Saturday, January 30, 2021

INATOSHA KUWA UNACHOKIFANYA NI KIZURI HUHITAJI PONGEZI ZA WATU

 Mitandao ya kijamii imeteka watu wengi na kuwaumiza wengi pale ambapo watu wanashirikisha maisha yao au matukio fulani ili watu wengine wawapongeze au kuwafurahia “likes” au “Comments”. Ikitokea mtu kashirikisha kitu iwe picha yake na hakuna mtu yeyote anayesema umependeza au unaonekana vizuri basi watu wengi wanaumia kuwa inaonekana watu hawajapenda nilichofanya. Watu wengi wanakazana lakini wanaumia kuwa wanachokifanya watu hawatoi mrejesho.

Zama tuishizo zimekosa subira pia katika kuweka mambo ya siri kuwa siri na ya umma kuwa ya umma. Ila watu wengi utaona maisha ya siri au mambo ya faragha wanasukumwa kushirikisha wengine kwa nia mbalimbali na moja ni kupongezwa na watu wengine. Matarajio makubwa ambayo mtu anaweka kuwa akishirikisha atapongezwa na asipopongezwa huumia ndani yake. Huu ni mtego na utumwa ambao unawaendesha watu wengi wasio na udhibiti wa maisha yao.

Mstoa Marcus Aurelius nanukuu “A man when he has done a good act, does not call out for others to come and see, but he goes on to another act, as a vine goes on to produce again the grapes in season.” Hii ikiwa na maana “Mtu ambaye kafanya tendo jema, hapaswi ita watu wengine waje na kuona, ila huendelea na tendo lingine jema. Hufanya vile mzabibu utoavyo zabibu kila vipindi vyake”. Matendo mema hujitangaza yenyewe na hutoa mchango mkubwa kwa maisha bila msukumo wa pongezi au hongera toka nje.

Huhitaji pongezi ndo uendelee kufanya kitu chochote kilicho bora katika maisha yako. Ondoa haya matarajio na huu utumwa ambao utakuzuia kufanya mambo mazuri katika maisha. Ikiwa unachokifanya ni kizuri basi furaha ya ndani kukifanya inatosha na huhitaji kulazimisha watu watoe pongezi kwa ulichokifanya. Wengi huu mtego hunasa hasa pale ambapo wanafanya vitu vizuri na wanasukumwa kuwashirikisha wengine kwa lengo la kusikia “hongera” au “keep it up”. Ukikosa mrejesho huo utaumiza hisia zako na kama wanafalsafa hatuhitaji kuumia kihisia kwa vitu vilivyo katika udhibiti wetu.

Endelea kutenda yaliyo mazuri bila msukumo wa nje kufanya hilo. Nguvu kubwa ambayo unaweka katika kufanya yaliyo na mchango chanya yanatengeneza utoshelevu mkubwa ndani ya mtu atendaye. Hili linatosha na mengine yatakayotokea ni ya ziada si lazima yatokee. Si lazima watu wakupongeze kwa kazi nzuri unayofanya, si lazima kupongezwa kwa hatua nzuri ulofikia. Usikubali kuwa mtumwa wa kuhitaji wengine watambue unachokifanya. Kazi yako ni kutenda kilicho kizuri na hili latosha katika safari ya maisha mengine ni ya ziada tu.

Jifunze kufanya kitu kilicho kizuri au kupiga hatua nzuri katika maisha na usiumizwe na hali zozote zitakazojitokeza za watu kutojali ulichokifanya, kutokupongeza au kupata utambulisho au utambuzi wa mchango wako “recognition”. Hesabia kuwa sehemu ya pongezi si jambo la lazima kupata. Inatosha kufanya kazi nzuri na ndani yako kupata utoshelevu na furaha. Shinda jambo hili ili uwe na utulivu mkubwa ndani yako. Zoezi hili linaweza kuwa gumu kuanza ila ukishazoea hutakwamishwa na chochote kile wala kuumizwa na matarajio “expectations” unayoweka maishani.

