Sunday, June 30, 2019

ASILI YA BIASHARA NI KUKUA NA KUFA.

Biashara ni kiumbe hai. Inatungwa, inazaliwa, inakua, inafikia makamo na kisha kufa. Hivi ndivyo mifumo yote ya maisha inavyokwenda. Kuanzia kwetu sisi binadamu, kabla hujazaliwa mimba inatungwa, anazaliwa mtoto, anakua, anafikia makamo na kisha anakufa.
Katika mfumo huu wa ukuaji wa biashara, utungwaji wa mimba ya biashara ni yale mawazo ya kuanza biashara ambayo mtu anakuwa nayo. Kisha kuanza kwa biashara ni sawa na mtoto anayezaliwa, kukua na kisha kufa. Sasa kama ilivyo kwenye asili, siyo mimba zote zinazotungwa zinazaliwa, nyingine zinaharibika kabla ya kufikia kuzaliwa. Na hata watoto wadogo wanaozaliwa, wengi hawafiki utu uzima, wanakufa kabla. Na wachache wanafika utu uzima na kufa.
Kwenye biashara, biashara nyingi huwa zinashindwa kabla hata ya kuanza, nyingi zinaishia kwenye mawazo pekee. Kwa zile ambazo zinaanza, nyingi huwa zinakufa kwenye uchanga, hazikui kufikia ukomavu. Na zile ambazo zinakua, huwa zinafikia ukomavu na kufa.
Lakini zipo biashara chache sana ambazo zimeweza kuondoka kwenye mfumo huo wa ukuaji na kufa. Biashara hizi zimekuwa zinajua kinachopelekea biashara kufa baada ya kukomaa ni bidhaa au huduma kuzoelekea na kutokuwa na kitu kipya.
Ili kuondokana na hali hiyo ya biashara kufika ukingoni na kufa, wafanyabiashara hao ambao biashara zao hazifi, wamekuwa wanakuja na bidhaa mpya au huduma mpya kila mara ambapo bidhaa au huduma ya zamani imefikia kilele chake cha mauzo. Hawasubiri mpaka mauzo yaanze kupungua na biashara kufa. Badala yake wanakuja na bidhaa au huduma mpya inayowafanya waendelee kuwa sokoni.
Huu ndiyo mfumo unaotumiwa na makampuni makubwa ya teknolojia, chukulia mfano wa kampuni ya Apple ambayo inazalisha simu aina ya Iphone. Kila mwaka huwa wanakuja na toleo jipya la simu zao, ambalo halitofautiani sana na toleo lililopita. Yote hii ni kuhakikisha kwamba wanaendelea kuwa sokoni. Kwa sababu kampuni ikishatoa toleo jipya, na watu wote wakawa nalo, hakuna tena fursa ya ukuaji. Lakini wanapokuja na toleo jipya, wale waliokuwa na toleo la zamani wanatamani kuwa na toleo jipya na hapo mauzo yanaanza upya.
Kwa biashara unayofanya, angalia jinsi unavyoweza kutumia njia hiyo ya kuwa na toleo jipya la bidhaa au huduma kila wakati ili biashara yako isife.

FURSA YA KUWEKA AKIBA----------- " Fursa Afrika Mashariki Blog "

KWA NINI WENYE UELEWA WA FEDHA SIYO WAZURI KWENYE BIASHARA.

Watu ambao wana uelewa mkubwa sana wa fedha, yaani wahasibu, wanahisabati, wachumi na hata washauri wa mambo ya fedha, huwa siyo wafanyabiashara wazuri. Yaani huwa wakiingia kwenye biashara hawafanikiwi ukilinganisha na wasiokuwa na uelewa mkubwa wa fedha.
Huku watu wasiokuwa na uelewa mkubwa wa fedha, ambao hawajui hata kuandika cheki vizuri, wakiingia kwenye biashara wanafanikiwa sana.
Katika maeneo mengi ya maisha, kadiri mtu anavyokuwa na uelewa mkubwa, ndivyo anavyochelewa kufanya maamuzi. Wale wenye uelewa mdogo, wanafanya maamuzi haraka, lakini wenye uelewa mkubwa wanahusisha mambo mengi kwenye maamuzi na hilo linawachelewesha kufikia maamuzi.
Inapokuja kwenye fedha, wasiokuwa na uelewa mkubwa kwenye fedha wanatumia hesabu za aina tano tu kwenye mambo ya kifedha, kujumlisha, kutoa, kugawanya, kuzidisha na asilimia. Ni hesabu hizo tu zinazotosha kuendesha biashara yenye mafanikio.
Wakati wale wenye uelewa mkubwa wa fedha wanakuwa na hesabu nyingi zaidi wanazotumia kwenye maamuzi, mfano, makadirio (projections), uwezekano (probaility), hatari (risk) na nyingine nyingi katika kufanya maamuzi, kitu ambacho kinawachelewesha na hata maamuzi wanayofanya yanakosa uhalisia.
Kama wewe una uelewa mkubwa wa kifedha na unataka kufanikiwa kwenye biashara, kubali kuweka sehemu ya uelewa wako pembeni na uendeshe biashara kwa  vitendo na siyo nadharia.
Unaposoma taarifa za kifedha, angalia zile hatua unazoweza kuchuka ili kukuza biashara yako sasa badala ya kuhangaika na vitu vya kufikirika.
Ukishajua MAGAZIJUTO basi una maarifa ya kifedha ya kukutosha kufanikiwa kwenye biashara yako. Muhimu ni kuzijua namba zako muhimu kwenye biashara kama masoko, mauzo, gharama za kuendesha biashara, faida na mtaji ili uweze kuendesha biashara yenye mafanikio makubwa.

Thursday, June 27, 2019

MAHUSIANO NI MUHIMU KULIKO BIDHAA KATIKA BIASHARA

  1. Ipo njia moja ya kupata chochote unachotaka na njia hiyo ni kuomba. Ombeni na mtapewa ni siri muhimu ya mafanikio kwenye biashara. Kama kuna kitu unataka, omba, na wengine watakuwa tayari kukupa. Huwezi kupata kitu bila kuomba.
  2. Unapoomba kazi, badala ya kutuma maombi kama wengine wanavyofanya, tafuta mikutano na wahusika wa eneo unalotaka kufanya kazi. Kwa kutumia mtandao wa kijamii wa LinkedIn, unaweza kukutana na mtu yeyote na ukaongeza nafasi zako za kupata kazi unayotaka.
  3. Biashara ni watu, haijalishi unajua nini, bali unamjua nani na nani anakujua wewe. Hivyo kazana kukuza zaidi mtandao wako wa watu unaowajua na wanaokujua.
  4. Mchukulie kila mtu unayekutana naye kama mtu mashuhuri, jua ni mtu muhimu, muoneshe umuhimu na watu watapenda kukutana na wewe. Ili kufanikiwa kwenye biashara unahitaji kutengeneza marafiki wengi.
  5. Kutana na watu, furahia na jifunze. Weka kipaumbele chako katika kujenga mahusiano imara kwenye biashara yako na kazi yako, fanya kile ambacho unapenda ukiwa umezungukwa na watu unaowapenda. Pia jifunze kupitia wale ambao unafanya nao kazi na wanaokuzunguka.
  6. Kuwa mtu wa shukrani, kila unapokutana na mtu, au mtu anapokufanyia kazi, chukua muda wa kumwandikia ujumbe wa shukrani, inaimarisha zaidi mahusiano yako.
  7. Wale uliosoma nao shule moja au chuo kimoja ni watu muhimu sana kwenye mafanikio yako. Kuwa nao karibu na tengenezeni mahusiano bora, kila mtu anaweza kunufaika kupitia kazi za wengine. Kama hakuna umoja wa wale mliosoma pamoja, una fursa nzuri ya kuuanzisha.
  8. Wafuatilie watu baada ya kukutana nao. Unapokutana na kujuana na mtu mara ya kwanza, endelea kuwafuatilia kwa mawasiliano, hili linaimarisha mahusiano mnayokuwa mmeanzisha.

