Tuesday, December 25, 2018

WEKA MALENGO YAKO MWEZI DISEMBA KABLA MWAKA HAUJAANZA.

Watu wengi wanakosea kuweka malengo kwa sababu wanayaweka kipindi ambacho siyo sahihi. Wakati wa mwaka mpya, watu wengi huwa wanakuwa na hisia kali za upya wa mwaka na kwa kuwa kila mtu anasema mwaka mpya mambo mapya, basi na wao wanajiunga na msafara huo.
Wengi wanajikuta wanaweka malengo ambayo siyo yao, wanapoona wengine wameweka malengo fulani basi na wao wanaona wanapaswa kuwa na malengo ya aina hiyo. Kitu kinachowapelekea kushindwa sana kwenye maisha yao.

Wakati sahihi wa kuyaweka malengo yako kwa mwaka mpya ni kabla mwaka haujaanza. Hivyo mwezi huu wa disemba, tenga muda na ukae chini ili kuweka malengo yako kwa mwaka unaofuata. Kupitia tafakari ya mwezi ulioisha uliyofanya, kupitia vipaumbele vya mwaka ulivyojiwekea, unaweza kuweka malengo ambayo ni bora sana kwako.

Weka malengo yako ya mwaka mpya mwezi disemba na wakati wengine wanakimbizana na malengo mwanzo wa mwaka, wewe unakuwa upo kwenye utekelezaji.

HERI  YA   X--MASS  NA  MWAKA  MPYA.

WEKA VIPAUMBELE ( PRIORITES ) MWEZI DISEMBA VYA MWAKA UNAOFUATA.

Kabla hujaweka malengo yoyote, anza kwanza na vipaumbele. Watu wengi wanakosea kwenye kuweka malengo kwa sababu hawajui na pia hawana vipaumbele kwenye maisha yao. Hilo linawapelekea kuweka malengo ambayo hata hawajui wanayafikiaje, kwa sababu yanakuwa hayaendani na hayajapangiliwa vizuri.

Chagua vipaumbele vichache kwa mwaka unaofuata, angalia yale maeneo ambayo ni ya muhimu zaidi kwenye maisha yako, ambayo ukiyasimamia vizuri na kuyafanyia kazi, utaweza kupata matokeo bora sana kwenye maisha yako.
Kwa kujua vipaumbele vyako, utaweza kuweka malengo ambayo ni sahihi kwako na yanafikika.

HERI  YA  X--MASS NA  MWAKA  MPYA.

KUWA MAKINI NA MSIMU WA SIKUKUU USIKUACHE MWEUPE PEPEEE !!

Mwezi disemba ni mwezi ambao huwa kuna sikukuu nyingi, ni mwezi ambao wengi wana mategemeo makubwa ya kupumzika na kusherekea. Lakini unapaswa kuwa makini sana na kipindi cha sikukuu kwa sababu wengi hujisahau na kuuanza mwaka wakiwa kwenye madeni makubwa.

Hakikisha unajiwekea bajeti ya matumizi yako kwenye msimu wa sikukuu, na usizidishe kabisa bajeti hiyo. Hakikisha unaamua mapema kabisa ni vitu gani utagharamia kwenye msimu huo wa sikukuu na vipi utaachana navyo.

Na kama kuna sherehe ambazo hazina ulazima, zisikuumize kichwa, achana nazo. Hakuna utakachokikosa kwa kuachana na baadhi ya sherehe na mapumziko. Pia kama utaanza kufanyia kazi malengo yako mapema, utakuwa bize kupiga hatua na sikukuu hazitakuwa na madhara kwako.

HERI  YA  X--MASS  NA  MWAKA  MPYA.

UTAFAKARI MWAKA UNAOKWENDA KUUMALIZA.

Watu wengi huwa wanauanza mwaka kwa matumaini makubwa, wanaweka malengo makubwa lakini huwa hayamalizi mwezi, wanaachana nayo na kurudi kwenye maisha ya kawaida.

Unapofika mwezi disemba ni wakati mzuri wa kuutafakari mwaka unaokwenda kuumaliza, kuangalia yale malengo na mipango uliyojiwekea na pia kuangalia kwa kiasi gani umeweza kutekeleza.

Kwa yale malengo uliyoachana nayo, jua tatizo ni nini, uliyaweka vibaya au uvivu na uzembe wako ndiyo umekufanya uachane nayo?
Angalia pia fursa mbalimbali ulizokutana nazo kwenye mwaka wako mzima, zile ulizofanyia kazi na zile zilizokupita.

Kwa kuutafakari mwaka unaokwenda kuumaliza, utaweza kuona wapi umefanya vizuri, wapi umekosea na marekebisho yapi ya kufanya.

HERI  YA  X--MASS  NA  MWAKA MPYA.

JIKUMBUSHE KUSUDI LA MAISHA YAKO MWEZI DISEMBA.

Kwa kelele za dunia ni mihangaiko yetu ya kila siku ni rahisi sana kusahau kusudi la maisha yako. Na ukishasahau kusudi la maisha yako, huna tofauti na meli ambayo haina uelekeo. Unaweza kwenda kasi sana, lakini haitakusaidia, kwa sababu unakuwa tayari umeshapotea.

Unapofika mwisho wa mwaka jikumbushe kusudi la maisha yako, jikumbushe kwa nini upo hapa duniani, jikumbushe nini kinakusukuma kutoka kitandani kila asubuhi.

Kusudi la maisha yako ndiyo linapaswa kukupa msukumo wa kufanya makubwa. Na unapolikumbuka mara zote, linakuwezesha kuchukua hatua sahihi ili kuweza kulitimiza.
Jikumbushe kusudi la maisha yako na jiulize yale unayofanya yanachangiaje kwenye kufikia kusudi la maisha yako.

HERI  YA  KRISMASI  NA  MWAKA  MPYA !

Saturday, December 22, 2018

TUMIA VIGEZO HIVI VITANO ( 5 ) KUYAFIKIA MALENGO YAKO.

(1).LENGO LINAPASWA KUWA MAALUMU (SPECIFIC).
Kigezo cha kwanza muhimu kwenye kuweka malengo ambayo utayafikia ni umaalumu wa lengo husika. Unapaswa kuweka lengo ambalo linaeleweka ni nini hasa unachotaka.
Unapaswa kujua ni nini kwa hakika unachotaka kwenye lengo hilo, unakipata wapi, utashirikiana na nani, kwa nini unakitaka na hatua zipi unapaswa kuchukua.
Tukienda kwenye mfano wetu wa fedha, usiweke lengo kwamba nataka fedha zaidi, au nataka kuwa bilionea. Unapaswa kuweka kiasi cha fedha unachotaka na kujua utakipataje kwa hatua zipi unazopaswa kuchukua.
Utaona tofauti kubwa kati ya hali hizo mbili, unaposema unataka fedha zaidi, ukipata elfu kumi ambayo hukuwa nayo ni fedha zaidi. Lakini unaposema unataka milioni 50 au bilioni moja, hapo sasa unakuwa na uhakika nini unataka.
Usiweke malengo yanayoelea hewani, jua kabisa nini unataka na nenda mbali zaidi kujua unakipataje na kwa kufanya nini. Pia unapaswa kuwa na kwa nini inayokusukuma kufikia lengo hilo.

(2). LENGO LIPIMIKE (MEASURABLE).
Kigezo cha pili kwenye kuweka malengo utakayoweza kuyafikia ni kila lengo linapaswa kuwa linapimika. Hapa unapaswa kuona kabisa ni jinsi gani kupata kile unachotaka kutabadili maisha yako.
Pia unapaswa kuligawa lengo lako kubwa kwenye hatua ndogo ndogo ambazo unaweza kuzitumia kupima maendeleo yako kwenye lengo hilo.
Kwa mfano kama lengo lako ni kupata milioni 50 kwa mwaka, unaweza kuligawa kwa miezi 12 na ukapata kama milioni 4 kwa mwezi, hii inakuwa rahisi kwako kujipima kila mwezi kuona unaelekeaje kwenye lango lako.
Kuweza kuligawa lengo lako kubwa kwenye hatua ndogo ndogo zinazopimika kutakuondolea kukata tamaa pale lengo linapoonekana ni kubwa sana.
Hakikisha kila lengo unaloweka unaweza kupata taswira ya ukiwa umelikamilisha kisha ligawe kwenye hatua ndogo ndogo ambazo ni rahisi kwako kupima.