Jitahidi kusoma kitabu cha mwandishi William Irvine cha “A Guide to Good Life” kikiwa kinampa msingi mwanafalsafa yeyote mchanga ambaye atapenda kujifunza falsafa ya Ustoa. Kisome na kiishi hakika utakuwa imara katika maisha yako.

KOCHA    MWL.  JAPHET   MASATU

WhatsApp  +255 716 924 136

USIPOTENGANISHA NGAZI HIZI TATU ZA MAHUSIANO , MAISHA YAKO YATAJAA FURAHA.

 Adui wetu wa kwanza katika chochote tunachotaka kukifanya katika maisha yetu ya kila siku ni Mwili. Mwili umeumbiwa tamaa katika asili yake na utumwa wowote wa maisha basi umekaa katika mwili wa mtu. Tamaa za mwili, tamaa za chakula, ulafi, ulevi vyote vinatoka katika utumwa wa mwili. Mwili unapokosa udhibiti toka ndani ya mtu ni njia rahisi ya maharibifu ya maisha kutokea. Hujaona watu wanavyobadilika kimaisha kwa kukosa udhibiti wa tamaa zitokanazo na mwili ?

Yote haya yanatokea katika mili yetu kwa kuwa hatutoi nafasi ya kujenga mahusiano mazuri na miili yetu. Hili ni kosa kubwa ambalo tunafanya na linatugharimu kushindwa kuishi maisha bora na ya kifalsafa. Mwili ndio ulio na ulimi, macho, miguu, via vya uzazi, ubongo, tumbo na kadhalika. Maeneo yote haya ya mwili yakikosa udhibiti toka ndani hutumika kuleta maisha ya mateso na masumbufu. Hebu fikiria unapokosa kutumia kiungo ulimi vizuri namna utaumiza wengine wengi kwa kauli zako au kutumia vibaya ubongo wako utafikiria mambo mabaya na yenye kuleta madhara kwa wengine.

Lini umekaa na kuushukuru mwili wako kwa mazuri na kuona ni chombo cha thamani kinachokupa heshima ya uwepo wako ?, Lini mwili wako umeupenda na kuupa chakula kizuri, maarifa safi, mapumziko na udhibiti wa mihemko?. Mahusiano mazuri unayojenga katika wewe na mwili wako ni mwanzo wa maisha bora na yenye furaha.

Hiyo ni ngazi moja ya mahusiano matatu makubwa ya maisha yetu. Maeneo mengine muhimu mawili ni “Utambuzi wa Asili yako Kiroho” na Tatu ni “Mahusiano ya Watu wanaokuzunguka Kutenda Haki na Ukarimu”. Ukiziweka ngazi hizi tatu kwa pamoja ni matokeo ya maisha bora na ya furaha.

Ngazi ya pili ya utambuzi wa asili yako kiroho ni mahusiano mengine ambayo watu wengi wamejisahau, wapo gizani na hawalipi uzito katika maisha yao. Kukosekana kwa mahusiano mazuri ya mtu na asili yake ndo panapozaliwa utupu “emptiness” ndani ya mtu. Hii utakuwa unaona mtu ni tajiri, maarufu, kiongozi mkubwa lakini asiye na furaha ndani yake licha kuwa mmiliki wa utajiri mkubwa. Mtu anaweza kuonekana nje ni mwingi wa utajiri ila ni maskini wa roho yake. Utajiri wa roho au utambuzi wa asili kiroho ni mahusiano yanayoleta tuone furaha na maana kubwa ya uwepo wetu katika maisha.

Ngazi hii ya kiroho inatupa kuwa na mtizamo mpana wa maisha. Inatupa tuweze kukabiliana na jambo lolote gumu linaloweza kujitokeza maishani. Ngazi hii inatuunganisha na umoja wetu wa asili na kuwa tu sehemu ya asili na tu wamoja. Ngazi hii inatukumbusha namna lolote tunalofanya kwa wengine si kuwa tunawafanyia hao bali sisi nasi tunaathirika kwa kutenda huko. Mahusiano ya ngazi hii ni sawa na pigo la maji na jiwe linavyoweza yatawanyisha wimbi moja hadi lingine. Ukikomaa ngazi hii utaona namna chochote kinachotokea katika asili kina maana na kinatufungua kufahamu mambo yaliyo zaidi ya kuona kwetu.

