Monday, February 25, 2019

NGUVU YA KUFANYA KWA MALENGO.

Kinachowatofautisha wale wanaofikia ubobezi na wale wanaoishia kuwa kawaida siyo wanachofanya, bali namna wanavyofanya kile wanachofanya. Watu wawili wanaweza kuwa wanafanya kitu kimoja, lakini mmoja akabobea na mwingine asibobee.
Mwandishi anatuambia zipo aina tatu za ufanyaji ambazo zinawatofautisha wanaobobea na wanaokuwa kawaida.
Aina ya kwanza ni kufanya kwa kawaida, hapa mtu anafanya kile ambacho amezoea kufanya kila wakati, hakuna kipya anachofanya na hivyo hawezi kubobea. Hivi ndivyo wengi wanavyoendesha maisha yao, wanaonekana kufanya sana lakini hakuna hatua wanapiga. Hii ni kwa sababu wanafanya kwa mazoea.
Aina ya pili ni kufanya kwa malengo, hapa mtu anafanya kitu kwa malengo, na hivyo anakuwa na hatua anazopanga kupiga zinazomsukuma kufanya zaidi. Katika kufanya kwa malengo mtu anapiga hatua zaidi kwa sababu malengo anayojiwekea yanamsukuma zaidi. Kwenye kufanya kwa malengo mtu anakuwa na sifa nne; moja anakuwa na lengo la wapi anataka kufika, mbili anaweka umakini wake wote kwenye kile anachofanya. Tatu anakuwa na njia ya kujipima na kupata mrejesho wa hatua anazochukua na nne anajisukuma kutoka nje ya mazoea, kufanya vitu vipya ambavyo vinamwezesha kupiga hatua zaidi.
Aina ya tatu ni kufanya kwa makusudi, kama mwandishi anavyoita DELIRATE PRACTICE, hapa mtu anakuwa na kusudi kubwa linalomsukuma kufanya kitu. Hii ndiyo aina ya ufanyaji ambayo inazalisha watu wenye ubobezi wa hali ya juu. Kufanya kwa makusudi kuna sifa kama za kufanya kwa malengo, lakini ina sifa nyingine mbili za nyongeza. Ya kwanza ni eneo ambalo mtu anakuwa amechagua kubobea linapaswa kuwa na wabobezi ambao wanaweza kuangaliwa na mtu akajifunza kwao. Mtu anapoweza kuwaangalia wabobezi na kujifunza kile wanachofanya na namna wanavyofanya, inakuwa rahisi kwake naye kufanya. Sifa ya pili ni kuwa na mwalimu au kocha ambaye anamfundisha na kumsimamia mtu kwenye hatua anazochukua. Kwa kuwa na mtu wa nje anayetoa maelekezo au kupima hatua mtu anazochukua na kutoa mrejesho, kunamfanya mtu apige hatua kubwa zaidi.
Hizo ndizo aina tatu za ufanyaji na aina ya tatu ndiyo mwandishi ameijadili kwa kina sana kwenye kitabu cha PEAK.

SIYO KIPAJI NI JUHUDI.