(3). LENGO LIWE NINAFIKIKA (ATTAINABLE).
Kigezo cha tatu ni lengo liwe linafikika. Tumekuwa tunayaelewa sana mafunzo ya maendeleo binafsi ambayo yanatufundisha kwamba ndani yetu tuna uwezo mkubwa na tunaweza kufanya chochote tunachotaka kufanya. Hili ni kweli kabisa kwamba tuna uwezo mkubwa na kuweza kufanya chochote tunachotaka.
Lakini inahitaji muda, nguvu na hata vipaji kufikia lengo lolote tunalojiwekea. Hivyo unapoweka lengo, lazima ujiulize je kwa muda, nguvu, rasilimali na hata vipaji ulivyonavyo utaweza kufikia lengo hilo? Kama siyo unajidanganya.
Kwa mfano kama mwaka huu kipato chako ni shilingi milioni moja kwa mwezi, kujiambia kwamba mwaka kesho unataka upate bilioni moja ni kujidanganya na kujiandaa kushindwa. Ni kweli lengo la bilioni moja linafikika, lakini linachukua muda, na linahitaji jitihada zaidi.
Kwenye kila lengo unalojiwekea, angalia rasilimali ulizonazo kisha weka lengo kubwa ambalo litakusukuma, lakini lisikukatishe tamaa.

(4). LENGO LIWE NA UHUSIANO NA KUSUDI LA MAISHA YAKO (RELEVANT).
Kigezo cha nne kwenye kuweka malengo utakayoyafikia ni lengo liwe na uhusiano na kusudi la maisha yako. Mara nyingi wengi wamekuwa wanaweka malengo ambayo siyo yao. Kwa sababu wamesikia wengine wakiweka malengo hayo basi na wao wanaona inabidi wayaweke la sivyo wataachwa nyuma.
Watu wengi wamekuwa wanafuata mkumbo kwenye uwekaji wa malengo, wanaweka malengo ambao hayahusiani kabisa na lile kusudi walilonalo kwenye maisha. Wanapokuja kugundua hili wanashindwa kuendelea na malengo yao.
Kwenye kila lengo unalojiwekea, hakikisha linaendana na kusudi kubwa la maisha yako. Hata kama ni lengo kubwa kiasi gani, kama halitokani na kusudi lako kubwa, utaishia kushindwa.
Usijiambie unataka kupata mabilioni ya fedha kupitia biashara fulani ambayo inaonekana kuwa yenye faida kubwa, wakati wewe unapenda kufanya kitu kingine tofauti kabisa. Lengo unaloweka liendane na kile unachopenda na kujali kufanya.

(5).LENGO LIWE NA UKOMO WA MUDA (TIMELY).
Kigezo cha tano katika kuweka malengo ambayo utayafikia ni kuwa na ukomo wa muda. Wote tunajua jinsi ambavyo ukomo wa muda unavyotusukuma kuchukua hatua. Watu wanaweza kupewa nafasi ya kufanya kitu kwa muda mrefu lakini wasifanye, inapofikia tarehe ya ukomo ndiyo kila mtu anafanya.
Tumia nguvu hii ya ukomo wa muda kwenye malengo unayoweka, kila lengo liwe na ukomo wake wa muda na ujikumbushe ukomo huo ili uweze kujisukuma kufanya zaidi na kufikia lengo hilo. Kwenye kila lengo ulilogawa kwenye hatua ndogo, jiwekee ukomo kwenye kila hatua na ufuate ukomo huo.
Kama umejiambia unataka kupata bilioni moja ndani ya miaka kumi, basi gawa kiasi cha kupata kila mwaka, kila mwezi, kila wiki na hata kila siku, kisha weka muda wa kufuatilia kila kiwango unachotaka kupata ili kuona maendeleo yako yakoje.
Rafiki, hivyo ndivyo vigezo vitano muhimu unavyopaswa kuvitumia kuweka malengo ambayo kwa hakika utayafikia. Tumia vigezo hivi katika kila lengo unaloweka na utaona jinsi utakavyolielewa lengo lako vizuri, kuona kila hatua unayopaswa kuchukua na kuwa na msukumo wa kuchukua hatua kabla muda uliojiwekea haujaisha.

WATU WENGI HUSHINDWA KUYAFIKIA MALENGO YAO ! KWANINI ----------------- ?

Wapo watu ambao wamekuwa wanayaendesha maisha yako kama saa ya mshale ambayo imeharibika. Kwa nje mishale inaweza kuonekana kama inafanya kazi, lakini kwa hakika imesimama.

Wapo watu ambao kila mwanzo wa mwaka huwa wanaweka malengo makubwa, malengo yanayowahamasisha sana na kuwafanya waone wanaweza kufanya makubwa kwenye maisha yao. Lakini siku chache baada ya kuweka malengo hayo, wanajikuta wamesharudi kwenye maisha ya mazoea na kusahau kabisa malengo waliyojiwekea.

Sasa kinachowafanya watu wafanane na saa iliyoharibika ni kwamba mwaka unapoisha na kuanza mwingine, wanaweka tena malengo yale yale na siku chache baadaye wanajikuta wameshayasahau. Hivyo kinachotokea ni mtu kwa miaka mingi anakuwa anarudi kuweka malengo yale yale lakini hachukui hatua wala kuyafikia.

Watu wengi wanaoweka malengo huwa wanashindwa kuyafikia kwa sababu hawavijui vigezo vitano muhimu sana vya kuweka malengo ambayo mtu ataweza kuyafikia.

Thursday, December 20, 2018

KAMILISHA MAJUKUMU YA KILA SIKU.

KAMILISHA majukumu unayojiwekea kila siku. Kila unachopanga kufanya, unapaswa kukifanya kwa muda uliopanga kufanya. Kamwe usiahirishe chochote, usijiambie nitafanya kesho, chochote kinachoweza kufanyika leo kifanye.

Pale wazo la kuahirisha kitu linapoingia kwenye akili yako, mara moja jiambie NITAFANYA SASA, rudia maneno hayo mara nyingi na utasahau kuhusu kuahirisha na kuweza kuchukua hatua mara moja.

Zoezi la kufanya; kila unachoorodhesha kufanya kwenye siku yako kifanye, usiwe mtu wa kuahirisha mambo. Wazo la kuahirisha linapokujia, jiambie NITAFANYA SASA, kisha fanya.

ISHI KILA SIKU KWA KIASI.

Kila unachofanya kwenye maisha yako, kinapaswa kuwa kwa kiasi, hupaswi kufanya kwa kiwango kidogo sana wala kufanya kwa kupitiliza.

Kuanzia kwenye maisha binafsi na hata kazi au biashara, fanya kwa kiasi. Usile kupitiliza, usinywe kupitiliza, usiwe na hisia kali kupitiliza na wala usipumzike kupitiliza.

Kuishi kwa kiasi ni tabia muhimu sana ambayo itakuwezesha kufika kwenye mafanikio makubwa. Kwa sababu unapofanya kupita kiasi, unauchosha mwili na unashindwa kufanya yale ambayo ni muhimu.

Zoezi la kufanya; kwa yale unayofanya kila siku kwenye maisha yako, fanya kwa kiasi, jidhibiti wewe mwenyewe usifanye jambo lolote kupitiliza. Usile kupitiliza, kunywa kupitiliza au kupatwa na hisia zilizopitiliza. Kufanya hivyo kutakupeleka kwenye matatizo makubwa.

JALI NA BORESHA MAHUSIANO YAKO.

Huwezi kufanikiwa wewe mwenyewe, kauli ya jeshi la mtu mmoja ni kauli ya kujidanganya, hakuna jeshi la mtu mmoja. Mafanikio yako yanahitaji timu kubwa sana ya watu, kuanzia familia yako, watu wako wa karibu, unaohusiana nao kwenye kazi na hata biashara na jamii inayokuzunguka kwa ujumla.
Moja ya tabia muhimu ya kujijengea kila siku ni kutengeneza na kuboresha mahusiano yako na watu wengine. Kila unachokitaka kinatoka kwa watu wengine hivyo mahusiano haya yanapokuwa bora, unaweza kupata zaidi kila unachotaka.
Zoezi la kufanya; yajue mahusiano muhimu kwenye kila eneo la maisha yako, kuanzia familia, marafiki, kazi, biashara na jamii kwa ujumla. Kisha tenga muda wa kuboresha mahusiano haya kupitia mawasiliano na hata kufanya vitu kwa ajili ya wengine.

JALI NA BORESHA AFYA YAKO KILA SIKU.

Yote unayotaka kwenye maisha yako yatabaki kuwa ndoto kama hutakuwa na afya bora. Kwa sababu kama afya siyo bora, hutaweza kuweka mapambano yanayohitajika. Pia kama utaweka juhudi sana kupata mafanikio na ukasahau afya yako, ukayapata mafanikio lakini afya ikawa mbovu hutaweza kufurahia mafanikio hayo.

Tengeneza tabia ya kujali afya yako kila siku. Na maeneo mawili ya kujali na kuboresha afya yako ni kwenye ulaji na mazoezi.

Kwenye ulaji unapaswa kula chakula bora kiafya na kula kwa kiwango ambacho siyo kingi. Epuka vyakula vinavyoandaliwa haraka maana huwa siyo vizuri kiafya.

