kutoka kwenye kitabu ulichosoma. Hii itakufanya ujisikie vizuri kwa ubora wa hoja utakazokuwa umeshirikisha.

Saturday, January 4, 2020

VITU 02 VYA KUFANYA ILI UWE NA MAISHA MAREFU

 Ili uweze kuwa na maisha marefu na kuepuka kufa kabla ya muda wako, kuna vitu viwili muhimu sana unavyopaswa kuvifanya.
( 1 ). ISHI  KWA   MATUMAINI.
Lazima uwe na matumaini makubwa kwenye maisha yako, lazima uwe na kitu kikubwa unachokifanyia kazi, kinachokupa matumaini kwamba maisha ya kesho yatakuwa bora kuliko maisha ya leo. Haijalishi ni hali ngumu kiasi gani unayopitia, unapokuwa na matumaini ya kitu bora zaidi siku zijazo, unapata nguvu ya kuendelea kupambana na maisha yako kuendelea.
Matumaini yanajengwa kutoka kwenye maana ya maisha ambayo mtu unakuwa nayo, kwa kujua kusudi lako hapa duniani, kisha kuwa na maono na ndoto kubwa ambazo unazifanyia kazi. Kwa kujua kwamba kuna kitu umeletwa kufanya hapa duniani, na kuona jinsi ambavyo kinawagusa wengine, unakuwa na matumaini makubwa.
Na hata kama hujajua maana au kusudi la maisha yako, basi jiwekee lengo lolote kubwa ambalo litakusukuma sana kulifikia, kisha jikumbushe lengo hilo kila siku na amini utalifikia.
Wapo watu wengi ambao walijiwekea malengo makubwa, wakajituma sana na kuyafikia, lakini baada ya kufikia malengo hayo wakafariki dunia. Hii ni kwa sababu kufanyia kazi lengo ndiyo ulikuwa msukumo mkubwa kwao, lakini baada ya kufikia lengo wakakosa msukumo na hivyo kukaribisha kifo.
Usikubali kukaribisha kifo rafiki yangu, kila wakati jua maana na kusudi la maisha yako, kuwa na maono makubwa unayotaka kufikia na jiwekee malengo makubwa. Na kila unapofikia lengo ulilojiwekea, weka lengo jingine kubwa zaidi ya hilo. Maisha yako yakikosa mahali pa kupata matumaini, yanakuwa mafupi.
( 2 ). KAMWE  USIKATE  TAMAA.
Haijalishi umekutana na nini, haijalishi unapitia hali gani, usikubali kabisa kukata tamaa, wala usiruhusu fikra hasi na za wasiwasi kuingia kwenye akili yako. Kila wakati jikumbushe kusudi la maisha yako, kumbuka maono yako na malengo uliyojiwekea na hilo litaondoa hali ya kukata tamaa.
Dunia haitakupa kila unachotaka kwa wakati unaotaka wewe. Utaweka mipango yako vizuri, lakini matokeo utakayokuja kupata yatakuwa ya tofauti kabisa. Utakuwa na mategemeo fulani, lakini utakachokuja kupata ni tofauti kabisa na mategemeo yako. Hivyo hakikisha hali hizo unazopitia hazikukatishi tamaa, chukulia ni sehemu ya kawaida ya maisha na endelea kuwa na matumaini kwamba kesho itakuwa bora kuliko leo, kisha nenda kachukue hatua ili hiyo kesho iwe bora kweli.
Winston Churchill ni mmoja wa watu walioweka juhudi kubwa na kuiwezesha vita kuu ya pili ya dunia kumalizika. Moja ya kauli zake ambayo aliiamini sana ilikuwa ni hii; “Never give in. Never give in. Never, never, never, never—in nothing, great or small, large or petty—never give in, except to convictions of honour and good sense. Never yield to force. Never yield to the apparently overwhelming might of the enemy.” Akimaanisha kawe usikate tamaa, kamwe, kamwe, kamwe, kwa chochote kikubwa au kidogo bali kwa yale yaliyo sahihi. Kamwe usikatishwe tamaa na nguvu ya adui.
Jiambie leo na jikumbushe hili kila siku; KAMWE SITOKATA TAMAA. Na ukiweza kuishi hali hii kila siku, basi utakuwa na maisha marefu.
Ili usikate tamaa zingatia haya; kuwa na maono makubwa, amini kwenye maono hayo, usitake dunia iende kama unavyotaka wewe, pokea kila kinachokuja kwako na kitumie vizuri na usiwe mtu wa kulalamika au kulaumu wengine.

KIPATO ,NJIA ZA KUTENGENEZA KIPATO NA KUKIONGEZA------ " FURSA AFRIKA MASHARIKI BLOG "