Wednesday, March 25, 2020

MWONGOZO WA KUFANYIA KAZI AU KUJISOMEA KWA WANAFUNZI NYUMBANI !!!

FAIDA  ZA  KUFANYIA  KAZI  / KUJISOMEA  NYUMBANI.
Kufanyia kazi zako nyumbani, iwe umeajiriwa au umejiajiri au  wewe  ni  mwanafunzi wa  shule  za   msingi , sekondari  au  chuo   kuna faida nyingi sana, baadhi ya faida hizo ni kama ifuatavyo;
  1. Unaokoa muda mwingi ambao huwa unaupoteza kwa kwenda eneo la kazi, shule au  chuo  Kuanzia muda unaotumia kwenda, kurudi na mwingine unaopotea, kwa kufanyia kazi nyumbani hupotezi muda wako.
  2. Unapunguza fursa za kupoteza muda zinazopatikana kwenye eneo la kazi, mfano mikutano mbalimbali ambayo hufanyika maeneo ya kazi, ambayo kwa sehemu kubwa haina tija.
  3. Unafanya kazi kwa mpango wako bila ya kusumbuliwa na wafanyakazi wengine.Kama  mwanafunzi  au  mwanachuo unaepuka  kelele  za  wanafunzi  wenzako . Japo kunakuwa na mawasiliano ya simu au njia nyingine za mtandao, ile hali ya kukatishwa na wengine wakati unafanya kazi  au  unajisomea  inapungua.
  4. Kwa sehemu kubwa unakuwa na uhuru wa kupanga muda wako mwenyewe, hasa kama kazi yako haihitaji kushirikiana na wengine wakati mnaifanya. Unaweza kupanga kufanya kwa muda unaofaa kwako.
  5. Unapata muda mwingi wa kupumzika, majukumu yako unayofanya ukiwa kazini, shule , chuo ukiyafanyia nyumbani itakuchukua nusu ya muda unaotumia kuyafanya ukiwa kazini , shule  au  chuo .Hivyo unapata muda mwingi wa kupumzika au kufanya mambo mengine.
Changamoto za kufanyia kazi nyumbani.
Hakuna kisichokuwa na changamoto, na katika kufanyia kazi nyumbani, zipo changamoto nyingi. Hapa ni baadhi ya changamoto hizo;
  1. Kushindwa kutekeleza majukumu yako kwa wakati kwa sababu hakuna anayekusimamia moja kwa moja au anayekuangalia. Unahitaji nidhamu kali sana kuweza kujisimamia mwenyewe.
  2. Usumbufu wa wanafamilia wakati unafanya kazi, wengi hawajui kwamba japo upo nyumbani pia upo kazini, hivyo kuingilia kazi zako pale wanapokuwa na mahitaji mbalimbali.
  3. Kukosekana kwa mipaka kati ya kazi na maisha. Kwa kuwa unafanyia vyote nyumbani, ni rahisi kushindwa kuweka mipaka, ukajikuta unaruhusu mambo ya kifamilia kuingia kwenye wakati wa kazi au mambo ya kikazi kuingia kwenye wakati wa familia.
  4. Wageni usiokuwa na miadi nao wanapokuja nyumbani na kujua upo, wanaingilia sana muda wako wa kazi. Wengi hawawezi kuelewa kwamba japokuwa upo nyumbani, upo kazini, hivyo kuhitaji muda wako mwingi.
  5. Ni rahisi kwa uvivu kukunyemelea, ukipatwa na usingizi kidogo ni rahisi kwenda kulala au kufanya mambo mengine ya kupoteza muda kama kuangalia tv, kuzurura mitandaoni na kadhalika.
MKAKATI  BORA  KWAKO  WA   KUFANYIA  KAZI  NYUMBANI.
Ili kupata manufaa ya kufanyia kazi nyumbani, pamoja na kuzuia changamoto zake zisiwe kikwazo kwako, tengeneza mkakati mzuri kwako kufanyia kazi nyumbani
Zingatia mambo yafuatayo katika kutengeneza mkakati wako wa kufanyia kazi nyumbani utakaokupa matokeo mazuri.
( 01 ). TENGA  ENEO  LA  KUFANYIA  KAZI.
Kitu cha kwanza muhimu kabisa kwako kufanya ni kutenga eneo la kufanyia kazi ukiwa nyumbani. Huwezi kuwa unafanyia kazi kila mahali na ukawa na nidhamu nzuri. Badala yake unapaswa kutenga eneo ambalo utakuwa unafanyia kazi zako, na ukiwa eneo hilo unachofanya ni kazi tu na siyo kitu kingine.