Kwa  miaka mingi watu wamekuwa wakiamini kwamba kuna watu ambao wamezaliwa na vipaji ambavyo vimewawezesha kufikia kwenye ubobezi mkubwa ana katika maeneo waliyobobea.
Na mifano ipo mingi sana, kwenye utunzi wa nyimbo na upigaji wa vyombo, Morzat anaonekana kuwa mmoja wa watu wenye kipaji kikubwa. Kadhalika kwenye mchezo wa golf, Tiger Woods anaonekana kuwa mchezaji ambao ana kipaji kikubwa kwenye mchezo huo. Na hata michezo mingine na hata kwenye taaluma mbalimbali, wale ambao wamefanikiwa sana wanaonekana kuwa na kipaji kikubwa.
Lakini unapokwenda kuchimba ndani, na kuangalia kwa undani maisha ya wale wanaosemekana wana vipaji, huoni kipaji bali unaona juhudi kubwa na za muda mrefu. Katika mifano niliyotoa hapa, Morzat ambaye anaonena alikuwa na kipaji, alianza kufundishwa kupiga vyombo vya muziki akiwa na miaka minne, ana akawa anafanya hivyo kila siku. Huyu ni mtoto ambaye alikuwa akijua kufanya kitu kimoja tu, muziki. Je utamlinganisha na mtu mwingine anayekuja kujifunza muziki ukubwani?
Ukiangalia kwa Tiger Woods pia, wazazi wake wanakiri kumpa michezo ya kitoto inayoendana na mchezo wa golf tangu akiwa na miezi tisa, huyu ni mtu ambaye tangu anapata utambuzi wake, anajua kitu kimoja tu, golf, je utaweza kumshindanisha na mtu mwingine ambaye amejua mchezo huo baadaye?
Chagua mtu yeyote unayeamini ana kipaji, iwe ni mchezaji, mwanasayansi na hata kiongozi, na angalia maisha yake tangu utotoni, utagundua kuna mazingira ambayo yalimweka kwenye juhudi ambazo zilimwandaa kufikia ubobezi huo. Hata wachezaji wenye ubobezi mkubwa kama Christiano Ronaldo na Messi, ukiangalia utoto wao, wametumia sehemu kubwa kwenye kujifunza mchezo wa mpira. Angalia maisha ya wanasayansi kama Eistein, Newton na wengineo, wote waliweka muda na juhudi kubwa kabla hawajafikia ubobezi ambao wengi wanakuja kuamini ni vipaji vimewafikisha pale walipo.
Hivyo ujumbe kwako rafiki yangu ni huu, unaweza kubobea kwenye jambo lolote lile, kama tu utaweka juhudi ambazo zinapaswa kuwekwa ili kufikia ubobezi. Na kwenye kitabu cha juma hili cha PEAK, tunakwenda kujifunza juhudi sahihi unazopaswa kuweka ili kufikia ubobezi.
Usijiambie tena kwamba huwezi kufikia ubobezi kwa sababu huna kipaji au uwezo. Tafiti zote ambazo zimefanywa kwenye ubobezi zimekuja na jibu moja, wale wanaofikia ubobezi wana uwezo mkubwa sana, lakini ni uwezo ambao upo ndani ya kila mmoja wetu. Kinachotutofautisha sisi na wale waliobobea sana ni kiasi ambacho tumeendeleza uwezo ambao upo ndani yetu.
Uwezo tayari unao, unachohitaji ni juhudi ili kubobea, aina gani ya juhudi utakwenda kujifunza kwenye kitabu cha juma.

Friday, February 22, 2019

JE , WAFAHAMU KILA KIUMBE KINA NGUVU YA UKUAJI NDANI YAKE ? KWANINI USIITUMIE NGUVU ULIYONAYO TAYARI KWA AJILI YA MAFANIKIO YAKO ?

Kwa asili, kila kiumbe kinachozaliwa kina nguvu ya ukuaji ndani yake. Sisi hatuna cha kufanya kukiwezesha kitu hicho kikue, badala yake jukumu letu ni kuondoa vikwazo vya ukuaji.

KILA MTU ANA NGUVU YA MAFANIKIO MAKUBWA NDANI YAKE . ONDOA VIKWAZO VYA MAFANIKIO YAKO.

Kila mtu ana nguvu ya mafanikio ndani yake, kitu pekee anachopaswa kufanyia kazi ni kuondoa vikwazo vya mafanikio yetu. Vitu kama tabia zetu wenyewe, hisia zetu na mengine yanatuzuia tusifikie mafanikio ambayo tayari yapo ndani yetu.
Kwa kifupi, hakuna kikubwa tunachoweza kufanya kuyabadili mafanikio yaliyopo ndani yetu, ni makubwa sana, kinachotufanya tusiyafikie ni vikwazo tunavyotengeneza au kuruhusu viingie kwenye maisha yetu.
Kadhalika kwenye fedha na utajiri, kila mtu tayari ana utajiri ndani yake, kinachomzuia mtu kufikia utajiri wake ni vikwazo anavyokutana navyo au anavyotengeneza kwenye maisha yake.
Hivyo rafiki yangu, kila wakati jiulize swali hili, ni kikwazo gani nimeruhusu au kutengeneza kwenye maisha yangu ambacho kinanizuia kufikia mafanikio makubwa yaliyo ndani yangu?
Ukijiuliza swali hili na kujipa majibu sahihi, utaweza kuifanya safari yako ya mafanikio kuwa rahisi. Utaacha kujitesa na kujiumiza kwa vikwazo ulivyojiwekea au kuruhusu vikuzuie na utakuwa na mpango mzuri kwa mafanikio yako.
Tayari mafanikio unayo, unachohitaji ni kuondoa vikwazo vinavyoyazuia yasije kwako.
Moja ya njia za kuondoa vikwazo vya ukuaji kwako ni kujifunza kwa kujisomea vitabu.

