Wednesday, January 30, 2019

UKIONA DALILI HII KATIKA MAHUSIANO JUA MAHUSIANO YANAELEKEA KUVUNJIKA.


Mara nyingi tumekuwa tunakaa kwenye mahusiano ambayo baadaye yanaishia kuvunjika bila ya sisi kujua nini kimepelekea mahusiano hayo kuvunjika.
 
Tunaona kama kila kitu kinakwenda vizuri mpaka pale changamoto zinapoanza kuonekana wazi kwenye mahusiano hayo na yanaishia kuvunjika.
 
Ni rahisi kuamini kwamba mahusiano yamevunjika ghafla na sababu haijulikani, lakini ukiwa mwangalifu na kufuatilia kila mahusiano uliyonayo, ni rahisi kuziona dalili za awali kabisa zinazoonesha mahusiano yanayoelekea kuvunjika.
 
Kuna dalili moja na ya awali ambayo inaonesha kwamba mahusiano uliyonayo na mtu yanaelekea kuvunjika. Na sababu inaweza kuwa wewe, mwingine au wote kwa pamoja.
 
Dalili hiyo moja muhimu ni kuhesabu yale ambayo umemfanyia mwingine na yeye hajakufanyia. Ukishaanza kuona kwenye mahusiano, wewe au mwingine anaanza kuhesabu mazuri aliyofanya ambayo mwingine hajayalipiza jua hayo mahusiano hayana tena muda mrefu.
 
Inapofikia kwenye mahusiano unafanya vitu kwa kuhesabu, basi huenda hufanyi kwa moyo mmoja au yule uliyenaye kwenye mahusiano hajali chochote unachofanya. Kwa vyovyote, mahusiano hayo hayataweza kudumu, na kama yataendelea changamoto zitakuwa nyingi.
 
Na hii ni kwa mahusiano yoyote yale, kuanzia mahusiano ya kimapenzi na ndoa, mahusiano ya kindugu na kirafiki na hata mahusiano ya kikazi na kibiashara.
 
Mkiishaanza kuhesabu nani kafanya nini na nani hajafanya nini, hapo mambo yameshaanza kwenda mrama.
 
Mahusiano bora na yenye afya ni yale ambayo kila aliyepo kwenye mahusiano hayo anakazana kufanya kilicho sahihi na bora kwa mwingine kwa sababu ndiyo amechagua kufanya na anajali. Na siyo pale ambapo mtu anafanya kwa sababu mwenzake kafanya au inabidi na yeye aonekane kafanya.
 
Boresha mahusiano yako kwa kufanya kile kilicho sahihi na kutokuhesabu, na kama upande wa pili haujali basi jenga mahusiano mengine bora na wale wanaojali zaidi.
 

Tuesday, January 29, 2019

JE, WEWE NI MJASIRIAMALI ? TAMBUA KUKABILIANA NA HOFU.

Wale wanaofanikiwa si kwamba ni watu ambao hawana hofu kabisa, ni watu ambao wana hofu kama wewe ila wanaamua kukabiliana na hofu zao hivyo hivyo pasipo kujali nini kinaendelea ndani mwao juu ya hofu hizo.
Hata wewe unaweza kukabiliana na hofu hizo hivyo hivyo kila siku. Kuna wakati utakutana na mambo yatakayokuwa  magumu kwako lakini unatakiwa kujifunza jinsi ya kukabaliana nayo na uatafika wakati utakuwa mshindi kweli.

JE , WEWE NI MJASIRIAMALI ? TAMBUA KUNA HALI HATARISHI.


Zipo hali hatarishi nyingi sana au ‘risk’ hasa pale unapochagua kuingia kwenye ulimwengu wa biashara. Hali hizi hatarishi unatakiuwa kupambana na kukabiliana pasipo na hofu yoyote kwani kwa kuzishinda huko ndiko unafanikiwa.
Kama umeamua kuingia kwenye biashara  au ujasiriamali na ukawa mwoga na hali hizi hatarishi basi utakuwa unapotea. Kwa kujua kuna hali hatarishi basi itakuwa ni njia sahihi ya namna ya wewe kuongozwa kwentye njia ya mafanikio ya ujasiriamali wako.

JE, WEWE NI MJASIRIAMALI ? TAMBUA JINSI YA KUKABILIANA NA HALI YOYOTE ILE.

Unapoingia kwenye biashatra na huku ukaingia na mawazo ya aina moja tu kwamba mimi naenda kupata, basi utakuwa unajiweka kwenye wakati mgumu sana. Kwa kuwa umechagua kuingia kwenye biashara ujie kabisa kuna kupata na kukosa.
Inapotokea umepata unashukuru Mungu, lakini inapotokea umekosa pia unashukuru Mungu kwa matokeo hayo na kuchukua uamuzi wa kusonga mbele. Usiingie kwa akili ya kupata moja kwa moja utapotea.

KILA MJASIRIAMALI ANAPENDA KUFANIKIWA SANA !! LAKINI --------------------!!

Kila mtu anatamani biashara anayoifanya ifanikiwe, kila mtu anatamani akiingia kwenye ujasiriamali mambo yake yanyooke sana na yawe ya mafanikio makubwa. Hiki ndicho kitu ambacho watu wengi sana wanapenda kiwe kwenye maisha yao.
Hata hivyo uelewe hivi, unapochagua kuingia kwenye biashara, ujue kabisa umechagua kabisa kuingia kwenye ulimwengu wa wapambanaji haswa, yaani ulimwengu wa ujasiriamali. Hivyo, unapoingia kwenye dunia ya ujasiriamali kuna mambo lazima uyajue kwanza.
Pasipo kuyajua mambo hayo, nakuhahakikishia kabisa, utakwama sana na itafika mahali utajiona wewe si kitu na si lolote.

Saturday, January 26, 2019

VITABU VIZURI VYA KUSOMA.

---The Monk who sold his Ferrari – Robin Sharma. Katika kitabu hiki, Sharma ananifundisha kuwa mafanikio ya nje hayana maana ikiwa mafanikio ya ndani (i.e. mwili, roho, na nafsi) hayajakaa sawa. Pia siri ya furaha si ngumu. Ni kutafuta kile unachokipenda kukifanya, kisha elekeza nguvu na maisha yako yote katika kukifanya hicho tu. Ukijijua, umeyajua maisha.

-----How to live on 24 hours a day - Arnold Bennett. Jamaa huyu ananifundisha kuwa, muda wa ziada kufanikisha mipango ya mafanikio unaweza kupatikana: mwanzoni mwa siku, kwa kuamka mapema, njiani kuelekea kazini, njiani kurudi nyumbani baada ya kazi, masaa ya jioni, mwisho wa wiki.

----Who Moved My Cheese? - Spencer Johnson. Kitabu kinaeleza kwa njia ya simulizi njia ya ajabu ya kushughulika na mabadiliko katika kazi na katika maisha. Kwa hiyo, mkao sahihi kwenye maisha ni kukubali kwamba mabadiliko yapo, yatarajie, fuatilia mabadiliko, endana na mabadiliko, badilika na yafurahia mabadiliko.

-----The Law of Success – Napoleon Hill. Ni hizi sarafu ndogondogo tunazozidharau na kuzipuuza zingeweza kutuletea uhuru wa kifedha kama tungedumu katika tungeziweka akiba na kuwekeza. “The nickels, dimes and pennies which the average person allows to slip through his fingers would, if systematically saved and properly put to work, eventually bring financial independence.”

---- How to achieve total success in life – Dr. C.S. Chopra. Kwa habari ya mafanikio, Chopra naye anakazia umuhimu wa kuanza na picha ya mwisho unakotaka kufika kisha kujenga mfumo wa kufika huko.

