Thursday, January 17, 2019

EPUKA MABISHANO KWA KUFANYA HIVI.

Hakuna kitu kinachochukua muda wako na nguvu zako kama mabishano.

Mabishano ya aina yoyote ile ni gharama kwako na hakuna chochote unachonufaika nacho.

Na ipo njia rahisi sana ya kukuwezesha kuepuka kila aina ya mabishano.
 
Njia hiyo ni kukubaliana na watu waliojiandaa kubishana. Waambie wapo sahihi na kile wanachoamini na kusimamia ndiyo kweli. Hapo hawatakuwa tena na cha kubishana na wewe na kila mtu ataendelea na yake.
 
Lakini kama unataka ubishani uibuke, ambao hautaisha, mwambie mtu hayupo sahihi, mwambie amekosea na hapo utaibua ubishani usio na kikomo. Tena pale unapogusa kile ambacho mtu anaamini kweli, atatafuta kila njia ya kukitatua.
 
Kubaliana na watu haraka na endelea na mambo yako ambayo ni muhimu zaidi kuliko mabishano ambayo hayana manufaa yoyote kwako.
 
Kubaliana na watu na hawatakuwa na sababu ya kubishana na wewe. Na unapokubaliana nao haimaanishi kwamba wapo sahihi, ila hutaki kusumbuana nao. Ndani yako unaweza kujua kabisa kwamba hawapo sahihi, lakini huwaambii hilo maana ubishi utakaoanza hautakuwa na kikomo.

No comments:

Post a Comment