Thursday, February 21, 2019

MUDA WA KUANGALIA TELEVISHENI , KUOGA, KULA TUNAO !! LAKINI LINAPOKUJA SUALA LA KAZI, BIASHARA , KUSOMA VITABU VISINGIZIO VINGI.

Kwenye maisha yetu ya kila siku, vitu vyote muhimu huwa hatuvifanyi mara moja na kuachana navyo, bali huwa tunavifanya kila siku. Na hakuna hata siku moja ambayo tunajiambia tumechoka na hivyo hatufanyi.


Fikiria yale tunayofanya kila siku ili maisha yetu yaende, unakula kila siku, unapumua kila siku, unasafisha mwili wako kila siku, na hata nyumba au nguo zako, unasafisha kila mara.


Lakini inapokuja kwenye kazi na biashara, huwa tunajipa kila aina ya sababu kwa nini tusifanye kwa baadhi ya siku. Huwa tunachukulia kazi na biashara zetu kama kitu cha ziada kwenye maisha yetu na siyo maisha yetu.


Kadhalika vitu kama kujifunza, mfano kusoma vitabu. Utasikia watu wakisema kabisa kwamba hawasomi vitabu kwa sababu hawana muda. Lakini hutawasikia watu hao wakisema wana siku mbili hawajala kwa sababu hawajapata muda.


Kwa kila kilicho muhimu kwenye maisha, huwa tunapata muda wa kukifanya, hata kama tumebanwa kiasi gani.


Hivyo ninachotaka uondoke nacho hapa rafiki yangu ni hiki, chagua vitu ambavyo lazima kila siku utavifanya na uvifanye kweli bila ya kusingizia muda au kuchoka. Na ukiacha vile ambavyo tayari unafanya ili uwe hai, kama kula na kadhalika, ongeza vitu kama kujifunza, kufanya majukumu yako na kukuza vipaji au kile unachopenda.


Kama wewe ni mwandishi basi hakikisha kila siku unaandika, usikubali siku ipite hujaandika. Na wengine kwa nafasi zao za kazi au biashara, hakikisha kila siku kuna kitu unakifanya cha kukufanya uwe bora zaidi.

Sunday, February 17, 2019

KULA MIMEA--NI SIRI YA KUISHI MIAKA ZAIDI YA 100.

Chakula chako kinapaswa kuwa mimea zaidi. Epuka kula nyama na vyakula vilivyosindikwa. Watu wengi walioishi miaka zaidi ya 100 sehemu kubwa ya chakula chao ni mimea. Nyama wanakula kwa kiwango kidogo sana na mara chache.
Ili kuongeza mimea zaidi kwenye vyakula vyako, zingatia mambo yafuatayo;
  1. Kula mbogamboga na matunda mara nne mpaka sita kwa siku. Kwa kila mlo wa siku, kuwa na matunda na matunda.
  2. Punguza ulaji wa nyama, kama unaweza acha kabisa, kama huwezi kula siyo zaidi ya mara mbili kwa wiki na kula kiasi kidogo cha nyama.
  3. Weka matunda sehemu ambayo ni rahisi kuyaona na kuyatumia unapokuwa unaendelea na shughuli zako. Hili litakusukuma kutumia matunda zaidi.
  4. Kula kunde zaidi. Vyakula vya jamii ya kunde vina virutubisho vya kutosha kwa mwili wako, fanya hivi kuwa sehemu kubwa ya chakula chako.
  5. Kula karanga kila siku, vyakula vya karanga na jamii yake, kama korosho na lozi vina mafuta mazuri kwa mwili wako na tafiti zinaonesha vinapunguza hatari ya magonjwa ya moyo.
  6. Kuwa karibu na karanga na vyakula vya jamii ya karanga ili iwe rahisi kwako kutumia mara kwa mara. Unaweza kuziweka kwenye chombo ambacho inakuwa rahisi kwako kutumia.