VITABU VIZURI VYA KUSOMA.

  1. )The Law of Success – Napoleon Hill. Nimejifunza na nafanyia kazi suala la kuweka lengo kuu la maisha (definite chief aim).
  2. You’re born an original, don’t die a copy – John Mason. Kubwa ninalofanyia kazi kutoka kitabu hiki ni namna ya kufanya maamuzi sahihi kwa wakati sahihi wakati wote. Mason anasema hatma ya mwanadamu imo katika maamuzi anayoyafanya
  3. Goals – Brian Tracy. Ananifundisha kuwa, malengo lazima uyaandike kila siku bila kuacha hata siku moja. Pia kuwa na dira (vision) ya maisha yangu. Yaani ule kutazama miaka mingi mbele kwa yale unayotaka yatokee na kufanya vitu fulani sasa vinavyokupeleka kwenye ile picha kubwa ya maisha unayoyajenga.
  4. Timiza Malengo Yako – Joel Arthur Nanauka. Nanauka ananifundisha kuwa, kwenye uwekaji malengo, pamoja na kuhakikisha kwamba yako SMART na yameandikwa, lakini lazima lengo kubwa kiasi cha kwamba ukiwaamba watu wakucheke, wahisi umechanganyikiwa. Kama hujachekwa na kushangawa, lengo bado halijawa kubwa ipasavyo. Pia lengo lazima liwekewe mpango wa utekezaji
  5. The magic of thinking $uccess – Dr. David J. Schwartz. Kitabu hiki kinanifundisha kuwa, mafanikio katika jambo lolote yanaanza kwanza kwa kujua kwa hakika kwamba ni nini unahitaji kwenye jambo hilo. Kama hujui unakokwenda, huwezi kufika wala huwezi kupotea. Safari pia haitakuwa na maana. Ndiyo maana lazima kwanza ujue unachohitaji, kisha mengine yafuate.
  6. A setback is a setup for a comeback – Willie Jolley. Katika kitabu hiki, nilijifunza kuwa, fursa yoyote ile imefungashwa kwenye changamoto. Hakuna fursa ya waziwazi, zote zinafikiwa kwa kuingilia mlango unaotwa changamoto.
  7. The impossible is possible – John Mason. Mason katika kitabu hiki ananifundisha kujipambanua. Yale wengine wanayosema hayawezekani, mimi nayafanya. Ni marufuku kufuata mkumbo. Tai huruka peke yao, lakini kunguru huruka katika makundi.
  8. The Power of your subconscious mind – Dr. Joseph Murphy. Nilijifunza kuwa, subconscious mind (akili isiyofikika) ni kama shamba. Usipopanda mazao ya kuliwa, yataota magugu au mimea mwitu. Subconscious mind haiwezi kukaa bure. Kwa hiyo kila mwanadamu (kwa kujua ama kutokujua; kwa kukusudia au kutokukusudia) anapanda mbegu (mawazo) kwenye subconscious mind yake kila siku kwa kadri ya mwelekeo wa tabia zake kimawazo. Hivyo apandacho mtu (kwenye subconscious mind yake), ndicho avunacho kwenye matokeo ya nje. Ili subconscious mind ituhudumie kwa usahihi, lazima tuilishe kwa usahihi pia. Mbegu zetu sasa (mawazo) na ziwe amani, furaha, matendo ya haki, nia njema na mafanikio.
  9. As a man thinketh – James Allen. Namheshimu sana Allen. Kwa ufupi kabisa, nimejifunza kuwa Hali ya nje ya mtu kimazingira, ni dhihiriko la hali yake ya ndani kimawazo. nakazana kuwaza kwa usahihi na najifunza kila siku ili kuboresha hali yangu ya ndani kwanza ili nichochee ubora wa hali yangu ya nje kimazingira.
  10. The science of getting rich – Wallace D. Wattles. Huu ni msaafu wangu wa kuongoza maisha. Ujumbe nilionao kutoka kwenye kitabu hiki ni kuwa, utajiri unapatikana kwa sayansi kamili kama zilivyo sayansi zingine – siyo ajali, bahati wala uchawi wowote. Kikubwa ni kuwaza kwa namna Fulani na kuweka mawazo hayo kwenye vitendo. Dunia haijawahi kupungukiwa na chochote. Hivyo yatupasa tuwaze katika utele, siyo katika uhaba. Fursa za mafanikio hazina kikomo, hakuna mtu mmoja (na pengine hatatokea) wa kumzuia mwingine kufanikiwa.
  11. The secret code of success – Noah ST. John. Kinachowanyima watu mafanikio ni kushindwa kutekeleza (ACTION) matumaini yao halisi, ndoto, na matarajio. Linapokuja suala la mafanikio, akili ya kufikika (conscious mind) si mahali sahihi kuanzia. Sehemu muafaka ya kuanzia ni kwenye subconscious mind maana 90% ya tabia zetu zinatoka huku.
  12. Secrets of the Millionaire Mind – T. Harv Eker. Mafanikio katika jambo lolote yanahitaji kubadili hali ya ndani kwanza kimtazamo ili kubadili matokeo kwa nje kimazingira. Waliofanikiwa kifedha wana picha ya tofauti sana ndani mwao kuhusu fedha ukilinganisha na picha walizo nazo watu maskini na wenye kipato cha kati.
  13. Acres of Diamonds - Russell H. Conwell. Najifunza kupitia simulizi ya jamaa aliyeamua kuuza shamba lake na kusafiri nchi za mbali kwenda kutafuta almasi – bahati mbaya hakuzipata na alifia huko. Huku nyuma, jamaa aliyenunua shamba lake, aligundua lile shamba lilikua limejaa almasi na alichimba akapata nyingi sana. Kwa hiyo, mtu ukiwa na ndoto ya mafanikio, nirahisi kuangalia nje kwa kuamini huko ndiko ndoto yako itatimia, lakini ukweli ni kwamba lazima tuanzie pale tulipo, akilini mwetu, mazingira yetu, na vile tulivyonavyo.
  14. Tatizo si raslimali zilizopotea – Godius Rweyongeza. Huyu Mtanzania kijana ananifundisha kuwa thamani ya mtu inapimwa kwa kile anachotoa si kile unachopokea. Kila mwanadamu angejijua mipaka ya uwezo wake, hakika tusingekuwa hapa leo.
  15. I can, I must, I will – Reginald Abraham Mengi. Kutoka kwa mzee Mengi, napigana Kukataa Hofu ya kushindwa. Hii ni moja ya vitu vikuu vya awali kabisa vinayotufanya watanzania wengi kushindwa kuingia kwenye Biashara. Mengi anasema, tunakosa the “I can” attitude.
  16. Why “A” students work for “C” students and “B” students work for the government – Robert T. Kiyosaki. Nimejifunza kuwa, tunakoelekea watakaoimudu dunia ni wale watakaokuwa na taarifa sahihi, na kuwa tayari kubadirika kadri dunia inavyobadirika na siyo kukinzana na mabadiriko.
  17. Before you quit your job – Robert T. Kiyosaki. Kiyosaki katika kitabu hiki ananifundisha mambo ya kuzingatia kabla ya kuanza safari ya ujasiriamali. Kuna habari ya dhamira, uongozi na timu ya watu. Hizi nguzo tatu, zinabeba ndani mambo matano: mtiririko wa fedha, mawasiliano, mifumo, masuala ya kisheria, na bidhaa. Mtu anapaswa kuwa tayari kwa changamoto zote zijazo. Japo anasema ujasiriamali siyo wa kila mtu, lakini anasisitiza kuwa mtu yeyote anaweza kuwa mjasiriamali.
  18. Increase your financial IQ – Robert T. Kiyosaki. Akili ya fedha si tu kuzalisha fedha zaidi, lakini pia kuzilinda zisipotee, kuzibajeti, kuifanya fedha izae kwa kuwekeza n.k., na kuhakikisha una taarifa sahihi za fedha wakati wote.
  19. Kuna uhusiano kati ya fedha yako na hali yako ya kiroho – Christopher Mwakasege. Fedha ina nguvu kuliko roho kwa mujibu wa maandiko ya biblia kwenye Matayo 6: 21 yanayosema, “Maana pale ilipo hazina yako ndipo utakapokuwa moyo wako”. Mwakasege ananifundisha kuwa, haiwezekani kuapata uhuru wa kiroho vizuri pasipo kwanza kuwa na uhuru wa kifedha. Kwa hiyo, fedha/utajiri ni muhimu sana ili kustawi kiroho.
  20. How to Raise your Own Salary – Napoleon Hill. Hapa najifunza kuwa, watu wenye mafanikio daima wanafanya kazi wanayopenda kufanya. Masaa si kitu kwao. Wanaona furaha katika kufanya kazi yao. Umaskini ni tabia. Mtu yeyote akikubali hali ya umaskini, hali hii ya akili inakuwa tabia. Mtu anakubali umasikini kwa kutokuweka mpango wa kupata utajiri.