Ngazi ya tatu na ya mwisho na ngumu ni “kuishi na watu wanaokuzunguka”. Mtu aliye na jina jema kwa watu wengine utagundua kitu kimoja kikubwa anakimiliki ndani yake. Hicho kitu ni kuwa na mahusiano mazuri ya ngazi mbili tulizozungumzia. Hii ikiwa na maana ana mahusiano mazuri ya yeye mwenyewe “mwili wake” na ana mahusiano mazuri na utambuzi wa kuwa yeye ni mtu wa kiroho. Hutaweza kuona taabu kutenda haki na ukarimu kwa watu wote endapo ndani yako kuna utajiri wa kujua binadamu wote tumeumbwa kusaidiana na kutegemeana. Matatizo yote tunayofanyiana sisi binadamu kwa ubaya ni kwa kuwa ndani yetu tu maskini wa kujitambua na kutambua asili yetu ya kiroho. Watu wote walowahi kuishi na kuacha alama za matendo yao mema basi wana sifa kuu ya haki, ukarimu, upendo, kujitoa na kuwa tayari kufa au kuteketea ili wengine wapate kufaidika.

Hitimisho, navutiwa na kazi za Marcus Aurelius katika kitabu chake cha “The Meditations” ikiwa na maana ya “Tahajudi/Tafakari za Kina” akisema “You have three relationships: First, to your own body; second, to the divine Source of all life and existence; third, to your fellow human beings. And so you have three responsibilities: First, to use your reason to master your body and make right judgments; second, to gratefully accept all that happens in the universe; third, to treat all people with justice and generosity”.

Maana ya kifungu hapo juu Marcus Aurelius anasema “Una mahusiano matatu: Mosi, juu ya mwili wako: Pili, juu ya kiini chako cha kiroho na uwepo wako duniani: tatu, ni juu ya binadamu wenzako. Katika mahusiano haya matatu una majukumu matatu: Mosi, kutumia kufikiri na kuutawala mwili wako na kuamua sahihi; pili, kuwa mwenye shukrani na kukubali kila litokealo katika asili; tatu, ni kuwatendea watu wote haki na ukarimu”.

Yaweke haya mambo matatu pamoja mwaka 2021 na siku zote za maisha yako. Haitakuwa rahisi kwa kuanza lakini kadri unavyoweka nia ndivyo utakavyoendelea kuimarika kwa hizi ngazi zote tatu kwa pamoja. Utoshelevu mkubwa unaokuja kwa kuishi ngazi hizi tatu hauelezeki.

KOCHA    MWL.  JAPHET   MASATU

WhatsApp +255 716 924 136

JIFUNZE KUHUSU ASILI NA ULIMWENGU KUJIHUSU WEWE.

Mwaka 2020 nilikuwa nikijipa zoezi kubwa la kubadilisha kila juma lilolokuwa likipita kwa kulipa jina na kukisoma kitu hicho kwa kina na kukiishi. Nilifanya majuma mengi yaloenda kwa majina kama “Utulivu”, Muziki, Upendo, Machozi, Utoaji na Asili. Somo la asili nilikuwa nikishirikisha tafakari nyingi kuhusu asili kwa siku saba kupitia mtandaoni tu kwa njia ya kuta za mtandao “Status wall”. Somo hili lilipendwa na wengi na wengi waliona namna wanapata nguvu mpya kuona kumbe asili ni mwalimu na mtunza siri za nguvu kubwa za Maumbile mbalimbali ulimwenguni.  

Nikatia uzito zaidi wa somo hili la asili nilipoona na Marcus Aurelius Mstoa naye kaandika katika kitabu chake cha “The Meditations”. Namnukuu “The more you learn about nature and the universe, the more you learn about yourself. For without knowing where you are, you can’t know who you are, or the role you have to play”. Maneno haya yakiwa na tafsiri ya “Kadri unavyojifunza zaidi kuhusu asili na ulimwengu, ndivyo unavyojifunza mengi kujihusu wewe. Kama ilivyo usipojua utokako, ni Kazi wewe kujijua wewe ni nani au una kazi gani kubwa hapa “duniani” ya kufanya. Maneno haya ndio yanayoenda kubeba msingi wa barua yetu ya leo.