Tuesday, June 25, 2019

FURSA YA VITEGA UCHUMI VISIVYOHAMISHIKA ------------ " Fursa Afrika Mashariki Blog "

FURSA YA KILIMO CHA MACHUNGWA------" Fursa Afrika Mashariki Blog "

SABABU TANO ( 5 ) ZINAZOUA BIASHARA NYINGI KUKUA

(1). MMILIKI  WA  BIASHARA.
Mmiliki wa biashara ni kikwazo cha kwanza kabisa kwenye ukuaji wa biashara. Pale ambapo biashara inamtegemea mmiliki wa biashara hiyo kwenye kila kitu haiwezi kukua. Kama mwanzilishi wa biashara ndiye anayetegemewa kufanya kila kitu kwenye biashara, biashara haiwezi kukua.
Ili biashara kukua lazima mmiliki aweze kujitofautisha na kujitenganisha na biashara hiyo. Ajenge biashara ambayo inaweza kujiendesha yenyewe bila ya uwepo wake.

(2). KUKOSA  WATEJA  WAPYA.
Biashara inakua kwa kutengeneza wateja wapya kila wakati. Biashara nyingi zimekuwa hazina mfumo mzuri wa kutengeneza wateja wapya kila wakati. Hivyo wanaendelea kuwa na wateja wale wale na hilo linakuwa kikwazo kikubwa kwenye ukuaji.
Ili biashara ikue lazima iwe inatengeneza wateja wapya kila wakati. Wateja wapya ndiyo wanaoleta ukuaji wa biashara.

 ( 3 ). KUKOSA   WAFANYAKAZI  BORA.
Wafanyakazi wa biashara ndiyo wanaoweza kuikuza au kuiangusha. Biashara nyingi hazina wafanyakazi sahihi na hilo limekuwa linazizuia biashara hizo kukua.
Wafanyabiashara wengi hawana mfumo mzuri wa kuajiri watu sahihi kwenye biashara zao na hilo limekuwa linawagharimu kwenye ukuaji. Ili biashara ikue, inahitaji kuwa na wafanyakazi bora ambao wanaweza kutekeleza majukumu yao vizuri.

 ( 4 ). MZUNGUKO  HASI  WA   FEDHA.
Fedha ndiyo damu ya biashara, mzunguko wa fedha ukiwa vizuri biashara inakua, ukiwa vibaya biashara inakufa.
Biashara nyingi zinazokufa zina mzunguko hasi wa fedha, ikiwa na maana kwamba matumizi ya biashara ni makubwa kuliko mapato.
Ili biashara ikue, inahitaji kuwa na mfumo bora wa kudhibiti mzunguko wa fedha ili uwe chanya. Mapato yawe makubwa kuliko matumizi.

 ( 5 ). MAUZO  YASIYOTOSHELEZA.
Mauzo ndiyo injini au moyo wa biashara. Mauzo ndiyo yanayosukuma mzunguko wa fedha kwenye biashara. Bila ya mauzo hakuna biashara.
Biashara nyingi zimekuwa hazina mauzo ya kutosheleza kuzalisha mapato yanayoiwezesha biashara hiyo kujiendesha kwa faida.
Biashara hizo hazina mfumo bora wa masoko ambao unawezesha mauzo kuwa mazuri na yanayoiwezesha biashara kujiendesha yenyewe.
Rafiki, hizi ndizo sababu tano kubwa zinazozuia biashara nyingi kukua, ukizikabili sababu hizi tano, biashara yako itaweza kukua sana.

Saturday, June 22, 2019

ACHA MAIGIZO KATIKA MAISHA YAKO, ISHI UHALISIA WAKO

Watu wanalalamika kwamba hawapati watu sahihi kwenye maisha yao, hawapati wenza sahihi, hawapati watu sahihi wa kushirikiana nao. Na hilo ni rahisi kupata sababu, ambayo ni kila mtu kuwa kwenye maigizo wakati wa kuanza. Na kwa kuwa tunajua maigizo huwa hayadumu muda mrefu, basi muda unapokwenda, rangi halisi za watu zinaonekana na watu kufikiri wenzao wamebadilika. Watu huwa hawabadiliki, ila wanajionesha, wanachoka kuigiza na mambo yanabaki wazi.


Acha kuigiza, acha kuishi maisha ya wengine, ishi maisha yako, ishi uhalisia wako, fanya kile chenye maana kwako, kile ambacho unakiamini kweli, kile ambacho upo tayari kukifanya hata kama hakuna anayekuangalia, hakuna anayekusifia, na kwa njia hii utakuwa na maisha yenye furaha, na pia utawavutia watu sahihi kwa kuwa kile unachoonesha ndicho kilicho ndani yako.

Na kwa kumalizia, waigizaji huwa wanavutia waigizaji, ukianza kuwa halisi, waigizaji wote wanakukimbia, kwa sababu hawataweza kuvumilia ule uhalisi wako.

FURSA YA KILIMO CHA MANANASI------------- " Fursa Afrika Mashariki Blog "

ELIMU YA FEDHA : KUPOTEZA FEDHA KUNAUMIZA KULIKO KUPATA

Kubadili tabia ambayo umeshazoea kuiishi kila siku ni kitu kigumu mno. Watu wamekuwa wanatumia motisha mbalimbali kwao na hata kwa wengine ili waweze kubadili tabia. Moja ya motisha ambayo imekuwa inatumika ni zawadi, kwamba mtu akibadili tabia yake basi anapata zawadi, labda ni ongezeko la mshahara au kupewa bonasi fulani.
Lakini motisha hii ya zawadi imekuwa haina nguvu sana. Kwa wengi ambao wameshazoea tabia za zamani, zawadi haiwasukumi kubadilika. Mfano kama una wafanyakazi ambao wanachelewa kukamilisha majukumu yao, unaweza kuwapa motisha kwamba atakayewahi kukamilisha anapewa ongezeko la fedha, lakini wachache sana watakaokamilisha kwa muda.
Ipo motisha nyingine ambayo ina nguvu sana ya kubadili tabia, kwa sababu ni motisha inayoumiza. Motisha hii ni mtu kupoteza fedha iwapo ataendelea na tabia ya zamani. Hakuna mtu anayepoteza fedha na hivyo tishio la kupoteza fedha linawafanya watu walazimike kubadilika. Kwa mfano huo hapo juu, ukiwaambia wafanyakazi kwamba yule anayechelewa kukamilisha majukumu yake kwa muda, anakatwa fedha kwenye malipo yake, utashangaa jinsi ambavyo wote wanakamilisha kwa muda.
Tafiti za kisaikolojia zinaonesha kwamba watu wanasukumwa zaidi pale panapokuwa na hatari ya kupoteza fedha kuliko panapokuwa na uwezekano wa kupata kiasi kile kile cha fedha. Hii ni nguvu unayoweza kuitumia kwa mabadiliko yako mwenyewe.
Kwa mfano kama kuna tabia ambayo umegundua ni sugu kwako, na ambayo unajitahidi kuibadili huwezi, basi waambie watu wako wa karibu wakufuatilie kwa karibu na kila utakapofanya tabia hiyo basi wakudai kiasi fulani cha fedha.
Mfano kama una tabia ya kuwakatisha watu wakiwa wanaongea, waambie watu wote wa karibu kwamba kila unapomkatisha mtu akiwa anaongea basi akudai shilingi elfu 10. Ukishalipa watu wawili au watatu, nakuhakikishia hutarudia tena, kupoteza fedha kutakuumiza na kukushikisha adabu.
Kadhalika kwenye tabia nyingine kama ulevi au uvutaji wa sigara, kutokufanya mazoezi, kula hovyo, kutumia maneno ya matusi na kadhalika. Tabia yoyote inayokupa shida kubadili, ingiza fedha na utabadilika haraka sana.

ELIMU YA FEDHA : MUDA WAKO NI PESA YAKO

Ndugu  yangu mpendwa, nimekuwa napenda kukuambia sana kauli hii, HAKUNA KITU CHA BURE. Ukiona mtu anakupa kitu bure, jua kuna namna unalipia ambayo wewe hujui au kuna mtu ameshalipa kwa ajili yako. Huu ni msingi ambao ukiweza kuuishi na kuusimamia kwenye maisha yako, utajiepusha na matatizo mengi mno. Mfano huwezi kutapeliwa kama utaishi kwa msingi kwamba hakuna kitu cha bure. 