KANUNI MUHIMU YA MAFANIKIO KWENYE BIASHARA.

Nakushirikisha kanuni muhimu sana ya mafanikio kwenye biashara, ambayo ukiifuata kwenye biashara yako, utapiga hatua sana.
Kanuni hiyo inasema; eneo sahihi, muda sahihi, suluhisho sahihi, mawasiliano sahihi, hatua sahihi, malipo sahihi, rudia.

  1. )ENEO  SAHIHI.
Kuna biashara nyingi ambazo zinaanzishwa maeneo ambayo siyo sahihi, unakuta biashara ni nzuri, lakini kwa ilipo haina wateja. Unapawa kuanzisha biashara kwenye eneo sahihi, eneo ambalo wateja wapo ili uweze kuendesha biashara.

  1. )MUDA  SAHIHI.
Kuna biashara ambazo zinaanzishwa kwenye eneo sahihi, lakini kipindi ambacho zinakuwa zimeanzishwa siyo sahihi. Labda watu wanakuwa hawajaielewa biashara hiyo, au siyo msimu wa watu hao kutumia kitu kinachouzwa. Unapaswa kuanzisha biashara kwa wakati sahihi.

  1. )SULUHISHO  SAHIHI.
Unaweza kuanza biashara eneo sahihi na lenye wateja wenye uhitaji, lakini usiuze kama kile unachouza hakiwasaidii wateja kutatua tatizo walilonalo. Biashara yako inapaswa kutatua tatizo sahihi la mteja.

  1. MAWASILIANO  SAHIHI.
Unaweza kuwa na biashara uliyoanzisha eneo sahihi, ukawa na suluhisho sahihi kwa wateja wako na bado usiuze, kama hautakuwa na njia sahihi ya kuwasiliana na wateja wako. Ili watu wajue na kununua unachouza, lazima uwasiliane nao, lazima uwe na mpango wa masoko ambao unawafikia wateja wa biashara yako na wanajua kuhusu uwepo wako na wananufaikaje na kile unachouza.

  1. )HATUA   SAHIHI.
Hatua unazochukua kwenye biashara yako ni muhimu sana. Ili biashara ikue na kuleta faida, lazima uchukue hatua kubwa, kuwafikia wengi na kuwapa huduma bora kabisa. Kama unafanya biashara kwa ukawaida, huendi hatua ya ziada, usitegemee matokeo makubwa kutoka kwenye biashara hiyo. Kwenye biashara na kwenye maisha kwa ujumla, unapata kile unachotoa.

  1. ).MALIPO  SAHIHI.
Unaweza kuwa na biashara sahihi, eneo sahihi, suluhisho sahihi na wateja wananunua sana. Lakini malipo yasipokuwa sahihi, hutaweza kupiga hatua. Kama unauza bei rahisi ili wengi wanunue, na unapata faida ndogo, hutaweza kutoa huduma bora na hata kupiga hatua kutakuwa kugumu. Lazima uipangilie biashara yako kwa namna ambayo malipo unayopata yanakuwezesha kuendesha maisha yako na hata kutoa huduma bora zaidi kupitia biashara hiyo.

  1. ).RUDIA.
Ukishaanzisha biashara inayokidhi vigezo vyote hivyo sita, hapo sasa unayo biashara, unayo mashine ya kuchapa fedha. Sasa ukishakuwa na mashine ya kuchapa fedha unahitaji nini tena? Ni kurudia huo mchakato kila wakati. Kila siku boresha biashara yako kwenye maeneo hayo, na pia angalia fursa nyingine ambapo unaweza kutumia kanuni hiyo kuanzisha na kukuza biashara mpya.

Thursday, January 17, 2019

EPUKA MABISHANO KWA KUFANYA HIVI.

Hakuna kitu kinachochukua muda wako na nguvu zako kama mabishano.

Mabishano ya aina yoyote ile ni gharama kwako na hakuna chochote unachonufaika nacho.

Na ipo njia rahisi sana ya kukuwezesha kuepuka kila aina ya mabishano.
 
Njia hiyo ni kukubaliana na watu waliojiandaa kubishana. Waambie wapo sahihi na kile wanachoamini na kusimamia ndiyo kweli. Hapo hawatakuwa tena na cha kubishana na wewe na kila mtu ataendelea na yake.
 
Lakini kama unataka ubishani uibuke, ambao hautaisha, mwambie mtu hayupo sahihi, mwambie amekosea na hapo utaibua ubishani usio na kikomo. Tena pale unapogusa kile ambacho mtu anaamini kweli, atatafuta kila njia ya kukitatua.
 
Kubaliana na watu haraka na endelea na mambo yako ambayo ni muhimu zaidi kuliko mabishano ambayo hayana manufaa yoyote kwako.
 
Kubaliana na watu na hawatakuwa na sababu ya kubishana na wewe. Na unapokubaliana nao haimaanishi kwamba wapo sahihi, ila hutaki kusumbuana nao. Ndani yako unaweza kujua kabisa kwamba hawapo sahihi, lakini huwaambii hilo maana ubishi utakaoanza hautakuwa na kikomo.

SHERIA YA ASILI: ( LAW OF NATURE )--UTAVUNA ULICHOPANDA.

Asili ina tabia ya kutoa hukumu yake hapo hapo, inatoa majibu mara moja.
Unapotenda dhambi, au kufanya kile ambacho wewe mwenyewe unajua siyo sahihi, utaanza kujisikia vibaya wewe mwenyewe. Na chochote utakachopata, hutaweza kukifurahia kama kitu ulichopata kwa uhalali.
Na zaidi ya hayo, asili lazima itakufanya ulipe kila unachofanya. Kanuni ya asili ni kulipa kila kinachofanywa, kwa kiwango kile kile.
Ukifanya wema, wema unarudi kwako kwa kiwango kile kile. Ukifanya uovu, uovu unarudi kwako kwa kiwango kile kile. Huwezi kutoroka hili, huwezi kuizidi asili akili.
Chagua kuishi kwa misingi sahihi, chagua kufanya kilicho sahihi mara zote, siyo kwa sababu unaogopa moto baadaye, bali kwa sababu unajua kila kitu kitalipwa sasa bila ya kuchelewa.