Pia kuwa na mpango wa mazoezi kila siku. Kila siku fanya mazoezi kwa angalau dakika 30. Mazoezi ya kukimbia ni mazuri kuliko mazoezi ya aina nyingine yoyote.

Zoezi la kufanya; pangilia mlo wako wa kila siku ili kuwa na afya bora. pia tenga nusu saa kwenye kila siku yako kwa ajili ya mazoezi.

JIENDELEZE ZAIDI KILA SIKU.

Ukomo pekee ambao unao kwenye maisha yako ni ule unaojiwekea ndani yako. Mafanikio yako hayawezi kukua zaidi ya unavyokua wewe. Hivyo tabia muhimu sana unayopaswa kujijengea ni ya kujiendeleza zaidi kila siku.

Jiendeleze kila siku kwa kujifunza na kujisomea angalau kwa dakika 30 kila siku. Yaani siku isipite kama hujajifunza kitu kipya. Tenga muda wa dakika 30 wa kujifunza ili uwe bora zaidi.

Soma vitabu, sikiliza vitabu, angalia mafunzo kwa njia ya video na kadhalika, lakini hakikisha kila siku unajifunza. Hakikisha siku inapoanza na kuisha, unakuwa bora zaidi kuliko ulivyoanza siku hiyo.

Zoezi la kufanya; tenga dakika 30 kwenye kila siku yako kwa ajili ya kujifunza na kuwa bora zaidi. Tenga vitabu utakavyosoma, kusikiliza na hata mafunzo utakayoangalia. Usikubali siku ipite hujajifunza kitu kipya.

KUWA NA MALENGO YA KILA SIKU, KILA WIKI, KILA MWEZI, KILA MWAKA NA YA MUDA MREFU.

Bila ya kuwa na malengo unayoyafanyia kazi, juhudi zozote unazoweka unapoteza. Unaweza ukachoka sana, lakini ukiangalia hakuna kikubwa ulichokamilisha.
Unapaswa kuwa na malengo unayoyafanyia kazi kila siku, malengo yako yanapaswa kugawanywa kwenye siku, wiki, mwezi, mwaka na muda mrefu.
Malengo ya siku unayaweka mwanzo wa siku, kwa kuweka orodha ya vile utakavyofanyia kazi siku hiyo.
Kila mwanzo wa wiki weka malengo ambayo unataka kuyakamilisha wiki hiyo. Kadhalika kwenye mwezi na hata mwaka.
Unapaswa kuwa na malengo ya muda mrefu, miaka 5, 10, 20 na mpaka 50 ijayo. Kila wakati unapaswa kuwa unasukumwa na malengo unayoyafanyia kazi.
Zoezi la kufanya; kaa chini na weka au pitia malengo uliyonayo, kisha yaweke kwenye mafungu ya malengo ya muda mrefu, malengo ya mwaka, ya mwezi, ya wiki na kisha ya siku. Anza kila siku yako ukiwa na malengo na mipango unayofanyia kazi na hutapoteza muda kabisa kwenye siku yako.

KUWA MTUMWA WA TABIA NZURI KILA SIKU.

Hatua ya kwanza kabisa kwenye kutengeneza mafanikio ni kujijengea tabia nzuri za kila siku na kuwa mtumwa wa tabia hizo. Na wala huhitaji kuanzia mbali sana kujenga tabia nzuri, bali anza na tabia ulizonazo sasa kisha zigeuze kuwa tabia nzuri.

Kwa mfano kama sasa hizi unatumia muda wako mwingi kuangalia tv au kwenye mitandao ya kijamii, jiwekee ukomo kwenye mambo hayo. Mfano jiambie utatenga saa moja pekee kwenye siku yako kwa ajili ya habari, tv na mitandao ya kijamii. Kwa tabia kama hii utaokoa muda wako mwingi ambao kwa sasa unaupoteza.

Kadhalika badili tabia ulizonazo sasa kwenye ulaji, unywaji, muda wa kuamka, muda wa kulala na mengine yote unayofanya kila siku ya maisha yako.
Zoezi la kuchukua; orodhesha tabia zote unazofanya kwenye kila siku yako, kisha angalia zipi ni nzuri kwako na zipi siyo nzuri kwako. Zile nzuri endelea na nazo na zile mbaya zigeuze kuwa nzuri.

KUWA NA FIKRA ZA KITAJIRI KILA SIKU.

Kuna fikra za kitajiri na fikra za kimasikini. Fikra za kitajiri ni fikra chanya, za hamasa na matumaini makubwa. Fikra za kimasikini ni fikra hasi, za kukata tamaa na kushindwa.
Ili uweze kufanikiwa unapaswa kuwa na fikra za kitajiri kila siku, unapaswa kuwa na kauli chanya ambazo unajiambia kila siku, kauli ambazo zinakupa hamasa na kukusukuma kusonga mbele zaidi. Jijengee taswira ya kile unachotaka kwenye maisha yako na mara kwa mara jione umeshapata kitu hicho. Kwa kufanya hivi unaipa akili yako kazi ya kuhakikisha unapata unachotaka.
Zoezi la kufanya leo; dhibiti fikra zako ziwe chanya na za kitajiri kila siku. Fikiria yale ambayo yanakufikisha kwenye kile unachotaka. Jione tayari umeshafika pale unapotaka na weka picha hiyo kwenye akili yako mara zote. Hili litakufanya uvutie mazingira yatakayokuwezesha kupata unachotaka.

WEKA AKIBA SEHEMU YA KUMI YA KIPATO CHAKO.

Kwenye kila kipato unachoingiza, asilimia kumi ya kipato hicho hupaswi kuitumia kwa shughuli nyingine yoyote, bali unapaswa kujilipa wewe mwenyewe. Hichi ni kipato ambacho unakiweka pembeni maalumu kwa ajili ya uwekezaji ambao utakulipa zaidi baadaye.
Unapopata fedha, kabla hujaanza kulipa bili mbalimbali unazodaiwa au kununua vitu unavyohitaji, jilipe wewe mwenyewe kwanza. Hii ni tabia moja rahisi ambayo imewawezesha wengi kufikia utajiri mkubwa, bila ya kujali kiasi cha kipato walichonacho. Unapaswa kujilipa kwanza kabla hujafanya matumizi, kwa sababu ukisema utumie halafu itakayobaki ndiyo ujilipe, hutabakiwa na kitu.
Zoezi la kufanya; kwenye kila kipato unachoingiza, kabla hujaanza kupangilia unakitumiaje, ondoa kwanza asilimia kumi ya kipato hicho na weka pembeni, weka mahali ambapo hutakitumia hata iweje. Kipato hicho ni kwa ajili ya uwekezaji, ndiyo kitakachokufanyia wewe kazi.

DHIBITI MAWAZO NA HISIA ZAKO KILA SIKU.


Ili uweze kufanikiwa, unapaswa kuzitawala hisia na mawazo yako kila wakati. Hupaswi kuruhusu mawazo hasi kuingia kwenye akili yako. Hisia hasi kama za hasira, wivu, huzuni, hofu na hata kukata tamaa, hazipaswi kupata nafasi ndani yako.
Unapaswa kuwa bize na malengo na mipango yako ya kila siku kiasi kwamba mawazo na hisia hasi havipati nafasi kabisa kwenye akili yako. Na ukiweza kufanya hivi hutapata nafasi ya kuwa na huzuni au kupata sonona.
Zoezi la kufanya; kila wakati kagua mawazo na hisia ambazo unazo, je ni hasi au chanya. Kama ni hasi badili mara moja kwenda chanya. Huwezi kufanikiwa ukiwa na mawazo na hisia hasi. Lazimisha akili yako ifikiri chana na mara zote jiweke kwenye hisia chanya. Hili litakuwezesha kuona matumaini na kujituma zaidi.

Tuesday, December 18, 2018

TABIA 33 ZA WAJASIRIAMALI WENYE MAFANIKIO MAKUBWA.


1. Anzia sokoni, wengi huanza kufanya kitu kwa mapenzi yao wenyewe na siyo mapenzi ya soko. Kama unataka kufanikiwa, anza kujua watu wanataka nini kisha wape hicho wanachotaka.
 
2. Usiogope kushindwa, kabla hujafanikiwa, utakutana na vikwazo na changamoto mbalimbali, utashinda kwenye mengi, lakini kama hutakata tamaa, mwishowe utashinda.
 
3. Gundua fursa zilizojificha kwenye majanga mbalimbali. Unapokutana na majanga au changamoto, usiangalie upande wa matatizo, badala yake jiulize ni fursa gani iko hapa, na utaziona fursa nyingi zilizojificha kwenye majanga.
 
