Saturday, June 22, 2019

ELIMU YA FEDHA : MAISHA ULIYOPOTEZA

Watu wengi wamekuwa wanakutana na hali hii, akiwa hana fedha anakuwa na mawazo na mipango mizuri sana ya kutekeleza anapopata fedha. Anakuwa mpole na mwenye akili nzuri juu ya matumizi ya fedha. Akiona wengine wanatumia fedha vibaya anajiambia kama mimi ningepata fedha hizo, basi ningefanya mambo mazuri sana.
Lakini mtu huyo huyo anapopata fedha, anajikuta anafanya vitu ambavyo hata hakupanga kufanya. Mtu akishapata fedha zile akili nzuri na mipango aliyokuwa nayo anasahau kabisa. Anajikuta ananunua vitu ambavyo hakupanga kununua, mahitaji muhimu ambayo hayakuwepo awali yanaanza kujitokeza. Ni mpaka fedha hiyo inapoisha ndiyo mtu anarudi kwenye akili zake na kujiuliza zile fedha zimeishaje bila kufanya mambo mazuri.
Kama umewahi kukutana na hali kama hii usijione kama una bahati mbaya, au ni mjinga sana inapokuja kwenye fedha. Jua hiyo ni hali inayowakumba watu wengi kwenye fedha, na inatokana na wengi kutokuielewa vizuri saikolojia ya fedha. Fedha ni nguvu, na nguvu yoyote isipodhibitiwa na kutumiwa vizuri inaleta uharibifu.
Leo nakwenda kukushirikisha dhana itakayokuwezesha kuwa na udhibiti mzuri kwenye fedha zako, dhana itakayokuzuia usitumie hovyo fedha pale unapokuwa nazo.
Dhana hii ni kuhesabu fedha kwa kulinganisha na maisha ambayo umepoteza kupata fedha hizi. Wote tunajua kwamba muda ni fedha, na pia tunajua kwamba muda ni maisha, hivyo basi maisha pia ni fedha.
Sasa chukua kipato chako unachopata kwa mwezi, kisha gawa kwa masaa unayofanya kazi. Mfano kama kipato chako ni milioni moja, halafu unafanya kazi masaa 8 kwa siku, siku 5 au 6 za wiki, kwa mwezi unafanya kazi kwa masaa 160 mpaka 200. Ukigawa milioni moja kwa masaa 200 utapata shilingi elfu 5. Hii ina maana kila saa unayofanya kazi unalipwa shilingi elfu 5.
Sasa kwa sababu muda ni fedha na maisha ni muda hivyo maisha ni fedha, kila elfu 5 unayoipata, unapoteza saa moja ya maisha yako. ukipata elfu 10 umepoteza masaa mawili.
Sasa kila unapotaka kununua kitu, kabla hujafanya maamuzi ya kukinunua jiulize kwanza swali hili, je kitu hiki ninachokwenda kununua, kina thamani sawasawa na maisha niliyopoteza?
Kwa mfano umekutana na nguo ambayo inauzwa shilingi elfu 20, umeipenda kweli na unataka kuinunua. Jiulize kwanza je nguo hii ina thamani sawa na masaa manne ya maisha yangu? Je kama nikiambiwa nichague kupata nguo hii na kupata masaa manne zaidi kwenye maisha yangu nitachagua nini?
Kwa kuchukulia fedha zako kama maisha ambayo unapoteza, utajijengea nidhamu kubwa sana ya fedha na kuacha matumizi ya hovyo, yasiyo na manufaa kwako. Pia utapata muda zaidi wa kufanya yale muhimu kwako, pamoja na kuwekeza fedha zako maeneo ambayo yanazalisha na hivyo kukusaidia usifanye kazi muda mrefu kupata fedha za kupoteza.
Linganisha kila fedha unayotaka kutumia na maisha unayopoteza, na utaona jinsi gani vitu vingi unavyopenda kununua havina thamani unayovipa.

No comments:

Post a Comment