Saturday, February 9, 2019

TUSIOGOPE WALA KUKIMBIA MAGUMU TUNAYOPITIA . NI KIPIMO CHA UWEZO MKUBWA ULIOPO NDANI MWETU.

Mara nyingi tumekuwa tunakwepa magumu kwenye maisha yetu, tumekuwa tunaomba tusikutane na magumu, kwa sababu tunaona magumu ndiyo kikwazo cha sisi kuwa na maisha tunayoyataka. Lakini hilo siyo sahihi, kama tusingekutana na magumu kabisa kwenye maisha yetu, maisha yangekosa maana na tusingeweza kuwa watu ambao tumekuwa sasa.
Magumu ambayo tumekutana nayo kwenye maisha ndiyo yametufanya tuwe watu ambao tumekuwa sasa. Hivyo badala ya kukataa na kukimbia magumu, tunapaswa kuyakaribisha kwa mikono miwili. Kwa sababu kupitia magumu ndiyo tunakua, na ndiyo tunafikia uwezo mkubwa uliopo ndani yetu.
Kufukuzwa au kukosa kwako kazi huenda kumekufanya ukaweza kuanza biashara yako. Kusumbuliwa kwenye mahusiano yako ya mwanzo na yakavunjika ndiyo kumekupelekea kutengeneza mahusiano mengine bora. Na hata kupata hasara na kufa kwa biashara yako ya mwanzo kumekuwa funzo la wewe kufanikiwa kwenye biashara nyingine.
Tusiogope wala kukimbia magumu, na wala tusiombe kutokukutana na magumu. Badala yake tuombe kuwa imara zaidi ili kuweza kukabiliana na kila gumu tunalokwenda kukutana nalo.

No comments:

Post a Comment