Sunday, March 28, 2021

ISHI SASA , ISHI KAMA HUTAISHI TENA.

Kuishi tunaishi mara moja na nafasi hii tunapoipoteza ndivyo tunavyopoteza dhahabu katika mikono yetu. Wakati ambao tunao sasa ni wa thamani mno kiasi kwamba ingetokea ni nafasi ya kupatikana tena basi watu wengi walokwisha yaaga maisha ya dunia wangeomba warudie kuishi tena. Ila haitokei tena hii nafasi ifikapo ukomo wake endapo hatutaweza kuipa uzito kuwa ni fursa ya muda mfupi mno.

Tunapokuta wengine wakiyapoteza maisha huwa tunakumbuka kuwa kumbe maisha yetu ni mafupi na yanakimbia mno kuisha. Ila ikitokea hakuna taarifa zozote za watu kufariki basi huwa tunasahau hilo na kuendelea kuyapoteza maisha yetu kwa vitu ambavyo havitupi nafasi ya kuishi vizuri au kutumia nafasi ya kuwa hai kwa utoshelevu. Maisha huendelea na hukatika kama kamba ilochakaa na kuanzia hapo hakuna tena marudio kuwa utaishi tena au upya.

Nafasi ya kuishi ni adimu mno na ya kuthaminiwa zaidi kuliko chochote kile. Maisha yana maana endapo mtu yu hai ila baada ya hapo mtu husahaulika. Nafasi hii ya kuishi inatupa mwaliko wa kuanza, kuthubutu, kupenda, kusaidiana na kuwa tayari kuandaa njia kwa ajili ya watu wengine ambao watakuja badala yetu sisi. Kila mmoja ambaye huwaza hili kuwa maisha huisha basi hupata mwamko na hamasa kubwa ya kuishi akijiandaa au akiandaa mazingira mazuri kwa watakaokuja nyuma yake.

Unaweza ukawa unapitia mambo magumu katika maisha ila ukitulia na kugundua bado moyo unadunda, pumzi bado unavuta huu ni utajiri mkubwa mno. Maana licha magumu umeyapata ila kama hayaondoi uhai wako basi ni njia bora ya kuimarika, kuwa mstahimilivu na mtulivu ukiwa na falsafa ya kuyaongoza maisha yako kuwa hakuna kitu kitakuwa kigumu wakati wote au hakiharibiwa na muda.

Furahia kila nafasi unayopata ya kuamka na kukuta bado unapumua na mwili unafanya kazi. Furahia hii zawadi kwa kuishi kwa ukubwa, kuishi kwa uzito na kuishi kana kwamba muda ulonao ni mdogo na pengine unachokifanya ndo unakifanya kwa mara ya mwisho haitakuja kutokea tena. Maisha ni haya haya yaendayo yasodumu hivyo thamini kila nafasi ya wewe kuwa hai.

NA KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU , DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.

WhatsApp + 255 716 924136 /  + 255 755 400128 /  + 255 688 361 539

 

HOFU YA WATU WATESEMAJE , ITAUA NDOTO NA MAONO YAKO. KUWA WEWE / BE YOURSELF.

Tunangoja kuishi tukijua kuwa watu wengi wanatufikiria kumbe hakuna anayekufuatilia watu wanahangaika na maisha yao pia. Pia wengi wameshindwa kuanzisha vitu kwa kuhofia namna watu watakavyowasema. Hii hofu imeua ndoto nyingi za watu wasijue kuwa hakuna aliyekuwa anajali au kuwafuatilia. Watu wana asili ya kusahau kadri muda unavyosogea.

Falsafa inatufikirisha namna miaka 100 ijayo watu wanaokuzunguka wengi hawatakuwepo na kumbuko la wengi litasahaulika kabisa. Jinsi ambavyo walowahi kuishi wamesahaulika ndivyo hata sisi tutakavyosahaulika. Kwanini uogope kuishi sasa ukiwa hai, kwanini uogope kutumia kipaji au kwanini uogope kuziishi ndoto zako wakati miaka 100 ijayo hakuna atakayekuwepo ?.

Hofu ya kuwafikiria watu wakati hawakufikirii wewe ni upotevu wa muda katika zawadi ya maisha. Watu wengi wanaishi wakihofu hofu kubadili maisha yao na kupata mafanikio kwa hofu za wale wanaowazunguka. Hili linanyima nafasi ya watu wengi kujitambua kuwa maisha ni ya mtu mwenyewe na kila mtu anapitia changamoto mbalimbali katika maisha kiasi kwamba hawatakuwa wanakuwazia wewe tu masaa yote 24 katika siku.

Anza kuishi, anzisha vitu, weka mpango wa kubadili maisha yako huku ukiondoa hofu kabisa juu ya watu watakuchukuliaje. Ikiwa ni kitu kizuri na kitakuwa na manufaa kwako na wale wanaokuzunguka hata kama si sasa basi ivuke hofu ya watu watasemaje. Usikubali kuishi kwa kuwapendeza watu huku unajiumiza ndani yako. Kuwa huru kuishi katika uhalisia wako, ishi wajue uhalisia wako na hili ndo jambo muhimu kulifanya. Wengi wanaishi maisha ambayo si yao kwa kuogopa watu ingawa wangependa kuishi vizuri kwa nafsi zao.

Kila wakati ambao utakuwa unafikiria kuwa watu sijui watanionaje katika mambo mazuri jikumbushe kuwa miaka 100 watu wote ambao unaona sasa watanionaje hawatakuwepo na pengine na wewe hutakuwepo. Kuhofia hilo ni kupoteza nafasi hii ya maisha ulopata. Ishi kwa uhalisia pasipo kuogopa watu maana hakuna atakayekukumbuka miaka 100 ijayo.

NA   KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU , DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.

 ( WhatsApp  + 255 716924136  ) /  + 255 755 400128  /   + 255 688 361 539 

EMAIL :  japhetmasatu@gmail.com

 

UWEZEKANO WA KUISHI MUDA MFUPI NA KUTENDA MAKUBWA UPO , TUMIA RASILIMALI MUDA VIZURI.

Muda ni rasimali muhimu sana katika kuleta mchango mkubwa duniani. Mtu hupimwa katika muda aloishi na namna katika kuishi alivyohusika katika kuleta mchango au athari fulani katika maisha ya watu. Si urefu wa maisha unaoweza kuleta mchango mkubwa ila ni katika uchache wa siku tuishizo mtu anavyozitumia vizuri kuwa mtu mwenye mchango au athari fulani inayobakia alama ya kudumu kunakothaminiwa.

Historia imebeba maelfu ya watu ambao hawakuishi muda mrefu ila alama walizoacha kwa vitu walivyofanya zimeendelea kudumu vizazi hadi vizazi. Ufupi wa maisha yao ulijenga uhai wa majina yao yaendelee kuishi daima. Muda haukuwa kikwazo kwao ila ilikuwa ni lulu ambayo walijua kuitumia vizuri kama nafasi inayoisha bila habari. Hili liliwasukuma sana kuchukua hatua, kuanzisha vitu na kufanya vitu vingi vinavyoendelea kuwasemea mema na alama njema walizoacha.

Napenda sana kufuatilia muziki wa Reggae na ninaposikiliza nyimbo hizi huwa najifunza kwanza kwa ujumbe uliomo hususani za Lucky Dube na Bob Marley, pili zinatengeneza utulivu wa akili na tatu zimeimbwa na watu ambao walipenda walichokifanya. Bob Marley anahesabika moja ya miamba mikubwa ya waanzilishi walokuwa na ushawishi kupitia muziki huu wa Reggae. Ushawishi wa muziki huu umeenea duniani kote licha Bob Marley kufariki dunia mwaka 1981 akiwa ni kijana wa miaka 36 tu. Unapozungumzia muziki huu huwezi msahau kumtaja huyu mwanamuziki

Maisha yetu ni mafupi na wakati mwingine katika ufupi wa hizi siku huwa hatuzitumii kwa uzito au utoshelevu. Ila watu wenye kupata ufahamu mapema kuwa maisha haya hukatika haraka kama kamba basi hufanya mambo makubwa kwa muda mfupi kwa njia ya kutumia muda wao vizuri kwa utoshelevu wakiweka akili zote kufanya mambo yaachayo alama. Ndivyo hutufundisha na sisi kutumia hii nafasi ya maisha tusojua inaweza kukoma lini kutumia kwa utoshelevu, kujisukuma, kufanya zaidi ya pale ambapo tumekwisha kufanya awali na kuandaa mazingira mazuri kwa ambao watakuja nyuma yetu.

Ili tuweze kutumia nafasi ndogo ya maisha kufanya makubwa kipindi kifupi ni kuanza kujifunza kuchukua hatua mapema, kutoghairisha, kutekeleza haraka iwezekanavyo. Haya mambo matatu ndio yanayofanywa na watu wote ambao huacha alama kubwa ndani ya kipindi kifupi cha maisha yao. Ni watu ambao huchukua hatua mapema, hawaghairishi mambo na tatu ni watu ambao wanatekeleza wanachosema haraka iwezekanavyo iwe mchana au usiku hutaka kuona matokeo.

Maisha tunaweza kuyafanya yawe marefu pale ambapo tunatumia nafasi ndogo hii ya maisha kufanya vitu kwa ukubwa. Tunapojifunza kutopoteza muda katika rasimali hii adimu ndivyo ambavyo tunatengeneza matokeo makubwa kadri siku zinavyoenda. Urefu wa maisha unawezekana kwa kutumia kila dakika na saa kwa kufanya mambo yatakayodumu na kufaidisha wengine kwa wakati wa sasa na ujao.

NA   KOCHA   MWL.  JAPHET   MASATU , DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.