Sasa tuje kwenye mitandao ya kijamii, orodhesha mitandao yote ya kijamii ambayo unaitumia. Je ni Instagram? Facebook? Whattsapp? Twitter? Snapchat? Na mingine zaidi. Swali ni je umekuwa unalipa kiasi gani ili kutumia mitandao hii ya kijamii?
Ukiacha bando (data) unazonunua ili kuweza kuingia mtandaoni, hulipi hata senti moja kutumia mitandao hii. Lakini unaweza kuitumia muda wowote, masaa 24 kwa siku, siku 7 za wiki.
Swali jingine unalopaswa kujiuliza ni je mitandao hii inapataje fedha za kujiendesha. Maana mitandao hii ina wafanyakazi wengi, na ambao ni wasomi kweli kweli, ina rasilimali nyingi na wamiliki wake ni matajiri wakubwa sana duniani. Ukichukua mfano wa mmiliki wa Facebook na Instagram, ambaye ni bilionea mkubwa duniani, ambaye yupo kwenye watu 10 matajiri zaidi duniani. Hizo fedha wanazitoa wapi?

Kama hujawahi kujiuliza swali hili basi leo unakwenda kupata mwanga, na utakufanya uangalie kwa mtazamo tofauti kabisa mitandao hii ya kijamii.
Mitandao ya kijamii inaingiza kipato kupitia MATANGAZO. Mfumo wao wa biashara uko hivi, kusanya watu wengi watumie huduma yako ya mtandao wa kijamii, kisha nenda kwa mtu mwenye biashara na mwambie unaweza kutangaza biashara yako kwenye mtandao wangu ambao una watumiaji wengi, na wanaotumia huduma hiyo kwa muda wao mwingi wa siku.
Sasa kama unavyojua tabia yetu binadamu, huwa tunafanya zaidi kile tunacholipwa ili kufanya. Kwa kuwa makampuni haya yanapata fedha kwa watu kutangaza kupitia mitandao yao, na kwa sababu wingi wa fedha unaamuliwa na wingi wa watembeleaji na muda ambao watembeleaji wanatumia kwenye mitandao hiyo, basi mitandao hii imekuwa inahakikisha inatumiwa na wengi, na ukishaitumia huachi, kila muda unataka kuitembelea. Kama nilivyokuambia kwenye kipengele namba moja, hujavutiwa kutembelea mitandao hii, umesukumwa kuitembelea kila wakati, kwa sababu unavyoitembelea zaidi, ndivyo wenye mtandao wanatengeneza kipato zaidi.
Hivyo basi, MUDA WAKO = PESA ZAO. Muda unaotumia kwenye mitandao ya kijamii ndiyo fedha ambazo zinawafanya wamiliki wa mitandao hiyo kuwa mabilionea wakubwa.
Swali jingine muhimu sana ni je, kwa matumizi yako makubwa ya mitandao ya kijamii, ni manufaa gani unayapata? Najua wengi mnajiambia naungana na marafiki na kujua yanayoendelea. Kama jibu hilo ni kweli, swali jingine litakuwa je unahitaji zaidi ya masaa mawili kwa siku kutembelea mitandao hii? Je kweli unahitaji kila baada ya nusu saa au saa moja kutembelea tena mitandao hii?
Rafiki, nafikiri unapata picha ni jinsi gani tumechagua kuharibu na kupoteza maisha yetu, kuwafaidisha wengine, huku sisi wenyewe tukibaki hatuna kitu.
Nikuache na mbinu moja ya kupima matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii kwako. Chukulia hili, kama kila dakika unayotumia kwenye mitandao ya kijamii ulikuwa unailipia shilingi elfu moja, je ungekuwa tayari kulipa shilingi ngapi kwa siku kutembelea mitandao hii?
Je ungekuwa tayari kulipa tsh 120,000/= kila siku ili tu utumie mitandao ya kijamii? (kwa wastani mtumiaji wa mitandao ya kijamii anatumia masaa mawili kila siku). Kama jibu ni hapana basi jua muda unaoweka kwenye mitandao hiyo unaupoteza. Kama kweli unatumia mitandao ya kijamii kuungana na marafiki na kujua yanayoendelea, utahitaji dakika 10 tu kwa siku kwa ajili ya hilo. Muda mwingine utakuwa na manufaa kwako kama utatumia kwenye mambo yenye tija.
Kila unapoingia kwenye mitandao ya kijamii jikumbushe hili, MUDA WAKO = PESA KWAO na jiulize kama kweli unataka kuendelea kuwa bidhaa inayouzwa.
Na mwisho kabisa, pima umuhimu wa mitandao hii kwa kujiuliza kama ungekuwa tayari kulipia ili kuitumia, maana bure inakudanganya na kukupotezea muda wako.

ELIMU YA FEDHA : CHANGAMOTO YA FEDHA

Fedha imekuwa changamoto kubwa sana kwenye zama tunazoishi sasa. Tunapoteza muda na maisha yetu kwenye kufanya kazi ngumu, lakini fedha tunazozipata tunazipoteza kwa kununua vitu ambavyo siyo mahitaji ya msingi.
Makampuni makubwa yanatumia mbinu za kisaikolojia kututangazia bidhaa na huduma zao kwa namna ambayo tunajisikia vibaya kama hatuna wanachouza.
Pia taasisi za fedha zimerahisisha sana matumizi yetu, hata kama mtu huna fedha za kununua kitu, basi ni rahisi kukopa fedha ili kununua unachotaka. Na hapo sasa mtu analipa mkopo pamoja na riba kubwa.
Yote haya ni matatizo ya kujitakia, kwa kushindwa kudhibiti tamaa zetu na kujilinganisha na wengine.
Ili kuondokana na changamoto hii ya fedha, fanya yafuatayo;
  1. Jua mahitaji yako ya msingi ambayo utayagharamia na yale ya anasa ambayo utaachana nayo. Mahitaji ya msingi ni manne, maji, chakula, moto na malazi. Mengine yoyote nje ya hapo ni anasa, yanaweza kusubiri.
  2. Kuwa na bajeti ya matumizi yako ya fedha, usitumie tu fedha kwa sababu unazo, bali weka bajeti na ifuate hiyo.
  3. Usikope fedha kwa ajili ya matumizi, ni kuchagua kupoteza fedha.
  4. Kwenye kila kipato unachoingiza, sehemu ya kumi hupaswi kuitumia kabisa, hivyo ni fedha unayojilipa kwa ajili ya uwekezaji wako wa baadaye.
  5. Usishindane na watu wengine wala kujilinganisha na yeyote kwenye mali, mavazi na hata maisha.
  6. Fanya tahajudi rahisi kabla hujanunua kitu. Kabla hujalipia jiulize je unachotaka kulipia ni hitaji la msingi au anasa. Hii itakuepusha kufanya manunuzi yasiyo muhimu.
  7. Fanya mfungo wa matumizi. Kwa mwezi mmoja, usinunue kabisa kitu ambacho siyo cha msingi. Jizuie kabisa kununua chochote ambacho siyo lazima kwa kipindi cha mwezi mzima, kisha ona jinsi maisha yako yatakuwa bora zaidi.
  8. Wekeza akiba yako kwenye maeneo ambayo yanazalisha zaidi baadaye.
  9. Usinunue vitu ambavyo thamani yake inashuka kadiri muda unavyokwenda.
  10. Ongeza kipato chako kwa kuwa bora zaidi kwenye kile unachofanya, toa huduma bora zaidi, wahudumie wengi zaidi na utaweza kuongeza kipato zaidi.