Monday, January 14, 2019

UFUNGUO MKUU WA MAFANIKIO.

  1. Huhitaji kutafuta nguvu nje yako, nguvu tayari zipo ndani yako. Unachohitaji ni kujua nguvu ulizonazo na kuweza kuzitumia. Kila binadamu ana nguvu kubwa ya kiroho ndani yake, na nguvu hii ya kiroho ipo ndani ya fikra zake. Kama akiweza kuzitumia vizuri fikra zake, zitampa chochote anachotaka.
  2. Magumu tunayokutana nayo kwenye maisha ni kwa sababu ya kutokujua nini hasa tunachotaka na pia kutokujua kile kilichopo ndani yetu. Ukishajua kilichopo ndani yako na ukajua kwa hakika nini unataka, na ukapeleka fikra zako kwenye hayo, hakuna kitakachokushinda.
  3. Usilalamikie chochote kinachotokea kwenye maisha yako, kwa sababu umekisababisha mwenyewe na nguvu ya kukibadili ipo ndani ya fikra zako. Fikra zako ndiyo kisababishi, na yale yanayotokea kwenye maisha yako ni matokeo. Hivyo kama hujayapenda matokeo, badili kisababishi ambacho ni fikra zako.
  4. Dunia inaendeshwa kwa upacha, kwenye dini kuna Mungu na shetani, kwenye sayansi tuna chanya na hasi, kwenye falsafa tuna wema na uovu. Lakini yote haya ni hali ya fikra zetu. Kama fikra zikisimamiwa vizuri zinaleta matokeo mazuri, kama zisiposimamiwa zinaleta matokeo mabaya.
  5. Tunaishi kwenye zama za fikra, zama za ubunifu. Wanaofanikiwa ni wale ambao wanaweza kutumia fikra zao vizuri. Kwa sababu dunia imekuwa na vitu vile vile miaka yote, bali wale waliotumia fikra zao vizuri ndiyo wamenufaika zaidi na dunia. Kwa mfano umeme tulionao sasa duniani hauna tofauti na umeme uliokuwepo miaka 200 iliyopita. Lakini leo tuna vitu vingi zaidi vinavyotumia umeme kuliko miaka 200 iliyopita kwa sababu watu wametumia vizuri fikra zao na kuja na vitu vipya.
  6. Zipo njia kuu mbili za kuendeleza na kutumia vizuri fikra zetu. Njia hizo ni umakini na msisitizo. Unaposisitiza fikra zako kwenye kitu kimoja, na umakini wako wote ukawa pale, fikra zina nguvu ya kukupa kile unachotaka. Ukikosa sifa hizo mbili, fikra zako zitakuwa zinahamahama na hutapata unachotaka.
  7. Baada ya kuweka umakini na msisitizo wa fikra zako kwenye kile unachotaka, unapaswa kuwa na taswira ya unachotaka na kuiweka taswira hiyo kwenye fikra zako. Pata picha ya kile unachotaka, kama vile tayari umeshakipata, jione ukiwa ndani ya kitu hicho. Kwa kutengeneza taswira hii, akili yako ya ndani itaona ndiyo maisha yako na kutengeneza maisha ya aina hiyo zaidi.
  8. Kusudi kuu la maisha ni kukua na kuongezeka. Na dunia nzima kwa asili inakua na kuongezeka. Angalia kila kiumbe, kuanzia miti, wanyama na hata samaki, wanaendelea kuzaliana na kukua zaidi. Hivyo ili kufanikiwa kwenye maisha, unapaswa kuwa na fikra za ukuaji.
  9. Tabia uliyonayo siyo kwa bahati mbaya, bali umeijenga wewe mwenyewe kwa juhudi kubwa sana. Umekazana wewe mwenyewe kujenga tabia zote ulizonazo, kwa kuanzia kwenye fikra zako, kwa namna unavyojitambulisha ndani yako. Hivyo ili kubadili tabia, anza kubadili fikra zako na weka juhudi kujenga tabia mpya.
  10. Hakuna uhaba kwenye dunia, bali kuna utele. Dunia ina kila kitu kwa wingi kadiri watu wanavyohitaji. Na hata vikipungua basi itatengeneza zaidi kadiri watu wanavyohitaji. Hivyo hupaswi kufikiri kwenye uhaba bali kwenye wingi, hupaswi kuona mwingine akifanikiwa basi wewe unashindwa. Dunia ina rasilimali za kumtosha kila mtu kufanikiwa.
  11. Maisha yanaendeshwa kwa sheria na kanuni fulani, ukizijua na kuziishi utafanikiwa. Lakini usipozijua basi zitakuumiza. Kwa mfano dunia ina nguvu ya mvutano, ambayo inavuta kila kitu kwenye dunia. Kama hujui kanuni hii na ukajaribu kuruka kama ndege, utaanguka kwenye dunia na kuumia sana. Kanuni ipo pale na kama huijui inakugharimu.
  12. Unahitaji vitu vitatu ili kuweza kunufaika na nguvu ya fikra iliyopo ndani yako. Moja unahitaji kujua kwamba una nguvu ndani yako, mbili, unahitaji kuwa na uthubutu wa kujaribu kuitumia nguvu hiyo na tatu unahitaji kuwa na imani ya kutumia nguvu hiyo.
  13. Sisi binadamu siyo viumbe wa mwili ambao tuna roho, bali sisi ni viumbe a kiroho ambao tuna mwili. Roho ndiyo inayoongoza maisha yetu na ndiyo yenye nguvu ya fikra. Mtu anapofariki, kinachoondoka ni roho, mwili unabaki pale na unakuwa hauna nguvu ya kufanya chochote. Hivyo kama unataka kujiendeleza, endeleza roho yako, endeleza fikra zako na hizi zitakupa unachotaka.
  14. Ulimwengu mzima ni kitu kimoja na tunaongozwa na nguvu moja. Kila kitu kwenye ulimwengu, ukikiangalia kwa undani unagundua ni nguvu ama nishati. Jua ni nishati ya mwanga na jito, ambayo ikifika kwenye mimea inabadilika na kuwa nishati ya kikemikali, mimea ikiliwa na wanyama nishati hiyo inahamia kwa wanyama. Kila kitu kwenye dunia ni nishati, hata sisi binadamu, ukivunja miili yetu mpaka kwenye ngazi ya seli, unagundua sisi ni nishati. Hivyo ulimwengu mzima ni kitu kimoja, nishati.
  15. Kukua ni kupoteza, kupata kipya ni kupoteza cha zamani, hii ni kanuni muhimu sana kwenye mafanikio. Hakuna kiumbe anayekua na kubaki na vitu vya zamani, na huwezi kupata kitu kipya kama bado unang’ang’ana na vya zamani. Ili ukue unahitaji kupoteza kile ambacho tayari unacho sasa. Matatizo mengi ambayo watu wanayapata ni kutokana na kung’ang’ana na vitu vya zamani.
  16. Ipo kanuni kuu ya maisha kwamba kila kitu kinazaliwa, kinakua, kuzalisha na kufa. Na kanuni hii inaenda kwa mzunguko. Kwa mfano kwetu sisi binadamu, kila baada ya miaka saba, maisha yetu yanabadilika kabisa na kuwa mapya. Miaka saba ya kwanza ni ya utoto, miaka saba inayofuatia ni ya kuanza kujifunza majukumu, saba inayofuata ni ya kuanza ukuaji wa utu uzima. Miaka saba mingine ni kufikia ukuaji kamili, inayofuatia ni ya kuzalisha na kuwa na mali na familia. Miaka saba inayofuata, 35 mpaka 42 ni kipindi cha mabadiliko makubwa kimaisha. Inafuatiwa na miaka saba mingine ya kujijenga upya kwenye utu uzima.
  17. Vitabu vya dini vinatuambia kwamba binadamu tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. Na hili lina maana kwamba tunazo sifa za uungu ndani yetu. Sifa hizi zipo kwenye fikra, mungu ana sifa ya kuumba na fikra zetu pia zina sifa ya kuumba. Kadhalika kwenye nguvu na ujuzi, fikra zetu zinajua mengi na zina nguvu kubwa. Tukiweza kuzitumia tunaweza kufanya makubwa sana.
  18. Usichotumia unakipoteza. Wengi hujiuliza kama fikra zetu zina nguvu sana kwa nini wengi hawazitumii. Sababu kubwa ni kwamba wengi hawajui kama wana nguvu kubwa kwenye fikra zao, na usichokijua huwezi kukitumia, na usichotumia unakipoteza. Hivyo hatua ya kwanza ya kutumia nguvu zako ni kujua zipo, na kuanza kuzitumia.
  19. Hofu ni matumizi mabaya ya nguvu ya fikra zako. Kwa kuwa na hofu unatumia fikra kutengeneza yale ambayo hutaki yatokee na kwa kuwa fikra zina nguvu, zinaleta hayo hayo unayofikiria. Hivyo unapaswa kuondokana kabisa na kila aina ya hofu, kwa kujua nguvu kubwa iliyopo ndani yako ya kukuwezesha kufanya chochote.
  20. Jukumu lako kuu kwenye maisha, na biashara pekee ambayo inalipa ni kufikiri. Wale wanaoweza kufikiri kwa kutumia akili zao ndiyo wanaokuja na vitu vipya na njia mpya za kufanya vitu na wananufaika sana. tumia nguvu yako ya fikra kufikiri na utaweza kufanya makubwa.
  21. Unapofikiri, unapaswa kufikiri mawazo makubwa sana. Ukifikiri kidogo nguvu iliyopo ndani yako inaleta matokeo madogo. Ukifikiri makubwa nguvu hiyo inaleta makubwa. Usiogope kufikiri makubwa, una nguvu ndani yako ya kupata chochote unachofikiri.
  22. Kinachotutofautisha ni kanuni ya mtetemo (law of vibration). Tumeona kwamba kila kitu duniani ni nishati, je nini kinakutofautisha wewe binadamu na mti? Ni kanuni ya mtetemo. Wewe ni binadamu kwa sababu seli zako zina mtetemo tofauti na za mti. Na hata nishati inapobadilika kutoka mfumo mmoja kwenda mwingine, kinachobadilika ni mtetemo wake. Hata baina ya watu, wale wanaofanikiwa ziadi wana mtetemo wa juu kuliko wale wanaoshindwa. Fikra zetu zinaendana na mtetemo, hivyo tunapokuwa na fikra za juu tunavutia mtetemo wa juu. Unaweza kufananisha nguvu hii ya mtetemo na kutafuta mawimbi ya redio, unasikia redio fulani pale unapofikia kwenye mawimbi yake.
  23. Kanuni kuu ya mafanikio ni HUDUMA. Tunafanikiwa kwa kadiri tunavyowahudumia wengine, tunapata kadiri ya tunavyotoa. Hivyo kama unataka zaidi, unapaswa kutoa zaidi, kama unataka kufanikiwa zaidi unapaswa kuwahudumia wengi zaidi na kwa ubora zaidi.
  24. Ili kuwa huru na ili kupata chochote unachotaka, unapawa kuujua ukweli. Kumbuka kauli inayosema IJUE KWELI NAYO ITAKUWEKA HURU. Watu wengi hawapo huru kwa sababu hawajui ukweli, na usipokuwa huru huwezi kuwa na mafanikio. Ujue ukweli kwa kujua nguvu kubwa iliyopo ndani yako na pia kwa kujua umoja wa dunia, kwamba kila kitu ni nishati na tunavuta vile vitu ambavyo vipo kwenye mtetemo wa fikra zetu.