Hii inakuandaa kisaikolojia kuheshimu eneo hilo na unapokuwa kwenye eneo hilo unajua cha kufanya ni kazi. Kama unaishi kwenye nyumba kubwa unaweza kutenga chumba utakachotumia kama ofisi. Lakini kama huwezi kufanya hivyo unaweza kutenga eneo kwenye chumba chochote, hata kile unacholala na kulitumia kama eneo la kazi.
Kama unatenga eneo ndani ya chumba chenye matumizi mengine, hakikisha unaweka kiti na meza kwa ajili ya kufanyia kazi. Hivyo unapokaa kwenye kiti na meza hiyo, unajua kabisa hili ni eneo la kazi. Usifanye kitu kingine unapokuwa kwenye kiti na meza ulivyoandaa kwa ajili ya kazi.
Epuka kufanyia kazi kitandani au kwenye kochi, kwenye maeneo hayo hutaipa kazi uzito kwa sababu kisaikolojia unayachukulia kama maeneo ya kupumzika
 ( 02 ). TENGENEZA  RATIBA  YAKO  YA  KILA  SIKU  NA  IFUATE.
Japokuwa una uhuru wa muda gani ufanye kazi unapokuwa nyumbani, uhuru huo una mipaka. Huwezi kufanya kazi zako pale unapojisikia, ukienda kwa mpango huo hutafanya chochote. Ndiyo una uhuru, lakini lazima utengeneze ratiba yako mwenyewe na uifuate kila siku.
Panga kabisa ni muda gani unaamka, ukiamka unafanya nini, muda gani unapumzika, unakula na unakuwa na familia. Yote hayo lazima uyapange na kisha kuyafuata.
Ukianza siku zako bila mpango, utajikuta umefanya mengi, umechoka lakini hakuna kikubwa ulichokamilisha.
Kwenye ratiba yako ya siku tenga kabisa masaa ambayo huhitaji usumbufu, hayo ni masaa ya kazi zinazohitaji umakini mkubwa.
( 03 ). VAA  KAMA  UNAENDA  KAZINI / SHULENI / CHUONI
Unapofanyia kazi nyumbani, una uhuru wa kuvaa utakavyo au hata kutokuvaa kabisa. Lakini hilo unapaswa kuwa nalo makini, kwa sababu lina madhara ya kisaikolojia kwenye utekelezaji wa majukumu yako ya kazi. Kama umevaa nguo za kawaida utajiona kama hauna majukumu makubwa.
Hivyo unapaswa kujiandaa vizuri kama vile unaenda kazini  shuleni, chuoni kwa kuvaa kabisa nguo zako za kazi na kisha kukaa eneo lako la kazi wakati unafanya kazi. Unapovaa nguo kama vile unaenda kazini, akili yako inakupa uzito wa kikazi na unatekeleza majukumu yako vizuri. 
( 04 ). WATU  WOTE  WAJUE  RATIBA  YAKO.
Ukishaweka ratiba yako ya siku, kila mtu kwenye familia anapaswa kuijua. Na waeleze wazi kwamba japokuwa upo nyumbani, lakini pia upo kazini au  unajisomea. Kwa muda ule wa kazi, mambo yote hapo nyumbani yanapaswa kuendelea kama vile wewe haupo kabisa.
Ule muda ambao umetenga usisumbuliwe, usisumbuliwe kweli, labda kwa jambo la dharura, ambalo hata kama ungekuwa kazini basi ungepigiwa simu. Na weka kabisa vigezo vya dharura ni vipi. Usipofanya hivi, watu watatumia uwepo wako kuuliza vitu mbalimbali na hilo kuathiri kazi zako.
Kuhusu wageni, kama kuna mgeni amekuja na hukuwa na miadi naye, usikutane naye wakati ambao unafanya kazi. Anapaswa kuelezwa ratiba yako na muda mzuri kwako kukutana naye. Na kama ni mgeni muhimu, unaweza kumsalimia na kumpa ratiba yako ilivyo na mkapanga muda gani mzuri wa kuwa na maongezi, kama yapo na ni muhimu.
( 05 ). TENGENEZA  MIPAKA YA  KAZI / KUSOMA  NA  MAISHA.
Kwa kuwa upo nyumbani na unafanyia kazi nyumbani, mpaka kati ya kazi na maisha unafutika kabisa. Wakati wa kazi utaingiliwa na mambo ya kifamilia na wakati wa familia utaingiliwa na mambo ya kikazi.