WhatsApp + 255 716 924136  /  + 255 755 400128  /  +  255 688 361  539

 

MCHEZO UITWAO MAISHA.

 

Chochote kile kinaweza kutokea au kumpata yeyote katika maisha yetu ya kila siku. Hii ndilo somo pana la maisha na asili linavyotuandaa kuwa lolote linaloweza kujitokeza bila kujali mtu, cheo au mazingira. Tumekuwa tunaona mfano kifo kinavyoweza kumkuta yeyote yule na wakati mwingine hata bila kutarajia tunasikia habari za vifo vya watu ambao tulifikiria huenda hawakutakia kufa sasa. Hilo ni moja linalojitokeza ambalo linatufundisha kuwa kwa yeyote yule kifo kinaweza kujitokeza.

Maisha ni mfululizo wa matukio ambayo yanaendelea kutokea na kutufundisha kuwa yale ambayo tulikuwa tukiamini hayawezi kujitokeza hujitokeza. Kuna namna huwa tunafikiria sisi kuwa mambo yataenda vizuri kwa kuwa tumejiandaa vizuri ila huwa tunashuhudia namna mambo yanavyoenda vibaya licha maandalizi yalikuwa mazuri. Asili wakati mwingine inatufundisha tuone mambo kwa sura mpya kabisa.

Maisha yetu yanapokaribia nafasi ya ujana na utu uzima huwa ni masomo mengi tunayoendelea kuyapitia kupitia visa na watu. Kuna mambo huwatokea watu wengine na hili linatuzindua akili kuwa hata kumbe watu wengine nao wanapitia magumu, wanaanguka, wanashindwa au wanafeli. Ukijifunza hili utajiandaa kuwa maisha yataenda kufundisha masomo magumu na kutuondoa ujuaji wetu wa mambo.

Falsafa inatuandaa kwa hili kuwa tutaenda kushuhudia mengi ambayo tulidhani hayawezekani kutokea yatakatokea. Hili litagusa pia hata maisha yetu moja kwa moja kuwa mengine ambayo tutafikiria kuwa hayawezi kujitokeza kwetu basi yatajitokeza. Maandalizi ya kuwa mambo yanaweza kwenda tofauti ni muhimu mno ili uepuke kushangaa au kushangazwa na mambo yatakavyokuwa tofauti. Wengi huwa hawaamini hili mpaka pale ambapo mambo hujitokeza na kugundua kuwa maisha mambo hujitokeza si vile tutakavyo sisi ila hujitokeza namna yalivyo yenyewe tu.

Katika kusubiri au kushuhudia wakati unaokuja mambo yaloonekana hayawezekani yakawezekana linaweza kujitokeza hata katika magumu au matatizo ambayo yapo sasa kuja kuwa na majibu wakati ujao. Magumu yalokuwepo jana na kuonekana ilikuwa ngumu kumalizika basi leo yamepata majibu. Ndivyo inavyojitokeza kuwa magumu ya sasa yataenda kupata majibu na njia itapatikana siku zijazo.

Maisha ni mchezo wa ajabu usoacha kutufunza na kutubadilisha namna tulivyokuwa tukichukulia mambo yalivyo.

NA  KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU , DAR  ES  SALAAM , TANZANIA

 (  WhatsApp + 255 716  924 136 / ) /  +  255 755 400128  /  + 255 688361  53 9

EMAIL :  japhetmasatu@gmail.com

KUWA TAYARI KUISHI UHALISIA WAKO , UACHE ALAMA NJEMA.

Maisha yetu mengine huanza pindi tunapomaliza maisha haya ya mwili. Awamu hii ya pili ya maisha ni kuishi katika mioyo ya watu wakikumbuka namna tulivyogusa maisha yao kipindi uhai wetu ulipokuwepo. Nafasi hii ya kushuhudia kila kitu ambacho kimeachwa kama alama tuachayo huchipua pindi ukomo wa maisha yetu ufikapo na hivyo huwa hatuoni namna alama iloachwa bali waloachwa hushuhudia.

Maisha yetu ni alama na nyayo tunazoacha kuwa tulikuwepo wakati fulani wa maisha. Alama za maisha yetu zinabebwa na kumbukumbu ambazo zinaachwa mioyoni mwa watu ambao huwa tayari kubeba masimulizi kwa vizazi vingine. Watu wenye alama njema alama ya matendo yao huchipua na kuendelea kuishi kwa muda mrefu.

Kuishi katika vipawa na vipaji ulivyopewa kwa ukubwa au kutojibakiza ndivyo alama njema inavyoacha katika mioyo ya watu. Jina la mtu atendaye mambo mema hudumu na kukua zaidi. Mtu hukumbukwa kwa vile alivyowagusa watu kwa namna mbalimbali

Moja ya mambo niaminiyo kuwa uwepo wetu wa maisha ni kuacha alama ya vipawa, vipaji, ujuzi na uzoefu kwa kuandaa njia kwa ajili ya watu wengine. Tulipo leo ni kwa sababu ya majitoleo ya watu wengi ambao majitoleo yao hawakuweza kuona matokeo ya mbegu walizopanda, majitoleo yao ndio unafuu ambao tunao sasa na majitoleo yao ni njia ambazo leo tunapita kwa sababu yao. Tupo tuishi na kuacha Dunia katika nafasi nzuri zaidi tofauti na vile tulivyoikuta.

Kuishi bila kujibakiza ni maisha yatakayo moyo, ni maisha ya kujitoa sadaka, ni maisha ya kujisahau wakati mwingine ili uwe daraja kwa watu wengine. Kuacha alama njema ni gharama na hugharimu hata watu maisha yao. Kujitoa usiku na mchana kuishi kikamilifu ni kujikana kuwa hutafanya kila kitu katika maisha haya bali utawekeza nguvu maeneo muhimu katika maisha ili kuandaa njia njema kwa wengine. Yataka moyo, yataka moyo thabiti, yataka ustahimilivu kujitoa na kuishi kitoshelevu.

Alama njema unayoweza kuitengeneza na kutoa zawadi yenye manukato kwa dunia ni kuwa tayari kuishi uhalisia wako, u tayari wa kujimimina kwa vipaji ulivyojaliwa, mawazo, ujuzi, uzoefu, maarifa kuisaidia jamii kujitambua, kukua na kuendelea. Hii alama huyapa maisha ya mtu kuwa marefu hata baada ya kufa kwake. Maisha ya mashujaa ambao tunawasoma na kuwakumbuka ni kwa sababu ya alama za matendo yao yasofutika mioyoni mwetu. Mimi na wewe tuna nafasi sasa tukiwa hai kuendelea kufanya mambo bila kujibakiza tukijitoa kadri tuwezavyo kuifanya Dunia kuwa sehemu salama ya kuishi.

KOCHA   MWL. JAPHET   MASATU , DAR   ES SALAAM

WhatsApp + 255 716924136  /    + 255 755 400128 / + 255 688 361 539

 

Friday, March 26, 2021

NYUMA YA PAZIA , KUNA MAUMIVU MAKALI , SI VILE ULIVYOKUWA UKIFIKIRIA.

Jambo lolote lile unaloweza kuliona kwa wengine unaweza kufichwa uhalisia wake na ukachukulia huenda ni jepesi au watu hao wanaofanya hivyo hawapitii changamoto zozote zile. Ni rahisi sana watu kutamani kuishi kama wengine ila wanapoanza kuishi kama hao watu wanakuja kugundua ukweli kuwa si vile walivyofikiria itakuwa. Unachokiona na unachokutana nacho huenda visiwe vinafanana kabisa na hili limefanya watu wengi wagundue kuwa maisha si vile wanavyoona kwa juu juu bali yana siri kubwa mno.

Unaweza kuona ni rahisi kusikia mtu ambaye kila siku anaamka asubuhi na mapema na kufanya mazoezi bila kuacha ukadhania kujenga nidhamu ya namna hiyo ni vyepesi. Ikiwa huna utamaduni huo na ukajisemea siku basi ngoja nianze kufanya mazoezi kila asubuhi bila kuacha utakuta umeanza siku ya kwanza vizuri, ya pili vizuri, ya tatu unaanza kukutana na vikwazo, ya nne unasema ngoja leo nipumzike, ya tano unapendezwa na mapumziko, siku zinapita hufanyi tena mazoezi. Unapotafakari haya unakuja kugundua kuwa wale wanaofanya mazoezi ya mwili au akili kila siku kwa kufanya matendo kama kukimbia au kusoma vitabu kila siku si rahisi na si wa kubezwa hata kidogo.

Unapopitia mwenyewe kufanya kitu ndivyo unavyoweza kuwa na uzoefu na kuweza kukielezea vizuri katika ugumu wake tofauti na unaposema mambo kwa nadharia au kuyasikia sikia tu. Jamii zetu nyingi hupenda kuona mambo rahisi huku hakuna ambaye ana uzoefu nayo bali ni kwa kusikia au kujifanya kujua ila inapotokea mtu inabidi ahusike kuyapitia ndipo anapokuja kugundua si rahisi kama alivyodhani au kuambiwa na watu wengine.

Wengine wanaweza kusema hiyo biashara unayofanya mbona ni rahisi au kama ni jambo la kuandika au kusoma kitabu mtu anaweza kuona anayefanya ni rahisi. Ila inapotokea mtu huyo aingie kuandika, kusoma au kufanya biashara ndipo anapokuja kugundua namna ilivyo ngumu kufanya hivyo vitu. Kuna msemo unaosema kama ingekuwa mambo rahisi basi watu wengi wangekuwa wameyapata isitoshe ni asili ya binadamu kuishi vizuri na kwa furaha. Ndivyo ambavyo hata njia ya kufanikiwa inavyotamaniwa na wengi ila si rahisi kama vile watu wanavyoingia katika mitego ya kuambiwa toa fedha sasa na utapata mara mbili yake au toa fedha na utajirike haraka. Wengi wameingia katika matatizo kwa kutamani kupita njia rahisi au wakijaribu kurahisisha mambo huku kiuhalisia mambo huwa si rahisi kama yanavyodhaniwa na wengi.