TENGENEZA GEREZA LA AKIBA.

Kila mwaka malengo ya watu yamekuwa ni kuweka akiba kwa ajili ya uwekezaji. Na kweli wanaweka sana akiba, wanajinyima na kuanza kutengeneza akiba zao.
Lakini haupiti muda inajitokeza dharura ambayo inawapelekea kutumia zile akiba walizokuwa wamejiwekea, hivyo wanarudi sifuri kabisa, wanakuwa hawana akiba yoyote.
Rafiki, iwe una fedha au huna, dharura hazitaacha kutokea kwenye maisha yako. Hivyo njia pekee ya kulinda akiba yako siyo kuombea usipate dharura, badala yake ni kutengeneza gereza kwa ajili ya akiba yako.
Gereza hili ni kuweka akiba eneo ambalo huwezi kuitoa hata ardhi ipasuke. Na ukishaweka huko unasahau kabisa, hivyo kama dharura itakuja, utaangalia njia nyingine za kuitatua na siyo kuangalia akiba hiyo.
Magereza ya fedha yapo mengi, unaweza kuziweka kwenye akaunti maalumu, ambayo huwezi kutoa fedha hiyo mpaka muda uliochagua uishe. Pia unaweza kufungua akaunti ya pamoja na mtu mwingine na makubaliano yakawa ni hakuna kutoa hata iweje. Pia unaweza kutumia mitandao ya simu, ukapoteza namba ya siri ya mtandao wa simu unaotumia kuweka fedha ili isiwe rahisi kwako kutoa.
Angalia njia bora kwako ni ipi na itumie, usiache akiba yako ikakaa kirahisi rahisi kiasi kwamba ukiwa na shida kidogo tu unaitumia. Iweke kwenye gereza ambalo hutaweza kuitumia kabisa.

SIFA YA WASHINDI KATIKA MAISHA.

“Victory belongs to the most persevering.” - Napoleon Bonaparte
Ushindi unaenda kwa wale ambao ni ving’ang’anizi na wavumilivu.
Huwa tunawaangalia wale waliofanikiwa na kupenda sana kufika walipofika. Lakini sisi wenyewe kuna vitu vingi ambavyo tulishawahi kuanza kwenye maisha yetu, lakini havikutufikisha mbali, kwa sababu tulikosa ung’ang’anizi na uvumilivu.
Sasa chagua kitu kimoja au vichache unavyotaka kwenye maisha yako, kisha weka juhudi zako zote na usikate tamaa mpaka umekipata, na ninakuhakikishia utakipata. Maana washindi wote wameng’ang’ana na kupata walichotaka.

Tuesday, January 8, 2019

HEKIMA.

