Friday, June 14, 2019

KILA MTU ATAKUFA , NI BORA UULIWE NA KAZI !


Kila mtu atakufa, hilo halina ubishi. Hii ni hukumu uliyoipata siku unayozaliwa, ambacho hujui ni siku gani hukumu hiyo itakamilika.
 
Lakini kuna kitu kingine muhimu sana kuhusu kifo ambacho wengi tumekuwa hatukitafakari, ambacho tukikielewa kitatusaidia sana.
 
Kila mtu kuna kitu kitakachomuua. Ndiyo, kuna kitu ambacho kitakuua, yaani kitachangia kwenye kifo chako.
 
Kuna ambao ulevi utawaua, kwa kuendekeza sana ulevi mwili unachoka na kupata magonjwa ambayo yanachangia kifo chao.
 
Kuna ambao chakula kitawaua, kwa kushindwa kula kwa nidhamu wanakuwa na afya mbovu ambayo inaleta magonjwa yanayowaua.
 
Kuna ambao wasiwasi na hofu vitawaua, kwa kuwa na wasiwasi na hofu mara zote kunaufanya mwili uwe haifu na hivyo kushindwa kuhimili magonjwa mbalimbali.
 
Kuna ambao mapenzi yatawaua, kwa kushindwa kudhibiti hisia zao za mapenzi na ngono wanajikuta kwenye hatari zinazoondoa maisha yao.
 
Kuna ambao kazi zitawaua, kwa kuweka muda na nguvu zao nyingi kwenye kazi zao kunachosha miili yao na kuibua magonjwa yatakayowaua.
 
Kuna ambao uvivu utawaua, kwa kukaa muda mrefu na kutokuwa na majukumu makubwa, mwili unakuwa mzembe na kushindwa kupambana na magonjwa na hilo kupelekea kifo.
 
Ndugu  yangu, hakuna atakayetoka hapa duniani akiwa hai, na kila mtu kuna kitu ambacho kitamuua.
 
Wito wangu kwako, chagua sumu yako vizuri, kile ambacho kitakuua, basi kiwe na maana kwako na hata wengine pia. Kuliko uuliwe kwa pombe, ulevi au ngono, ni bora uuliwe na kazi, maana kazi hiyo itakuwa na maana kwako na kwa wengine pia.

No comments:

Post a Comment