4. Toa thamani kubwa kwa wateja wako, wateja wataendelea kununua kwako kama kuna thamani wanaipata. Hakikisha mteja hakusahau kabisa, kwa namna unavyompa thamani ya kipekee.
 
5. Amka asubuhi na mapema, hii ni tabia moja ambayo itakupa ushindi mkubwa sana kwenye siku yako. Unapoamka mapema kuliko wengine na ukatumia muda huo kwa maandalizi na kufanya yaliyo muhimu, utaweza kupiga hatua sana.
 
6. Tenga muda wako na fanya jambo moja kwa wakati. Watu wengi huwa wanafikiria kufanya mambo mengi kwa pamoja ni kuokoa muda, lakini matokeo ni kinyume, kadiri mtu anavyofanya mengi kwa pamoja, ndivyo anavyopoteza muda na umakini wake. Kama unataka kukamilisha mengi, tenga muda wako na kisha fanya jambo moja kwa wakati.
 
7. Fanya mambo yanayoendana pamoja. Unapopanga ratiba ya kufanya vitu vyako, vile vitu ambavyo vinaendana, panga kuvifanya pamoja, hasa pale vitu hivyo vinapokuwa havihitaji umakini mkubwa. Kwa njia hii inakuwa rahisi kwako kukamilisha yale yanayoendana. Na hii haipingani na namba sita ya kufanya jambo moja kwa wakati, ila hapa unayaweka pamoja yale yanayoendana ili uweze kuyakamilisha.
 
8. Kuwa na mapumziko ya mara kwa mara. Kazi zetu nyingi tunafanya tukiwa tumekaa, hili linaleta uchovu na pia ni hatari kiafya. Suluhisho ni kuwa na mapumziko ya mara kwa mara ambapo unasimama na kutembea kidogo au kujinyoosha kabla ya kuendelea na jukumu jingine.
 
9. Kuwa na orodha mbalimbali, popote unapokuwa, kuwa na orodha unayofanyia kazi. Na unapopata wazo jipya, liandike mahali, usiamini kumbukumbu zako, utaishia kusahau mengi au kuijaza akili yako vitu visivyo muhimu kwenye kile unachofanya kwa wakati huo.
 
10. Weka malengo ambayo unaweza kuyafanyia kazi, malengo yanayopimika na unayoweza kuona ni wapi unakwenda na unafikaje pale. Bila ya malengo unayoweza kufanyia kazi, hutaweza kupiga hatua kubwa kwenye maisha yako.
 
11. Tumia vizuri muda wa uzalishaji mkubwa kwako. Kila mmoja wetu ana muda ambao anakuwa na uzalishaji mkubwa sana. Huu ni muda ambao akili ya mtu inakuwa inafikiri kwa umakini na mwili unakuwa na nguvu ya kutosha. Jua ni wakati gani wa siku unakuwa kwenye hali hii kisha weka yale majukumu muhimu kwenye muda huo.
 
12. Pima maendeleo yako kibiashara kwenye yale maeneo muhimu. Kila biashara ina maeneo yake muhimu, ambayo hayo yakienda vizuri basi biashara inakuwa ya mafanikio makubwa. Yajue maeneo muhimu kwenye biashara yako kisha pima maendeleo yako, pima hatua unazopiga ukilinganisha na malengo uliyojiwekea. Hii ndiyo njia rahisi ya kupima hatua unazopiga.
 
13. Epuka kujilisha vitu visivyo na maana. Habari, mitandao ya kijamii na kelele nyingine zimekuwa zinachukua muda wa wengi na wanashindwa kufanya yale muhimu. Epuka kujilisha vitu hivyo visivyo na maana na tumia muda wako kwa yale majukumu muhimu kwako.
 
14. Tengeneza muda wa kujitenga na teknolojia. Teknolojia zinarahisisha sana maisha, lakini pia zimekuwa usumbufu mkubwa sana kwenye maisha yetu. Tenga muda ambao utajitenga na teknolojia hizi, ili uwe na utulivu unaokuwezesha kufikiri kwa kina na hata kutekeleza majukumu ambayo ni muhimu kwako, yanayohitaji utulivu wa hali ya juu.
 
15. Weka mkazo kwenye uimara wako. Kuna maeneo ambayo una uimara na maeneo ambayo una udhaifu, unachopaswa kufanya ni kuweka mkazo kwenye uimara wako kuliko kukazana na madhaifu wako. Tafuta wenye uimara kwenye madhaifu wako na wape wafanyie kazi maeneo hayo.
 
16. Jitofautishe na wengine. Ukifanya kile ambacho wengine wanafanya utapata wateja wa kawaida. Ukifanya kile ambacho hakuna mwingine anayefanya utapata wateja wengi na wakipekee. Unapaswa kujitofautisha kabisa na wengine ili kupata wateja wa kipekee, ambao wanakuwa mashabiki wa biashara yako.
 
17. Tumia vizuri muda uliokufa kujifunza na kupiga hatua. Moja ya hitaji la kila mjasiriamali ni kuendelea kujifunza na kupiga hatua zaidi. Lakini mahitaji ya kila siku yanamfanya mtu akose kabisa muda wa kujifunza. Pamoja na majukumu mengi unayoweza kuwa nayo, bado kuna muda mwingi unaokuwa nao ambao huwezi kufanya chochote. Huu ndiyo muda uliokufa. Mfano muda unaokuwa kwenye foleni barabarani au kusubiri huduma fulani, muda unaofanya mazoezi au kufanya kazi zisizohitaji umakini mkubwa. Unaweza kutumia muda huo kujifunza zaidi.
 
18. Soma kwa dakika 30 kila siku. Huwezi kupiga hatua kama husomi na kujifunza, hivyo kila siku tenga angalau dakika 30 ambazo utazitumia kusoma. Na linda muda huo usiupoteze kwa kingine chochote. Hata kama una mengi kiasi gani, usikose kutenga muda wa kujisomea, ni muhimu sana kwa ukuaji wako.
 
19. Jifunze ujuzi mpya unaoweza kuutumia kuikuza biashara yako zaidi. Pamoja na kusoma kila siku, unahitaji kujifunza na kuongeza ujuzi ambao utaweza kuutumia kupiga hatua zaidi kibiashara. Biashara zinabadilika kila siku, ushindani unazidi kuwa mkali, unapaswa kuwa na ujuzi wa ziada ambao utakuwezesha kupiga hatua zaidi.
 
20. Kamata mawazo bora yanayokujia kwenye siku yako kwa kuyaandika chini kabla hujayasahau. Unaweza kufanya hivi kwa kuwa na kijitabu kidogo na kuandika, au pia unaweza kutumia simu yako kuandika mawazo unayokutana nayo. Usikubali wazo lolote linalokujia likupotee.
 
21. Tengeneza na kuza mtandao wako. Huwezi kufanikiwa wewe mwenyewe, unahitaji msaada wa wengine ili kuweza kufanikiwa. Hivyo unahitaji kutengeneza na kukuza mtandao wako wa kibiashara. Utengeneze mahusiano bora na wafanyabiashara ambao wanapiga hatua zaidi ambao watakusukuma na wewe upige hatua zaidi.
 
22. Timiza ahadi unazotoa. Njia rahisi ya kuwapoteza wateja kwenye biashara ni kuwaahidi vitu halafu usivitekeleze. Jijengee sifa nzuri kwenye biashara yako kwa kuwa mtekelezaji wa kila unachoahidi, kwa kufanya hivyo wateja wanakutegemea na kukuamini.
 
23. Tumia nguvu ya HAPANA. Kinachowafanya wengi kushindwa kutimiza ahadi wanazotoa ni kusema NDIYO haraka bila ya kufikiri kwa kina. Kadiri unavyokubali mambo mengi, ndivyo unavyotawanya muda na nguvu zako na ufanisi wako unashuka. Jifunze kusema HAPANA ili kuweka mkazo kwenye yale maeneo muhimu ya biashara yako. Kama kitu siyo muhimu sema HAPANA, na usione aibu waka kuogopa.
 
24. Kuwa kiongozi na siyo meneja. Unapowaajiri watu wakusaidie kazi kwenye biashara yako, kuwa kiongozi kwa kuwahamasisha kuchukua hatua na kuwapa uhuru wa kuweza kutumia uwezo mkubwa uliopo ndani yao. Usiwe meneja ambaye kila kitu kwenye uchukuaji hatua unakisimamia wewe na mtu hawezi kufanya kitu mpaka wewe umwelekeze kwanza. Hilo litakuchosha sana.
 
25. Jifunze kuongea. Mtu anayeweza kuongea kwa kujiamini kuhusu kile anachouza anaaminika zaidi na wateja. Na asiyeweza kuongea vizuri, hata kama anauza kitu kizuri, wateja hawatamwamini sana. Jifunze jinsi ya kuongea vizuri, kwa ushawishi na ubobezi na utawafanya watu waamini kwenye kile unachowaelezea.
 