Bila ya hekima, fedha na afya tunazopigania kuwa nazo, zitatupoteza kabisa. Hekima ndiyo inayotuongoza vizuri kwenye maisha yetu, ndiyo inayotuwezesha kufanya maamuzi sahihi kwetu ambayo yanafanya maisha yetu yawe bora zaidi.
KUSOMA; kila siku ya maisha yako, soma angalau kwa dakika 30, na soma vitabu vinavyoongeza maarifa na uelewa wako kwenye kile unachofanya na hata maisha kwa ujumla. Tenga na linda sana muda huu wa kujisomea, ndiyo utakaokutoa hapo ulipo sasa na kukufikisha mbali zaidi.
UZOEFU WA WENGINE; chagua watu ambao utajifunza kupitia wao, hawa tunawaita menta. Unapaswa kuwa na mtu ambaye unataka kufikia hatua ambazo amefikia yeye, kisha kujifunza kila kitu kuhusu yeye. Kama yupo hai na yupo karibu unaweza kutafuta nafasi ya kuonana naye. Na kama yupo mbali huwezi kumfikia au alishafariki basi jifunze kupitia maandiko yake na hata maandiko yaliyoandikwa kuhusu wewe. Mazuri aliyofanya na pia jifunze makosa aliyoyafanya ili uweze kuyaepuka.
KUTAFAKARI; Unapaswa kuwa na muda wako mwenyewe, muda wa kutafakari, kuyatafakari maisha yako na kutafakari kila unachofanya, kuanzia ulikotoka, ulipo sasa na kule unakokwenda. Kila mwisho wa siku yako tafakari kila hatua uliyochukua kwenye siku hiyo na angalia wapi umefanya vizuri, wapi umekosea na wapi unahitaji kurekebisha na kuboresha zaidi. Majibu ya maswali mengi uliyonayo kuhusu maisha tayari unayo, ni wewe kutafakari na kujisikiliza na utapata majibu mengi sana.

UTAJIRI.

Fedha ni sehemu muhimu sana ya maisha yetu, ukiondoa pumzi ambayo kila mtu anaipata bure, kila kitu kinahitaji fedha. Na hata hiyo pumzi unapoumwa inaacha kuwa bura na unaanza kuilipia. Fedha ni hitaji muhimu sana kwenye maisha yetu, kwa sababu ndiyo inatuwezesha kupata kila tunachotaka.
KIPATO; ongeza kipato chako kwa kutoa thamani zaidi, kujituma zaidi na kuwafikia wengi zaidi. Kama umeajiriwa tekeleza majukumu mengi zaidi na magumu zaidi. Kama unafanya biashara wafikie wateja wapya na wengi zaidi. Fanya zaidi ya ulivyozoea kufanya huko nyuma na kipato chako kitaongezeka.
MATUMIZI; Dhibiti sana matumizi yako, peleka fedha zako kwenye yale mambo ambayo ni muhimu pekee kwenye maisha yako, kama kitu siyo muhimu, achana nacho. Matumizi huwa yana tabia ya kukua kadiri kipato kinavyokua, usipoyadhibiti yatakurudisha nyuma.
UWEKEZAJI; Hutakuwa na nguvu za kufanya kazi kama unavyofanya sasa  miaka yako yote. Hivyo unahitaji kuifanya fedha yako ikufanyie kazi na kukiingizia kipato. Na hapa ndipo uwekezaji unapokuwa muhimu. Weka akiba na wekeza akiba hiyo kwenye maeneo ambayo yanazalisha zaidi kwa baadaye.

AFYA

Afya ndiyo mtaji wa kwanza na muhimu sana kwenye maisha yetu, bila ya afya bora na imara huwezi kufanya chochote kikubwa kwenye maisha yako. Afya unaweza kuichukulia kirahisi sana unapokuwa nayo, lakini ukishaipoteza gharama zake ni kubwa sana.

KULA VYAKULA vya kiafya kwa kuepuka sukari, kupunguza wanga na kuongeza zaidi mbogamboga, matunda, mafuta na protini. Sumu namba moja kwenye afya zetu ni wanga na sukari, ukiweza kudhibiti hili utakuwa na afya bora.
KUFANYA MAZOEZI, kila siku fanya mazoezi ya kukimbia kwa angalau nusu saa. Mazoezi ya kukimbia ni mazoezi bora kabisa na yasiyo na gharama kwako. Hakikisha unafanya haya kila siku.
KUPUMZIKA, pata muda wa kutosha wa kulala kulingana na uhitaji wa mwili wako. Kwa wastani binadamu tunahitaji masaa 6 mpaka 8 ya kulala kwa siku. Jua mwili wako unahitaji kiasi gani na kila siku upe muda huo. Hili litakufanya uwe imara na kuweza kuweka juhudi kwenye shughuli zako.

Sunday, January 6, 2019

JINSI UTAJIRI UNAVYOKUJA KWAKO.

 Utajiri unakuja kwako kwa njia ya thamani. Unapaswa kutoa thamani kubwa zaidi ya matumizi kuliko thamani ya fedha ambayo mtu anakupa. Ili kupata zaidi lazima uwe tayari kutoa zaidi.
 
Usiwalangue watu, wala usitumie mbinu kuwashawishi wanunue kitu ambacho hakitawasaidia. Wape watu kitu ambacho kitakuwa na msaada kwenye maisha yao na wewe utaweza kupata kile unachotaka.

USIWE MTU WA KULALAMIKA AU KUKOSA SHUKRANI.

Tumeona kwamba kuna mfumo wa fikra ambao unatupa kila ambacho tunakifikiri kwa muda mrefu. Njia pekee ya kushirikiana na mfumo huu ni kuwa na shukrani.
 
Kwa kushukuru, mfumo huu wa fikra unajua kwamba upo tayari kupokea zaidi na hivyo kukuwezesha kupata zaidi.
 
Usiwe mtu wa kulalamika au kukosa shukrani, mara zote shukuru na utaweza kupata zaidi. Shukuru kwa kidogo na utafungua milango ya kupata kikubwa zaidi.

NAMNA FULANI YA KUFIKIRI ILI KUVUTIA UTAJIRI.

 Hatua muhimu ya kupata kile unachotaka ni kujua kwa hakika nini hasa unachotaka. Huwezi kupata kile usichokijua, hivyo lazima ujue kwa undani kile unachotaka na kukifikiria kwa ukamilifu wake ndiyo uweze kukipata.

Unapaswa kutengeneza picha kwenye fikra yako ya kile unachotaka, kwa namna unavyokitaka kisha weka picha hii kwenye fikra zako mara nyingi. Kila unapokuwa na muda ambao huna kazi, tumia muda huo kufikiria picha hiyo na kujiona tayari umeshapata kile unachotaka.
Unapoifikiria picha ya kile unachotaka, unapaswa kuwa na imani kwamba tayari umeshakipata kwa namna unavyokitaka. Ona kama tayari unacho. Kwa njia hii, mfumo wa fikra unaoongoza dunia utakuwezesha kupata kile unachotaka.

JINSI YA KUTUMIA MATAKWA YAKO ILI KUVUTIA UTAJIRI.


Katika kutumia sayansi ya kupata utajiri, hupaswi kutumia matakwa yako kwa kitu chochote kilichopo nje yako. Usitumie nguvu ya matakwa yako kuwaendesha wengine kama unavyotaka wewe.


Sayansi ya kupata utajiri haitaki wewe uingilie maisha ya wengine, na pale unapofanya hivyo, kwa kutumia matakwa yako kuingilia maisha ya wengine, unaharibu mfumo mzima unaopaswa kutengeneza utajiri kwako. Kadiri unavyohangaika na ya wengine, ndivyo unavyopoteza ya kwako.



Tumia nguvu ya matakwa yako katika kufikiri na kutenda kwa namna ambayo itakuwezesha wewe kupata kile unachotaka. Na katika kuweka nguvu ya matakwa yako kwenye kupata utajiri, usijihusishe kwa namna yoyote na umasikini, usiufikirie umasikini, usitake kujua kwa nini watu ni masikini na wala usisome au kusikiliza vitu vinavyoeleza kuhusu umasikini. Ukatae umasikini kabisa na fikra zako zielekeze kwenye namna bora ya kufikiri ili kutengeneza utajiri.

PELEKA MAWAZO NA AKILI ZAKO ZOTE KWENYE UTAJIRI.