Usiwe mwepesi kuvunja moyo watu au kuchukulia vitu kirahisi hasa kama hujawahi kuvipitia au huvijui kiuzoefu wake. Inawezekana ukijaribu hutaweza kuvifanya kama wengine wanavyofanya.

KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU.

WhatsApp + 255 716924136 /  + 255 755 400128

EMAIL :  japhetmasatu@gmail.com

 

Monday, March 22, 2021

STADI ZA KAZI---DARASA LA SABA ( STD 7 )---KILIMO NA UFUGAJI----NUKUU ZA SOMO---NOTES---KWA SHULE ZA MSINGI---TANZANIA---( PDF )

 

JE , NI ALAMA GANI UTAKAYOIACHA UKISHAMALIZA SAFARI YA KUISHI KWAKO HAPA DUNIANI ?

Mtu akisikia habari za kifo huogopa na kuona maisha hayana maana yoyote. Hususani habari za kifo za wale tunaowajua hutuumiza mno na kutuachia maumivu yasomithilika. Tunaumizwa na kifo kwa sababu kubwa mbili. Moja ni namna watu hao walivyoyagusa maisha yetu kwa namna nzuri kiasi kwamba tungetamani wadumu milele. Pili ni namna tulivyojenga ukaribu nao hao watu na hivyo wanapokufa huwa tunaona ndani yetu limeachwa pengo, ombwe au upweke usopimika. Kifo ni sehemu ya maisha yetu ambayo imekuwapo toka vizazi hadi vizazi.

Kifo ni kufunga kwa ukurasa wa maisha ya mtu ya kimwili. Baada ya kufa kwa mtu kinachoanza kuelezwa ni juu ya matendo aloyaacha mtu nyuma yake au alama alizoacha katika namna mbili. Moja ni alama katika mioyo ya watu, hapa tunaona namna watu walikufa zamani ila bado unazo kumbukumbu zao namna walivyogusa maisha yako kiasi huwezi kuwasahau. Pili ni alama za vitu kama majengo, viwanda, vitabu, picha, nyimbo na kadhalika. Tatu ni watoto walowaacha nyuma baada ya kufa kwa mtu. Hizi ni alama kubwa ambazo hubakia na mtu kuendelea kukumbukwa.

Hatujui lini siku tutakayokufa na ikiwa wanaojua siku ya kufa kwao basi ni wale wenye bahati kupata kugundua kuwa hizi ni dakika zangu za mwisho wa maisha basi huandaa wosia, kuandaa msimamo au wengine huandika hata vitabu. Ila kwa watu wengi kifo hutokea kama ajali wakati mwingine. Mtu hajui hili wala lile maisha yanapotea kupitia ajali, kuvamiwa, ghafla, magonjwa na kadhalika. Hili ndilo lifanyalo kuwa kifo kionekane ni FUMBO. Hatujui ni kwa namna gani tumebakiza siku zetu za kuishi.

Kifo ni njia yetu sote ambayo hakuna aliye hai ataiepuka kuwa ataondoka katika Dunia bila kufa. Kifo kipo na kila mmoja kwa nafasi yake na namna yake atamaliza siku alizopewa za kuishi. Nini kitakachobakia baada ya mtu kufa ndilo jambo la muhimu pia tunapoendelea kuishi na tukiwa tungali bado hatujafikia mwisho wa maisha yetu.

Wengi hatuna utaratibu wa kutafakari ukomo wa maisha yetu maana ni habari zenye kutisha mno, tunaziogopa na huwa hatudhanii kuwa tutakufa. Ukweli ni kuwa hata tusipowazia bado njia ya kifo hatuwezi kuiepuka maana ni njia halisi katika maisha yetu ya kila siku baada ya kuisha maisha haya.

Tukifa ndipo huwa tunaanza kuishi katika mioyo ya watu, watu huanza kutukumbuka baada ya kufa kwetu. Ni wakati ambao watu huanza kukufuatilia juu ya kazi ulizowahi kufanya, urithi uloacha au alama yoyote uloiacha kipindi uko hai. Maisha ya mtu huelezwa sana pindi anapokufa kuliko anapokuwa hai. Wengi watafahamu mengi kukuhusu wewe pale watakaposikia umefariki. Alama unazoacha sasa iwe ni kitabu, biashara, namna ya utu wako ulivyogusa watu ni nafasi ya maandalizi itakayosimulia sana ukishamaliza safari ya kuishi kwako hapa duniani.

Je ni alama gani ukatayoiacha katika nafasi ambayo bado ipo sasa ukiwa hai ?. Swali zito ila litakupa maana kubwa ya kuanza kuishi kitoshelevu.

 
NA  KOCHA   MWL.  JAPHET  MASATU
WhatsApp + 255 716924136 ) /  + 255 755 400 128 
EMAIL :  japhetmasatu@gmail.com

 

TUMEUMBIWA MASIKIO MAWILI NA MDOMO MMOJA. KUWA MSIKILIZAJI SANA KULIKO KUONGEA.

Tumeumbiwa masikio mawili na mdomo mmoja ambapo masikio mawili tusikilize zaidi na mdomo mmoja kuongea kidogo. Wale wanaosikiliza zaidi hupata mengi kupitia wale wanaongea. Kuongea sana ni kujipa nafasi ya kurudiwa na kile unachoongea na kujikuta unachoongea kisiwe halisia na kile unachokifanya. Tafiti fulani zilifanyika na kuonesha kuwa kadri unavyoongea juu ya mipango yako au kitu chochote ndivyo ilivyo nafasi ndogo ya kukifanya au kukitenda. Hili ndo limezalisha na kuwa ukiona mtu ni muongeaji sana basi ni mtendaji kidogo. Watendaji wengi si waongeaji ukilichunguza hili utaona.

Akiba ya maneno ni ya muhimu mno katika zama tuishizo sasa kuliko zile zilizowahi kuwepo. Tunaishi katika mifumo ya kumbukumbu kupitia mitandao ya simu kiasi kwamba yale ambayo tunayaandika au kuyaongea watu huyahifadhi na baadaye huyatumia kama fimbo au hukumu unapokuwa umeyasaliti maneno yako. Watu huwa hawafikirii namna neno huishi zaidi ndani ya wale wanaosikiliza.

Kuongea ni kujiandalia mtego hasa hasa pale unapotaka kuchangia mazungumzo fulani ya mambo. Kuongea sana kunapelekea mtu aanze kuongea vitu visivyo kweli ili wale wanaomsikiliza waendelee kumsikiliza. Watu wengi wamefungwa kwa maneno yao ambayo walishindwa kujizuia kuongea. Kusikiliza kunaepusha migorogoro mingi sana katika maisha ya watu na ndiko kunakozalisha watu kuwa na hekima.

Inaleta maswali mengi kuwa tupo katika zama ambazo kila mtu anasukumwa kuongea, kutoa maoni na tunakosa watu ambao huwa kimya na wasikivu kipindi ambacho kila mmoja anasukumwa kuongea ongea. Utaona namna katika majukwaa mbalimbali ya mtandaoni watu wasivyo na subira katika kuyazungumza mambo au kuyaongea. Kila mmoja anaona atapitwa kuongea juu ya jambo fulani au tukio fulani. Katika kufanya hili watu wengi wamepoteza utulivu wa maisha na kujikuta wanahangaishwa na kile walichokiongea kinapoenda tofauti na namna wanavyoishi sasa.

Huwa ninafaidika sana katika mazungumzo ninapokuwa msikilizaji. Ninapokuwa nasikiliza iwe ni mazungumzo ya watu, mijadala au watu watoa maoni napata mengi mno nilokuwa sijajui kupitia kusikiliza watu wanaozungumza au kuongea. Kusikiliza kunatengeneza yule anayeongea aone anathaminiwa tofauti na mtu mmoja anaongea na mwingine analeta mazungumzo kati kati.

Kama wanafalsafa tujiepushe na kuongea kama watu wengine ambao wanakosa udhibiti wa kujizuia kuongea kwa kila wanachokiona. Pili ni kuongeza nafasi ya kuwa wasikilizaji maana hata katika kusikiliza ndipo kunakozaliwa ufahamu wa mambo. Mtu anayesikiliza vizuri huweza hata kufafanua alichokisikia. Si lazima uongee kwa kila kinachotokea hususani zama hizi tuishizo za usumbufu, kelele na mihemko kila kona.

NA   KOCHA  MWL.  JAPHET  MASATU , DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.
 ( WhatsApp + 255 716 924136  )  /  + 255 755 400 128
EMAIL :  japhetmasatu@gmail.com

 

STADI ZA KAZI---DARASA LA SABA ( STD 7 )--ELIMU YA VIUNGO NA MICHEZO---NUKUU ZA SOMO---NOTES----KWA SHULE ZA MSINGI---TANZANIA---( PDF )

 

UNAPOMALIZA KUTATUA CHANGAMOTO MOJA NI MWANZO WA CHANGAMOTO NYINGINE.

Kutambua kuwa maisha ni mfululizo wa matukio, magumu na masumbuko kunarahisisha zaidi kuyaelewa maisha mbali na yule ajuaye maisha huenda yatakuwa rahisi kadri anavyoishi. Mapambano katika maisha ni mchezo endelevu unaokomea tu pale mtu anapofika ukomo wa maisha yake. Ukiwa hai basi mapambano hayaishi bali hupokezana gumu moja na kuja lingine. Ukweli huu wengi hawapendi kusikia au kuamini ila kadri muda unavyokwenda na matukio katika maisha yanavyojitokeza ukweli huu unaanza kuwa wazi kwa mtu na kujua kuwa ni kweli mapambano hayakomi katika maisha ya kila siku.

