Monday, February 25, 2019

SIYO KIPAJI NI JUHUDI.

Kwa  miaka mingi watu wamekuwa wakiamini kwamba kuna watu ambao wamezaliwa na vipaji ambavyo vimewawezesha kufikia kwenye ubobezi mkubwa ana katika maeneo waliyobobea.
Na mifano ipo mingi sana, kwenye utunzi wa nyimbo na upigaji wa vyombo, Morzat anaonekana kuwa mmoja wa watu wenye kipaji kikubwa. Kadhalika kwenye mchezo wa golf, Tiger Woods anaonekana kuwa mchezaji ambao ana kipaji kikubwa kwenye mchezo huo. Na hata michezo mingine na hata kwenye taaluma mbalimbali, wale ambao wamefanikiwa sana wanaonekana kuwa na kipaji kikubwa.
Lakini unapokwenda kuchimba ndani, na kuangalia kwa undani maisha ya wale wanaosemekana wana vipaji, huoni kipaji bali unaona juhudi kubwa na za muda mrefu. Katika mifano niliyotoa hapa, Morzat ambaye anaonena alikuwa na kipaji, alianza kufundishwa kupiga vyombo vya muziki akiwa na miaka minne, ana akawa anafanya hivyo kila siku. Huyu ni mtoto ambaye alikuwa akijua kufanya kitu kimoja tu, muziki. Je utamlinganisha na mtu mwingine anayekuja kujifunza muziki ukubwani?
Ukiangalia kwa Tiger Woods pia, wazazi wake wanakiri kumpa michezo ya kitoto inayoendana na mchezo wa golf tangu akiwa na miezi tisa, huyu ni mtu ambaye tangu anapata utambuzi wake, anajua kitu kimoja tu, golf, je utaweza kumshindanisha na mtu mwingine ambaye amejua mchezo huo baadaye?
Chagua mtu yeyote unayeamini ana kipaji, iwe ni mchezaji, mwanasayansi na hata kiongozi, na angalia maisha yake tangu utotoni, utagundua kuna mazingira ambayo yalimweka kwenye juhudi ambazo zilimwandaa kufikia ubobezi huo. Hata wachezaji wenye ubobezi mkubwa kama Christiano Ronaldo na Messi, ukiangalia utoto wao, wametumia sehemu kubwa kwenye kujifunza mchezo wa mpira. Angalia maisha ya wanasayansi kama Eistein, Newton na wengineo, wote waliweka muda na juhudi kubwa kabla hawajafikia ubobezi ambao wengi wanakuja kuamini ni vipaji vimewafikisha pale walipo.
Hivyo ujumbe kwako rafiki yangu ni huu, unaweza kubobea kwenye jambo lolote lile, kama tu utaweka juhudi ambazo zinapaswa kuwekwa ili kufikia ubobezi. Na kwenye kitabu cha juma hili cha PEAK, tunakwenda kujifunza juhudi sahihi unazopaswa kuweka ili kufikia ubobezi.
Usijiambie tena kwamba huwezi kufikia ubobezi kwa sababu huna kipaji au uwezo. Tafiti zote ambazo zimefanywa kwenye ubobezi zimekuja na jibu moja, wale wanaofikia ubobezi wana uwezo mkubwa sana, lakini ni uwezo ambao upo ndani ya kila mmoja wetu. Kinachotutofautisha sisi na wale waliobobea sana ni kiasi ambacho tumeendeleza uwezo ambao upo ndani yetu.
Uwezo tayari unao, unachohitaji ni juhudi ili kubobea, aina gani ya juhudi utakwenda kujifunza kwenye kitabu cha juma.

No comments:

Post a Comment