Ni lazima utengeneze mpaka kati ya kazi na maisha, ufanye kazi wakati wa kazi na maisha wakati wa maisha. Jisukume kutekeleza majukumu yako ya kazi kwa wakati uliopanga kufanya kazi na ule wakati uliopanga kupumzika au kuwa na familia basi usiruhusu kazi au  masomo kuingilia wakati huo.
( 06 ). TUMIA  VIFAA  VYA  KUONDOA  USUMBUFU.
Kama mazingira ya nyumbani kwako siyo rafiki kwako kupata utulivu wa kazi au kusoma, labda kuna kelele mbalimbali za majirani na watu wengine, basi tumia vifaa vya kuondoa usumbufu.
Hapa unapaswa kuwa na spika za masikioni (headphone au earphone) ambazo utazivaa wakati wa kufanya kazi. Kuna ambazo zina sifa ya kufunga kelele za nje zisikuingie na hivyo kukupa utulivu mkubwa wa kufanya kazi zako.
Pia kitendo cha kuvaa spika hizo, kinamfanya mtu asikusemeshe mara kwa mara, kwa sababu anajua humsikii. Pia mtu anapokusemesha, jifanye kama humsikii, hata kama unamsikia, hasa pale jambo linapokuwa siyo muhimu.
Inayoendana na hii ni kuandaa orodha ya nyimbo (playlist) zinazokupa utulivu na kuitumia wakati unafanya kazi zako. Hapa unasikiliza nyimbo hizo kwa kujirudia rudia na hilo linafanya akili yako izame kwenye kazi unayofanya na kuepuka usumbufu.
( 07 ). JALI  AFYA  YAKO.
Unapofanyia kazi nyumbani, kama kazi zako ni za kutumia akili na unazipenda sana, unaweza kujikuta umekaa kwenye kazi siku nzima na hujatoka kabisa nje ya nyumba yako. Pia ulaji ni rahisi sana unapokuwa nyumbani kuliko ukiwa kazini, ni rahisi kula mara kwa mara ukiwa nyumbani kuliko ukiwa kazini.
Hivyo unapaswa kuwa na mkakati wa kujali na kuboresha afya yako. Kitu cha kwanza muhimu ni kufanya mazoezi, tenga muda wa kufanya mazoezi ambayo yatakutoa jasho. Cha pili ni kudhibiti ulaji, usile kwa sababu kuna kitu cha kula, bali kula kwa utaratibu maalumu na kuwa makini na kile unachokula. Cha tatu ni muda wa kupumzika, unaweza ukakosa mapumziko mazuri japo uko nyumbani na hilo likaathiri afya yako.
(08 ). PANGILIA  MUDA  UNAOENDANA  NA  WEWE  NA  UNAOEPUKA  USUMBUFU.
Kitu kimoja ambacho kimekuwa kinanisaidia sana mimi binafsi kuweza kukamilisha sehemu kubwa ya uandishi ni kutenga muda wa uandishi ambao unaendana na mimi na pia unaepuka usumbufu.
Huwa ninaamka saa kumi kamili asubuhi kila siku na baada ya kufanya tahajudi na tafakari kisha kuipangilia siku, kuanzia saa kumi na nusu mpaka saa 12 kamili huo ni muda wa kuandika tu, sifanyi kingine kwenye muda huo. Kwa muda huo, nimekuwa na uwezo wa kuandika kwa kiwango kikubwa sana, kwa sababu akili inakuwa na utulivu na hakuna usumbufu, maana watu wengine wanakuwa wamelala kwenye muda huo.
Hivyo na wewe pangilia majukumu yanayohitaji utulivu na umakini kulingana na wewe binafsi na mazingira. Yaani yapange kwenye muda ambao akili yako iko vizuri lakini pia hakuna usumbufu wa nje.
Watu tumegawanyika kwenye makundi mawili; kuna ambao wanaweza kuamka asubuhi na mapema na akili zao zikawa vizuri (early birds) na kuna ambao wanachelewa kulala na muda wa usiku ndiyo akili zao zinakuwa vizuri (night owls). Jijue wewe uko kundi gani, kisha tenga muda ambao wengine wamelala na ufanye kuwa wa kazi.