Ukirejea maisha yako nyuma kidogo kuna kipindi umewahi pitia cha magumu kweli na hadi ukafikiria huenda gumu hili halitapita au ni gumu zaidi hayatatokea mengine magumu zaidi ya hayo. Ila muda unapopita unakuja kukutana na jambo lingine ambalo ni gumu kuliko lile la awali. Hili hujitokeza katika maisha yetu ya kila siku namna tunavyokabiliana na mambo. Latoka hili laja hili na mzunguko huendelea hivi bila kuachana.

Zipo nyakati za maisha zinazojitokeza ambazo mtu hufikiria gumu linalojitokeza likiisha litampa mapumziko ila isiwe hivyo. Kuna watu wanafikiria kuwa watakapofanikiwa basi matatizo yataisha yote ila hujawahi ona watu licha kuwa wana utajiri ila wanakutana na ugumu wa namna wanakosa muda na familia zao. Kweli utajiri wameupata ila wanapoteza muda wa kuwa na familia kwa sababu ya muda mwingi kupambana na biashara zao. Wangapi umewasikia namna familia zimelaumu kuwa licha baba au mama kuwa na mafanikio ila wanakosa muda kuwa na wazazi wao wapo bize au kutingwa na mambo ya biashara. Hili limechangia watoto kukosa ukaribu na wazazi na hata malezi kuwa hafifu.

Kuna mwingine anaweza kuona akishapata umaarufu basi magumu yataisha ila umaarufu unakuja na gharama zake au magumu yake. Kuna mambo ambayo mtu akifanya ni ya kawaida ila akifanya mtu mwenye umaarufu haiwi kawaida. Hili linawatesa watu wengi walio maarufu kukosa uhuru wa kuishi maisha ya kawaida hata kama wanayatamani kuyaishi. Ila wanakabiliwa na ugumu wa vipi watu watanionaje, vipi watanifikiriaje ?. Maisha haya ni magumu mno kwao na huwa mabaya zaidi pale wanapokutana na hali za kushuka kimaisha au kiuchumi.

Mifano ni mingi namna maisha ni mapambano na mfululizo wa magumu katika kuishi kwetu. Kila panapojitokeza mafanikio basi magumu nayo yapo karibu. Magumu na mafanikio yapo pamoja hayaachani. Mtu anapofanikiwa kwa kitu fulani basi ina maana ni mshindi wa mambo fulani magumu aloyakabili iwe kwa watu kumwona au yeye mwenyewe kuyapitia kimya kimya. Huu ni ukweli wa maisha ambao mtu akiutambua mapema hatachukia magumu au kuyakimbia bali kuyakabili na kuyafurahia maana ni kupitia magumu ndipo palipo na maana ya maisha na mafanikio.

KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU.

WhatsApp + 255  716924136  /  + 255 755  400  128 

EMAIL : japhetmasatu@gmail.com

 

Saturday, March 20, 2021

KWANINI UKIPATA PESA MAWAZO MAZURI YANAPOTEA ?

Naamini umewahi kujikuta kwenye hali hii, unakuwa na mawazo na mipango mizuri sana.

Unapanga vizuri kwamba utakapozipata fedha, basi utakamilisha vizuri mipango hiyo.

Lakini pia unawashangaa sana wale wenye fedha kwa jinsi wanavyozitumia hovyo, unajiambia kama ungezipata basi ungefanya mambo ya tofauti kabisa.

Inatokea na wewe unazipata fedha, na hapo unasahau kabisa mipango mizuri uliyokuwa nayo, unazitumia fedha vibaya mpaka pale zinapoisha ndiyo unakumbuka ile mipango yako mizuri.

Na ukitaka kudhibitisha hilo, angalia wale watu ambao wanapata fedha nyingi kwa wakati mmoja.

Labda ni kushinda bahati nasibu, au kupata mafao au kufanya biashara yoyote ambayo inaleta kipato kikubwa kwa mara moja.

 Wengi huwa kama akili zinahama , wanafanya mambo ya ajabu, na fedha zinapoisha ndipo akili zinarudi na wanaanza kujutia walivyozitumia vibaya.

Siyo kama watu hao akili zao zinahama, bali kinachotokea ni fedha wanazokuwa wamezipata , zimepitiliza kiwango cha fedha walichonacho kwenye akili.

Hivyo akili inashindwa kufikiri kwa usahihi na kufanya kile ambacho ni rahisi.

Wanatumia fedha hizo mpaka zikiisha ndipo akili zinaanza kutafuta fursa za kufanya.

Watu hao hawana tofauti kabisa na wewe, ambaye ukipata pesa mawazo mazuri yanapotea.

Ndio mnafanana.

Umekuwa unajizuia wewe mwenyewe kupata fedha zaidi, kwa sababu kiwango chako cha kifedha kwenye akili ni kidogo.

Umeridhika sana na mshahara unaoupata, au faida unayopata kwenye biashara yako ya sasa.

Na umeyajenga maisha yako kuhakikisha mambo yanaenda hivyo.

Maana angalia hata wale wanaokuzunguka, utaona wote mna viwango vya fedha vinavyofanana.

Mnaishi maisha ya aina moja, hadithi mnazopiga zinafanana na hata changamoto za kifedha kwenu ni zilezile.

Ni mpaka pale utakapoamua kuongeza kiwango chako cha kifedha kwenye akili, ndipo unaweza kutoka hapo ulipo sasa.

Ndipo utakapoweza kuacha kujizuia kupata fedha zaidi ya unavyopata sasa. 

Hili litakuondoa kwenye mazoea na utajisukuma kuchukua hatua zaidi.

Utaanza kuongea hadithi tofauti, utaanza kujichanganya na watu tofauti na utaanza kutafuta taarifa tofauti , ambazo zitakusukuma wewe kuwa zaidi.

 

STADI ZA KAZI---DARASA LA SABA ( STD 7 )----MUZIKI--Kusoma na kuandika Muziki , Utunzi na Uimbaji Nyimbo , Ala za Muziki---NUKUU ZA SOMO----NOTES----KWA SHULE ZA MSINGI---TANZANIA-----( PDF )

 

Sunday, March 14, 2021

MAPUMZIKO NI KAMA KUJICHAJI KAMA BETRI , ILI UREJEE TENA KAZINI.

Maisha yana matukio mengi ambayo yanatuchosha na kufanya miili yetu iwe imeishiwa nguvu wakati mwingine. Tunapopata mapumziko au kulala basi tunajikuta kama tumeongezewa nguvu tena ya kuendelea na kazi. Nafasi ya mapumziko imekuwa ni njia inayofanya watu wapate kuchangamka na kuwa na ari mpya tena. Tunaona namna vipindi vya mapumziko vipo mashuleni, semina, michezo mbalimbali na hata sehemu za kazi ili watu wapate kurejea tena mara baada ya kazi au kufanya jambo kwa muda mrefu.

Watu wanapotoka kutoka katika mapumziko huwa na nguvu za kuendelea na nafasi nyingine ya mambo. Huwa nafurahia sana ninapoona wachezaji wa mpira wanapopata dakika chache za mapumziko na marejeo yao ya dakika nyingine 45 huwa na ari mpya, nguvu na kasi mpya. Hivi ndivyo ilivyo nguvu ya mapumziko inapofanywa kwa kiasi ili kurejesha nguvu.

Zama tuishizo sasa watu huzidisha mapumziko na kufanya zaidi ya mapumziko. Mapumziko haya hupelekea uzembe na uvivu ambao watu hujisahau kuwa faida ya mapumziko ni muda mfupi kisha unarejea kazini. Wengine wamefanya mapumziko ya kazi hadi wamepoteza kazi, wapo ambao wamefanya mapumziko hadi wamesahau tena kurejea kusoma na wapo ambao walifunga biashara wakaishia katika mapumziko ambayo yaliwaletea hasara baada ya faida.

Mapumziko ni sawa na pale ambapo betri limeishiwa chaji basi linachajiwa na likishajaa basi linatumika kufanikisha tena kazi. Likijaaa halafu lisitumike kuna nafasi ya kuharibika baada ya muda kupita. Kitu kinachopumzika muda mrefu huanza kuharibika. Jaribu kuangalia vitu kama magari yakiachwa muda mrefu bila kufanyiwa chochote huanza kuharibika tairi na kutu huwa inaanza kushambulia maeneo ya gari. Mapumziko yakidumu bila kuangalia muda ni kutayarisha kufa kwa kitu.

Fanya kazi kweli kweli ila jipe nafasi fulani ya muda kupumzika kwa lengo kuikuza afya na nguvu na si kufanya ulevi wa mapumziko. Mstoa Marcus anasema “Rest is for recharging, not for indulgence. Take only what is sufficient for your health and vitality. Too much rest—like too much food or drink—defeats its purpose, weakening the body and dulling the spirit”. Ikiwa na tafsiri “Mapumziko ni kwa kujichaji, sio ulevi. Chukua mapumziko kwa kutoshea afya na nguvu. Mapumziko ya kuzidisha ni sawa na ulaji au unywaji ulopitiliza moja kwa moja huondosha fokasi, hudhoofisha mwili na kuitia kiza roho”.

Muda wa mapumziko husisha kutuliza akili yako, kulala kwa muda wa kiasi, kuwa mbali na mitandao, tafuta eneo zuri la asili au fanya matembezi ya maeneo tulivu. Utulivu huu husaidia mapumziko yawe imara na kumsaidia mtu kumaliza likizo au muda wake wa mapumziko akiwa na nguvu na ari mpya ya kurudi ulingoni. Maisha ni mapambano kuna wakati unatoka kidogo kupumzika kupata amsho jipya la kupambana.