Asili ni mwalimu wa falsafa ya utoaji usiokoma. Ona jua linavyofanya kazi pasipo kuchoka kwa watu wote, ona namna usiku na mchana usivyokoma, ona namna asili ina mimea na wanyama ambao kwa mategemeano kuna chakula na hewa safi inayosaidia viumbe hai kuendelea kuishi. Ona namna asili licha kuwepo kwa vifo vya viumbe bado inaleta uzao mpya usiokoma vizazi hadi vizazi. Utoaji huu unafanya asili iendelee kustawi na kukua kusikokoma.

Asili ni mhifadhi wa hazina ya hekima kupitia vilivyomo kuanzia mimea, wanyama, watu, milima, bahari, mito na mabonde. Masomo makubwa ya maisha hutayakosa ukijifunza moja kwa moja kutoka katika asili. Watu hutalii maeneo mbalimbali duniani ili wajifunze maisha na kujifahamu zaidi. Hazina ya hekima iliomo katika asili haipimiki na haielezeki. Mimea hutufunza juu ya utoaji, juu ya ustahimilivu, juu ya utetezi wa uhai na juu ya upendo usiokoma. Mafunzo yamehifadhiwa na asili kwa viumbe wote wenye udadisi kuyafaidi na kujifunza.

Asili ina Nguvu zisizokoma zinazofanya kustajaabisha namna mambo hufanyika. Kila eneo la asili linaloonekana na lisiloonekana limefanywa katika nishati. Nishati au nguvu zimebeba maana ya maisha na nguvu hii haiharibiwi na chochote isipokuwa hubadilika umbile lake. Kila kitu unachokiona ni nishati kwa udogo wake. Karatasi unayoiona nayo ni nishati tulivu ambayo inaweza kubadilika kuwa nishati mwanga, sauti au joto. Choma karatasi ambalo awali uliona ni tulivu lisilo na madhara uone namna karatasi hilo linawaka, linaang’aza na kutoa sauti. Watu wote wanaojua wao ni sehemu ya hii Nguvu ya Asili hufanya mambo makubwa yasowezwa kupimwa.

Asili ina utajiri na utele kwa viumbe wake wote na haiwezi kukaukiwa kwa kuwa inatoa isivyo kawaida. Hutaona asili inaishiwa isipokuwa watu wanaokaa wanaweza tu kuharibu maumbile kwa hasara tunayoitengeneza wenyewe. Walio na utulivu na kupenda kuithamini asili basi ina wingi wa utajiri wa mambo yasowezwa kumalizwa na mtu awaye yeyote kwa mara moja. Kila kitu unachokiona kipo kwa ukubwa usioweza kubebeka. Unaweza kusema umeona mtu ni mkarimu au mwenye upendo ila hujakutana na mtu mwenye upendo kuzidi huyo.

Unajifunzaje kujihusu wewe kupitia asili?, tumeona asili ina nguvu na kuwa kila kilichomo ni nishati au nguvu ilofichwa katika maumbile tu. Watu wote bila kujali chochote kwa maana ya jinsi, umri au utaifa kuna nguvu ndani yetu. Kila kitu chenye umbile kina nguvu iliyofichika ndani yake. Nguvu ndio kiini cha maisha na matokeo makubwa yoyote tunayoyaona. Iwe ni ubunifu, kuamka kiroho, ugunduzi na utoaji ni muunganiko wa nguvu zilizopo ndani yetu zilizo mamoja na asili na mazingira yanayotunguka. Kadri unavyojifunza asili iwe kwa kutazama kwa utulivu na kupata kuzijua siri na ajabu zake, au kufanya tahajudi ndivyo unavyojikuta u sehemu moja na asili na huu ndio mwanzo wa kujua kusudi kubwa la uwepo wa mtu kuwa hapa Duniani.

