Friday, April 26, 2019

JIWEKE KWENYE VIATU VYA MWINGINE HUTAKUWA NA SABABU YA KUUMIZWA NA CHOCHOTE TOKA KWA WENGINE


Njia ya kuondokana na msongo na kupata utulivu kwenye maisha yako ni kujiweka kwenye viatu vya wengine, kukaa kwenye nafasi ya mwingine ili kuweza kuelewa kwa nini mtu amefanya kile ambacho amefanya.

Chanzo kikubwa cha hasira, msongo na hata migogoro kwenye maisha yetu ni mahusiano yetu na wengine. Pale wengine wanapofanya vitu ambavyo hatukutegemea wafanye, tunapatwa na hasira na msongo. Tunaona kama wamefanya kwa makusudi au wamepanga kutuumiza kwa namna fulani.

Lakini mara nyingi sana watu wanafanya vitu kwa nia njema, hasa kwa upande wao. Ni wachache sana ambao wanafanya kitu kwa makusudi ili kumuumiza mtu mwingine. Ukitaka kuelewa kwa nini mtu amefanya kile alichofanya, jaribu kwanza kujiweka kwenye nafasi yake.

Kila mtu huwa ana sababu nzuri ya kufanya kile ambacho amefanya, iwe ni kizuri au kibaya kwako. Ukichukua nafasi ya kuelewa sababu hiyo, hasa kwa kujiweka kwenye nafasi yako, utagundua huna sababu ya kuwa na hasira au msongo. Kwa sababu huenda na wewe ungekuwa kwenye nafasi kama yake ungefanya kama alivyofanya yeye.

Tambua kwamba watu wana mitazamo tofauti, vipaumbele tofauti, uelewa tofauti na hata imani tofauti. Ukichukua nafasi ya kuelewa hayo kuhusu wengine, utaona huna sababu ya kuumizwa na chochote ambacho wengine wanafanya.

BADILI MPANGILIO WA VIPAUMBELE PALE MAMBO YANAPOKWENDA TOFAUTI.

Njia ya kuondokana na msongo na kuwa na utulivu kwenye maisha yako ni kubadili mpangilio wa vipaumbele vyako kulingana na mazingira unayojikuta upo. Kila mmoja wetu ana mpangilio wake wa vipaumbele, na tunapenda mpangilio huo uende hivyo bila ya kubadilika. Inapotokea hali inayobadili mpangilio huo tunapatwa msongo na kuona hatuna udhibiti wa maisha yetu.

Hatua bora za kuchukua hapa ni kubadili mpangilio wa vipaumbele vyako. Mfano inawezekana familia kwako ni kipaumbele cha kwanza, kazi au biashara ni kipaumbele cha pili. Sasa unajikuta kwenye kazi au biashara ambayo inataka muda wako mwingi na kukunyima muda wa kukaa na familia, ambayo ndiyo kipaumbele cha kwanza. Hali hii inaweza kukuletea msongo mkubwa na kukosa utulivu, kwa sababu vipaumbele vyako vinavurugwa. Lakini unaweza kuchukua hatua ya kubadili mpangilio wa vipaumbele vyako kulingana na hali uliyonayo. Kwa kipindi fulani kuweka kipaumbele cha kwanza kuwa kazi au biashara kabla ya familia, na baada ya kujijengea msingi mzuri ukarudi kwenye vipaumbele vyako vya awali.

Hilo pia linakwenda kwa vipaumbele vingine kwenye maisha, mfano kama umekuwa unapendelea kufanya kazi mwenyewe, lakini ukajikuta kwenye kazi inayokutaka ushirikiano na wengine, kama hutabadili kipaumbele kuwa kufanya kazi na wengine utakuwa na msongo kipindi chote cha kazi. Kadhalika kwenye mahusiano na maeneo mengine ya maisha, pale mazingira yanapobadilika au unapokutana na uhitaji tofauti, kuwa tayari kubadili vipaumbele vyako.