KOCHA   MWL.  JAPHET   MASATU , DAR  ES  SALAAM.

WhatsApp + 255 716924136  /  + 255  755 400128

 

 

WAZA SASA , FANYA SASA , IJAYO HAIPO ISIKUSUMBUE SANA.

Wasiwasi au hofu ambazo huingia ndani ya maisha yetu ni pamoja na kufikiria wakati ujao utakuja na mambo gani tusoyajua. Mabadiliko yanayoweza kujitokeza wakati ujao ni chanzo kikubwa cha kutawaliwa na hofu na wasiwasi. Tunajawa na wasiwasi namna maisha yetu ya baadaye namna uchumi utakuwa, afya, magonjwa na mabadiliko mbalimbali ya mambo.

Si rahisi kusema usiwazie wakati ujao ikiwa sasa una mambo magumu unapitia, kipato ni kidogo, misiba inatokea, biashara zinaanguka, umaskini na habari za kutisha kama milipuko ya magonjwa na maeneo mengine yanakabiliwa na vita na njaa. Ni ngumu sana mtu kukuelewa kuwa achana kuifikiria kesho wakati hofu na wasiwasi upo juu ya hali zitakavyokuwa baadaye. Wakati wa sasa huachwa hivi hivi kwa wasiwasi ambao mtu anakuwa anatarajia namna mambo yatakavyokuwa mabaya siku zijazo.

Hofu na wasiwasi ni hali za kawaida zinazotutokea maishani ila zinapokuwa zimezidi hili ni tatizo la udhibiti wetu wa kujua mambo yepi yapo katika uwezo wetu na yepi yalo nje ya uwezo wetu. Habari kuhusu wakati ujao ni jambo usiloweza kulizuia kutokea ila una nafasi ya kuitumia sasa ikaweza kusaidia kukabiliana na mambo yatakavyotokea baadaye. Inawezekana mtu akawa na wasiwasi juu ya maisha yake kiuchumi yatakavyokuwa ila unaloweza kufanya sasa ni kufanya maandalizi ya uchumi wako, kuweka akiba, kuweka dharura na kufanya uwekezaji. Ijayo itakuja na tusiwe na udhibiti nayo ila nafasi ya sasa au wakati wa sasa tunaweza kufanya kitu au jambo.

Kujifunza jambo ambalo hujazoea kulifikiria siku za awali jua itakuwa ngumu sana kuliweza. Hivi ndivyo inavyokuwa ngumu kwa watu wengi kutoacha kuiwazia baadaye na wakapoteza kuitumia kabisa leo. Unajifunza kuipa uzito sasa kwa kujifunza kuituliza akili yako yote kufanya kitu kwa umakini wako wote bila kufikiria kuwa ipo kesho. Weka umakini katika maisha yako ya sasa, furahia mchakato wa maisha sasa bila kufikiria hadi upate kitu fulani siku moja. Ishi kwa wakati wa sasa na ijayo usiiwazie bali ije ikukute unaendelea kuishi kwa kuipa uzito sasa. Wakati ujao ni kiini macho maana unaposema utaikuta ijayo au kesho hutaikuta bali utaihesabu ijayo kama sasa. Kwanini upoteze uzito wa nafasi ya muda ulonayo sasa kwa kuwazia hali isiyo ya kweli bali kiinimacho ?.

Unapoacha kuiwazia ijayo unapata muda wa utulivu wa kufanya kitu kwa umakini na ufanisi. Unapokuwa na wasiwasi mkubwa wakati mwingine hufanyi chochote kile, wengine utakuta hali ya hofu inawafanya washindwe kutuliza akili, wanatetemeka, wanapoteza hamasa maana muda wote wanashindwa kufanya chochote wakitawaliwa na namna mambo siku za baadaye yatakavyokuwa mabaya au hatari. Ukiishinda hii hali unajenga nafasi ya kutumia wakati wa sasa vizuri na unakuwa imara zaidi.

Jifunze kuanzia leo kuwa kwa kila utakachokuwa unakifanya weka akili yako iwe sasa. Hili litakujengea nguvu na kuondoa hofu na wasiwasi wowote kuhusu wakati usio sasa. Mstoa Marcus anasema “Don’t worry about the future. By doing your best today, you’ll build the strength and resources to handle whatever tomorrow may bring”. Hii ikiwa na tafsiri “Usiwe na wasiwasi kuhusu ijayo. Ila Fanya kwa uzuri sasa, hili litakujengea nguvu na rasimali za kutosha kukabiliana na kesho itakavyokuja.

KOCHA  MWL.  JAPHET  MASATU , DAR  ES SALAAM.

WhatsApp + 255  716924136 /   + 255 716  924136


 

HIVI NDIVYO UNAVYOWEZA KUTAJIRIKA-----ANZA HAPO ULIPO.

Utajiri ni kitu ambacho kila mtu anakipenda, kwa sababu fedha ni hitaji muhimu kwenye maisha yetu ya kila siku.

Ila kwenye jamii yoyote ile, ni wachache sana wanaofikia utajiri, kwa sababu wachache hao kuna siri wanazozijua kuhusu fedha na utajiri, ambazo wengi hawazijui.

Je ungependa kuzijua siri hizo ili na wewe uweze kufikia utajiri kwenye maisha yako? Kama jibu ni ndiyo basi kaa hapa, maana umefika mahali sahihi.

Kabla hatujaendelea nikukumbushe kwamba kinachowatofautisha tajiri na masikini siyo umri, kuna matajiri vijana na wazee, na wapo masikini vijana na wazee.

Na wala siyo kiwango cha elimu, kuna matajiri ambao hawajasoma kabisa na waliofika viwango vya juu ambao ni masikini.
Na wala hawatofautiani kwa rangi, kabila au jinsia.

Kwenye kila kundi la watu, kuna matajiri na masikini.

Hivyo kitu pekee kinachowatofautisha matajiri na masikini ni kile wanachojua na hatua wanazochukua.

Hayo mawili tu, WANACHUJUA na WANACHOFANYA.

Hiyo ina maana kwamba kama ukijua kile matajiri wanachojua na ukifanya wanachofanya, lazima na wewe uwe tajiri.

Je upo tayari kujua, ili uweze kufanya na utoke hapo ulipo sasa? Kama jibu ni ndiyo, basi karibu ujue kile matajiri wanajua na kikusaidie kufanya wanavyofanya na uwe tajiri.

Kuna maeneo kumi kuhusu fedha ambayo matajiri wanajua tofauti na masikini na hatua wanazochukua kwenye maeneo hayo ni tofauti na wanazochukua masikini.

Eneo la kwanza ni dhana halisi ya fedha, wanavyoichukulia fedha matajiri ni tofauti kabisa na masikini.

Eneo la pili ni kipato, matajiri wanajua jinsi ya kuingiza kipato hata wakiwa wamelala.

Eneo la tatu ni matumizi, masikini ni wazuri kwenye matumizi na hapo ndipo wanaachwa nyuma.

Eneo la nne ni madeni, matajiri wanajua madeni mazuri na mabaya na wanayatumia kwa umakini mkubwa.

Eneo la tano kutengeneza kipato kisicho na ukomo, vipato vya matajiri huwa havina ukomo.

Eneo la sita ni kuweza kuendelea kuingiza kipato hata wanapokuwa wamestaafu, matajiri wanajua kujiandaa kwenye hilo mapema.

Eneo la saba ni kodi, matajiri huwa wanalipa kodi ndogo kuliko masikini na wanafanya hivyo kisheria kabisa.

Eneo la nane ni kulinda utajiri usipotee, kupata utajiri ni jambo moja, kuuliza usipotee ni jambo jingine ambalo wengi hawalijui.

Eneo la tisa kuwaandaa watoto kuridhi na kukuza utajiri waliotengeneza, matajiri wa kweli wanawaandaa watoto wao vizuri ili mali walizopata zisipotee.

Eneo la kumi ni utoaji, matajiri wanajua utajiri wao siyo wao peke yao, hivyo wamekuwa wanatoa kwa jamii na wanapotoa ndivyo wanavyopata zaidi.

MAAMUZI MAGUMU YANA GHARAMA , NDIO NJIA YENYE MATOKEO BORA KATIKA MAISHA.

Ukiangalia maisha yako utajishukuru kuwa katika maamuzi magumu ulowahi kuyafanya ndio yalokujengea uimara au kukupa mabadiliko makubwa maishani mwako. Ukiangalia unaona namna bila kuamua maamuzi magumu pengine usingekuwepo ulipo sasa. Maamuzi magumu hayaanza kufanyika sasa ila toka zama zilizopita miaka 2000 huko Ugiriki ambapo tunakutana na habari za Mgiriki aitwaye Demosthenes.

Demosthenes alizaliwa mwaka 384 kabla ya Kristu huko Ugiriki ya Zamani. Utoto wake alizaliwa mtu ambaye alikuwa si imara katika mwili wake, alikuwa na tatizo la kutamka au kigugumizi na tatu alipoteza wazazi wake ambapo walezi walipora mali za urithi zote alizoachiwa na baba yake ambazo zilkuwa dola milioni 11 za Kimarekani sawa na shilingi bilioni 25 na milioni 454 kwa sasa. Walezi walichomwachia ni nyumba ndogo tu na pesa wakaondoka nazo. Hali hii alopitia Demosthenes hata leo inajitokeza ambapo watoto wanaachiwa mali na wazazi wao ila ndugu au walezi wanatumia nafasi kudhulumu haki zao.