26. Jifunze kusikiliza. Kuongea tu hakutakusaidia sana kama hutakuwa msikilizaji, jifunze kusikiliza pale wengine wanapoongea. Na siyo unasikiliza tu kwa masikio, bali pia unaangalia lugha za vitendo ambazo mwongeaji anakuwa anatumia, hivi ni viashiria ambavyo vitakueleza mengi zaidi.
 
27. Fanya mazoezi mara kwa mara. Mazoezi ya viungo yana manufaa makubwa sana kwako kiafya na kiufanisi kwenye majukumu yako, hivyo tenga muda wa kufanya mazoezi kila siku. Ukiweza kupata dakika 30 za mazoezi kila siku, utapunguza hatari ya magonjwa kama kisukari na presha, na pia utaongeza ufanisi wako kwenye kazi zako. Pia tafiti zinaonesha watu wanaofanya mazoezi wana kipato kikubwa kuliko watu wasiofanya mazoezi. Hebu anza kufanya mazoezi kila siku na utashangaa jinsi kipato chako kitakavyoanza kuongezeka.
 
28. Ishi maisha bora kiafya. Mazoezi ni hatua moja ya kuwa na afya bora. Hatua nyingine ni ulaji na kujikinga na hatari za magonjwa. Kula kiafya, epuka vyakula vya haraka, epuka vilevi, sigara, madawa ya kulevya na jiepushe na vihatarishi vya magonjwa. Afya yako ni mtaji muhimu sana kwako, isipokuwa imara hutaweza kufanya chochote kikubwa.
 
29. Pata usingizi wa kutosha. Wajasiriamali wengi hujisifia kwa jinsi wanavyoweza kulala kidogo na kufanya kazi masaa mengi. Usiingie kwenye mtego huo, hakikisha unapata muda wa kutosha wa kulala, kulingana na uhitaji wa mwili wako. Miili yetu inatofautiana, kwa wastani masaa nane yanashauriwa kiafya, lakini wapo wanaohitaji machache zaidi ya hayo na wapo wanaohitaji mengi zaidi. Hivyo jua uhitaji wa mwili wako, kama masaa nane ndiyo yanakutosha basi pata masaa nane. Kama masaa 6 au 7 yanakutosha pata muda huo wa kulala. Kitu muhimu zaidi kupima kwako siyo masaa mangapi hujalala, bali umezalisha nini kwenye muda wako. Kadiri unavyopumzika zaidi, ndivyo unavyoweza kuzalisha zaidi.
 
30. Fanya tahajudi au kuandika jarida lako kila siku. Tahajudi ni zoezi ambalo huwa linafanywa na karibu dini na falsafa zote. Kila dini au falsafa watu wana utaratibu wao wa kutuliza fikra zao na kutafakari yale muhimu. Pia unaweza kuandaa zoezi lako la tahajudi kwa kutafakari yale muhimu zaidi kwako. Pia unaweza kufanya zoezi la kuandika jarida lako kila siku, kila siku unakaa chini na kuandika mawazo yako kwenye kijitabu chako, kwa njia hii unapata utulivu wa kipekee kwako.
 
31. Fanya kile unachopenda kufanya. Pamoja na kuwa kwenye biashara, unapaswa kutenga muda wa kufanya kile unachopenda kufanya, ambacho hakihusiani na biashara yako. Hupaswi kuwa mtu wa kufanya na kufikiria kazi muda wote. Tenga muda wa mapumziko ambao utautumia kufanya vile vitu unavyopenda kufanya, ambavyo havihusiani na kazi au biashara yako.
 
32. Wasaidie wengine. Ni rahisi kukazana na malengo ambayo umejiwekea na kuona huna muda wa kuwasaidia wengine. Lakini njia rahisi ya kupata chochote unachotaka ni kuwasaidia wengine kupata kile wanachotaka. Mara kwa mara jitolee kufanya kazi za kijamii, wasaidie wanaoweza na hata biashara yako iwe ina lengo la kuyafanya maisha ya wengine kuwa bora zaidi na siyo tu kupata faida.
 
33. Jiamini. Kadiri unavyokuwa kwenye ujasiriamali, ndivyo hali ya wasiwasi inavyojijenga ndani yako. Unapata hali fulani ya hofu kwamba huenda mafanikio unayopata ni bahati tu na ipo siku mambo yatabadilika na kila mtu atagundua kwamba hukuwa na mafanikio halisi bali bahati tu. Jua hali hii humpata kila anayepiga hatua za mafanikio, na njia pekee ya kuishinda ni kujiamini wewe mwenyewe. Hata kama kuna bahati umekutana nayo, amini juhudi na maandalizi uliyoweka yamekusaidia. Na pia jua hata kama utapoteza kila ulichonacho, utaweza kuanza tena na kufanikiwa.

Wednesday, December 5, 2018

TEGEMEA NGUVU ZAKO NA SIYO HURUMA ZA WENGINE.

Kwenye MAISHA, kwa chochote unachochagua kufanya basi unapaswa kutegemea zaidi nguvu zako, uimara wako na siyo kutegemea huruma za wengine. Kila unapoanza kutegemea huruma za wengine, ndipo unapoingia kwenye shimo zaidi na kukosa uhuru wako.
 
Kila unapokuwa unategemea wengine wafanye kitu ndiyo wewe uweze kupata unachotaka, utajikuta unakosa uhuru wa kuishi maisha yako kwa namna unavyotaka wewe.
 
Kwa sababu yeyote yule unayemtegemea sana, ambaye huwezi kupiga hatua fulani bila yeye, anageuka na kuwa kikwazo kwako, kwa sababu asipofanya kama unavyotegemea, basi wewe hutaweza kupata kile unachotaka kupata.
 
Unapaswa kuyatengeneza maisha yako kwenye msingi huu wa KUJITEGEMEA binafsi kwenye mambo mengi ya maisha yako, kujua namna ya kutumia uwezo mkubwa uliopo ndani yako na kutoruhusu mtu mmoja au watu wachache wawe na maamuzi ambayo yanaweza kuathiri sana maisha yako.
 
Kama maisha yako yanategemea sana maamuzi ya mtu mmoja au watu wachache, utakosa uhuru mkubwa kwenye maisha yako, kwa sababu hata kama mtu huyo hakusumbui, bado ndani yako utakosa amani, kwa sababu hujui ni namna gani mtu huyo anaweza kubadilika siku za mbeleni.
 
Maisha ya uhuru kamili, maisha ya kupata kile unachotaka ni kuweza kutumia uwezo wako mkubwa, kutengeneza maisha ambayo hayana utegemezi mkubwa kwa mtu mmoja au watu wachache. Hilo linajumuisha hata wewe binafsi.
 
Kwa mfano kama kipato chako kinategemea wewe ufanye kazi, bado hujawa huru, kama huwezi kuingiza kipato hata kama wewe hufanyi kazi, unaendelea kuwa mfungwa kwenye upande wa kipato. Lazima uwe na mfumo huru unaoweza kutengeneza kipato iwe unafanya kazi au la.
 
Una uwezo mkubwa sana ndani yako, una nguvu kubwa sana ambazo kama utaanza kuzitumia, utayabadili sana maisha yako, utawafanya wengine wakutegemee wewe zaidi kuliko unavyowategemea wao. Na kadiri wengi wanavyokutegemea wewe, ndivyo unavyokuwa huru zaidi.
 
Na hili ni zuri na muhimu sana kwa wale watu ambao wanapenda kufanya kazi zao za ajira, lakini wanapenda kuwa huru. Kwa mfano mtu anaweza kuwa anapenda kufanya kazi fulani, lakini ataifanya vizuri kama atakuwa ameajiriwa sehemu fulani. Kwa mtu huyu kutumia vizuri uwezo wake mkubwa na nguvu zake, anajitengenezea hali ya kutegemewa kwenye kile anachofanya, kitu ambacho kinamfanya aheshimiwe na kuwa na uhuru zaidi kuliko wale ambao hawategemewi na badala yake wanategemea zaidi kazi wanayofanya

PATA MUDA WA KUKAA MWENYEWE KWENYE CHUMBA KWA UTULIVU. USIJIOGOPE WEWE MWENYEWE.

Mwanasayansi na hisabati Blaise Pascal aliwahi kusema matatizo yote ya binadamu yanatokana na mtu kushindwa kukaa mwenyewe kwenye chumba kwa utulivu.
 
Na hili ni sahihi kabisa, kinachowafanya watu wengi kuingia kwenye matatizo mbalimbali, ni kushindwa kutulia na mawazo yao, kukosa ujasiri wa kukaa na kutafakari chochote walichonacho kwenye mawazo yao.
 
Mimi nakwenda mbali na kusema kwamba watu wengi tunajiogopa sisi wenyewe. Ndiyo maana tukikutana na upweke tu tunakimbia haraka sana.
 