Unapobadili vipaumbele kulingana na mazingira au hali inapobadilika, unakuwa tayari kutumia kila hali unayokutana nayo badala ya kupambana nayo.

Tuesday, April 23, 2019

KUWA KING"ANG"ANIZI NA MVUMILIVU UTAFANIKWA SANA.

Kila kitabu kinachohusu mafanikio kinasisitiza sana ung’ang’anizi na uvumilivu ili kuweza kufanikiwa. Lakini siyo kila ung’ang’anizi na uvumilivu utakufikisha kwenye mafanikio. Bali unahitaji ung’ang’anizi sahihi, na kukubali pale ambapo umekosea ili kuboresha zaidi.
Tunapaswa kuwa ving’ang’anizi ili kupata utajiri na mafanikio, tunapaswa kujaribu tena na tena na tena kila tunaposhindwa. Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba kufanya jambo lile lile kwa njia ile ile halafu kutegemea kupata matokeo tofauti ni maana sahihi ya ujinga.
Tunapaswa kung’ang’ana kwa njia sahihi, tunapaswa kubadili njia tunazotumia, ambacho hatupaswi kubadili ni lengo ambalo tumejiweka. Tunapaswa kuendelea na mapambano mpaka pale tutakapopata tunachotaka.
Wote tunajua jinsi ambavyo dunia ina uangalifu, haikubali kutoa kitu kwa mtu ambaye hajaonesha kweli anakitaka na yupo tayari kulipa gharama kukipata. Jioneshe kwamba wewe unautaka utajiri kweli, kuwa tayari kulipa gharama na ng’ang’ana kwa njia sahihi na utapata unachotaka.

JIAMINI WEWE MWENYEWE.

Kama hujiamini wewe mwenyewe, hakuna yeyote anayeweza kukuamini na hutaweza kufanikiwa kwenye jambo lolote maishani mwako.
Unapaswa kujiamini wewe mwenyewe, unapaswa kuamini kwamba una uwezo mkubwa ndani yako wa kukuwezesha kupata chochote unachotaka, unapaswa kuamini hakuna kinachoweza kukuzuia kupata kile unachotaka. Tunaambiwa imani inaweza kuihamisha milima, na hii ndiyo imani unayopaswa kuwa nayo ili kufanikiwa na kufikia utajiri.
Katika safari yako ya kusaka utajiri utakutana na vikwazo vya kila aina, utapatwa na hofu nyingi, wapo watakaokukatisha tamaa kwa kukupa mifano ya wengi walioshindwa. Kitu pekee kinachoweza kukuvusha kwenye hali hizo ni kujiamini wewe mwenyewe.
Pia hakuna utakachopanga na kikaenda kama ulivyopanga, utashindwa kwenye mambo mengi licha ya kufanya kila unachopaswa kufanya. Kujiamini ndiyo kutakupa nguvu ya kuamka kila unapoanguka ili uweze kuendelea na safari ya mafanikio.
Jiamini wewe mwenyewe na hakuna kitakachoweza kukuzuia kufanikiwa.

AMINI SAUTI YAKO YA NDANI.