Maisha ya Demosthenes yangetosha kukata tamaa na pengine kutoona mwelekeo wa siku zijazo. Akiwa katika huo huo umri mdogo kabla ya miaka 20 alifanya maamuzi magumu ambayo yamebakia historia katika maandiko ya Kigiriki na hata leo tunamsoma kujifunza kwake. Maamuzi makubwa matatu aloyafanya ambayo yalimwinua kuwa moja ya wazungumzaji nguli kuwahi kutokea huko Ugiriki huwezi msahau Demosthenes na pia inasemekana ni moja ya waanzilishi wa sanaa ya uzungumzaji Duniani.

Demosthenes alipenda sana uzungumzaji licha kuwa na kigugumizi ila hilo halikuzuia kuamua kujifungia chini ya handaki na kunyoa nusu ya nywele katika kichwa ili asitoke nje. Ndani ya handaki alikuwa akisoma kwa kina vitabu kuhusiana na siasa, tamaduni za kigiriki na maarifa mengi.

Pili aliamua kujifunza kuzungumza huku akiwa na vijipande vidogo vidogo vya mawe mdomoni huku akikimbia. Zoezi hili halikuwa jepesi kwake kuwa unarudia rudia sentensi za kuzungumza huku na vijimawe na unakimbia katika upepo mkali. Maamuzi haya yalichangia kuzalisha mzungumzaji bora kuwahi kutokea Ugiriki. Zoezi lingine alikuwa akizungumza na huku anajitazama katika kioo mara kwa mara.

Maamuzi magumu aloyafanya Demosthenes ni mwaliko wa maisha tunayoishi sasa kuwa ili tuvuke hatua fulani kubwa katika maisha lazima tuwe tayari kulipa gharama ya kufanya maamuzi magumu ambayo yanaweza kutugharimu kwa muda ila yakazalisha matokeo makubwa siku zijazo. Unaweza kuwa unatamani kuwa na maisha bora ila unaogopa kufanya maamuzi magumu kuhusu maisha yako kwa kuanzisha mfumo wa maisha wenye kuhitaji ujitoe, ujitose, ujikaze na usijihurumie ili kuzalisha matokeo bora.

Maamuzi magumu yatakutisha na kukuogopesha sasa ila utakapoweza kuvuka njia ya maamuzi magumu hutabakia mtu wa kawaida. Fanya maamuzi magumu kwa chochote kile ukijua kwa kufanya maamuzi magumu hayo kuna mchakato utapitia utakaokuwa na maumivu ya muda ila wenye matokeo mazuri baadaye. Changamoto ni njia kwa watu wanaishi falsafa na changamoto hazikimbiwi.

KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU , DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.

WhatsApp + 255 716 924136 /  + 255 755  400 128

 

Saturday, March 13, 2021

HUWEZI KUYAPINGA MABADILIKO , LAZIMA YATOKEE NA NDIO ASILI TANGU KALE NA WAKATI UJAO.

Unapoangalia maisha ya ukuaji wa mtoto au mmea utaona namna ukuaji wake ukienda kubadilika kadri muda upitavyo. Mtoto hubadilika umbile lake, hubadilika fikra na kutoka utoto mtu huwa mtu mzima na akawa tegemezi ya watu wengi. Kwa mtu anayeangalia juu juu tu akafikiria alivyomuona mtoto basi hubakia hivyo kumbe mtoto ndani yake ana ujana, utu uzima na uzee ni suala la muda tu mambo hubadilika.

Huwa tunachukulia mambo au matukio yanayotokea kana kwamba ndio mwisho wake kuwa hivyo tusijue asili inafanya vitu vibadilike na hakuna kinachoweza kuwa hivyo hivyo wakati wote. Hili linafanya kuonekana kuwa kile ambacho tunakiona kimekamilika kumbe baada ya muda hakikukamilika ila kina mwelekeo wa kuendelea kubadilika. Mfano kama leo wazee walowahi kuishi miaka ilopita na hawakuwa na mitandao ya kijamii basi kwa wakati wao waliishia kuona njia za kizamani za mawasiliano zingebakia hivyo miaka yote kumbe vitu huenda kubadilika.

Yote ambayo tunayaona sasa iwe ni mifumo ya mitandao, mifumo ya uongozi na kuishi ipo katika ngazi ya ukuaji kama alivyo mtoto na haijakamilika ila inaenda ikibadilika. Miaka 100 ijayo mambo mengi yatakuwa yamebadilika mno kuanzia watu wanavyoishi, mifumo ya mawasiliano, mifumo ya uongozi hadi mifumo ya kidunia inavyojiendesha. Hata itakapotokea watu wa miaka 300 ijayo wakawepo wataona mabadiliko makubwa ambayo huenda sisi tusipate nafasi ya kushuhudia hayo mabadiliko.

Zamani njia za kuwasiliana zilikuwa chache na njia kama ya kusafiri sehemu moja uende kupeleka habari sehemu nyingine sidhani kama walidhani kuwa ipo siku njia za mawasiliano kurahisishwa na kuwa nyingi kama sasa. Siku hizi mawasiliano au kupeleka ujumbe umefanyika kirahisi zaidi kwa njia ya simu, barua pepe, mitandao ya kijamii, luninga na redio. Ikitokea wengine wakirudi sasa na kuishi watashangaa mno kuona dunia imebadilika na si kama walivyoishi huko zamani. Ni somo la asili namna hakuna kitu kimeishia hapo isipokuwa kipo katika ukuaji na mabadiliko.

Kwa kujua hili basi tunahimizwa pia kuona kila mtu ambaye anatuzunguka tusimkatie tamaa yoyote ile awapo hai maana nafasi ya kubadilika ni kubwa kuliko kuona ni hitimisho la yale anayoyafanya. Kuna mifano mingi katika jamii zetu ambapo watu walipoanguka au kufeli kitu fulani tukadhani ndio mwisho wa kufanikiwa kwao ila sivyo ilivyo. Wengi ambao wamepitia kufeli, kushindwa na magumu ndio wenye mafanikio makubwa zaidi katika jamii zetu.

Unapitia magumu ila jua ni magumu yanayopita na hayakumalizii hapo tu isipokuwa yanakuandaa kukupa mabadiliko makubwa. Magumu ni njia nzuri inayozalisha watu bora, imara na wenye nguvu zaidi katika jamii zetu. Mabadiliko lazima yatokee na ndio asili ilivyo tangu kale na wakati ujao. Mabadiliko hayana budi kuja kwa chochote kinachokuwepo sasa. Wengi huwa wanaogopa mabadiliko ila huja hivyo hivyo kwa sababu ni asili inasema hilo. Huwezi kuyapinga mabadiliko maana hakuna kitu kinachoweza kukamilika bila kuendelea kubadilika kila siku. Asili ni mabadiliko na inajitahidi kujiendeleza. Maendeleo na mabadiliko ni mapacha katika asili.

Everything that exists now is a seed of what is to come. Nothing around you is in its final form- Marcus Aurelius

KOCHA  MWL.  JAPHET  MASATU

WhatsApp + 255 716924136 /  + 255 755 400128


 

MAANGUKO KATIKA MAISHA YASIKUKATISHE TAMAA , INUKA NA ENDELEA MBELE.

Inawezekana kweli umedhamiria kuacha tabia fulani au mwenendo fulani wa maisha ila unajaribu na kuangukia tena katika ule ule mtindo wa zamani. Usiumie kwa hilo unalopitia maana kuanzisha vitu vipya ni kazi maana mwili huwa ndo kikwazo cha kwanza kabisa katika safari ya mabadiliko. Utatamani kuanza kitu toka ndani ila mwili utaanza kukupa sababu za kushindwa, kujihisi umechoka kuendelea na hatua za mabadiliko. Hili linawakatisha tamaa watu wengi ambao wamejitoa kutamani kuona wakiacha na mambo wasoyapenda kufanya.

Hutaweza kitu kwa siku moja kikakaa kwa uimara. Utaanza na kuanguka, utainuka na kujaribu tena na tena. Ni vile mtoto anavyoanza kujifunza kutembea huwa haanzi mara moja tu kutembea bali hujaribu kushikilia vitu, kuanza kujaribu mwenyewe huku anaanguka na hadi kuanza kutembea mwenyewe. Ila hadi kufikia kutembea mwenyewe huwa anakuwa amepitia hatua nyingi za kuanguka anguka na kuinuka. Ndivyo hali hiyo apitiayo mtoto katika ukuaji hujitokeza katika maisha ya kila siku.

Utapenda kuishi falsafa na kuanza kuiishi ila unajikuta kuna wakati unashawishika kurejea maisha yako ya kale na hili linawatokea watu wengi. Je urudi nyuma ? au usonge mbele ndo wakati ambao kila mmoja aliyeanzisha safari fulani ya maisha husukumwa kubakia pale pale.  Ukiwa tayari kutaka mabadiliko lazima ulipie gharama ya kukubali kuwa utakutana na hali za kuanguka na kuinuka tena. Ukianguka usikate tamaa kuwa siendelei mbele bali ni kuendelea kujaribu tena na mwisho utaweza.

Si wakati wote yale unayoyajua utayaishi maana kuna muda utayasikia ila unakumbana na kikwazo cha kuyaishi. Ila usikate tamaa ikiwa shauku yako haishuki katika kutamani kuishi kile unachojifunza kila siku. Endelea kujaribu, kujifunza na kuishi falsafa na unapoanguka usirejee maisha ya zamani.

Inuka na endelea mbele kila unapoendelea kujifunza kukiishi kitu. Hili ni jambo la kawaida hujitokeza katika maisha kuwa unapotaka kuishi kitu kipya utakutana na nafasi za kuanguka ila ukianguka inuka na uendelee mbele. Utapata ukinzani wa watu mbalimbali unapojitoa kwa moyo wako wote kuishi maisha yenye kanuni au falsafa.