ELIMU YA FEDHA : MAISHA ULIYOPOTEZA

Watu wengi wamekuwa wanakutana na hali hii, akiwa hana fedha anakuwa na mawazo na mipango mizuri sana ya kutekeleza anapopata fedha. Anakuwa mpole na mwenye akili nzuri juu ya matumizi ya fedha. Akiona wengine wanatumia fedha vibaya anajiambia kama mimi ningepata fedha hizo, basi ningefanya mambo mazuri sana.
Lakini mtu huyo huyo anapopata fedha, anajikuta anafanya vitu ambavyo hata hakupanga kufanya. Mtu akishapata fedha zile akili nzuri na mipango aliyokuwa nayo anasahau kabisa. Anajikuta ananunua vitu ambavyo hakupanga kununua, mahitaji muhimu ambayo hayakuwepo awali yanaanza kujitokeza. Ni mpaka fedha hiyo inapoisha ndiyo mtu anarudi kwenye akili zake na kujiuliza zile fedha zimeishaje bila kufanya mambo mazuri.
Kama umewahi kukutana na hali kama hii usijione kama una bahati mbaya, au ni mjinga sana inapokuja kwenye fedha. Jua hiyo ni hali inayowakumba watu wengi kwenye fedha, na inatokana na wengi kutokuielewa vizuri saikolojia ya fedha. Fedha ni nguvu, na nguvu yoyote isipodhibitiwa na kutumiwa vizuri inaleta uharibifu.
Leo nakwenda kukushirikisha dhana itakayokuwezesha kuwa na udhibiti mzuri kwenye fedha zako, dhana itakayokuzuia usitumie hovyo fedha pale unapokuwa nazo.
Dhana hii ni kuhesabu fedha kwa kulinganisha na maisha ambayo umepoteza kupata fedha hizi. Wote tunajua kwamba muda ni fedha, na pia tunajua kwamba muda ni maisha, hivyo basi maisha pia ni fedha.
Sasa chukua kipato chako unachopata kwa mwezi, kisha gawa kwa masaa unayofanya kazi. Mfano kama kipato chako ni milioni moja, halafu unafanya kazi masaa 8 kwa siku, siku 5 au 6 za wiki, kwa mwezi unafanya kazi kwa masaa 160 mpaka 200. Ukigawa milioni moja kwa masaa 200 utapata shilingi elfu 5. Hii ina maana kila saa unayofanya kazi unalipwa shilingi elfu 5.
Sasa kwa sababu muda ni fedha na maisha ni muda hivyo maisha ni fedha, kila elfu 5 unayoipata, unapoteza saa moja ya maisha yako. ukipata elfu 10 umepoteza masaa mawili.
Sasa kila unapotaka kununua kitu, kabla hujafanya maamuzi ya kukinunua jiulize kwanza swali hili, je kitu hiki ninachokwenda kununua, kina thamani sawasawa na maisha niliyopoteza?
Kwa mfano umekutana na nguo ambayo inauzwa shilingi elfu 20, umeipenda kweli na unataka kuinunua. Jiulize kwanza je nguo hii ina thamani sawa na masaa manne ya maisha yangu? Je kama nikiambiwa nichague kupata nguo hii na kupata masaa manne zaidi kwenye maisha yangu nitachagua nini?
Kwa kuchukulia fedha zako kama maisha ambayo unapoteza, utajijengea nidhamu kubwa sana ya fedha na kuacha matumizi ya hovyo, yasiyo na manufaa kwako. Pia utapata muda zaidi wa kufanya yale muhimu kwako, pamoja na kuwekeza fedha zako maeneo ambayo yanazalisha na hivyo kukusaidia usifanye kazi muda mrefu kupata fedha za kupoteza.
Linganisha kila fedha unayotaka kutumia na maisha unayopoteza, na utaona jinsi gani vitu vingi unavyopenda kununua havina thamani unayovipa.

KWANINI UTAKE KUUZA BIASHARA YAKO ?

"John  Warrillow "  katika  Kitabu   Chake  " BUILT  TO  SELL " anatuambia zipo sababu mbalimbali za wewe kutaka kuuza biashara unayokuwa umeianzisha.
  1. Biashara yako inaweza kuwa ndiyo chanzo chako cha mafao unapostaafu, hivyo kuweza kuiuza kunakupa kiasi kikubwa cha fedha cha kustaafu bila ya shida.
  2. Unaweza kuwa unataka kuanzisha biashara nyingine. Wajasiriamali huwa wanachoka kitu haraka, hivyo ukianzisha biashara na kuona tayari umeichoka na kuna biashara nyingine unapenda kuingia, unaweza kuuza ile uliyonayo sasa.
  3. Unaweza kuwa na uhitaji mkubwa wa fedha kutatua matatizo mbalimbali yanayokukumba. Biashara yako inaweza kuwa kama akiba au uwekezaji wako, ambao unaweza kuuza pale unapokuwa na uhitaji mkubwa wa fedha kutatua changamoto mbalimbali za maisha yako.
  4. Unaweza kuwa unahitaji kupata muda zaidi kwa ajili yako na familia yako. Pale unapoona biashara yako inachukua muda kuliko unavyoweza kuipa, unaweza kuchagua kuiuza.
  5. Unaweza kuwa unahitaji kulala vizuri usiku bila ya wasiwasi, kwa sababu unapokuwa mjasiriamali, unakuwa na usiku mwingi ambao hulali, unafikiria biashara itakuaje, ushindani utaushindaje, mishahara utalipaje, mikopo unarejeshaje na mengine mengi ambayo yatakunyima usingizi. Lakini unapojua kwamba unaweza kuiuza biashara hiyo muda wowote, unakuwa na utulivu mkubwa wa akili.

KWANINI BIASHARA NYINGI HAZIFAI KUUZA ?

Biashara nyingi hazifai kuuza kwa sababu zinaendeshwa kwa vurugu. Kwa nje biashara inaweza kuonekana inakwenda vizuri, lakini kwa ndani mambo ni vurugu. Hakuna mpangilio wowote wala mfumo ambao unafuatwa. Kila kitu kinafanywa kwa namna ambavyo mtu anajisikia kufanya. Hakuna viwango vyovyote vinavyofanyiwa kazi.
Wateja wanaokuja kupata huduma kwenye biashara, hawaji kwa sababu ya biashara, bali wanakuja kwa sababu ya mtu. Na wengine wanasema wazi kwamba wanataka kuhudumiwa na fulani tu.
Wafanyabiashara wengi hufurahia pale wateja wanapotaka wahudumiwe na wao tu, wakiona ni wateja wanawaamini na kuwakubali sana. Lakini wasijue kama hicho ndiyo kifungo chao.
Huwezi kuuza biashara ambayo haiendeshwi kwa mfumo na kila kitu kinamtegemea mmiliki wa biashara hiyo.
Na biashara ya aina hii inakuwa mzigo kwa mmiliki na kumnyima uhuru.
Karibu tujifunze jinsi ya kutengeneza biashara inayokupa uhuru na unayoweza kuiuza muda wowote na hili litakuwezesha kuwa na biashara bora na isiyokutegemea kwa kila kitu. Na hata kama hutaki kuuza biashara yako, kitendo cha biashara kuweza kujiendesha yenyewe bila ya wewe kuwepo, utakuwa ushindi mkubwa sana kwako.