Mfano kama uko vizuri kwenye kuamka asubuhi basi amka asubuhi na mapema sana, labda saa tisa au saa kumi na kisha tumia masaa mawili ya kwanza kwenye kazi inayohitaji umakini wako na utulivu. Muda huo wengi wanakuwa wamelala na hivyo usumbufu unakuwa mdogo.
Na kama unachoelewa kulala basi tenga masaa mawili ya usiku mnene ambapo wengine wamelala na akili yako imetulia kufanya kazi.
Ukiweza kutenga masaa mawili ambapo akili yako imetulia na ina umakini na hakuna usumbufu wa nje, kisha kuyaweka masaa hayo mawili kwenye kazi, utatekeleza majukumu makubwa kuliko anayefanya kazi siku nzima kwenye ofisi isiyo na utulivu.
Rafiki yangu mpendwa, mdau  wangu  huu ndiyo mwongozo sahihi kwako wa kufanyia kazi nyumbani .(  kama  wewe  ni  MWAJIRIWA , UMEJIAJIRI , MWANAFUNZI , MWANACHUO  ni  mwongozo  mzuri  sana  kuufuata.

Sunday, March 15, 2020

UMEHITIMU SHAHADA NA HUJUI CHA KUFANYA !! FANYA YAFUATAYO.

Haya hapa ni mambo matano unayoweza kufanya kama umehitimu na huna kazi.
( 1 ). UZA  NGUVU   ZAKO.
Hapa unachagua kutafuta kazi ambayo inahitaji nguvu zako kuifanya, hapa elimu yako haina nafasi, bali ni nguvu pekee.
Zipo kazi nyingi za kufanya ambazo zinahitaji nguvu za watu, iwe ni kusaidia kwenye shughuli za ujenzi, kilimo, na kazi nyingine, tafuta nafasi ya kutoa nguvu zako na fanya hivyo.
Kama huna kazi yoyote unayoifanya, usijiambie huwezi kufanya kazi ya kutumia nguvu, unachohitaji sasa ni kitu cha kufanya, hivyo tumia nafasi hiyo kuanza kujenga misingi yako.
( 2 ). UZA  TAALUMA  YAKO  KWA  MLAJI  WA  MWISHO.
Elimu imekuandaa kuuza taaluma yako kwa mtu wa kati, ambaye anaiuza kwa mlaji wa mwisho. Yaani kama ni mwalimu basi unategemea uajiriwe na shule kisha utoe taaluma yako kwa wazazi wenye watoto.
Sasa kama hilo linashindikana, wewe nenda moja kwa moja kwa mlaji wa mwisho. Uza taaluma yako moja kwa moja kwa wale wenye uhitaji nayo.
Hivyo kama ni mwalimu, nenda moja kwa moja kwa wazazi wenye watoto wanaosoma, kisha wape huduma ya masomo ya ziada kwa watoto wao kupitia taaluma yako na wao wakulipe.
Kadhalika kama umesomea uhasibu, badala ya kusubiri kuajiriwa na taasisi fulani, nenda moja kwa moja kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati na wape huduma zako za kihasibu, ambazo wanazihitaji sana ila hawajui wanazipata wapi.
Kwa taaluma yoyote uliyosomea, kuna nafasi ya kwenda moja kwa moja kwa mlaji wa mwisho na ukamuuzia taaluma hiyo. Usisubiri mpaka upate ajira rasmi, andaa sasa huduma unazoweza kutoa na nenda kwa walaji kuwashawishi wakupe nafasi ya kuwauzia taaluma yako.
 ( 03 ). UZA   VIPAJI   VYAKO.
Kabla hata hujaingia kwenye mfumo wa elimu na kupata shahada, kuna vitu ulikuwa unapendelea kufanya au kufuatilia. Vitu hivyo uko tayari kuvifanya hata kama hakuna anayekulipa.
Sasa ni wakati mzuri wa kugeuza vitu hivyo kuwa sehemu ya wewe kuingiza kipato. Angalia ni nini unapenda kufanya, kisha jiulize ni watu gani wanaweza kuwa na uhitaji wa kitu hicho, kisha wapatie na wao wakulipe.
Kama unapenda michezo angalia ni jinsi gani unaweza kuwapa wengine thamani kupitia mapenzi yako ya michezo na wao wakakulipa, labda ni kwa kuchambua vizuri michezo au kushauri vizuri maeneo hayo na kadhalika.
Kama unapenda kusoma vitabu angalia ni kwa namna gani wengine wanaweza kukulipa kwa usomaji wako wa vitabu, labda ni kwa kuwachambulia vitabu au kutafuta vitabu vizuri na kuwashawishi wengine wanunue kwa kuwaeleza kile kilichopo ndani.