Kusudi la mtu lipo katika nguvu ambayo inafanya njia kwa ajili ya watu wengine “Mtengeneza Njia”. Si watu wote hupata nafasi ya kuamka “uwezo wa kuona mbali” na kujitambua kuwa wana nguvu na wana uwezo fulani wa kufanya makubwa. Watu wanaopata nafasi ya kujitambua husaidia na wengine wajitambue na wajifahamu zaidi walivyo. Hili ni zao kubwa la kila anayejibiidisha kujifunza kutokana na asili na ulimwengu.

Tenga muda katika maisha yako kuwa na utulivu wa kutembelea maeneo tulivu kama mbuga, mashamba, misitu, sehemu za milima na pata saa za kutafakari na kutuliza akili uone namna asili iko karibu na wewe na inao utajiri mkubwa, upendo, makazi na nguvu kubwa ya kusaidia watu kuelekea kujitambua na kuamka kihisia, kimwili, kiakili hadi kiroho.

KOCHA   MWL.  JAPHET   MASATU

WhatsApp +255 716  924 136

WAWEZA KUPOTEZA BAADHI YA VITU , ISHI KWA KUTHAMINI VITU VINGI ULIVYONAVYO SASA.

 Nyakati nyingi huwa tunajisahau kukumbuka na kushukuru namna licha tutapitia magumu mengi katika maisha lakini bado tukawa hatujapoteza kila kitu katika maisha yetu ya kila siku. Inaweza ikawa imetokea ajali ila umeharibu gari pekee ila umepona wewe hujajeruhiwa na chochote ila unasahau kuwa umepona hilo ukakosa kushukuru. Watu wengi wanakosa kuona walivyobakiwa navyo baada ya kupoteza walivyokuwa navyo kwa kutokujua kuwa kila kitu tulichonacho sasa kipo kwa muda tu kuna siku tunaweza kuvipoteza.

Usiwe kama wengine wanaochukulia kiwepesi vitu walivyonavyo sasa. Usiwe kama watu wengine wasio na shukurani kuwa licha wamepitia magumu bado maisha yanaendelea mfano; bado wapo hai, hawajapoteza kila kitu kama wanavyolaumu. Marcus anatusisitiza namna tunahitaji kushukuru kwa kila kitu kuhakikisha kuwa tunashukuru kwa vile tumebakiwa navyo mbali na tulivyovipoteza.

Hivi umewahi kufikiria ulivyonavyo sasa ungekuwa huna ungesikiaje au kuishije?. Kweli unapitia magumu lakini una watoto, una afya, una ujuzi, una marafiki, una wazazi, una mke au mume. Vipi endapo licha kupoteza vingine ungepoteza na ulivyonavyo sasa ingekuaje. Ona haja ya kushukuru kuwa hujapoteza bali unavyo sasa. Usije kusahau kuwa kwa kila utakachokipoteza vipo utakavyobakiza na hata usipobakiza basi kuna jambo utajifunza kupitia kupoteza ulivyokuwa navyo.

Huwa tunachukulia kiwepesi baraka tulizonazo katika maisha kama kuwa na familia, kuwa hai, kuna na marafiki au watoto, uwezo wa kula au kutembea. Usichukulie kiwepesi vitu kama hivi ambavyo wengine hawana ila wewe unavyo. Hesabu Baraka zako namna unavyomiliki ni vingi pengine ulivyovipoteza. Utaona ukiwa unahesabu vitu ulivyonavyo ni vingi kuliko vile ulivyovipoteza.

Kuhesabu na kushukuru ulivyonavyo vinakupa nguvu na kuthamini zaidi ulivyoachiwa uendelee kuwa navyo. Watu wote wenye moyo wa shukrani wamekwisha kutambua kuwa kila kitu tulichonacho sasa kipo kwa mkopo au kuna siku kitaondoka. Watu hawa huthamini vitu hivi vinavyokuwepo kabla ya kutoweka kwake.