Kama unabisha jiangalie tu tabia yako, huwa unafanya nini pale unapojikuta upo mwenyewe. Lazima utatafuta kitu cha kuchukua muda wako na kushika mawazo yako. Labda utaanza kuchezea simu, utaanza kusoma kitu au hata kuwatafuta watu ambao hukuwa umepanga kuwatafuta.
 
Yote hayo ni kuepuka tu kuwa peke yako, upweke umekuwa hofu kubwa kwetu, hatutaki kabisa kukaa wenyewe, tukiwa tumeachwa na fikra zetu.
 
Rafiki, hebu acha kujiogopa, hebu rudisha urafiki kwako binafsi. Unapopata nafasi ya kuwa na upweke, itumie hiyo kuyatafakari maisha yako, itumie hiyo kujijengea taswira ya kule unakoenda.
 
Usijiogope na kukimbia kila unapojikuta mpweke, badala yake tumia nafasi hiyo kujenga urafiki na wewe binafsi na hata kujijua zaidi na kujua kwa kina kule unakokwenda.

Friday, November 30, 2018

SAFARI YA MAFANIKIO INAANZA NA WATU WENGI SANA. WENGI HUISHIA NJIANI, KWANINI ??


Watu wengi wanakata tamaa kwenye safari ya mafanikio kwa sababu ya kutokujua kwamba mafanikioo yanataka muda mrefu. Katika kipindi cha kutafuta mafanikio yako unatakiwa ujitoe hasa, kuvumilia na kutoa kila ulichonacho hadi ufanikiwe.
Kwa mfano, ilichukua muda wa miaka 11 hadi program ya ‘Microsoft’ ya bilionea mkubwa duniani kuanza kufanya kazi na kuleta mafanikio makubwa. Mafanikio yake hayakutokea tu ghafla kuna miaka ilikataika hapa katikati.
Pia ilimchukua miaka 29 kwa Abraham Lincoln hadi kuweza kuwa Rais wa marekani. Ipo mifano mingi inayoonyesha kwamba mafanikio si kitu cha mara moja tu, unatakiwa kuwekeza muda ili uweze kufanikiwa kwenye mafanikio hayo uyatakayo.
Kwenye akili yako sasa weka wazi, mafanikio ni safari ya muda mrefu. Unatakiwa kabisa utenge miaka angalau kuanzia 5 hadi 15 ya kutafafuta mafanikio yako ya kweli na ya kudumu. Ukikurupuka na kutaka mafanikio ya chapu chapu utakwama.
Kama utakuwa ni mtu wa kutaka mafanikio na halafu ukategemea mafanikio hayo yakatokea ghafla ghafla kwa muda mchache ni rahisi sana kwako kuweza kukata tamaa na kuona ni kitu ambacho hakiwezekani au mafanikio ni ya watu wa aina fulani tu lakini si wewe.

JIWEKEE MUDA WA UKOMO KWA CHOCHOTE UNACHOPANGA KUFANYA.

Mtu mmoja amewahi kusema kwamba jukumu huwa linachukua muda uliopangwa lifanyike. Akimaanisha kama kuna jukumu ambalo linapaswa kufanywa kwa masaa mawili, litakamilika ndani ya masaa mawili. Jukumu hilo hilo likipangwa kufanyika ndani ya masaa matano, litachukua masaa matano.
Huwa tunasukumwa kufanya zaidi pale ambapo muda unakuwa mdogo, na tunaahirisha mambo pale muda unapokuwa mwingi. Ndivyo maana wanafunzi ni vigumu sana kusoma siku za kawaida, lakini mtihani unapokaribia, hamasa ya kusoma inakuwa juu.
Jiwekee muda wa ukomo kwa chochote unachopanga kufanya, na muda huo uwe mfupi kuliko muda uliozoeleka. Kwa kuwa na muda huu na kuufuata, utaweza kujisukuma kufanya zaidi. Kadiri unavyokuwa na muda mfupi wa kutekeleza jambo, ndivyo mawazo ya kuahirisha yanavyopotea kwenye akili yako. Waahidi watu kwamba jukumu litakamilika mapema kuliko kawaida, na tekeleza hilo uliloahidi.

KUWA NA MAMBO YAKO MATANO KWA SIKU AMBAYO UTAYATEKELEZA.

Kila siku unayoianza, ainisha mambo matano muhimu ambayo ukiyafanya siku hiyo yatakusogeza karibu na mafanikio unayotaka kuyafikia. Mambo hayo matano unapaswa kuyafanyia kazi bila ya kujali mazingira yapoje. Inyeshe mvua au liwake jua, hayo matano ni muhimu kwa siku yako na unapaswa kuyafanyia kazi.
Kwa kuwa na tano za siku, unajiweka kwenye nafasi ya kutekeleza yale muhimu na kuepuka kupotezwa na kelele ambazo zimekuzunguka kila mahali.

TUMEZOEA KUSIMAMIWA : KUWA NA MTU WA KUKUSIMAMIA.

Sisi binadamu ni wabaya sana kwenye kujisimamia wenyewe, huwa tunajionea sana huruma na ni rahisi sana kujidanganya. Unaweza kuwa na orodha yako ya siku, umepanga mambo yako matano muhimu na hata kujiwekea ukomo. Lakini katikati ya siku yako ukawa hujisikii kuendelea na yale uliyopanga, ni rahisi kujihalalishia kwamba labda umechoka au ni kitu hakiwezekani.
Lakini unapokuwa na mtu wa pembeni, mtu ambaye jukumu lake ni kuhakikisha umekamilisha uliyopanga na hapokei sababu bali matokeo, utalazimika kufanya kile ulichopanga kufanya.
Tafuta mtu wa karibu kwako, ambaye hakuonei huruma kisha mtake akusimamie kwa karibu ili utimize unachotaka. Kama huwezi kupata mtu wa karibu basi kuwa na kocha au menta ambaye atakusimamia kwa karibu.

JIAMBIE HIVI " NAFANYA SASA , MUDA HUU ".

Kuna wakati unakuwa umeshapanga kabisa nini utafanya na kwa wakati gani. Lakini inapofika muda wa kufanya, mawazo ya kuahirisha yanaanza kukuingia. Unaanza kuona labda hujawa tayari au ni bora kusubiri.
Ni katika wakati kama  huu ndiyo unapaswa kujiambia kauli hii, NAFANYA SASA HIVI, rudia kauli hiyo mara nyingi uwezavyo na utajikuta umeanza kufanya. Kila unapofikiria kuahirisha kufanya kitu, jiambie kauli hiyo kwamba unafanya. Kila unapoanza kujiambia kwambe umechoka, anza kujiambia kauli hiyo.
Kwa kurudia rudia kujiambia kauli hiyo, unaanza kuiamini na kujiamini wewe mwenyewe na kuanza kufanya.

TUNA MIPANGO MINGI SANA NA MIZURI, TATIZO NI UTEKELEZAJI WAKE ???

Mipango ni rahisi sana, kila mtu anapanga na msimamishe mtu yeyote njiani na muulize mipango yake ni ipi, atakupa mipango mizuri sana.

Pamoja na kila mtu kuwa na mipango mizuri, ni wachache sana ambao wanaweza kufanyia kazi mipango hiyo na ikawa uhalisia kwenye maisha yao. Wengi wamekuwa wanabaki na mipango tu, lakini haiwi uhalisia.

Kinachowazuia wengi kutekeleza mipango waliyonayo ni tabia ya kuahirisha mambo. Hii ni tabia ambayo ni asili yetu sisi binadamu, huwa hatupendi kufanya chochote ambacho kinatuumiza au kinataka tuweke kazi.

Huwa tunapenda kutumia muda wetu kwa vitu visivyo na maana. Kwa muda ule ule na kwa nguvu zile zile, huwa tunaona ni bora kutumia kufanya vitu ambavyo vitatupa raha ya muda mfupi, kuliko kufanya vitu ambavyo havina raha ya muda mfupi lakini kwa muda mrefu vina maana.

Kinachowatofautisha wale wanaopata mafanikio makubwa kwenye maisha yao na wale wanaoshindwa siyo bahati wala akili wala fursa. Kinachowatofautisha ni namba wanavyoweza kuishinda tabia ya kuahirisha mambo. 

Wanaofanikiwa na wanaoshindwa wote wanakuwa kwenye mazingira sana, wanakutana na fursa sawa, lakini wale wanaoshindwa huwa wanasubiri wakati wanaofanikiwa wanachukua hatua.

FANYA BIASHARA HIZI UTAPIGA PESA SANA. UTAFANIKIWA SANA.