UWEKE MWILI WAKO KATIKA MWENDO---NI SIRI YA KUISHI ZAIDI YA MIAKA 100.

Mazoezi ya mwili ni siri ya kwanza ya kuishi miaka mingi. Katika utafiti wake, Dan aliweza kuona hili kwa kila aliyeishi miaka mingi. Watu hawa wamekuwa ni watu ambao kila siku miili yao iko kwenye mwendo. Siyo watu ambao wanakaa eneo moja kwa muda mrefu. Na licha ya kuwa na miaka zaidi ya 100, wengi bado walikuwa wanafanya majukumu yao wenyewe.
Na mazoezi ambayo yanakuwezesha kuishi miaka mingi siyo mazoezi magumu sana, bali mazoezi madogo madogo ambayo yanaufanya mwili utumie vyakula unavyokuwa umekula.
Katika kuiishi siri hii ya kuweka mwili kwenye mwenzo, zingatoa yafuatayo;
  1. Ondoa urahisi kwenye maisha yako. Hapa jisukume kutembea na kufanya kitu badala ya kutumia urahisi uliopo. Kwa mfano kama kuna ghorofa unapanda na kuna lifti na ngazi, wewe panda ngazi badala ya lifti. Kama unaangalia tv na uko mbali nayo, kama unataka kubadili chaneli au kuongeza sauti, badala ya kutumia rimoti amka na uende ukabadili mwenyewe. Mazoezi madogo madogo kama haya yanakusaidia sana.
  2. Fanya mazoezi kuwa kitu unachofurahia. Usifanye mazoezi magumu na ya kukuumiza, badala yake fanya mazoezi ambayo unayafurahia, kama kuna eneo la karibu unaloenda, badala ya kutumia gari basi tembea au nenda kwa baiskeli. Kadiri unavyopata nafasi kama hizi za kuupa mwili wako mazoezi, zitumie.
  3. Kuwa na muda wa matembezi kwenye siku yako. Kuwa na matembezi ya peke yako au pamoja na wengine kunaufanya mwili wako kuwa kwenye mwendo.
  4. Kuwa na mkutano wa kutembea. Kama kuna mtu ambaye unataka kuwa na mazungumzo naye, iwe ni ya kikazi, kibiashara au hata ya kindugu na kirafiki, unaweza kutumia mkutano huo kuwa sehemu ya mazoezi. Mnaweza kufanya mazungumzo yenu mkiwa mnatembea eneo tulivu na hii itakuwa msaada zaidi kwenu.
  5. Kuwa na bustani. Kwa kuwa na bustani ambayo unaihudumia kila siku ni zoezi tosha kwa mwili wako. Kupanda, kupalilia na hata kuvuna mazao kwenye bustani yako kunatosha kuupa mwili wako zoezi.
  6. Jiunge na darasa la yoga. Yoga ni mazoezi ya mwili yanayouwezesha mwili wako kuweza kuwa na usawa. Ukiweza kufanya zoezi hili la yoga angalau mara mbili kwa wiki inakusaidia sana.

TENGENEZA FURAHA KILA HATUA UNAYOPIGA KILA SIKU, USISUBIRI MPAKA UFIKE MWISHO

Miaka 2300 iliyopita, mwanafalsafa Aristotle alijumuisha kwamba watu wanatafuta furaha kuliko kitu kingine chochote. Kwamba lengo kuu la kila ambacho tunafanya kwenye maisha yetu, ni kutegemea kupata furaha mwishoni.

Na hili ndiyo linawasukuma watu kuchukua hatua mbalimbali, kuanzia kuboresha afya zetu, kuboresha mwonekano wetu, kupata fedha na hata madaraka ni kwa lengo la kutengeneza furaha kwenye maisha.
 
Lakini sasa tunapofanya furaha kuwa lengo la mwisho, hapo ndipo tunapojiangusha. Kwa sababu wengi wanafika mwisho wa kile walichofikiri kitawapa furaha, lakini hawapati furaha ambayo walifikiria wangeipata.
 
Hivyo njia bora ya kuipata furaha, siyo kusubiri mpaka mwisho wa kile tunachofanya, bali kutengeneza furaha wakati unakifanya.
 