HATUA NANE (8 ) ZA KUTENGENEZA BIASHARA INAYOJIENDESHA YENYEWE NA UNAYOWEZA KUIUZA MUDA WOWOTE

Kutoka kwenye kitabu "BUILT TO SELL", mwandishi " John Warrillow " anatushirikisha hatua nane za kufuata katika kutengeneza biashara ambayo inaweza kujiendesha yenyewe bila ya kuwepo kwa mwanzilishi wa biashara hiyo na pia inaweza kuuzwa muda wowote.
(1). Chagua bidhaa au huduma yenye uwezo wa kukua.
Hatua ya kwanza kabisa kwenye kutengeneza biashara inayojiendesha yenyewe na unayoweza kuiuza ni kuchagua bidhaa au huduma ambayo ina uwezo wa kukua.
Bidhaa au huduma yenye uwezo wa kukua ina vigezo vitatu;
Moja, inafundishika. Ni rahisi kumfundisha mtu mwingine jinsi ya kufanya kitu hicho na akaelewa.
Mbili; ina thamani kwa mteja. Hivyo mteja anakuwa tayari kulipa bei ambayo umeiweka. Kama kitu kinapatikana kwa wengine, mteja ataenda kwenye bei rahisi. Lakini kama kinapatikana kwako tu na mteja anakihitaji kweli, atakuwa tayari kulipa bei uliyopanga.
Tatu; manunuzi ni ya kujirudia. Mteja anahitaji kuwa anarudia tena na tena kununua. Isiwe ni kitu ambacho mteja ananunua mara moja kwenye maisha yake.
Baada ya kuchagua bidhaa au huduma ambayo inafundishika, ina thamani na manunuzi yake ni ya kujirudia, unahitaji kukaa chini na kuandika mchakato mzima wa jinsi unavyofanya biashara yako. Kila kitu kinachohusika kwenye biashara kinapaswa kuandikwa kwa namna ambayo mtu mwingine anaweza kufundishwa na akaelewa na kufuata. Huu unakuwa ndiyo mwongozo mkuu wa ufanyaji wa biashara yako.
Baada ya kuwa na mwongozo, unapaswa kuipa jina bidhaa au huduma yako. Unaipa jina kuitofautisha na bidhaa au huduma nyingine, hivyo inakuwa ya kipekee kwa wateja wako. Kadiri bidhaa au huduma inavyokuwa ya tofauti na zinazopatikana sokoni, ndivyo inakuwa na thamani kubwa kwa wateja wako.
Baada ya kuwa na jina linaloitofautisha bidhaa au huduma yako, andika maelezo mafupi kuhusu bidhaa au huduma hiyo ambayo yanajumuisha faida zake na jinsi inavyotatua changamoto za wateja wako, na tumia maelezo hayo kwenye masoko.
Katika hatua hii ya kwanza unachagua bidhaa au huduma moja au chache ambao unaweza kuweka nguvu zako zote na ukawafikia wateja wengi na biashara kukua pia. Ukifanya hatua hii kwa bidhaa au huduma nyingi utashindwa.
(2). Tengeneza mzunguko chanya wa fedha kwenye biashara.
Mzunguko wa fedha ndiyo uhai wa biashara yako. Yeyote anayetaka kununua biashara yako, akishaangalia kama inajiendesha yenyewe, anakwenda kuangalia mzunguko wa fedha wa biashara hiyo.
Mzunguko wa fedha kwenye biashara unaweza kuwa chanya au hasi. Mzunguko unakuwa chanya pale mapato ni makubwa kuliko matumizi na hasi pale matumizi ni makubwa kuliko mapato.
Ili kutengeneza mzunguko chanya wa fedha kwenye biashara yako, bidhaa au huduma unayouza inapaswa kuwafanya wateja walipe kwanza kabla ya kuipata. Epuka kuendesha biashara ambayo mteja anapata bidhaa au huduma kwanza halafu analipa baadaye. Hii inaifanya biashara ikae muda mrefu bila ya fedha na hivyo kuwa na mzunguko hasi wa fedha.
Biashara inapokuwa na mzunguko chanya, yule anayetaka kuinunua atakulipa zaidi kwa sababu tayari biashara inazalisha, tofauti na biashara yenye mzunguko hasi ambayo inahitaji kupokea fedha nyingi ili kujiendesha.
(3 ). Ajiri timu ya mauzo.
Baada ya kutengeneza bidhaa au huduma ambayo utaiuza kwa wateja kulipa kabla ya kuipata, unahitaji kujiondoa kwenye kuiuza bidhaa au huduma hiyo. Na hapa ndipo unapohitaji timu ya mauzo, watu ambao wanaenda kuuza bidhaa au huduma kwa niaba yako.
Hii ni hatua muhimu sana ambayo wengi hukwama, unapouza bidhaa au huduma yako mwenyewe, unawafanya wateja wakutegemee wewe. Lakini unapokuwa na mfumo wa mauzo, ambao unaendeshwa na watu wa mauzo, wateja hawakutegemei wewe bali wanategemea mfumo wa biashara.
Kazi yako kama mjasiriamali ni kuuza kampuni yako, siyo kuuza bidhaa au huduma za kampuni hiyo. Ajiri na tengeneza timu bora ya mauzo na ipe mwongozo wa kuuza bidhaa au huduma yako na wewe utapata muda mwingi wa kuikuza zaidi kampuni yako.
Unapoajiri watu wa mauzo, ajiri ambao wana uzoefu wa kuuza bidhaa na epuka sana watu ambao wana uzoefu wa kuuza huduma. Hii ni kwa sababu wauzaji wa bidhaa huwa wanamuuzia mteja kile kilichopo, wakati wauzaji wa huduma wanabadilika kulingana na mahitaji ya mteja. Kwa sasa biashara yako inauza bidhaa, hata kama ni huduma, unapaswa kuiuza kama bidhaa, hivyo watu waliozoea kuuza bidhaa watakusaidia kuuza vizuri bila ya kutaka kubadili chochote.
Pia unapoajiri watu wa mauzo, ajiri angalau wawili. Hii inaleta hali fulani ya ushindani baina yao na inawasukuma kujituma zaidi. Mfano kama mmoja ameuza kwa wateja 10 kwa wiki, na mwingine akauza kwa wateja 7, yule wa wateja saba atakazana naye afike wateja 10. Kadhalika wa wateja kumi atakazana zaidi ili asipitwe. Watu wa mauzo huwa wanapenda kujipima kwa namba, unapokuwa na wawili na kuendelea, wanakuwa na ushindani ambao unawasukuma zaidi.
(4 ). Acha kuuza vitu vingine vyote.
Tumeona chanzo cha biashara nyingi kutokuuzika ni zinaendeshwa kwa vurugu, kila kitu kinauzwa na mteja akisema anataka kitu cha tofauti anapatiwa. Sasa hutaweza kuikuza wala kuiuza biashara kama inaendeshwa kwa vurugu kiasi hicho.
Hivyo baada ya kuchagua bidhaa au huduma moja kuu unayouza kwenye biashara yako, acha kuuza vitu vingine vyote. Inawezekana kuna vitu vingine ulikuwa unauza ambavyo vinakuingizia faida. Lakini kama vipo nje ya ile bidhaa au huduma uliyoiainisha kama msingi mkuu wa biashara yako, basi unapaswa kuacha kuuza vitu hivyo vingine.
Unahitaji kuweka nguvu zako zote kwenye kuikuza biashara yako kupitia bidhaa au huduma yenye fursa ya ukuaji zaidi. Unapojihusisha na kuuza vitu vingine, unawapa wateja wako wakati mgumu kukuelewa na kukutegemea.
Wateja wana tabia ya kujaribu wafanyabiashara, watakujaribu kwenye kutaka bei ya chini zaidi, watakujaribu kwenye kutaka kitu cha tofauti na unachotoa na watakujaribu kwa kutaka uboreshe zaidi kile unachotoa kiendane na wao. Epuka sana mitego na majaribu haya ya wateja, simamia kile ulichopanga na wateja wanapojifunza kwamba unasimamia nini, wanakuheshimu kwa hilo na kuwa tayari kununua kile unachouza.
Muhimu ni uzingatie hatua ya kwanza ya kuwa na bidhaa au huduma yenye thamani kwa wateja na ambayo hawawezi kuipata sehemu nyingine yoyote.
(5). Kuwa na mpango bora wa motisha kwa mameneja wako.
Kadiri biashara yako inavyokwenda, inazidi kukua. Timu ya mauzo inaleta wateja na biashara inakuwa kwenye mzunguko chanya wa fedha. Kwa kuwa wewe huhusiki moja kwa moja kwenye mauzo na wala kuandaa bidhaa au huduma, unahitaji kutengeneza viongozi kwenye biashara yako.
Hata mtu anayetaka kununua biashara yako, anaanza kuangalia uongozi uliopo kwenye biashara hiyo. Hivyo utahitaji kuwapandisha cheo wafanyakazi wako na kuwafanya kuwa mameneja, kisha kuajiri wafanyakazi wengine watakaofanya kazi chini ya usimamizi wao.
Ili mameneja hawa wajitume kweli unahitaji kuwa na mpango bora wa motisha kwao.
Zipo njia mbalimbali za kutoa motisha kwa mameneja wako, ipo njia ya kuwalipa bonasi mwisho wa mwaka kutokana na ongezeko la faida, hii inawasukuma kujituma zaidi ili kutengeneza faida kubwa.
Lakini pia baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wanawapa mameneja wao sehemu ya umiliki wa biashara hiyo, kwa kuwapa hisa. Kama lengo lako ni kuuza biashara yako, usitumie njia hii, kwa sababu ukishawapa umiliki, mchakato wa kuiuza biashara hiyo unakuwa mgumu zaidi.
Tumia mfumo wa kulipa bonasi kutokana na ongezeko la faida. Na pale biashara inapouzwa, basi wape zawadi ya bonasi kutokana na mauzo hayo.
(6).Tafuta dalali sahihi kwako.
Baada ya biashara yako kuwa inajiendesha yenyewe, kwa kuwa na timu bora ya uongozi na mzunguko chanya wa fedha, sasa unaanza kuangalia uwezekano wa kuiuza.
Hapa ndipo unapohitaji kutafuta dalali au wakala ambaye atakuunganisha na wanunuaji wa biashara. Zipo kampuni ambazo hizi ndiyo kazi zake, kuwakutanisha wafanyabiashara na wawekezaji au wanunuaji wa biashara.
Unahitaji kuchagua kampuni ambayo utafanya nayo kazi, ambayo itakuwa upande wako. Hivyo ongea na watu mbalimbali mpaka upate ambaye unaona anaweza kukuwakilisha vizuri kwa wanunuzi wa biashara hiyo.
Kampuni hizi za udalali huwa zinalipwa kwa asilimia ya mauzo bada ya mauzo kufanyika, lakini zinakusaidia sana kukutana na wanunuzi na kuweza kuuza biashara yako.
(7). Iambie timu yako ya uongozi kuhusu mpango wa kuuza biashara.
Timu ya uongozi wa biashara yako ni watu ambao wana imani kubwa sana na wewe. Ni watu ambao wanajitoa sana ili biashara yako ikue zaidi. Hivyo unahitaji kuwa makini sana pale unapotaka kuuza biashara yako.
Kwanza unahitaji kufanya mchakato huo kwa siri mwanzoni wakati unatafuta mteja. Ukishapata mteja sasa, unahitaji kuiambia timu yako kuhusu mpango wako wa kuuza.
Inaweza kuwa wakati mgumu sana kwako kuiambia timu ambayo inakuamini kwamba unapanga kuuza biashara hiyo, wapo ambao watakuchukulia wewe ni msaliti na huwajali wao bali unajali fedha tu.
Hivyo unapopanga kuwaambia, waoneshe kwamba biashara inapouzwa, hata wao pia wananufaika. Mfano biashara ikinunuliwa na kampuni ambayo ni kubwa zaidi, wao wanapata nafasi ya kukua zaidi. Wanakuwa kwenye mazingira bora zaidi ya kufanya kazi na pia wanaweza kupata nafasi za juu zaidi.
Pia waahidi kupata bonasi pale ambapo biashara itauzwa. Kwa njia hii watakubaliana na wewe na watakuwa tayari kusaidia ili mchakato wa mauzo ukamilike vizuri.
Ni muhimu uiambie timu yako kwa sababu anayenunua atahitaji kukutana na timu yako ya uongozi na pia kuna ukaguzi wa kina utakaofanyika kwenye biashara yako, ambao utahusisha kila aliyepo kwenye timu ya uongozi.
Hatua ya nane; geuza ofa kuwa makubaliano ya kisheria.
Wale wanaoonesha nia ya kununua biashara yako huwa wanatoa ofa ya kiasi wanachopanga kulipa ili kununua biashara hiyo. Lakini ofa siyo makubaliano, wakati wowote wanaweza kubadilika.
Na katika makubaliano ya kibiashara, watu huwa wanakuwa na mbinu mbalimbali za kupata kitu kwa bei ya chini. Mfano kwenye kuuza biashara, mtu atatoa ofa yake, kisha atafanya uchunguzi kwenye biashara na baadaye atakuja na matokeo ya uchunguzi na kukuambia kuna mambo ambayo ameyaona na hataweza kulipa ofa ya kwanza na hivyo kupunguza.
Ili kuepuka kujikuta kwenye hali hiyo, kwanza chagua ni kiasi gani upo tayari kupokea kwa kuuza biashara yako. Hivyo wanapokuja na ofa ya juu ya kiasi hicho kubali. Lakini pia wape muda wa ukomo, la sivyo zoezi litachukua muda mrefu zaidi.
Wanapofanya uchunguzi na kuja na majibu yao, ambapo watapunguza ofa yao, angalia kama bado inaendana na mpango wako wa awali. Kama ndiyo basi kubaliana nao na kamilisheni dili. Kama ofa yao iko chini ya mpango wako wa awali kataa na tafuta mnunuzi mwingine.
Zoezi la kutengeneza biashara ambayo inaweza kujiendesha yenyewe linategemea zaidi mfumo unaoweka kwenye biashara hiyo, unapokuwa na mfumo bora ndivyo kazi inakuwa rahisi kwako.
Zoezi la kuuza biashara yako huwa ni gumu na linalokuweka kwenye wakati mgumu mno. Hivyo kama unachagua kuuza biashara, lazima ujue una kipindi kigumu mbele yako, kuanzia kupata mnunuzi mpaka kufikia makubaliano.
Iwe unapanga kuuza biashara yako au la, bado utanufaika sana kama biashara yako inaweza kujiendesha yenyewe bila ya kukutegemea wewe moja kwa moja. Hivyo fuata hatua hizi nane na utaweza kutengeneza bishara bora sana kwako.