KOCHA  MWL.  JAPHET  MASATU

WhatsApp  + 255  716924136 /  + 255 755 400128


 

TUTUMIE NAFASI NZURI TUNAZOPATA KABLA YA MAJUTO.

Ni kawaida kwa watu wengi mambo yanapoenda vibaya au tunapoangukia kufanya mambo mabaya au mambo yasofaa au yasokubaliwa na jamii huwa tunajilaumu kwanini tulifanya hayo mambo. Huenda tulifanya hayo mambo sababu ya ujinga, uchanga wetu au katika hasira ila matokeo yanapokuja ndipo huwa tunajilaumu kwanini tuliamua kufanya vile. Ila inaweza isiwe mara kwa mara kujilaumu kwa fursa nzuri au nafasi nzuri zilizowahi kujitokeza katika maisha zikapita bila kuzifanyia chochote tusijue zimebeba kitu kikubwa kwa ajili yetu.

Tunajua kabisa au kuona namna watu fulani wanachokifanya ni kitu kizuri ila hatusemi mpaka pale ambapo wanaacha kufanya au kuishia njiani. Wanapoangukia katika kwenda njia mbaya tunaanza kuwasema au kujilaumu huenda tungewatia moyo au kuwapongeza wangefika mbali. Hili linajitokeza zaidi katika kuathiri watoto pale wanapoonesha mwelekeo mzuri wa vipaji vyao ila wazazi hawawapi pongezi na wao ni rahisi kuvunjika moyo na kuacha kuendeleza vipaji vyao. Ila si kwa watoto hata watu wazima wengi wameishia njiani katika mambo mazuri waloyaanzisha ila waliowazunguka hawakuwaunga mkono.

Mfano mmoja mkubwa ambao unaendelea kujitokeza katika jamii zetu ni kufikiria kuwa kila tulichonacho kitaendelea kuwepo hususani watu wetu wa karibu; wazazi, wenza, watoto, rafiki na wafanyakazi wanaotuzunguka. Nafasi yao ya kuwa nasi huwa tunaichukulia kiwepesi na pengine huwa tuna mipango mikubwa ya kufanya dhidi yao kama kuwashukuru, kupiga nao picha, kufanya mazungumzo na kusikiliza hekima zao, kuwapa tuzo au kuwapongeza ila ngoja ngoja hiyo nafasi hufika kikomo pale wanapohama, kupoteza uwezo fulani au kufa kabisa.

Kuna nafasi inaweza kujitokeza ambapo ulikuwa na nafasi ya kusaidia mtu ila pengine hukuchukulia uzito ikapita na ukasikia matokeo ambayo unajua ungehusika matokeo mabaya yasingetokea. Huenda ni mtu mgonjwa au mtu anahitaji ushauri wako ambapo kwa msaada wako ungeweza kuepusha matatizo kama ya watu kujiondoa uhai na kadhalika. Katika jamii kumekuwepo na matukio kama ya watu kuingia katika vitendo hatarishi, kujikatisha maisha kwa sababu ya watu wanaowazunguka kushindwa kutumia nafasi zao kuwasaidia na huenda wangeepusha mambo mengi yafananiayo na hayo.

Huwa tunasahaulishwa sana pale mambo yanapoenda vizuri na kudhania yataendelea kuwa hivyo siku zote. Hivyo zile nafasi nzuri tunazokuwa tunazipata hatuzipi uzito mpaka pale ambapo zinapita. Unaweza kupata nafasi kubwa ya kuwa mtu mwenye ushawishi na kuna vitu ambavyo unajua kwa nafasi yako ungeweza kufanya na kusaidia watu wengi ila mtu haitumii nafasi mpaka anapokuja kuipoteza. Mstoa Marcus anasema tujilaumu pia pale ambapo nafasi nzuri zinajitokeza ila hatuzitumii zinapita.

Anza leo kutumia nafasi zote nzuri unazokuwa nazo kuhakikisha kabla hazijapotea unakuwa umezitumia vizuri na usijilaumu kwa baadaye. Una nafasi ya kuwa na watu basi ishi nao vizuri, una nafasi ya wazazi basi waheshimu na fanya yale ulotegemea kuwafanyia, una mtu unataka kumpongeza au kumshukuru kwa namna kakusaidia basi mshukuru akiwa hai au tamka ajue hilo. Usije kuanza kujilaumu baadaye kuwa ulikuwa na nafasi zote ila ukaziacha tu bila kufanya chochote.

Nukuu ya Mstoa Marcus ina mengi ya kutufikirisha zama za sasa tuishizo. Nanukuu toka katika kitabu cha MEDITATIONS, “We need to repent not just for the bad things we do, but for the good things we don’t do—such as helping a person in need when we have the opportunity.” Ikiwa na maana “Tunapaswa Kujirekebisha sio kwa Vitu Vibaya Tunavyofanya, Lakini Hata kwa Vitu Vizuri Ambavyo Hatukuvifanya”.

KOCHA   MWL.  JAPHET   MASATU

WhatsApp  + 255 716924136  /    +  255 755400128

    

Sunday, March 7, 2021

JINSI UNAVYOWEZA KUJIJENGEA BAHATI YA MAFANIKIO KWENYE MAISHA YAKO.

Watu wote ambao wanafikia mafanikio makubwa, huwa kuna bahati wanazokutana nazo kwenye safari yao ya mafanikio, japo siyo wote wanaoziona. Na pia bahati hizo haziwafuati kitandani wakiwa wamelala, badala yake wanakutana nazo wakati wanapambana.




Naval Ravikant anasema kuna aina kuu nne za bahati;

Aina ya kwanza ni bahati kipofu, hii ni pale mtu anapokutana na bahati ambayo hakuitegemea kabisa kwenye maisha yake. Mfano unatembea barabarani na kukutana na jiwe la dhahabu, hiyo ni bahati ambayo imekutokea tu, hakuna namna unaweza kujisifu umechangia kuipata.

Aina ya pili ya bahati ni ile inayotokana na mtu kuweka juhudi na ung’ang’anizi kwenye kile anachofanya. Hapa mtu anakuwa amechagua kufanya kitu, lakini anakutana na changamoto na vikwazo ambavyo hajui hata atavivukaje, lakini hakati tamaa, anaendelea kuweka juhudi na baadaye anakutana na fursa nzuri inayomwezesha kufanikiwa. Bahati hii inatengenezwa kwa sababu kama mtu angekata tamaa mapema, asingekutana nayo.

Aina ya tatu ni ile inayotokana na ujuzi maalumu, ambapo mtu unakuwa na uwezo wa kuona kitu ambacho wengine hawakioni. Kuna watu wanaona vitu ambavyo wakivifanyia kazi, vinawapa matokeo makubwa na kwa wengine inaonekana ni bahati. Bahati ya aina hii inaweza kutengenezwa, hasa kwa mtu kujipatia ujuzi ambao wengine hawana.

Aina ya nne ni pale unapojijenga sifa ya kipekee ambapo bahati inakufuata mwenyewe. Aina hii ya bahati ni ngumu kwa sababu mtu unakuwa umejijengea sifa fulani ambayo kwa sasa unaweza usione matumizi yake, lakini siku moja kikatokea kitu ambacho hakuna anayeweza kukifanya, ila wewe kwa sifa uliyonayo, ndiye pekee unayeweza kufanya na hapo ukapata fursa kubwa. Kujenga aina hii ya nne ya bahati, jua ni kitu gani unacho ambacho wengine hawana, kisha kiendeleze na jijengee sifa kwenye kitu hicho. Na ipo siku usiyoijua, watu watakutafuta uwasaidie kwenye kitu hicho na watakuwa tayari kukupa chochote unachotaka.

 

Jinsi ya kujijengea bahati.

Ukiachana na aina ya kwanza ya bahati ambayo inatokea bila wewe kujua, aina tatu za bahati unaweza kujijengea kwenye maisha yako.

Na unaweza kufanya hivyo kupitia kujijengea sifa ya kipekee kupitia kile unachotaka kufanikiwa.

Na sifa ya kwanza muhimu kabisa unayopaswa kujijengea ni kuwa mtu wa kufanya na siyo tu kupanga na kuahidi.

Wengi kwenye maisha huwa wanaweka malengo makubwa, wanakuwa kabia na mipango ya kufikia malengo hayo, lakini inapokuja kwenye kuchukua hatua, ndipo wanaofanikiwa na wanaishindwa wanapotofautiana.

Wanaoshindwa huwa ni watu wa kutafuta sababu kwa nini hawawezi kufanya na hata wanapoanza ni rahisi kuahirisha.

Lakini wale wanaofanikiwa, wanaposema wanafanya, wanafanya kweli, ni watu wa matendo na siyo maneno pekee, siyo watu wa kutoa sababu, bali ni watu wa kutoa matokeo.

Hivyo kama unataka kujijengea bahati itakayokufikisha kwenye mafanikio, chagua eneo unalotaka kufanikiwa na chukua hatua kila siku. Siyo kupanga pekee, bali kuchukua hatua kila siku.

Kwa kuchukua hatua kila siku, unajiweka kwenye nafasi kubwa ya kukutana na bahati kuliko yule asiyechukua hatua kabisa au anayechukua hatua pale anapojisikia pekee.

Kufanya siyo rahisi, hasa kwa namna ambavyo wengi wamejijengea tabia kwenye maisha yao. Hivyo hii ni tabia unayopaswa kuweka juhudi kubwa kwenye kuijenga.

Kwa wengi, kufanya kila siku siyo kitu wanachoweza kujisimamia na wakakikamilisha. Hivyo nimeandaa programu maalumu ya kuwasaidia wale wanaotaka kujijengea tabia ya ufanyaji.