Kama unataka furaha ya kweli kwenye maisha, basi usisubiri mpaka mwisho wa kile kitu unachofanya ndiyo uwe na furaha, badala yake tengeneza furaha kwenye kila hatua unayopiga. Furaha inapaswa kuwa matokeo ya kile unachofanya kila siku, na siyo kusubiri mpaka ufike mwisho.
 
Na hili ndiyo tunakwenda kujifunza kwa kina kwenye kitabu cha juma hili.
 
Tafiti zinaonesha kwamba furaha siyo kitu kinachotokea kwa bahati na wala siyo kitu ambacho fedha inaweza kununua au madaraka kulazimisha. Furaha haitegemei matokeo ya nje badala yake inategemea jini tunavyotafsiri yale yanayotokea.
 
Furaha ni hali ambayo inapaswa kuandaliwa, kutengenezwa na kulindwa na kila mtu, kwa kuwa na tafsiri sahihi ya kila kinachoendelea kwenye maisha yako.
 
Ni kwa kujihusisha moja kwa moja na kila kinachoendelea kwenye maisha yako, kiwe kizuri au kibaya ndiyo tunapata furaha. Siyo kwa kukimbia au kutoroka yale yanayotokea au kujaribu kuikimbiza furaha, bali kuyaishi maisha yako kwa namna yalivyo, ndiko kunakokuletea furaha.
 
Hivyo jibu fupi la kuwa na furaha kwenye maisha yako ni kujihusisha moja kwa moja na maisha yako na kupokea kila kinachokuja kwako, iwe kizuri au kibaya.

Tuesday, February 12, 2019

WEKA KIPAUMBELE KWA FAMILIA--NI SIRI YA KUKUWEZESHA KUISHI ZAIDI YA MIAKA 100.


Wote ambao wameweza kuishi kwa miaka zaidi ya 100, wamekuwa na kipaumbele kikubwa kwa familia zao. Wengi wanakuwa wanaishi na familia zao, na hata wale ambao wanaishi wenyewe, wana muda wa kuwa pamoja na familia zao. Tafiti zinaonesha wazee ambao wanaishi na watoto wao wanaishi kwa muda mrefu kuliko wale wanaoishi wenyewe au wanaoishi kwenye vituo vya kulea wazee.

Familia ndiyo msingi mkuu wa maisha bora, ya kiafya na mafanikio. Wale wanaoweka kipaumbele cha kwanza kwenye familia wanakuwa na maisha marefu.

Mambo muhimu ya kuzingatia ili kuweka kipaumbele kwa familia;

Weka mazingira ya kuwa karibu na familia. Kwa kuishi kwenye nyumba moja kunawafanya muwe karibu zaidi kama familia. Pia kuishi kwenye nyumba ambayo ni ndogo, ambayo wote mnaweza kuonana kila siku kuna manufaa zaidi.
Kuwa na utaratibu wa familia, utaratibu ambao unawaleta pamoja. Mfano kuwa na mlo mmoja kila siku ambao mnakula kwa pamoja kama familia kunawafanya kuwa karibu kuliko pale ambapo kila mtu anakula kwa muda wake.
Tengeneza eneo la kumbukumbu ya familia. Mnaweza kuwa na chumba au eneo ambalo kumbukumbu mbalimbali za kifamilia zinatunzwa. Mnaweza kuweka picha za matukio mbalimbali ya kifamilia. Mtu anapokuwa kwenye eneo hilo anapata kumbukumbu ya umoja wenu wa kifamilia.
Weka familia yako mbele. Tenga muda wa kukaa na wale wa muhimu kwako, watoto wako, mwenza wako na hata wazazi wako. Mahusiano bora yanajengwa kwa muda na kujali.

Saturday, February 9, 2019

TUSIOGOPE WALA KUKIMBIA MAGUMU TUNAYOPITIA . NI KIPIMO CHA UWEZO MKUBWA ULIOPO NDANI MWETU.