1. USAFIRI.
Moja ya biashara ambayo inaaminika hasa kwa bara la afrika ikiwa utaifanya kwa utulivu na ukafata misingi yake ni biashara ya usafiri. Hapa unaweza ukawa na kampuni yako ya kusafirishia abiria kutoka sehemu moja na kwenda nyingine.
Kwa sasa hitaji la usafiri bado ni kubwa, kama si mjini hata kijijini. Watu wanataka kusafiri kila siku na kwa bahati mbaya wengi hawana uwezo huo wa kumiliki vyombo vya usafiri. Hii ni mojawapo ya biashara ya kuifikiria kuifanya kama unaweza, kwani itakupa mafanikio sana.

2. AFYA.
Kama pia utajikita na kufanya biashara inayohususha mambo ya afya, basi upo uwezekano mkubwa zaidi wa wewe kufanikiwa sana. Huduma za afya katika maeneo mengi bado hazijafikiwa kisawasawa na zinahitajika kweli.
Hivyo kwa kufanya biashara hii, kama ukifungua hospitali au zahati au duka la dawa, utapata pesa na hapo pia utakuwa imeisaidia jamii. Kikubwa kubali kuzunguka kuangalia ni wapi ambapo ukifanya huduma au biashara hii wewe itakulipa.

3. CHAKULA.
Hakuna mtu asiyekula, hiyo ikiwa na maana ukianzisha biashara ya vyakula na ukaifanya kwa ufanisi mkubwa utafanikiwa. Hapa unaweza ukauza chakula, lakini si maanishi uje na picha ile ya mama ntilie ‘pasee.’
Ukiamua kuja na biashara ya kuuza chakula ifanye kwa ukisasa zaidi. Zipo sehemu bado nyingi zinazohitaji huduma hii ya chakula safi, mazingira safi, lakini hawaipati kwa uhakika kwahiyo unatakiwa ujue jinsi ya kuanza ili uanze kupiga pesa.

4. VIWANDA  VIDOGO  VIDOGO. 
Huwezi  kuendelelea sana kama utaendelea kuwa mlanguzi wa biashara za watu wengine. Changamsha akili na anza mchakato wa kuweka viwanda vidogo vidogo ambavyo vitasaidia wewe kuweza kukupa kipato kikubwa.
Uzuri wakuwa na kiwanda kidogo wewe ndio unakuwa mzalishaji wa kwanza kwa hiyo ni lazima utapata faida kubwa sana. Hapa unaweza ukatengeneza kiwanda chako cha kutengeneza juisi au unga wa sembe na lishe, uamuzi ni wako.

Thursday, November 22, 2018

KILA MTU NA HAMSINI ZAKE. HAKUNA ANAYEJALI SANA MAISHA YA WENGINE.

Maisha ya sasa hivi naweza kusema yamekuwa ni kama ya kuishi kisiwani, watu wamekuwa hawajali sana watu wengine kwa kiasi kikubwa, ukilinganisha na zamani. Kwa sasa ukipata changamoto kubwa wewe jua hiyo ni changamoto yako tu, inabidi ukomae nayo hadi utoke.
Kutokana na hili kuendelea kudumu kunafanya maisha yanazidi kuendelea kuwa magumu sana hadi watu wanakosa msaada ambao ungeweza kuwasaidia. Ubinafsi ambao wengi wanao imekuwa ni kichocheo kikubwa sana cha ugumu wa maisha.

KUTEGEMEA CHANZO KIMOJA CHA MAPATO , HUPELEKEA MAISHA KUWA MAGUMU SANA !

Kutokana na maisha kubadilika na gharama za maisha kupanda karibu kila siku, suala la kutegemea kipato kimoja, ni moja ya chanzo cha maisha kuwa magumu. Watu wengi wanategemea kipato kimoja, zaidi kwa wengi ikiwa ni ajira.
Kwa bahati mbaya kipato kimoja hakiwezi kukidhi mahitaji yote hata iweje. Sasa kwa sababu hiyo ya maisha kupanda mara kwa mara, ni lazima tu ugumu wa maisha uonekane. Hata siku moja usitegemee maisha yako yakawa rahisi kama bado una kipato kimoja.

Saturday, November 17, 2018

TABIA YA FEDHA. FEDHA NI ZAO LA HAMASA.

 FEDHA  ni kama mchumba mwenye wivu, mchumba ambaye anataka muda wote uwe naye, muda wote umfikirie yeye tu. Na mchumba huyu akigundua humfikirii na kumjali yeye anaondoka na kwenda kutafuta wengine wanaomjali na kumfikiria.
Hivi ndivyo fedha zilivyo, kama huna muda nazo hazitakuwa na muda na wewe. kama huzijali na kuzifikiria muda wote zitaenda kwa wale wanaojali na kuzifikiria.

Fedha ni zao la hamasa, chochote ambacho kinakuhamasisha, kile unachopenda kweli, kila ambacho unakifanya muda wote bila ya kuchoka, ndiyo kitu kitakachokuletea kipato kikubwa sana.
Hivyo rafiki, unapofikiria kuhusu fedha, anza kufikiria nini kinakupa hamasa sana, nini unapenda kufanya sasa kisha weka maisha yako yote kwenye kufanya hicho, na fedha hazitakuwa tatizo kubwa kwako.

Tatizo kubwa kwenye hili ni watu huwa wanakosa uvumilivu, wakiona kile wanachofanya kinachelewa kuwaletea matokeo wanayopata, na kuona wengine wakifurahia matunda ya vile wanavyofanya, wanajidanganya kule ndiyo kwenye fedha, wanaacha wanachofanya na kwenda kufanya vitu vingine. Wanahangaika sana, na hawapati fedha walizofikiria kupata. Na hata wakizipata, bado maisha yao yanakuwa na utupu fulani, kwa sababu kile wanachofanya siyo kinachowahamasisha zaidi.

Friday, November 16, 2018

HUDHURIA SEMINA AU WARSHA MBALIMBALI ZA KIBIASHARA UJIFUNZE MBINU MPYA ZA KIMAUZO. DUNIA INABADILIKA KILA SIKU. ACHANA NA MBINU ZA KIZAMANI ZA KIMAUZO.

Inapotokea mbinu zako za kimauzo zimepitwa na wakati huwezi kuendelea kuwapata wateja wengi. Hapa ndipo maana kampuni kubwa zikaja na kitengo cha huduma kwa wateja ili kila siku kuweza kumudu kuboresha huduma ili kuleta mafanikio. Kama kila wakati utaendelea kuwa na mbinu zile zile za kimauzo pasipo kuzibadilisha na kutegemea muujiza utakaokupa wateja wengi, naomba nikwambie kwenye hilo jambo lisahau kabisa. Ni muhimu ukabadilika kwanza wewe na wasaidizi wako.

NINI UFANYE ???
Kila mara pata mafunzo ya jinsi ya kuboresha huduma kwa wateja na unaweza kuyapata kupitia semina au warsha mbalimbali za kibiashara. Pia jenga urafiki na wateja ili wakusaidie kupata wateja wengine zaidi na zaidi ili kufikia mafanikio.

Ndimi  Mwl  Japhet  Masatu, Dar  es  salaam , Tanzania, Afrika  Ya  Mashariki.

EMAIL: japhetmasatu@gmail.com 

Call: + 255 716 924136 ( WhatsApp ) , + 255 755 400128

HUDUMA MBOVU, HUPOTEZA SANA WATEJA.

Huwezi kukwepa kukosa wateja kama una huduma mbovu kwa wateja wako. Unaweza usiwe wewe, hapa wanaweza wakawa ni wasaidizi au wafanyakazi wako  ndio wanaokuharibia pasipo wewe kujua kitu chochote na ukaona uko sawa.
Wengi kwa kushindwa kujua kwamba wanahuduma mbovu ndio wanajikuta ni chanzo cha kuanza kupoteza wateja wengi tena bila kujua. Huduma yako mbovu inaweza ikawa kwenye bidhaa au mazingira au  hata jinsi ya kuwahudumia wateja na wakaridhika.

NINI  UFANYE ?
Hapa kuwa makini sana na mazingira yote yanayoweza kupelekea huduma mbovu ikatolewa, kama wafanyakzi wako, mazingira na bidhaa unazozitoa. Vitu hivyo unatakiwa kuvihakiki mara kwa mara ili visiwe chanzo cha huduma ya hovyo kwako na kupelekea kukosa wateja. 

Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania, Afrika  Ya  Mashariki

+255 716 924136 ( WhatsApp ) , +255 755 400128 
EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

Wednesday, November 14, 2018

KATIKA MAISHA USIBWETEKE NA YALE ULIYOKAMILISHA TUU !!!

Katika MAISHA watu hufurahia zaidi yale waliyokamilisha pekee huku wakiyasahau kabisa yale ambayo hawajayafanya au kuyakamilisha.
 
Pia kitendo cha kuyafurahia yale ambayo umeyafanya na kujiona wewe ni bora zaidi hukufanya uzidi kubweteka na kuachana na yale unayoyakosea katika maisha.