Kwenye programu hiyo, unachagua kitu utakachokifanya kila siku kwa siku 100 bila kuacha. Programu hiyo ina nguvu ya kukusukuma ufanye kitu hicho kwa siku 100 kweli.

Kama ungependa kujijengea tabia ya ufanyaji, basi hii siyo programu ya wewe kukosa, kwani ambao wanaishiriki tayari wanapiga hatua kubwa kila siku.

Usikubali kuendelea kuwaona wengine wakikutana na bahati kwenye maisha yako huku wewe ukijiambia huna bahati. Bahati haiwezi kukufuata kitandani, ila utakutana nayo wakati unafanya.

 

UKIWA NA RAFIKI KAMA HUYU USIMPOTEZE MAISHANI.

Kipimo ninachotumia kujua faida ya kuwa na rafiki maishani mwangu ni yule aliye na utayari wa kunisaidia nipate kukua na kukomaa katika kuyaelewa mambo na kuyachukulia mambo. Ukuaji na kukomaa “growth & maturity” ndio lengo mama la maisha yetu ya kila siku. Kadri tunavyokua na kukomaa kimwili, kihisia, kiroho na kiakili ndivyo tunavyoweza kuyatawala maisha, kujidhibiti na kujizuia. Unapopata rafiki anayekusaidia ujitambue, ukue na kukomaa ni kupata dhahabu katika maisha yako. Wengi wana marafiki ambao hawawasaidii kutimiza hayo mambo mawili; kukua na kukomaa.

Maisha ya mstoa Marcus Aurelius ni maisha ninayoyapenda mno ingawa mstoa huyu alipata wahi kuishi yapata miaka zaidi ya 2000 ilopita. Namna alivyoishi kupitia rekodi ya maandishi yake aloyaandika kwa siri kupitia kijitabu “Meditations” yamekuwa ni msingi mkubwa wa falsafa ya Ustoa duniani kote. Lengo kubwa la kuandika au kufanya tahajudi ambazo zilikuwa zikimzalia tafakari na kuandika kimekuwa ni chanzo kizuri cha miongozo mizuri ya kuishi kifalsafa na kuyaongoza maisha katika utulivu, kiasi, hekima na ujasiri.

Katika kitabu chake cha “Meditations” Marcus Aurelius anaandika katika kifungu kidogo cha maneno kumhusu rafiki yake Rusticus na ndipo nami nimepata mambo machache ambayo tunaweza kujifunza kutoka kwa Rusticus yatakayoweza kutusaidia kukua na kukomaa katika maisha yetu ya kila siku. Marcus anasema “Rusticus showed me that my character needed discipline and development. He taught me not to be led astray by sophists or by speculative, esoteric philosophies. Not to show off, whether in flowery orations, feats of asceticism, or public acts of charity. To speak and write simply, without rhetorical flourish, following the example of his letters. To react calmly when wronged or offended; not to hold grudges; to reconcile with others as soon as they show willingness. To read books deeply, not superficially. He loaned me books from his own collection, and introduced me to the teachings of Epictetus”.

Maana ya maneno hapo juu Marcus Aurelius anasema“Rusticus alinionesha kuwa tabia au mwenendo wa maisha huhitaji nidhamu. Yeye alinifundisha kutotenda yaliyo kinyume, kuepuka kujionesha kwa chochote kile kwa watu. Nizungumze na kuandika kwa maangalifu huku nikizingatia barua zake. Nijifunze kukabiliana na hali zozote za maisha katika utulivu, kutokuwa na kinyongo; ila katika kusuluhisha na watu pindi wanapokuwa tayari. Kusoma vitabu kwa kina, na kuepuka kusoma kwa juu juu. Rusticus aliniazimisha vitabu toka katika maktaba yake, na kunitambulisha na mafundisho ya Epictetus”.Maneno haya anaandika Marcus Aurelius akitafakari namna rafiki yake Rusticus alimwachia mafunzo makubwa ambayo kwa zama tuishizo kumpata rafiki wa aina hii huenda pakawa ni nadra.

Kutoka katika maandishi haya ya Mstoa Marcus tunapata mafunzo makubwa sita ambayo tutagusia na kujifunza kutoka kwa rafiki yake Rusticus.

Nidhamu Kama Nguzo ya Maisha na Maendeleo;

Nidhamu inaanza katika kujisimamia katika ulichopanga kufanya bila kuanzisha visingizio. Hii ni ngazi ngumu kwa wengi maana wanaweza kufanya kazi pale tu wanaposimamiwa na wengine ila wanapokuja kujisimamia wenyewe wanashindwa kufanya hivyo. Nidhamu binafsi kama kujali muda, kujielimisha, kujidhibiti ni mwanzo wa maisha matulivu na kuweza kuendelea katika maisha. Unapokosa uwezo wa kujisimamia ni dalili ya kutokuwa imara katika nidhamu binafsi ambayo ukiweza inakusaidia kukua na kukomaa.

Kuepuka Kusema au Kuweka Mambo Yako Yote Wazi “Usiri”;

Tunaishi katika zama ambazo watu hawana kujizuia kusema au kuweka mambo yao yote hadharani. Usiri umepungua na watu wanatamani kila wanachokifanya hadi visivyopaswa kushirikishwa katika mtandao wanasukumwa kuwashirikisha wengine. Ukikosa usiri katika zama tuishizo ni kukaribisha kukosa utulivu na sio lengo la falsafa hii kuwa uwe mtu unayeshindwa kujidhibiti katika kuyaweka mambo yako mengine katika usiri au udogo “low profile life”. Epuka kusema ovyo bila kufikiri na epuka mambo yako yote kuyaweka wazi.

Kuepuka Kuzungumza Sana;

Usizungumze kila kitu kwa kusukumwa kutoa maoni kwa mambo yote yanayojitokeza katika maisha. Watu wengi huwa hawana akiba ya maneno pale ambapo wanajaribu kuwa wasemaji wa kila kitu kinachojitokeza hasa kupitia majukwaa ya mtandaoni. Rusticus anamwambia Marcus Aurelius ajiepushe na kuzungumza sana maana katika kuzungumza sana kuna kukosea kwingi kuliko mtu asiyezungumza mara kwa mara.

Kupokea Hali Zote Katika Utulivu;

Watu wengi ikitokea wametukanwa, wamesikia habari za misiba, wamesikia habari za hofu wanavurugika kabisa katika hisia na akili. Ni kweli watu hutofautiana katika kupokea habari au kukabiliana na hali mbalimbali ila kwa walio na msingi wa falsafa Rusticus anamwambia Marcus kuwa ajifunze na kuwa mtulivu nyakati zote anapokuwa katika hali mfano kutukanwa, kuudhiwa, misiba, habari za hofu. Unapokuwa na utulivu unajipa nafasi ya kufikiri na kutambua yaliyo katika uwezo wako na yaliyo nje na uwezo wako. Wengi wasio na msingi wa ustahimilivu si wavumilivu wanapokutana na hali mbalimbali katika maisha. Wakitukanwa nao wanataka kujibu au kulipiza matusi, wakiudhiwa wanakasirika.

Kuachilia Vinyongo;

Unapoweka kinyongo unaziba nafasi ya furaha na utulivu. Unapoweka kinyongo unabaki kuteseka na mawazo au picha kuhusu hali fulani au mtu fulani. Huwezi ukatulia ukafikiria vingine bila kumfikiria mtu aliyekutendea vibaya. Huu ni utumwa mkubwa na kukosa utulivu katika maisha. Rusticus anamwambia Marcus ajifunze kuachilia vinyongo. Funzo hili lipo hata kwetu kuwa tuachilie vinyongo ili tuwe huru, tuache nafasi ya kuwa na furaha. Maisha ni zaidi ya vinyongo

Kutafuta Kusuluhisha Migogoro mapema;

Kuomba msamaha na kuhitaji suluhu ya matatizo ni njia safi na yenye maana kwa maisha ya mwanafalsafa. Rusticus anatoa angalizo kuwa unapohitaji kutatua matatizo basi tafuta suluhu mapema na wakati ambao watu wapo tayari kufanya hivyo. Wakati mwingine watu huwa hawahitaji suluhu na hilo ni suala lililo nje ya uwezo wako. Inapotokea suluhu ipo ifanye ili uendelee na hatua zingine katika maisha.

Kusoma Vitabu Kwa Kina;

Rusticus anajitolea hadi kumpa vitabu Marcus Aurelius ili asome na kukomaa. Pia anamtambulisha katika mafundisho ya kifalsafa ya Epictetus. Rafiki anayekuhimiza kusoma vitabu tena kwa kina anakupa msingi mkubwa wa kujitambua, kukua na kukomaa. Angalizo kubwa analotoa Rusticus ni kuwa Marcus asome vitabu kwa kina na kuepuka kusoma juu juu. Kusoma vitabu kwa kina kuhahusisha kusoma kwa kukirudia kitabu, kufanya tafakari, kuishi au kuyajaribu yaloandikwa na hata kuweza kukosoa kitabu. Usomaji wa namna hii unakupa kukielewa kitabu kwa kina zaidi. Kupitia hili kumenifunza kusoma vitabu vingi kwa kuvirudia mara nyingi zaidi kunakonipa nielewe vizuri na kwa kina.

Umpate wapi rafiki kama Rusticus ?. Kama unaye anayefanana na Rusticus hakikisha unamtunza maishani maana hutabaki ulivyo. Utakua na kukomaa unapoendelea kuishi. 

 

KOCHA    MWL.  JAPHET   MASATU , DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.

 ( WhatsApp  + 255 716924136 )    /   +  255 755  400  128  /  + 255 688  361  539