Mara nyingi tumekuwa tunakwepa magumu kwenye maisha yetu, tumekuwa tunaomba tusikutane na magumu, kwa sababu tunaona magumu ndiyo kikwazo cha sisi kuwa na maisha tunayoyataka. Lakini hilo siyo sahihi, kama tusingekutana na magumu kabisa kwenye maisha yetu, maisha yangekosa maana na tusingeweza kuwa watu ambao tumekuwa sasa.
Magumu ambayo tumekutana nayo kwenye maisha ndiyo yametufanya tuwe watu ambao tumekuwa sasa. Hivyo badala ya kukataa na kukimbia magumu, tunapaswa kuyakaribisha kwa mikono miwili. Kwa sababu kupitia magumu ndiyo tunakua, na ndiyo tunafikia uwezo mkubwa uliopo ndani yetu.
Kufukuzwa au kukosa kwako kazi huenda kumekufanya ukaweza kuanza biashara yako. Kusumbuliwa kwenye mahusiano yako ya mwanzo na yakavunjika ndiyo kumekupelekea kutengeneza mahusiano mengine bora. Na hata kupata hasara na kufa kwa biashara yako ya mwanzo kumekuwa funzo la wewe kufanikiwa kwenye biashara nyingine.
Tusiogope wala kukimbia magumu, na wala tusiombe kutokukutana na magumu. Badala yake tuombe kuwa imara zaidi ili kuweza kukabiliana na kila gumu tunalokwenda kukutana nalo.

NGUVU YA FURAHA KATIKA SAFARI YA MAFANIKIO.

Wengi wamekuwa wanafikiri kwamba wakifanikiwa ndiyo watakuwa na furaha. Lakini ukweli ni kwamba furaha ndiyo inaleta mafanikio.
Mwandishi  Dean anatushirikisha hatua muhimu za kuchukua ili kujijengea furaha ambayo itatuwezesha kupata mafanikio makubwa;
  1. Jua nini maana ya furaha kwako, kinachokupa furaha wewe siyo kinachowapa furaha wengine.
  2. Ishi kwenye wakati uliopo saa, siyo wakati uliopita wala wakati ujao.
  3. Acha kufikiria sana kuhusu vitu, hasa vile ambavyo hakuna hatua unazoweza kuchukua.
  4. Angalia upande chanya wa kila jambo, hata kama jambo ni baya kiasi gani, lina upande ambao ni mzuri, angalia huo.
  5. Linda amani na utulivu wako wa ndani, ondokana na hali zote hasi.
  6. Elewa kwamba kuteseka ni kuchagua, chagua kutokuteseka.
  7. Pokea kushindwa kwa mikono miwili na chukua hatua ili kuwa bora zaidi.
  8. Usiwe na kinyongo na yeyote, samehe kila mtu.
  9. Usiweke matarajio makubwa na kutegemea kila kitu kitaenda kama ulivyopanga.
  10. Shukuru kwa kilichopo mbele yako.
  11. Usiridhike na kile ulichozoea, usifanye mambo kwa mazoea.
  12. Kuwa sehemu ya kitu kikubwa, jijenge zaidi kiroho na kiimani.

Friday, February 8, 2019

MVUTO NA USHAWISHI KATIKA SAFARI YA MAFANIKIO.

Mvuto na ushawishi ni vitu viwili ambavyo kila anayetaka kufanikiwa na kutengeneza kipato kikubwa anapaswa kuwa navyo. Dean anaita vitu hivi viwili kichocheo cha utajiri, vikikosekana huwezi kufikia mafanikio makubwa na utajiri.
 
Mvuto na ushawishi ni njia nyingine ya kusema MASOKO NA MAUZO. Kila tunachofanya kwenye maisha ni masoko, na kila kinachotuingizia kipato ni mauzo.

Hivyo tunaweza kusema kazi zetu kubwa kwenye maisha ni mbili, MASOKO NA MAUZO. Tunapaswa kujiweka kwa njia ambayo watu wayajua uwepo wetu, na pia tuweze kuwashawishi watu hao kutupa kile ambacho tunataka watupe.