Huwezi kutengeneza na kutunza maono ya utajiri kama unahamisha mawazo yako kwenda kwenye picha inayokinzana mara kwa mara. Hupaswi kufikiria kitu kinachopingana na utajiri unaotaka kwenye maisha yako. Muda wako wote fikiria ile picha ya utajiri uliyojitengenezea.
 
Usizungumzie kuhusu umasikini uliokuwa nao au wazazi wako waliokuwa nao, usizungumzie kuhusu hali mbaya ya uchumi au mabaya yoyote yanayoendelea. Hata kama mambo ni magumu kiasi gani, hayo yanapita, hayadumu milele. Hivyo usiharibu fikra zako kwa kuyafikiria au kuyazungumzia.
 
Peleka mawazo na akili zako zote kwenye utajiri na ipe picha unayotaka kufikia na waache wengine wahangaike na hayo mengine.

NAMNA FULANI YA KUFIKIRI NA KUTENDA / KUCHUKUA HATUA ILI KUVUTIA UTAJIRI..

Fikra zina nguvu kubwa sana ya kuumba, pale unapofikiri kwa namna fulani, unatumia nguvu ya mfumo wa fikra unaoongoza dunia katika kukuletea kile unachotaka. Lakini kile unachotaka hakitatokea kwa muujiza, badala yake kitatokana na matendo na hatua unazochukua.
Ipo namna fulani ya kutenda ambayo inakuwezesha kupata kila unachotaka kwenye maisha yako. Na bila ya kuchukua hatua kwa namna fulani, hata kama ungekuwa na fikra bora kiasi gani, hazitaweza kuleta unachotaka.
Chochote unachokitaka sasa, kipo kwenye mikono ya wengine, na ili hao wengine wakupe hicho unachotaka, lazima wewe uwape kwanza kile wanachotaka. Hivyo lazima uwe na namna bora ya kuchukua hatua, namna inayoendana na fikra ulizonazo na kuchukua hatua ukiwa na imani na uhakika wa kupata unachotaka na utakipata.
Unapaswa kuchukua hatua sasa, kwa kuweka nguvu zako zote kwenye kile unachofanya kwa wakati huo, usifikirie kuhusu jana wala kesho, badala yake fikiria kuhusu kile unachofanya kwa wakati husika, hili litakuwezesha kufanya vizuri kile unachofanya.

CHUKUA HATUA ZENYE UFANISI ILI KUVUTIA UTAJIRI.

Kama pale ulipo sasa hapakuridhishi, kama unataka kupiga hatua zaidi kwenye maisha yako na kwa kile unachofanya, unapaswa kukua zaidi ya pale ulipo sasa. Unapaswa kuijaza ile sehemu uliyopo sasa kiasi kwamba hakuna tena nafasi kwa ajili yako na hivyo inakubidi ukue zaidi.
 
Chochote unachofanya sasa kifanye kwa viwango vya juu sana kuliko ilivyozoeleka. Na unapofanya kwa viwango vya juu, mfumo wa fikra unaoendesha dunia utakupeleka kwenye hatua za juu kuliko hapo ulipo sasa.
 
Kila siku fanya kile unachopaswa kufanya bila ya kuahirisha, na kifanye kwa ufanisi mzuri. Usifanye kitu chochote kwa haraka au njia ya mkato. Mafanikio kwenye maisha ni kufanya vitu kwa ufanisi wa hali ya juu.
 
Kwa kila hatua unayochukua, kuwa na picha ya matokeo unayotaka kupata na fikiria picha hiyo mara zote. Hili litaweka fikra zako kwenye kile unachofanya na utaweza kupata matokeo bora.

INGIA KWENYE BIASHARA SAHIHI KWAKO ILI KUVUTIA UTAJIRI.

Biashara au kazi yoyote inayo uwezo wa kutengeneza utajiri mkubwa kwa mtu yeyote. Lakini siyo kila aina ya biashara au kazi itaweza kutengeneza utajiri kwako.
 
Utapata utajiri na kufanikiwa kwa kuingia kwenye kazi au biashara ambayo inaendana na wewe. Biashara ambayo inatumia vipaji na uwezo mkubwa uliopo ndani yako.
 
Utafanikiwa zaidi kwa kufanya kile unachopenda na unachojali, kwa sababu utafanya kwa kupenda na siyo kufanya kama kazi.
 
Jua kipi unapenda na kujali na jua vipaji na uwezo mkubwa uliopo ndani yako kisha chagua kazi au biashara inayoendana na vitu hivyo. Hii ndiyo itakayokuletea utajiri mkubwa.

MWONEKANO WA UKUAJI KATIKA KUVUTIA UTAJIRI.

 
Kwa kazi au biashara unayoifanya, usifanye kwa mazoea au kufanya vile vile kila wakati. Badala yake fanya kwa ukuaji kila siku. Kila siku kazana kupiga hatua kubwa zaidi ya ulizopiga siku zilizopita.
 
Ni mwonekano huu wa ukuaji ndiyo unaowavutia watu kwako. Watu wanapenda kujihusisha na wale ambao wanakua zaidi, wanatoa thamani kubwa zaidi kila siku.
 
Mazoea yanaharibu na kuua kabisa kile ambacho kipo ndani ya mtu. Lakini ukuaji unakuza zaidi kile ambacho kipo ndani ya mtu.

UKUAJI BINAFSI KATIKA KUVUTIA UTAJIRI.

 
Ili kuvutia utajiri kupitia kile unachofanya na ili kuziona fursa mpya kila mara, lazima wewe binafsi uwe unakua. Kwa chochote unachofanya sasa, hata kama ni kidogo kiasi gani, unapaswa kukua zaidi ya kitu hicho.
 
Hata kama upo kwenye kazi au biashara ambayo ni ndogo, ifanye kama kubwa na tekeleza majukumu yako kwa ukubwa. Tekeleza majukumu yako kwa ufanisi wa hali ya juu na wahudumie watu kwa namna ambayo inaongeza thamani kubwa kwao.

SAYANSI / KANUNI YA KUPATA UTAJIRI


1. Kuna mfumo wa kufikiri ambao kutoka ndani yake vitu vyote vinatengenezwa na ambao kwa uhalisia wake unaruhusu, kupenyeza na kuujaza ulimwengu wote.
 
2. Fikra kwenye mfumo huu inazalisha ile taswira inayotengenezwa na fikra.
 
3. Mtu anaweza kutengeneza vitu kwenye fikra zake na kwa kuziweka kwenye mfumo huu wa kufikiri kile anachofikiri kinaumbwa.
 
4. Ili kufanya hivi, mtu anapaswa kuondoka kwenye fikra za ushindani na kwenda kwenye fikra za ubunifu. Vinginevyo hataweza kuendana na mfumo wa fikra ambao mara zote upo kwenye hali ya ubunifu na siyo ushindani.
 
5. Mtu yeyote anaweza kuendana na mfumo huu wa fikra kwa kuwa mtu wa shukrani kwa baraka ambazo amezipata. Shukrani inaunganisha fikra za mtu na mfumo wa fikra unaoendesha ulimwengu.
 
6. Mtu lazima atengeneze picha ya kifikra ya vitu anataka kuwa navyo na kuifikiria picha hii mara zote huku akiwa na imani kwamba ataipata na kushukuru kwamba mfumo wa fikra unamwandalia mazingira ya kupata kile anachotaka. Tumia muda wako wa mapumziko kufikiria picha ya utajiri unaotaka kuwa nao na mfumo wa fikra utaipanga dunia kwa namna ambayo itakuletea kile unachotaka.
 