 Hivyo NDUGU yangu MDAU  wangu  katika maisha haya unatakiwa kukumbuka ya kwamba yale uliyoyapanga na kuyakamilisha ni jambo jema sana, ila kama unataka kuwa bora zaidi ya hapo ulipo sasa unatakiwa kushughulika na yale machache yalikuwa ni vikwazo ambayo yamekufanya ushindwe kufanya vizuri zaidi.

Asante sana   kwa   kusoma , Ndimi  MWL   JAPHET  MASATU , DAR  ES  SALAAM, TANZANIA,  AFRIKA  YA  MASHARIKI.

Friday, November 2, 2018

TENGENEZA UHURU KAMILI KWENYE MAISHA YAKO UTAPATA FURAHA YA KWELI

Wapo watu ambao wameajiriwa na wanalipwa mshahara mkubwa sana, kipato chao kinawawezesha kupata chochote wanachotaka, kwa upande wa kipato, lakini bado wanakosa furaha kwenye maisha yao. Na sababu kubwa ni kukosa uhuru wa maisha yao. Kwa sababu kadiri mtu anavyolipwa, ndivyo anavyotumika zaidi. Kadiri kipato cha ajira kinavyokuwa kikubwa, ndivyo majukumu yanakuwa mengi na kutegemewa kuwa tayari na kazi wakati wowote. Mtu hawezi kuchagua afanye nini na maisha yake, ni mpaka aombe ruhusa kwanza.

Uhuru ni kiungo muhimu sana cha furaha, huwezi kuwa na furaha kama huna uhuru.
Na uhuru siyo kwenye eneo la fedha na kazi pekee, bali hata kwenye fikra za wengine. Kama una chuki na wengine haupo huru, hivyo huwezi kuwa na furaha. Kama unashindana na wengine huwezi kuwa huru, kwa sababu muda wote utakuwa unawaangalia wanafanya nini.
Ili kuwa na furaha ya kudumu kwenye maisha yako, lazima uwe na uhuru na maisha yako. Kadiri unavyokuwa huru, ndivyo unavyokuwa na furaha.

UFUNGUO  WA  FURAHA:Tengeneza uhuru kamili kwenye maisha yako, ondoa utegemezi wako kwa wengine au vitu fulani ndiyo maisha yako yakamilike. Hata kama huna kila unachotaka, kitendo cha kuwa huru na muda wako na maisha yako, kinakuwezesha kuwa na furaha ya kudumu kwenye maisha yako.

JENGA MAHUSIANO CHANYA UTAPATA FURAHA YA KWELI KATIKA MAISHA YAKO

Mahusiano yetu na wengine yana mchango mkubwa sana wa namna maisha yetu yanavyokuwa. Kama utakuwa na mahusiano chanya, mahusiano ya kuelewana na wale watu unaojihusisha nao, mahusiano ya kujaliana, mahusiano ya kuwa tayari kutoa zaidi, kwa kuhusiana na wanaotoa zaidi, basi maisha yako yatakuwa ya furaha.

Kitendo cha kujua kuna watu wapo kwa ajili yako, na wewe upo kwa ajili ya wengine kinakufanya uridhike na maisha na kuwa na furaha.
Kwa upande mwingine mahusiano hasi, yasiyo na maelewano, yenye msuguano mara zote, ni chanzo cha kukosa furaha kwa wengi.

UFUNGUO WA FURAHA:Tengeneza mahusiano chanya kwenye maisha yako, chagua wale watu ambao ni wa muhimu kwako na unapenda kuwa na mahusiano bora na wao, kisha wape muda na wajali zaidi. Kuwa tayari kujitoa zaidi kwa ajili yao, na wao watakuwa tayari kujitoa kwa ajili yako.

KUWA STADI UTAPATA FURAHA YA KWELI KATIKA MAISHA YAKO.

Umahiri katika jambo fulani unalofanya kwenye maisha yako. Mtu unakuwa na furaha pale unapojua kwamba kuna kitu unaweza kukifanya vizuri na kikawa na msaada kwenye maisha ya wengine.

Mtu unakuwa na furaha pale unapofanya kitu chenye maana kwako na kuweza kukifanya kwa ustadi na umahiri wa hali ya juu. Hata kama kitu ni kigumu kiasi gani, unapoweza kukifanya vizuri, unajijengea kuridhika ndani yako na hiyo ndiyo inakufanya uwe na furaha ya kudumu.

Ukitaka kudhibitisha hili angalia watu ambao wanapata fedha nyingi bila ya kufanya kazi. Labda wameshinda bahati nasibu au wamepata urithi, maisha yao huwa mabovu sana licha ya kuwa na fedha nyingi. Ni kwa sababu wanakuwa hawajafanya kitu kikubwa kupata fedha hizo, na wengi huishia kuzipoteza.

UFUNGUO  WA   FURAHA: Chagua kitu au eneo utakalokuwa na ustadi nalo kwenye maisha yako, eneo ambalo utafanya vizuri na utaongeza thamani kwenye maisha ya wengine. Kama ni mwalimu fundisha vizuri sana, kama daktari tibu vizuri, kama mwandishi andika vizuri vitu vinavyowasaidia watu. Kadhalika kwenye kilimo, ufundi, uwakili na ujuzi mwingine wowote.

Monday, October 22, 2018

KABLA HUJAINGIA BIASHARA YOYOTE JIULIZE MASWALI HAYA

Yapo maswali mawili muhimu sana kwa kila mtu kujiuliza kabla ya kuingia kwenye biashara yoyote ile. Kwa kujiuliza maswali haya, utaingia kwenye biashara ukiwa na uelewa sahihi, na ukijua ni hatua zipi sahihi kwako kuchukua ili kufanikiwa zaidi kwenye biashara unayofanya.

 (1). NI   NANI  MWENYE  FEDHA  ZANGU?

Nilishakuambia siku za nyuma kwamba hutafuti fedha bali unakusanya fedha. Fedha unayoitaka sasa, ipo kwenye mikono ya mtu mwingine. Hivyo hatua ya kwanza kabisa kwenye kufikiria biashara yako ni kujiuliza nani mwenye fedha zako.
Hapa unahitaji kuwajua wateja halisi wa biashara yako, watu ambao wana shida, wana changamoto, wana uhitaji ambao unaweza kuutimiza. Pia watu hao wana fedha ya kuweza kukulipa wewe kwa kile ambacho unawapa.
Kama hujawajua watu wenye fedha zako, ukianzisha biashara utakuwa unapoteza muda wako. Kwa sababu hata kama unaona wengine wanauza sana, utashangaa unakaa kwenye biashara na hupati mauzo makubwa kama wengine.
Kwa sababu unakua hujajua nani mwenye fedha zako na kumfuatilia huyo zaidi.
Kama uliingia kwenye biashara bila kujiuliza swali hili, kaa chini sasa hivi na jiulize nani mwenye fedha zako? Orodhesha sifa za watu ambao wanaweza kunufaika na aina ya biashara unayofanya, na wenye uwezo wa kulipia kile unachouza.
Ukishajua kwa hakika nani mwenye fedha zako, ni rahisi kumlenga huyo na ukaweza kumhudumia vizuri na wote mkanufaika sana.

(2).JUA  NI  KITU  GANI  UNABADILISHANA  NAO  ILI  WAKUPE  FEDHA.
Baada ya kuwajua wenye fedha zako, unahitaji kujua kitu gani unahitaji kuwapa ili nao wakupe fedha walizonazo. Kwa sababu kila mtu amepata fedha yake ka uchungu, na hivyo hataki kuipoteza. Lazima uwe na sababu kubwa ya kumshawishi mtu akupe fedha zako. Kumbuka akishakupa fedha wewe, hawezi tena kuitumia kwa mambo yake mengine.
Hapa unahitaji kujua kwa hakika ni thamani gani unatoa kwa wateja wa biashara yako. Hapa unahitaji kujua kwa hakika ni mahitaji gani waliyonayo wateja wako ambayo unayatimiza, ni maumivu gani ambayo unayatuliza.
Kama huna sababu ya kutosha, ya kumshawishi mteja akupe fedha yake aliyoipata kwa shida, hutaweza kufanikiwa kwenye biashara yako.
Kwa sababu kumbuka mteja hanunui kwa sababu wewe unauza, wala hanunui kwa sababu anakuonea huruma. Bali mteja ananunua kwa sababu ana uhitaji, ana maumivu ndani yake ambayo hawezi kuendelea nayo na kuna mtu amemshawishi kwamba ana kitu cha kutimiza mahitaji yake au kutuliza maumivu yake.
Hivyo baada ya wewe kujua ni nani mwenye fedha zako, jua maumivu yake ni yapi, kisha mweleze jinsi kile unachouza kinavyoweza kutuliza maumivu aliyonayo.