Kila mmoja wetu ana sauti iliyopo ndani yake, hisia fulani unazozipata ambazo huwezi kuzielezea, ambazo zinakuashiria kama kitu ni kibaya au kizuri, kama ni sahihi au siyo sahihi. Mara nyingi huwa tunapuuza sauti hii na matokeo yake tunafanya makosa makubwa. Kuna wakati ndani yako unapata msukumo wa kufanya au kutokufanya kitu, lakini ushawishi wa nje unakufanya uende kinyume na sauti hiyo na unakuja kugundua ungejisikiliza ungekuwa sahihi zaidi.
Jifunze kuamini sauti yako ya ndani, hata kama inaendana na uhalisia wa nje. Kuna kitu kwa nje kinaweza kuonekana ni sahihi, lakini sauti yako ya ndani ikakuambia siyo sahihi, au kitu kwa nje kikaonekana siyo sahihi, lakini sauti yako ya ndani ikakuambia ni sahihi. Jifunze kusikiliza sauti yako ya ndani, inajua zaidi kuliko wewe na itakuongoza kwa usahihi mara zote.
Watu wote ambao wamefikia utajiri na mafanikio makubwa, kuna hatua ambazo wamewahi kuzichukua, ambazo watu wa nje waliwaambia wanakosea, lakini wao walifanya, kwa sababu sauti ya ndani iliwaambia ndiyo kitu sahihi kufanya.
Unapojikuta njia panda na hujui hatua ipi sahihi kuchukua, isikilize sauti yako ya ndani, inajua njia sahihi na utaweza kufanya kilicho sahihi.

SIKILIZA NA JIFUNZE.

Kusikiliza ndiyo silaha yenye nguvu sana katika safari ya mafanikio. Ukiwa msikilizaji mzuri, utajifunza mambo mengi sana kwa watu wengine. Kuanzia wale unaofanya nao kazi na hata wale ambao inabidi upatane nao kwenye makubaliano mbalimbali.
Kusikiliza ni kugumu sana, na wengi hawawezi kusikiliza kwa umakini ndiyo maana hawajifunzi, hawajui watu wanataka nini na kuweza kuwapatia. Ukiwa mtu wa kusikiliza kwa umakini, kwa lengo la kuelewa na kujifunza, utajua mengi na pia utazijua tabia za watu, ambazo utaweza kuzitumia kwa mafanikio zaidi.
Ukiwasikiliza wateja wako utayajua mahitaji yao hata kama hawajakuambia wazi na kuweza kuwatimizia. Ukiwasikiliza wafanyakazi wako utajua kinachowahamasisha na ukiwapatia watajituma zaidi. Ukiwasikiliza unaotaka kufikia nao makubaliano, utajia udhaifu wao uko wapi na kuweza kuutumia.
Katika safari ya mafanikio na utajiri, kusikiliza na kujifunza ni hitaji muhimu sana. Hata watu wanawaheshimu sana wale ambao wanachukua muda na kusikiliza. Tumia nguvu hii kwa manufaa yako na ya wengine pia.

KUWA NA VYANZO VINGI VYA KIPATO.

Chanzo kimoja cha kipato ni utumwa, iwe ni kazi au biashara, huwezi kutajirika kwa kutegemea chanzo kimoja pekee. Angalia matajiri wote wakubwa, hakuna hata mmoja ambaye anategemea chanzo kimoja pekee cha kipato.
Kila biashara huwa ina changamoto zake, hakuna biashara ambayo inafanya vizuri wakati wote, kila biashara kuna kipindi inafanya vizuri na kipindi kingine inafanya vibaya. Unapotegemea biashara moja pekee, kila wakati utakuwa kwenye kupanda au kushuka.
Dawa ya kuondoa hali hiyo ya kupanda na kushuka ni kuwa na vyanzo vingi vya kipato, na ambavyo havitegemeani. Hivyo unapokuwa na changamoto eneo moja, eneo jingine linakuwa linaenda vizuri.
Kanuni hii haiwahusu wale wanaoanza, unapokuwa unaanza, anza na kitu kimoja na kiwekee msingi imara wa kuweza kujiendesha chenyewe. Baada ya kuhakikisha kitu cha kwanza kimekuwa imara, hapo sasa unaweza kuanzisha kitu kingine. Kuanza vitu vingi kwa wakati mmoja ni njia ya uhakika ya kushindwa.

UKWELI KUHUSU UTAJIRI.