USIOGOPE KUCHEKWA , JIFUNZE KUPUUZA


Kwenye maisha, wapo watu wengi sana ambao watakucheka. Labda ni kwa kile ulichosema au unachofanya. Wengi wanapochekwa, hukata tamaa na kuona hawawezi na hawafai pia. Hivyo huacha kabisa kile ambacho wanafanya na kurudi kwenye maisha ya kawaida, kitu ambacho kinaua ndoto zao.
 
KWANINI  WATU  WANAKUCHEKA ?
 
Sababu ya kwanza ni kama unachekesha, kama umeongea au kufanya kitu ambacho kinachekesha, basi watu watacheka. Kama unafanya vituko, watu hawawezi kujizuia, watacheka.
 
Sababu ya pili ni kama hawakuelewi, kama watu hawaelewi kile ambacho umeongea au unafanya, watakucheka. Na hapa ndipo kundi kubwa la watu wanaocheka lipo. Kwa sababu kila ambaye alikuja na wazo la kufanya mambo makubwa, alichekwa. Mwanzilishi wa simu alichekwa, waliotengeneza ndege kwa mara ya kwanza walichekwa, wanasayansi wakubwa kama kina Newton na Einstein walichekwa kwa nadharia zao na hata Viongozi wakubwa wa kifalsafa na kiimani kama Yesu, Mohamad na wengine walichekwa sana wakati wanaanza na maono yao.
 
Hivyo basi, watu wanapokucheka, chagua ni kwa sababu ipi kati ya hizo mbili, kama ni kwa sababu unachekesha basi endelea, maana kuwapa watu kitu cha kucheka ni jambo jema pia. Na kama ni kwa sababu hawakuelewi, endelea kufanya, itafika hatua na watakuelewa, kama wote waliochekwa huko nyuma walivyokuja kueleweka baadaye. Kwa vyovyote vile, usiache kufanya unachofanya, na wala usiogope kusema unachotaka kusema kwa sababu watu wanakucheka. Watu kukucheka hakuna uhusiano wowote na wewe kuacha, ni wao wenyewe.

Thursday, June 20, 2019

ISHI MAISHA YAKO, USIWE MTU WA CHUKI, SAMBAZA UPENDO

Kuna  watu wenye chuki, ambao kwa sababu tusizozijua, wanaamua kutuchukia, kwa jinsi tulivyo au kwa kile tunachofanya.
 
