Monday, January 14, 2019

TENGENEZA GEREZA LA AKIBA.

Kila mwaka malengo ya watu yamekuwa ni kuweka akiba kwa ajili ya uwekezaji. Na kweli wanaweka sana akiba, wanajinyima na kuanza kutengeneza akiba zao.
Lakini haupiti muda inajitokeza dharura ambayo inawapelekea kutumia zile akiba walizokuwa wamejiwekea, hivyo wanarudi sifuri kabisa, wanakuwa hawana akiba yoyote.
Rafiki, iwe una fedha au huna, dharura hazitaacha kutokea kwenye maisha yako. Hivyo njia pekee ya kulinda akiba yako siyo kuombea usipate dharura, badala yake ni kutengeneza gereza kwa ajili ya akiba yako.
Gereza hili ni kuweka akiba eneo ambalo huwezi kuitoa hata ardhi ipasuke. Na ukishaweka huko unasahau kabisa, hivyo kama dharura itakuja, utaangalia njia nyingine za kuitatua na siyo kuangalia akiba hiyo.
Magereza ya fedha yapo mengi, unaweza kuziweka kwenye akaunti maalumu, ambayo huwezi kutoa fedha hiyo mpaka muda uliochagua uishe. Pia unaweza kufungua akaunti ya pamoja na mtu mwingine na makubaliano yakawa ni hakuna kutoa hata iweje. Pia unaweza kutumia mitandao ya simu, ukapoteza namba ya siri ya mtandao wa simu unaotumia kuweka fedha ili isiwe rahisi kwako kutoa.
Angalia njia bora kwako ni ipi na itumie, usiache akiba yako ikakaa kirahisi rahisi kiasi kwamba ukiwa na shida kidogo tu unaitumia. Iweke kwenye gereza ambalo hutaweza kuitumia kabisa.

No comments:

Post a Comment