Wengi wanapoingia kwenye safari hii ya utajiri, huwa wanaona mambo mazuri tu mbele, kwamba wakishapata utajiri maisha yatakuwa mazuri na watakuwa na furaha.
Felix anatupa ukweli kuhusu utajiri, kupitia maisha yake binafsi, ili tuelewe ni kitu gani tunakwenda kukutana nacho mbele, na tujiandae vizuri.
Kwanza kabisa anasema utajiri haujawahi kumletea yeye furaha, zaidi umemletea matatizo makubwa ya kiafya baada ya kujihusisha na ulevi, madawa ya kulevya na uzinzi.
Pili anasema utajiri unakufanya uwe chambo ambapo kila mtu atatumia kila njia kupata fedha zako. Wapo watakaotumia njia za kuomba, wengine kuiba na hata wengine kukushitaki kwa kitu ambacho hujafanya.
Tatu utajiri utaharibu mahusiano mengi uliyonayo. Mahusiano ya ndoa, kwa wengi yanaathirika sana. mahusiano ya kifamilia na kindugu nayo yanaathiriwa sana na safari yako ya utajiri na hata baada ya kufikia utajiri.
Kwa kifupi kadiri unavyokuwa tajiri siyo kwamba matatizo uliyonayo yanaondoka, bali yanakuwa makubwa zaidi. Hivyo jiandae kukabiliana nayo, na kazana kujijengea busara zaidi kadiri unavyoendelea kutajirika. Kwa sababu utajiri bila busara utakuwa ni kujichimbia kaburi lako mapema.

JE, NI KWELI WALIOFANIKIWA WANA BAHATI ?


Felix Dennis katika kitabu chake anatuambia ni kweli kwamba watu waliofanikiwa wana bahati kuliko wale ambao hawajafanikiwa. Lakini kitu tunachopaswa kujua ni hiki, bahati hazikuwafuata vitandani kwao wakiwa wamelala. Bali walikutana na bahati katika mapambano yao.

Hivyo ili ufanikiwe unahitaji kupata bahati, lakini bahati hiyo haitakutafuta wewe, itabidi uitafute wewe. Lazima uweke kazi, lazima ujitume sana, na katika kujituma kwako ndiyo utakutana na fursa ambazo wengine hawawezi kuzitumia kwa sababu hawana maandalizi kama uliyonayo wewe.

Hivyo tunajumuisha kwa kusema, bahati ni pale maandalizi yanapokutana na fikra. Kama unataka bahati zaidi, hakikisha unakuwa na maandalizi bora zaidi.

Wednesday, April 17, 2019

KWA KUFANYA MACHAGUO HAYA TUTAWEZA KUDHIBITI MAISHA YETU.


1. Kuwa wewe, usiwe wao.
 
2. Fanya zaidi, tarajia kidogo.
 
3. Kuwa chanya, usiwe hasi.
 
4. Kuwa suluhisho, usiwe tatizo.
 
5. Kuwa mwanzilishi, usiwe mkwamishaji.
 
6. Hoji zaidi, amini kidogo.
 
7. Kuwa mtu fulani, usiwe mtu yeyote.
 
8. Penda zaidi, chukia kidogo.
 
9. Toa zaidi, pokea kidogo.
 
10. Ona zaidi, angalia kidogo.
 
11. Weka akiba zaidi, kuwa na matumizi kidogo.
 
12. Sikiliza zaidi, ongea kidogo.
 
13. Tembea zaidi, kaa kidogo.
 
14. Soma zaidi, angalia kidogo.
 
15. Jenga zaidi, bomoa kidogo.
 
16. Sifia zaidi, kosoa kidogo.
 
17. Safisha zaidi, chafua kidogo.
 
18. Ishi zaidi, usiwe upo upo tu.
 
19. Kuwa majibu, usiwe maswali.
 
20. Kuwa mpenzi, usiwe adui.
 
21. Kuwa mtuliza maumivu, usiwe mtoa maumivu.
 
22. Fikiri zaidi, itikia kidogo.
 
23. Kuwa wa tofauti, usiwe wa kawaida.