Wengi wamekuwa wanashangaa inakuwaje watu wawachukie, na hili ni kupoteza muda. Watu wenye chuki huwa wanachukia, na huna lolote unaloweza kufanya kuwafanya wasikuchukie.
 
Watu wenye chuki hawabadiliki na kuacha kuwa na chuki kwa sababu wewe umefanya kitu fulani, bali wataendelea kupata sababu za kuwa na chuki zaidi.
 
Hivyo badala ya kuishi maisha ya kutaka kuwaridhisha wengine, hasa wale wenye chuki, ishi maisha yako, fanya kile ambacho ni muhimu kwako na simamia kile unachoamini.
 
Wenye chuki watachukia iwe unaishi maisha yako au unafanya wanachotaka wao.
 
Usiyumbishwe na wenye chuki, chagua kuyaishi maisha yako.
 
Na kwa upande wa pili, usiwe mtu wa chuki, sambaza upendo.

FURSA YA MUZIKI---STADI ZA KAZI--DARASA LA SITA ( STD 6 )---SHULE ZA MSINGI---TANZANIA-------- " Fursa Afrika Mashariki Blog "

Friday, June 14, 2019

KILA HATUA UNAYOPIGA HUZALISHA KIKWAZO

Kwenye fizikia, kuna kanuni tatu kuu za mwendo ambazo mwanasayansi Isaac Newton alizigundua.
 
Kanuni ya kwanza inasema kitu kilichopo kwenye mwendo kinaendelea kuwa kwenye mwendo mpaka nguvu ya nje itakapotumika kukizuia.
 
Kanuni ya pili inasema nguvu ya kitu kilichopo kwenye mwendo inategemea uzito wake na mwendokasi wake.
 
Na kanuni ya tatu inasema kila mwendo huwa unazalisha upinzani.
 
Ni kanuni ya tatu ambayo tunakwenda kuijadili hapa kwenye dakika moja ili uelewe kwa nini baadhi ya vitu vinatokea kwenye maisha yako na hatua sahihi kwako kuchukua.
 
Kila mwendo unaoanzisha, kuna mwendo mwingine utakaoanzishwa kuzuia mwendo huo.
 
Unapojaribu kwenda mbele, kuna mtu atajitokeza kukurudisha nyuma.
 
Hii ndiyo inasababisha mafanikio kuwa magumu. Kwa sababu siku unayoamua kwamba unataka kufanikiwa, zitaibuka kila aina ya nguvu kukupinga, kutaibuka kila kikwazo kwenye njia yako ya mafanikio.
 
Unapojua hili, unajipanga kwa upinzani kwa kila hatua unayopanga kupiga na hujidanganyi kwamba mambo yataenda vizuri yenyewe kama wengi wanavyofanya.
 
Usishangae pale ambapo marafiki ulionao sasa watageuka kuwa maadui zako pale unapotangaza kwamba unataka kufanikiwa sana. ulipokuwa kawaida mlikuwa marafiki, unapopanga kupiga hatua zaidi wanakuwa maadui, hiyo ni kanuni ya asili, huwezi kupingana nayo.
 
Usikubali kipingamizi chochote kikuzuie wewe kupiga hatua zaidi kwenye maisha yako, jua kwa kila hatua utakayopanga kuchukua kuna kipingamizi kitaibuka na hivyo jiandae kukivuka.

KILA MTU ATAKUFA , NI BORA UULIWE NA KAZI !


Kila mtu atakufa, hilo halina ubishi. Hii ni hukumu uliyoipata siku unayozaliwa, ambacho hujui ni siku gani hukumu hiyo itakamilika.
 
Lakini kuna kitu kingine muhimu sana kuhusu kifo ambacho wengi tumekuwa hatukitafakari, ambacho tukikielewa kitatusaidia sana.
 
Kila mtu kuna kitu kitakachomuua. Ndiyo, kuna kitu ambacho kitakuua, yaani kitachangia kwenye kifo chako.
 
Kuna ambao ulevi utawaua, kwa kuendekeza sana ulevi mwili unachoka na kupata magonjwa ambayo yanachangia kifo chao.
 
Kuna ambao chakula kitawaua, kwa kushindwa kula kwa nidhamu wanakuwa na afya mbovu ambayo inaleta magonjwa yanayowaua.
 
Kuna ambao wasiwasi na hofu vitawaua, kwa kuwa na wasiwasi na hofu mara zote kunaufanya mwili uwe haifu na hivyo kushindwa kuhimili magonjwa mbalimbali.
 
Kuna ambao mapenzi yatawaua, kwa kushindwa kudhibiti hisia zao za mapenzi na ngono wanajikuta kwenye hatari zinazoondoa maisha yao.
 
Kuna ambao kazi zitawaua, kwa kuweka muda na nguvu zao nyingi kwenye kazi zao kunachosha miili yao na kuibua magonjwa yatakayowaua.
 
Kuna ambao uvivu utawaua, kwa kukaa muda mrefu na kutokuwa na majukumu makubwa, mwili unakuwa mzembe na kushindwa kupambana na magonjwa na hilo kupelekea kifo.
 
Ndugu  yangu, hakuna atakayetoka hapa duniani akiwa hai, na kila mtu kuna kitu ambacho kitamuua.
 
Wito wangu kwako, chagua sumu yako vizuri, kile ambacho kitakuua, basi kiwe na maana kwako na hata wengine pia. Kuliko uuliwe kwa pombe, ulevi au ngono, ni bora uuliwe na kazi, maana kazi hiyo itakuwa na maana kwako na kwa wengine pia.

TABIA ZA WATU WALIOFANIKIWA SANA

(1). HAMASA.

Sifa ya kwanza ambayo watu waliofanikiwa wanaitaka kuwepo kwenye kile wanachofanya na chenye maana kwao ni hamasa. Wanapokuwa na nafasi ya kuchagua kipi cha kufanya, wale waliofanikiwa sana wanachagua kile ambacho wana hamasa kubwa ndani yao ya kukifanya.

Kitu hicho wanakuwa wanakipenda kutoka ndani ya mioyo yao na hivyo kusukumwa kukifanya vizuri kuliko wengine. Wanakuwa tayari kukifanya muda wote bila ya kuchoka na hawaangalii sana ni kiasi gani wanalipwa katika kukifanya.

Unapofanya kile unachopenda kufanya, kile ambacho una hamasa kubwa ndani yako kukifanya, unakuwa hufanyi kazi, bali unafanya maisha na hivyo nafasi ya wewe kufanikiwa inakuwa kubwa zaidi.

Kila siku jiulize swali hili muhimu; ni kitu gani kinanipa hamasa kubwa kwenye maisha yangu, kazi yangu na biashara yangu? Kisha nenda kafanye hicho, utazalisha matokeo bora zaidi kuliko wengine na hilo litakuwezesha kufanikiwa zaidi.


( 2 )MAHUSIANO.
Mahusiano ya kijamii ni muhimu sana kwenye maana ya maisha. Wale wanaokuwa wametengwa na watu wengine huwa wanaripoti maisha yao kupoteza maana. Maana ya maisha yetu ni matokeo ya vile ambavyo wengine wanapokea kile tunachofanya.

Watu waliofanikiwa sana wamekuwa wakichagua kwa umakini watu wanaojihusisha nao kwenye kazia au biashara wanazofanya. Wanafanya kazi au biashara zinazowawezesha kutengeneza mahusiano bora na wale ambao wanawapenda, wale ambao tabia walizonazo zinaendana nao.

Watu waliofanikiwa pia huwa wanapenda kuzungukwa na watu wanaowapa changamoto ya kupiga hatua zaidi. Hivyo wanafanya kazi au biashara ambayo wamezungukwa na watu wanaofanikiwa na wanaopiga hatua kufanikiwa zaidi. Watu hawa wanakuwa msukumo kwao kupiga hatua zaidi.

