Monday, February 25, 2019

NGUVU YA KUFANYA KWA MALENGO.

Kinachowatofautisha wale wanaofikia ubobezi na wale wanaoishia kuwa kawaida siyo wanachofanya, bali namna wanavyofanya kile wanachofanya. Watu wawili wanaweza kuwa wanafanya kitu kimoja, lakini mmoja akabobea na mwingine asibobee.
Mwandishi anatuambia zipo aina tatu za ufanyaji ambazo zinawatofautisha wanaobobea na wanaokuwa kawaida.
Aina ya kwanza ni kufanya kwa kawaida, hapa mtu anafanya kile ambacho amezoea kufanya kila wakati, hakuna kipya anachofanya na hivyo hawezi kubobea. Hivi ndivyo wengi wanavyoendesha maisha yao, wanaonekana kufanya sana lakini hakuna hatua wanapiga. Hii ni kwa sababu wanafanya kwa mazoea.
Aina ya pili ni kufanya kwa malengo, hapa mtu anafanya kitu kwa malengo, na hivyo anakuwa na hatua anazopanga kupiga zinazomsukuma kufanya zaidi. Katika kufanya kwa malengo mtu anapiga hatua zaidi kwa sababu malengo anayojiwekea yanamsukuma zaidi. Kwenye kufanya kwa malengo mtu anakuwa na sifa nne; moja anakuwa na lengo la wapi anataka kufika, mbili anaweka umakini wake wote kwenye kile anachofanya. Tatu anakuwa na njia ya kujipima na kupata mrejesho wa hatua anazochukua na nne anajisukuma kutoka nje ya mazoea, kufanya vitu vipya ambavyo vinamwezesha kupiga hatua zaidi.
Aina ya tatu ni kufanya kwa makusudi, kama mwandishi anavyoita DELIRATE PRACTICE, hapa mtu anakuwa na kusudi kubwa linalomsukuma kufanya kitu. Hii ndiyo aina ya ufanyaji ambayo inazalisha watu wenye ubobezi wa hali ya juu. Kufanya kwa makusudi kuna sifa kama za kufanya kwa malengo, lakini ina sifa nyingine mbili za nyongeza. Ya kwanza ni eneo ambalo mtu anakuwa amechagua kubobea linapaswa kuwa na wabobezi ambao wanaweza kuangaliwa na mtu akajifunza kwao. Mtu anapoweza kuwaangalia wabobezi na kujifunza kile wanachofanya na namna wanavyofanya, inakuwa rahisi kwake naye kufanya. Sifa ya pili ni kuwa na mwalimu au kocha ambaye anamfundisha na kumsimamia mtu kwenye hatua anazochukua. Kwa kuwa na mtu wa nje anayetoa maelekezo au kupima hatua mtu anazochukua na kutoa mrejesho, kunamfanya mtu apige hatua kubwa zaidi.
Hizo ndizo aina tatu za ufanyaji na aina ya tatu ndiyo mwandishi ameijadili kwa kina sana kwenye kitabu cha PEAK.

No comments:

Post a Comment