Ishi kila siku kana kwamba chochote kinachojitokeza kuwa tayari kukiona kama ni baraka. Unapotanguliza mtizamo huu kila kitakachokutokea utachagua upande chanya wa kitu hicho. Kila kinachojitokeza huwa kina pande mbili “Double handles”. Moja upande chanya na mwingine hasi. Hata kama utapoteza vitu vingi bado vitakubakizia somo kubwa namna unahitaji kushukuru pia kwa vidogo utakavyobakiziwa katika maisha. Ishi katika moyo wenye kuthamini na kuheshimu vitu vingi ulivyonavyo sasa.


KOCHA  MWL.   JAPHET   MASATU

WhatsApp  +255 716924136

Sunday, January 24, 2021

HATUA SABA( 07 ) ZA KUWAFIKIA WATU WENGI NA KUINGIZA KIPATO KUPITIA MAFUNZO UNAYOTOA MTANDAONI

Moja; Chagua unaowalenga.

Hatua ya kwanza kabisa kwenye biashara ya maarifa ni kuchagua watu gani unaowalenga na maarifa unayoandaa na kutoa.

Ndiyo unatoa maarifa ya hamasa, lakini je unataka kuhamasisha watu gani? Unataka kuhamasisha wanafunzi wafaulu? Au wafanyakazi wapige hatua? Au wafanyabiashara wakue zaidi kibiashara.

Kamwe usijidanganye kwamba mafunzo yako yanamlenga kila mtu, kwa kuanza na kila mtu unakuwa huna unayemlenga kabia. Utatoa mafunzo ya wazi ambayo hayamlengi yeyote na hivyo hakuna atakayekuwa anakufuatilia.

Nakumbuka wakati naanza kufanya biashara hii ya mafunzo, nilijifunza kuhusu kutengeneza msomaji unayemlenga, kumpa sifa anazokuwa nazo. Nilifanya zoezi hilo na mpaka sasa sehemu kubwa ya wasomaji wanaonifuatilia wanaingia kwenye sifa zile kwa kiasi kikubwa.

Jua kabisa maarifa yako yanawalenga watu gani, ili unapoyatoa yawe yanaenda kwao moja kwa moja badala ya kuwa ya wazi kwa wote. Cha wote siyo cha yeyote.

Mbili; Jua changamoto zao kubwa.

Ukishachagua watu unaowalenga kwenye maarifa unayotoa, jua changamoto yao kuu.

Kila mtu kwenye maisha kuna changamoto anakabiliana nayo, inayomzuia asipige hatua.

Hivyo lazima uwe na njia ya kujua wale unaowalenga wana changamoto gani. Inaweza kuwa kupitia maoni wanayoyatuma wanaposoma, kuangalia au kusikiliza mafunzo yako, inaweza kuwa yale wanayokutafuta uwasaidie na kadhalika.




Tatu; Wape maarifa ya kuvuka changamoto hizo.

Baada ya kujua changamoto kuu za wale unaowalenga, sasa mafunzo yote unayoyaandaa yanapaswa kuwa ya kuwasaidia kuvuka changamoto hizo.

Jua watu hawana muda kabisa, na hawaji kusoma kwa sababu umeandika, bali wanakuja kusoma kwa sababu wana changamoto, wana maumivu ambao hawawezi kuendelea nayo.

Hivyo kama unakuwa na maarifa yenye manufaa kwao, watakuja kuyapata ili waweze kuondokana na changamoto zao.

Kitu kingine kikubwa nilichojifunza wakati naingia kwenye tasnia hii ni kuhakikisha kwa kila mafunzo unayoandaa, kuna hatua ya mtu kuchukua, hata kama ni ndogo, lakini itakayompa matokeo tofauti.

Kuna ambao watafurahia tu kujifunza na kufurahia, hao huwezi kuwategemea sana, lakini wale watakaojifunza na kuchukua hatua kisha wakapata matokeo tofauti, unaweza kuwategemea kuwa wataenda na wewe kwa muda mrefu, watajifunza, watakulipa na wataleta watu wengine.

Hivyo andaa mafunzo yenye hatua za mtu kuchukua ili kuondoka kwenye changamoto zinazomkabili, kadiri anavyopata matokeo mazuri ndivyo atakavyoendelea kuwa na wewe.

