Monday, October 22, 2018

KABLA HUJAINGIA BIASHARA YOYOTE JIULIZE MASWALI HAYA

Yapo maswali mawili muhimu sana kwa kila mtu kujiuliza kabla ya kuingia kwenye biashara yoyote ile. Kwa kujiuliza maswali haya, utaingia kwenye biashara ukiwa na uelewa sahihi, na ukijua ni hatua zipi sahihi kwako kuchukua ili kufanikiwa zaidi kwenye biashara unayofanya.

 (1). NI   NANI  MWENYE  FEDHA  ZANGU?

Nilishakuambia siku za nyuma kwamba hutafuti fedha bali unakusanya fedha. Fedha unayoitaka sasa, ipo kwenye mikono ya mtu mwingine. Hivyo hatua ya kwanza kabisa kwenye kufikiria biashara yako ni kujiuliza nani mwenye fedha zako.
Hapa unahitaji kuwajua wateja halisi wa biashara yako, watu ambao wana shida, wana changamoto, wana uhitaji ambao unaweza kuutimiza. Pia watu hao wana fedha ya kuweza kukulipa wewe kwa kile ambacho unawapa.
Kama hujawajua watu wenye fedha zako, ukianzisha biashara utakuwa unapoteza muda wako. Kwa sababu hata kama unaona wengine wanauza sana, utashangaa unakaa kwenye biashara na hupati mauzo makubwa kama wengine.
Kwa sababu unakua hujajua nani mwenye fedha zako na kumfuatilia huyo zaidi.
Kama uliingia kwenye biashara bila kujiuliza swali hili, kaa chini sasa hivi na jiulize nani mwenye fedha zako? Orodhesha sifa za watu ambao wanaweza kunufaika na aina ya biashara unayofanya, na wenye uwezo wa kulipia kile unachouza.
Ukishajua kwa hakika nani mwenye fedha zako, ni rahisi kumlenga huyo na ukaweza kumhudumia vizuri na wote mkanufaika sana.

(2).JUA  NI  KITU  GANI  UNABADILISHANA  NAO  ILI  WAKUPE  FEDHA.
Baada ya kuwajua wenye fedha zako, unahitaji kujua kitu gani unahitaji kuwapa ili nao wakupe fedha walizonazo. Kwa sababu kila mtu amepata fedha yake ka uchungu, na hivyo hataki kuipoteza. Lazima uwe na sababu kubwa ya kumshawishi mtu akupe fedha zako. Kumbuka akishakupa fedha wewe, hawezi tena kuitumia kwa mambo yake mengine.
Hapa unahitaji kujua kwa hakika ni thamani gani unatoa kwa wateja wa biashara yako. Hapa unahitaji kujua kwa hakika ni mahitaji gani waliyonayo wateja wako ambayo unayatimiza, ni maumivu gani ambayo unayatuliza.
Kama huna sababu ya kutosha, ya kumshawishi mteja akupe fedha yake aliyoipata kwa shida, hutaweza kufanikiwa kwenye biashara yako.
Kwa sababu kumbuka mteja hanunui kwa sababu wewe unauza, wala hanunui kwa sababu anakuonea huruma. Bali mteja ananunua kwa sababu ana uhitaji, ana maumivu ndani yake ambayo hawezi kuendelea nayo na kuna mtu amemshawishi kwamba ana kitu cha kutimiza mahitaji yake au kutuliza maumivu yake.
Hivyo baada ya wewe kujua ni nani mwenye fedha zako, jua maumivu yake ni yapi, kisha mweleze jinsi kile unachouza kinavyoweza kutuliza maumivu aliyonayo.

No comments:

Post a Comment