Haijalishi unapenda vitu gani au una vipaji gani, wapo wengine wengi ambao wanaweza kunufaika na kile unachofanya. Muhimu ni wewe kuwajua na uweze kuwafikia.
( 04 ). UZA  VITU  VYA   WENGINE.
Kuna makampuni mengi ambayo yana bidhaa na huduma nzuri, lakini hayajalifikia soko vizuri. Wewe unaweza kutumia nafasi hiyo kwa kuwa muuzaji kwenye makampuni hayo.
Kuna makampuni ambayo tayari yana mfumo wa kuchukua wauzaji na kuwalipa kwa kamisheni, kama ukipata kampuni ya aina hii unaweza kujiunga nayo, ukawa muuzaji na ukalipwa kwa kamisheni.
Kuna makampuni mengine hayana mfumo huo, lakini unaweza kuyashawishi na yakakupa nafasi ya kuuza bidhaa zao. Kwa mfano umetumia bidhaa fulani na ukaikubali sana, na unawaona wengine wanaihitaji lakini hawajui kama wanaweza kuipata. Unaweza kuishawishi kampuni husika ikupe bidhaa hiyo ukauze kwa wengine, au ukanunua na kwenda kuuza kwa mfumo huo.
Hapa pia unaweza kujiunga na kampuni zinazofanya biashara kwa mfumo wa mtandao (Network Marketing). Huu ni mfumo unaoruhusu mtu yeyote kuweza kuingia kwenye biashara kwa mtaji kidogo au bila mtaji kabisa.

 ( 05 ). ANGALIA  UNACHOWEZA  KUWASAIDIA  WENGINE.
Hata kama yote uliyojifunza hapo juu yameshindikana, basi angalia ni msaada gani unaoweza kutoa kwa wengine wenye uhitaji na wao wakakulipa. Iko hivi rafiki, fedha ni zao la thamani, kama unataka kupata fedha, zalisha thamani zaidi kwa wengine.
Kama umesoma mpaka kupata shahada, basi akili yako imefunguka, tumia akili hiyo iliyofunguka kuona watu wana uhitaji gani ambao unaweza kuwasaidia.
Wacha nikupe mfano mmoja ambao utakufungua zaidi, halafu baada ya hapo jiongeze mwenyewe. Chukua mfano wewe ni mtumiaji mzuri wa mitandao ya kijamii, kila siku lazima uingie kwenye mitandao hii kufuatilia yanayoendelea. Lakini hapo ulipo kuna wafanyabiashara wengi wadogo ambao hawajui jinsi ya kutumia mitandao hii kupata wateja wengi zaidi. Wewe unayo nafasi ya kuwasaidia kwenye hilo, unaweza kuwafungulia akaunti kwenye mitandao hii, kuendesha kampeni mbalimbali ambazo zitawapa wateja zaidi na wao wakakulipa kulingana na wateja wa ziada wanaopata. Kuna mengi kama haya unaweza kufanya, fungua akili yako, angalia mahitaji ya watu kisha ona ni jinsi gani unaweza kuwasaidia kuyatimiza.
Anza sasa kufanya mambo haya uliyojifunza hapa, mambo yote haya hayahitaji uwe na akili zaidi au uwe na mtaji ndiyo uanze kufanya, yanahitaji maamuzi kwamba utafanya na uanze kufanya.
Fikiria umekaa nyumbani miaka miwili bila kufanya chochote tangu umehitimu, hebu pata picha kama ungekuwa unafanya kimoja tu kati ya hivi, kwa miaka miwili ungekuwa wapi?
Endelea kusubiri ajira, endelea kutuma maombi, lakini wakati huo usiyasimamishe maisha yako, chagua kile ambacho utakifanya katika haya uliyojifunza hapa, kisha kifanye kila siku, kazana kutoa thamani zaidi kila siku. Na miaka miwili ijayo, hutahitaji hata kuwa na hiyo ajira unayoisubiri sasa, maana utakuwa umepiga hatua kubwa, kama utajitoa kweli sasa.

NGUVU : ONGOZA KWA UJASIRI---PATA UJASIRI WA KUJITOA MHANGA-----NA DR. KAZUO INAMORI

IF WE ENCOUNTEER A MAN OF RARE INTELECT , WE SHOULD ASK HIM WHAT BOOKS HE READS-----Ralph Waldo Emerson