Saturday, January 4, 2020

VITU 02 VYA KUFANYA ILI UWE NA MAISHA MAREFU

 Ili uweze kuwa na maisha marefu na kuepuka kufa kabla ya muda wako, kuna vitu viwili muhimu sana unavyopaswa kuvifanya.
( 1 ). ISHI  KWA   MATUMAINI.
Lazima uwe na matumaini makubwa kwenye maisha yako, lazima uwe na kitu kikubwa unachokifanyia kazi, kinachokupa matumaini kwamba maisha ya kesho yatakuwa bora kuliko maisha ya leo. Haijalishi ni hali ngumu kiasi gani unayopitia, unapokuwa na matumaini ya kitu bora zaidi siku zijazo, unapata nguvu ya kuendelea kupambana na maisha yako kuendelea.
Matumaini yanajengwa kutoka kwenye maana ya maisha ambayo mtu unakuwa nayo, kwa kujua kusudi lako hapa duniani, kisha kuwa na maono na ndoto kubwa ambazo unazifanyia kazi. Kwa kujua kwamba kuna kitu umeletwa kufanya hapa duniani, na kuona jinsi ambavyo kinawagusa wengine, unakuwa na matumaini makubwa.
Na hata kama hujajua maana au kusudi la maisha yako, basi jiwekee lengo lolote kubwa ambalo litakusukuma sana kulifikia, kisha jikumbushe lengo hilo kila siku na amini utalifikia.
Wapo watu wengi ambao walijiwekea malengo makubwa, wakajituma sana na kuyafikia, lakini baada ya kufikia malengo hayo wakafariki dunia. Hii ni kwa sababu kufanyia kazi lengo ndiyo ulikuwa msukumo mkubwa kwao, lakini baada ya kufikia lengo wakakosa msukumo na hivyo kukaribisha kifo.
Usikubali kukaribisha kifo rafiki yangu, kila wakati jua maana na kusudi la maisha yako, kuwa na maono makubwa unayotaka kufikia na jiwekee malengo makubwa. Na kila unapofikia lengo ulilojiwekea, weka lengo jingine kubwa zaidi ya hilo. Maisha yako yakikosa mahali pa kupata matumaini, yanakuwa mafupi.
( 2 ). KAMWE  USIKATE  TAMAA.
Haijalishi umekutana na nini, haijalishi unapitia hali gani, usikubali kabisa kukata tamaa, wala usiruhusu fikra hasi na za wasiwasi kuingia kwenye akili yako. Kila wakati jikumbushe kusudi la maisha yako, kumbuka maono yako na malengo uliyojiwekea na hilo litaondoa hali ya kukata tamaa.
Dunia haitakupa kila unachotaka kwa wakati unaotaka wewe. Utaweka mipango yako vizuri, lakini matokeo utakayokuja kupata yatakuwa ya tofauti kabisa. Utakuwa na mategemeo fulani, lakini utakachokuja kupata ni tofauti kabisa na mategemeo yako. Hivyo hakikisha hali hizo unazopitia hazikukatishi tamaa, chukulia ni sehemu ya kawaida ya maisha na endelea kuwa na matumaini kwamba kesho itakuwa bora kuliko leo, kisha nenda kachukue hatua ili hiyo kesho iwe bora kweli.
Winston Churchill ni mmoja wa watu walioweka juhudi kubwa na kuiwezesha vita kuu ya pili ya dunia kumalizika. Moja ya kauli zake ambayo aliiamini sana ilikuwa ni hii; “Never give in. Never give in. Never, never, never, never—in nothing, great or small, large or petty—never give in, except to convictions of honour and good sense. Never yield to force. Never yield to the apparently overwhelming might of the enemy.” Akimaanisha kawe usikate tamaa, kamwe, kamwe, kamwe, kwa chochote kikubwa au kidogo bali kwa yale yaliyo sahihi. Kamwe usikatishwe tamaa na nguvu ya adui.
Jiambie leo na jikumbushe hili kila siku; KAMWE SITOKATA TAMAA. Na ukiweza kuishi hali hii kila siku, basi utakuwa na maisha marefu.
Ili usikate tamaa zingatia haya; kuwa na maono makubwa, amini kwenye maono hayo, usitake dunia iende kama unavyotaka wewe, pokea kila kinachokuja kwako na kitumie vizuri na usiwe mtu wa kulalamika au kulaumu wengine.

No comments:

Post a Comment