7. Mfumo wa kufikiri unafanya kazi kupitia njia za asili za ukuaji na za kijamii. Kila ambacho kinafikiriwa kwa muda mrefu kwa imani na bila ya shaka, ndiyo kinacholetwa kwenye uhalisia.
 
8. Ili kupokea kile ambacho mtu anataka, lazima mtu achukue hatua kwa namna fulani ambayo inamwezesha kujaza pale alipo sasa. Lazima afanye zaidi, lazima atoe thamani kubwa kwa wengine kuliko thamani anayopokea na lazima akue zaidi na akuze zaidi kile anachofanya.

Friday, January 4, 2019

TUMIA KAULI HII KILA SIKU , " MIMI NI TAJIRI MAFUNZONI " NA EPUKA KAULI HII , " MIMI NI MASKINI " AU " SISI NI WATU MASKINI "

Ndugu yangu, mdau  wangu  kama kuna kitu kimoja unachopaswa kukikataa kwa mwaka 2019 basi ni kukiri umasikini. Usikiri kwa kinywa chako kwamba wewe ni mtu masikini au mtu mnyonge, utaendelea kubaki kwenye hali hiyo.
Hata kama huna fedha, usijiite masikini, badala yake jiite tajiri mafunzoni. Tumia kauli chanya kuhusu fedha na utajiri na hilo litakaribisha fedha kwako zaidi na zaidi.

EPUKA KAULI HII MWAKA MPYA 2019 , " KAZI YA FEDHA NI MATUMIZI / KUTANUA / PONDA MALI KUFA KWAJA " ILI UWE NA MAFANIKIO MAKUBWA KIFEDHA KWAKO.

Hivi ndivyo wengi wanavyotengeneza mahusiano yao na fedha, wakizipata watazitumia mpaka ziishe ndiyo waweze kutulia.
Hupaswi kutumia kila fedha unayoipata mpaka iishe, na kwa hakika unapaswa kuweka akiba na kuwekeza kabla hata hujaanza kutumia fedha uliyonayo.
Acha kujiambia kazi ya fedha ni matumizi, au kutumia kauli kama tumia fedha ikuzoee. Kila fedha unayopata weka fungu fulani pembeni kwa ajili ya akiba na uwekezaji kabla hujaanza kutumia.

EPUKA KAULI HII MWAKA MPYA 2019, " FEDHA NI NGUMU " ILI UWE NA MAFANIKIO MAKUBWA KIFEDHA KWAKO.

Kamwe usikiri kwamba fedha ni ngumu kupatikana au inabidi uumie ndiyo uipate. Jua fedha ni mabadilishano ya thamani, angalia thamani unayoweza kuitoa kwa wengine na wao watakupa fedha.
Ukikiri fedha ni ngumu, utakata tamaa na kushindwa kutoa thamani kwa wale wenye uhitaji.
Kiri fedha ni matokeo ya thamani na kazana kuzalisha thamani zaidi ili kupata fedha zaidi.

EPUKA KAULI HII MWAKA MPYA 2019, " FEDHA SIYO KILA KITU " ILI UWE WA MAFANIKIO MAKUBWA KIFEDHA KWAKO.

Usemi huu ni maarufu sana kwa wengi, hasa masikini, kwamba usijisumbue sana na fedha kwa sababu fedha siyo kila kitu. Hii kauli siyo sahihi kwa asilimia 100, ni kweli kuna vitu muhimu kwenye maisha ambavyo tunavipata bura, kama hewa tunayopumua. Lakini ukiwa mgonjwa na huwezi kuvuta hewa mwenyewe, utauziwa hewa hiyo kwa bei ya juu sana.
Usitumie kauli hii ya fedha siyo kila kitu, kiri kwamba fedha ina mchango mkubwa sana kwenye maisha yako na kazana kuipata ili maisha yako yawe bora.
Vitu kama mahusiano yako na wengine unaweza kuona havihitaji fedha, lakini unapokuwa huna fedha ndiyo unagundua ni vigumu kiasi gani kuendesha mahusiano yako na wengine.

Tuesday, January 1, 2019

MAMBO 18 YA KUFANYA KILA SIKU ILI KUPATA MAFANIKO MAKUBWA SANA.

1. Amka asubuhi na mapema sana, angalau masaa mawili kabla ya muda wako wa kuanza kazi.


2. Unapoamka cha kwanza kufanya shukuru, kwa sala au tahajudi.


3. Andika malengo yako makubwa kila siku unapoamka, malengo ya mwaka, miaka 5, miaka 10 na hata miaka 50. Lazima uwe na malengo ya aina hii.


4. Ipangilie siku yako kabla hujaianza, weka vipaumbele vyako kwa siku husika, viwe kati ya 3 mpaka sita. Andika kabisa nini utafanya na kwa muda gani wa siku hiyo.


5. Soma kitabu au pata maarifa yoyote chanya na ya hamasa kabla hujaianza siku yako. soma angalau kurasa kumi za kitabu kila siku.


6. Fanya mazoezi ya viungo kabla ya kuianza siku yako, mazoezi bora kabisa ni kukimbia.


7. Epuka habari au kitu chochote hasi muda wa asubuhi. Usisikilize redio, wala kuangalia tv au kusoma magazeti.


8. Unapoingia kwenye kazi au biashara yako, fuata vipaumbele ulivyoweka vya kufanya kazi, na unapokamilisha jukumu weka alama ya vema kisha nenda kwenye jukumu jingine.


9. Fanya jambo moja kwa wakati, usifanye mambo mengi kwa wakati mmoja, unapoteza nguvu na umakini.


10. Unapofanya kazi, akili na mawazo yako yote yawe kwenye kile unachofanya, usiwe unafanya kazi huku unafikiria vitu vingine.


11. Kula kwa afya, punguza sana vyakula vya wanga na sukari, kula matunda na mbogamboga kwa wingi na kunywa maji mengi zaidi, angalau lita tatu kwa siku nzima.


12. Ondoka kwenye mitandao yote ya kijamii unayotumia kama haikuingizii fedha moja kwa moja. Sheria ya kutumia mitandao ya kijamii iwe hii, iwe inakuingizia fedha moja kwa moja. Kama hakuna fedha inayoingia kupitia mitandao hiyo, achana nayo mara moja.


13. Acha kabisa kutumia kilevi cha aina yoyote ile, kuanzia pombe, sigara, madawa ya kulevya na hata viburudisho kama kahawa.


14. Kwenye kila kipato unachoingiza, sehemu ya kumi ya kipato hicho usitumie kwa namna yoyote ile, hicho ni kipato ulichojilipa na utakitumia kwa kuwekeza kwa ajili ya baadaye.


15. Imarisha sana mahusiano yako na watu wote wa karibu kwako, kuanzia familia yako, ndugu, jamaa na marafiki na pia wale unaohusiana nao kwenye kazi au biashara.


16. Imalize siku yako kwa kutafakari yale uliyofanya, matokeo uliyopata, makosa au changamoto ulizokutana nazo na namna unavyoweza kufanya kwa ubora zaidi siku inayofuata.


17. Lala mapema ili uweze kuamka mapema, kama hufanyi kazi za usiku, saa nne inapaswa kukukuta kitandani ukiwa umeshalala.


18. Tumia neno HAPANA mara nyingi uwezavyo, neno hapana ndiyo litakupa uhuru wako. Kama kitu hakikuwezeshi kufika kule unakotaka kufika, sema hapana bila ya kuona aibu.
Ndimi  MWL  JAPHET   MASATU, DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.
MOBILE  PHONE: WhatsApp +255 716924136 / +255 755400128 /   +255 688 361 539
EMAIL: japhetmasatu@gmail.com