Katika kuboresha masoko na mauzo kwenye biashara zetu, kazi zetu na hata maisha yetu kwa ujumla, Mwandishi Dean anatushirikisha hatua zifuatazo za kuchukua;

------Kuwa muwazi na mwaminifu mara zote. Uaminifu unalipa.
------- Kuwa wewe na kuwa na hamasa, usijaribu kuingiza kuwa mtu mwingine.
--------Amini kwenye utele na siyo uhaba, amini kuna wingi wa chochote kwa ajili ya kila mtu.
------Wape watu kile wanachotaka na siyo wanachohitaji.
-----Tumia hadithi, watu wanaelewa na kusukumwa zaidi na hadithi na mifano kuliko maelezo pekee.
------Usiwe mwongeaji sana, ukishaeleweka nyamaza.
Kuwa na msukumo wa ndani wa kile unachofanya.
-------- Endelea kutengeneza mahusiano na wale ambao unawauzia au wameshakubaliana na wewe.
-----Tengeneza mtazamo wa shukrani.
-------Zingatia zaidi kujenga mahusiano kuliko kipato, fanya kile ambacho kitaboresha mahusiano yako na unayetaka kumuuzia au akubaliane na wewe.

MWAMSHE SHUJAA ALIYE NDANI YAKO.

Kila mmoja wetu ana shujaa aliye ndani yake. Shujaa huyu ni uwezo mkubwa na wa kipekee ambao mtu anao, uwezo usio na ukomo na ambao hakuna mwingine anao hapa duniani.

Njia ya kumwamsha shujaa aliye ndani yako ni kujijengea kujiamini. Tatizo la wengi ni kutokujiamini, kushindwa kusimamia kile wanachotaka, hasa pale ambapo wengine hawakubaliani nao.

Katika kujijengea kujiamini, zingatia vitu vitatu muhimu; uthubutu wa kufanya kitu kipya, dhamira ya kufanya kitu hicho na kutumia uwezo wa ndani yako kufikia kile unachotaka kufikia.

Watu wengi hawajui kwamba ndani yao wana uwezo mkubwa wa kufanya chochote wanachotaka. Wengi huangalia nje na kukosa msaada. kama utaanza kuangalia ndani yako utapata msaada mkubwa kwako kufika unakotaka kufika.

TENGENEZA HADITHI YENYE NGUVU KWAKO.

Kila mmoja wetu kuna hadithi ambayo anaiishi, hadithi ambayo umekuwa unajiambia kila siku na imekuwa kikwazo kwako kupiga hatua. Kwa mfano kama umetokea familia masikini na huna elimu, hadithi yako inaweza kuwa kwamba wewe huwezi kufanikiwa kwa sababu umetoka familia masikini na huna elimu kubwa.
Lakini hadithi hiyo ni uongo, ni kweli unaweza kuwa umetoka familia masikini na huna elimu kubwa, lakini hicho siyo kinachokuzuia kufanikiwa. Wapo wengi waliotoka kwenye umasikini mkubwa kuliko wako na hata hawakupata elimu kabisa lakini wamefanikiwa.
Hivyo badili hadithi inayokuzuia kufanikiwa na tengeneza hadithi mpya ya mafanikio yako ambayo itakusukuma kufanikiwa zaidi. Hadithi yako ya mafanikio iguse yale maeneo ambayo una uimara na uyatumie kama sababu ya wewe kufanikiwa.
Hadithi yako mpya iwe ni kinyume kabisa na ile iliyouwa inakuzuia. Ukishaandika hadithi hii jiambie na kujikumbusha kila siku mpaka iwe sehemu ya fikra zako.

MSINGI MKUU WA MAFANIKIO YOTE.

Changamoto kubwa ya zama hizi ni kwamba kila mtu anakwenda kasi, lakini cha kushangaza hajui anakwenda wapi. Kila mtu yupo bize kila siku, anaamka asubuhi na mapema na kuchelewa kulala, lakini hajui wapi anayapeleka maisha yake.

Haijalishi unakwenda kiasi gani, kama hujui unakokwenda, kasi uliyonayo inakupoteza tu.

Msingi mkuu wa mafanikio yote ni kujua nini hasa ambacho unakitaka, kuwa na maono ya kile unachotaka kwenye maisha yako. Ukishajua kwa hakika nini unachotaka, hutasongwa tena na mambo ambayo siyo muhimu kwako.

Kama kila siku upo bize na huna muda wa kukamilisha mambo yako, ni dalili kwamba hujui unachotaka au hujui unakokwenda.

Anza kwa kujua nini hasa unachotaka, wapi hasa unakotaka kufika, kisha jua hatua zipi muhimu za kuchukua ili kufika unakotaka kufika, kisha puuza mengine yote ambayo hayachangii wewe kufika unakotaka kufika