Nne; Tengeneza mfumo wa watu kujiunga ili kupata maarifa zaidi.

Usijenge nyumba kwenye kiwanja cha kukodi, naweza kusema hili ni jambo nililojifunza kwenye hii tasnia na ambalo limekuwa na manufaa makubwa mno kwangu.

Iko hivi rafiki, unapotoa mafunzo kupitia mitandao ya kijamii, pale siyo kwako, hivyo chochote unachofanya huko, hakipo kwenye udhibiti wako. Unaweza kuwa na wafuasi wengi kwenye mtandao ya kijamii kama instagram, facebook, youtube na twitter, lakini jua mitandao hiyo ina nguvu ya kukufungia kwa sababu yoyote ile na ukapoteza kila kitu. Kama unafuatilia yanayoendelea duniani unajua raisi wa Marekani anayemaliza muda wake, Dinald Trump amefungiwa kabisa na mitandao mikubwa, pamoja na kuwa na mamilioni ya wafuasi kwenye mitandao hii.

Nilipojifunza dhana hii ya kutokujenga nyumba kwenye kiwanja cha kukodi, niligawa majukwaa kwenye sehemu tatu;

Sehemu ya kwanza ni mitandao ya kijamii, hii niliita ni kijiwe, unaweza kukutana na mtu kijiweni mkaongea mengi, lakini kile kijiwe siyo chako na mtu huyo anaweza asiwe rafiki kwako, mnakutana tu.

Sehemu ya pili ni blogu unayoimiliki mwenyewe, hii niliita nyumbani, mtu unayemkaribisha nyumbani kwako ni rafiki na unamwamini na yeye anakuamini zaidi ya yule mnayekutana naye kijiweni.

Sehemu ya tatu ni mfumo wa email (email list), hii niliita chumbani, mtu unayemruhusu kuingia chumbani kwako ni unayemuamini kweli kweli, na yeye anakuamini kweli kweli na kuwa tayari kufanya yale unamwambia.

Hivyo nikawa nashauri watu hili, kama upo kwenye mitandao ya kijamii, lengo lako siyo kujenga hadhira kule, lengo lako ni kuileta hadhira kwenye blogu yako. Na watu wakishafika kwenye blog, washawishi wajiunge kwenye email list yako.

Mitandao ya kijamii huimiliki, lakini blog ni yako, hata wakitaka kuifungia, bado unaweza kuipakua na usipoteze chochote. Email list ndiyo mali yako zaidi, maana hapo wasomaji wako wanakupa taarifa zao na mawasiliano yao, email na namba za simu. Hata kama jukwaa unalotumia kuendesha mfumo wa email watataka kukufungia, unapakua taarifa za wasomaji wako na kwenda nazo kwenye jukwaa jingine.

Pamoja na kushauri hilo kwa kina, bado wengi wamekuwa hawalipi uzito, sasa hivi nimeona watu wanafanya kosa kubwa zaidi, wanaandaa mafunzo na kuyatoa kwa njia ya wasap status, kitu ambacho siyo kibaya, ila mafunzo hayo yanapotea kila baada ya masaa 24, huoni ni kazi bure.

Nirudie msisitizo ambao nimekuwa natoa, kama unajihusisha na utoaji wa maarifa, iwe ni kwa kuandika, sauti au video, hakikisha unakuwa na hatua zote tatu, unatumia mitandao ya kijamii kuwaleta watu kwenye blog kisha kwenye blog unawapeleka kwenye email list yako na huko kwenye email ndiyo mambo mazuri yanaendelea.




Tano; Waombe wawakaribishe na kuwashirikisha wengine.

Wale ambao watakuwa wanajifunza kwako na kurudi mara kwa mara watakuwa wanakutumia shuhuda na kukushukuru jinsi ambavyo maarifa waliyopata kwako yamewasaidia.

Washukuru kwa hilo na wape ombi moja muhimu, wakusaidie kuwakaribisha wengine ambao nao wanaweza kunufaika kama wao.

Kuna njia mbili za kupata wateja wapya, kwa wewe kuwatafuta au kuwatumia wateja ulionao kuleta wateja zaidi.