Usikubali kufanya kazi au biashara ambayo wengi unaoshirikiana nao hamuendani kitabia wala kimtazamo, itakuwa kikwazo kikubwa kwako kufanikiwa. Lakini pia kazana kuzungukwa na watu ambao wanakusukuma uwe bora zaidi, zungukwa na watu ambao wanapiga hatua zaidi ili iwe chachu kwako kupiga hatua zaidi.

Mahusiano yako na wengine kwenye kazi au biashara unayofanya yanapokuwa mabovu, maisha yako yanakuwa mabovu pia na hilo linachangia maisha yako kukosa maana.

( 3 ).KURIDHIKA.

Maisha yanakuwa na maana pale ambapo kile unachofanya kinakuridhisha, pale moyo wako unaporidhika na kile unachofanya unafurahia maisha yako na kuona yana maana kubwa.

Watu waliofanikiwa sana wamekuwa wanachagua kufanya kazi au biashara ambayo inawapa hali ya kuridhika, na hilo limekuwa linawawezesha kufanikiwa zaidi kupitia kile wanachofanya.

Kuridhika kwenye kile tunachofanya kunachangiwa na vitu viwili;

Moja ni ukuaji binafsi. Huwa tunaridhika pale ambapo kile tunachofanya kinatusukuma kukua zaidi ya pale tulipo sasa. Kama unajiona ukipiga hatua kadiri unavyokwenda, unaridhika zaidi.

Mbili ni mchango kwa wengine. Huwa tunaridhika pale ambapo kile tunachofanya kinakuwa na mchango kwa wengine. Pale wengine wanapotushukuru kwa kile tunachofanya, tunaridhika sana.

Hivyo chagua kazi au biashara ambayo inakupa nafasi ya kukua zaidi, ambayo unapiga hatua kadiri unavyokwenda na siyo kudumaa au kushuka chini. Pia kazi au biashara hiyo iwe inagusa maisha ya wengine, inaongeza thamani kwa wengine na kuwafanya kuwa bora kuliko walivyokuwa. Watu hao wanapokushukuru kwa mchango ambao umekuwa nao kwao, unaridhika sana na maisha yako yanakuwa na maana.

( 4 ). UMUHIMU.

Kila tunachofanya au kinachotokea kwenye maisha yetu, huwa tunakilinganisha na maeneo mengine ya maisha yetu. Kama kitu hicho kinaendana na maeneo mengine ya maisha yetu, basi tunaona maisha yetu yanakuwa na maana kubwa. Lakini kama kinachotokea hakiendani na maeneo mengine ya maisha yetu, maana inakosekana.

Watu waliofanikiwa sana wamekuwa wanachagua kufanya vitu ambavyo ni muhimu kwao, ambavyo vinaendana na haiba zao, sifa zao na hata maeneo mengine ya maisha yao.

Kama mtu anajichukulia kuwa mwaminifu, kazi au biashara inayojenga mazingira ya uaminifu inakuwa muhimu zaidi kwake na kuleta maana kwake. Lakini mtu huyo akafanya kazi ambayo haina uaminifu, anaweza kupata fedha, lakini ndani yake atakosa maana, kwa sababu kile anachofanya hakiendani na vile yeye alivyo.

Chagua kufanya kazi au biashara ambayo inaendana na wewe, ambayo inatumia na kukuza zile sifa binafsi zilizopo ndani yako na pia inachangia katika kuyakamilisha maisha yako. Yaani ukiangalia kila unachofanya, kinachangia maisha yako kukamilika.

Rafiki, hizo ndiyo sifa nne za kuangalia wakati unachagua kazi au biashara ya kufanya ili iwe na maana kwako na uweze kufanikiwa zaidi.

Kama tayari upo kwenye kazi au biashara ambayo unaona haina maana kwako, una hatua mbili za kuchukua ili uweze kupata maana na kufanikiwa zaidi.

Hatua ya kwanza ni kutafuta maana kwenye kazi au biashara hiyo. Huenda hujapata maana kwa sababu hujaitafuta, umekuwa unafanya tu kwa mazoea siku zote na hivyo hujawahi kutafakari na kuona maana. Anza kwa kuangalia sifa hizi nne kwenye kile unachofanya, jiulize ni kitu gani kinakupa HAMASA sana kwenye kazi au biashara unayofanya. Angalia wale ambao UNAHUSIANA nao kupitia kazi au biashara hiyo na ona ni watu gani bora zaidi unaoweza kutengeneza nao mahusiano. Tafuta KURIDHIKA kwa kukua zaidi na kufanya maisha ya wengine kuwa bora kupitia kazi au biashara unayofanya. Na mwisho angalia ni jinsi gani kazi au biashara hiyo ina UMUHIMU kwenye maisha yako, angalia inayakamilishaje maisha yako kwa kuendana na sifa zako nyingine.

Hatua ya pili ni kuondoka kwenye kazi au biashara hiyo na kwenda kufanya ile yenye maana kwako. Kama umejifanyia tathmini na hujaweza kupata maana kwenye kazi au biashara unayofanya sasa, kuendelea kubaki hapo hakutaleta maana kwenyewe. Badala yake chukua hatua ya kuondoka kwenye kazi au biashara hiyo na kwenda kufanya ile ambayo ina maana kwako. Hata kama hutaweza kuondoka kwa haraka, lakini lengo linapaswa kuwa kutengeneza maisha yenye maana.

FURSA YA KILIMO CHA MAPARACHI---------- " Fursa Afrika Mashariki Blog "

Wednesday, June 12, 2019

JE, WAJUA BIASHARA NI KAMA KIUMBE ?? HUZALIWA , HUKUA , HUDUMAA NA KUFA ?

" BIASHARA "  ni kiumbe hai, ambacho kinazaliwa, kinakua au kudumaa na mwishowe kinakufa. Biashara ni kitu ambacho kina maisha yake ya kujitegemea na jinsi ambavyo kinapewa uhuru wake ndivyo inavyofanikiwa zaidi.
Lakini pia biashara huwa inakuwa na tabia zake, ambazo zinaweza kuifanya ifanikiwe zaidi au kuizuia isifanikiwe. Tabia hizi za biashara huwa zinatokana na tabia ambazo mwanzilishi wa biashara hiyo anazo

Na hii ndiyo maana kwenye kila biashara kuna utaratibu na utamaduni fulani uliopo, ambao huwa ni mgumu sana kubadilisha. Hata wafanyakazi wapya wanapokuja kufanya kazi kwenye biashara hiyo, baada ya muda hujikuta wameshavaa utamaduni huo wa biashara.

Utaratibu na utamaduni uliojengeka kwenye biashara nyingi huwa ni matokeo ya tabia za mwanzilishi wa biashara, huwa siyo kitu ambacho kimetengenezwa kwa makusudi ambacho kinaweza kuwa na msaada kwenye biashara hiyo.

Hivyo unakuta biashara imejijengea tabia ambazo siyo nzuri na zinakuwa kikwazo kwa maendeleo ya biashara hiyo. Ukiangalia tabia za biashara hiyo, zinakuwa zinaendana sana na tabia za mwanzilishi wa biashara hiyo.

Mfano kama mwanzilishi wa biashara ni mzito kwenye kufanya maamuzi, basi ufanyaji wa maamuzi wa kila mtu kwenye biashara unakuwa ni mzito sana. Maamuzi hayafanyiki kwa wakati na biashara inazikosa fursa nzuri za kukua zaidi.

Kama mwanzilishi wa biashara hawezi kupangilia vitu vyake vizuri kwenye maisha yake binafsi, unakuta biashara nayo haina mpangilio mzuri, vitu vipo hovyo hovyo na hakuna utaratibu wowote unaotumika kwenye kufanya vitu.

Kama mwanzilishi wa biashara ana tamaa, biashara nzima inaendeshwa kwa tamaa, kila aliyepo kwenye biashara hiyo anakuwa na tamaa na kujali mambo yake zaidi kiliko ya biashara.

Hivyo popote ambapo biashara imekwama, kwa hakika ndipo ambapo mmiliki wa biashara hiyo amekwama. Biashara haiwezi kukua zaidi ya ukuaji wa mmiliki wa biashara hiyo.