Njia ya kutumia wateja ulionao huwa ina nguvu kubwa, kwa sababu mtu anayeambiwa na mtu wake wa karibu na anayemuamini aje kwako kujifunza, atazingatia zaidi kuliko akisikia wewe ukijinadi.

Kwa kila mfuatiliaji uliyenaye, lenga kupata watu wengine angalau kumi na kisha kuwa na njia mbalimbali za kuwashawishi walete wafuatiliaji zaidi. Hiyo ndiyo njia nzuri na ya uhakika ya kukuza hadhira yako.

Kuna njia nyingine za matangazo, unaweza kuzitumia lakini kwa uzoefu wangu huwa hazileti watu ambao ni bora.

Sita; Endelea kutoa kazi bora zaidi.

Kosa moja kubwa la kuepuka kwenye biashara ya maarifa ni ‘kukopi na kupesti’. Kama unachukua maarifa ya watu wengine na kuyafanya kama yako halafu unategemea upate wasomaji wanaokuamini na kuwa tayari kukufuatilia unajidanganya.

Unaweza kuwadanganya watu kwa muda, lakini baadaye watajua na hilo litakuwa anguko lako.

Kwa maarifa yoyote uliyochagua kutoa, toa mapya na halisi kabisa, kwa namna unavyoona wewe ni sahihi. Weka utu na upekee wako kwenye maarifa unayoyatoa kwa kuzingatia kuwasaidia watu kutatua changamoto zao.

Toa maarifa ambayo watu hawawezi kuyapata kwingine kule isipokuwa kwako tu na hicho ndiyo kitawafanya waendelee kuja kwako.

Na usihofie watu kuiba maarifa yako na kuyatumia kama yao, wewe toa kazi halisi, kazi bora na wale wanaokopi wanakutengenezea wateja wa baadaye, kuna siku watajua chanzo na kuja kwenye chanzo.

Saba; Tengeneza mfumo wa kuingiza kipato.

Nimalizie hatua ya mwisho ya kuchukua katika biashara hii ya maarifa, ambayo nimeona wengi wakifanya makosa makubwa hapa.

Wengi huingia kwenye biashara hii kama hobi, wanatoa maarifa kwa sababu ndiyo kitu wanapenda. Lakini kadiri wanavyokwenda wanajenga hadhira kubwa ambayo inataka mtu aipe vitu zaidi na zaidi. Mtu anajikuta akiendelea kutoa, mpaka inafika mahali anakuwa anatumia muda mwingi kuihudumia hadhira kuliko uwezo wake.

Lakini ubaya anakuwa ameizoesha hadhira hiyo kupata huduma bure kutoka kwake. Siku akipata wazo la kuitaka hadhira ilipie, inamuona kama mtu mwenye tamaa na hapo mtu anaogopa kuitaka hadhira imlipe, anaishia kuitumikia bure, kitu kinachokuwa kinamuumiza.

Usifanye kosa hili, wakati unaanza weka kabisa mfumo wa hadhira kukulipa. Yagawe maarifa unayotoa kwenye makundi mawili, kuna kundi la maarifa ambayo unayatoa bure kabisa halafu kuna kundi la maarifa ambayo ili mtu ayapate anapaswa kulipia.

Na watu wajue tangu mwanzo, mtu anapojifunza na kufurahia kisha kukutafuta akitaka zaidi, mwambie ndiyo yapo zaidi, lakini unalipia kiasi fulani kupata zaidi. Hapo unaijenga hadhira yako mapema kulipia ili kupata zaidi.

Kama umeshachelewa, tayari una hadhira kubwa na hukuweka mfumo wa kulipwa, anza sasa. Endelea na mpango wa maarifa ya bure unayotoa lakini anza mpango mwingine wa maarifa ya kulipia na ieleze hadhira yako kwamba kama kuna wanaotaka kujifunza zaidi basi kuna maarifa ya kulipia.

Andika vitabu kulingana na maswali yanayoulizwa sana na mtu anapokuomba ushauri kwenye eneo husika basi mwambie asome kwanza kitabu ulichoandika. Andaa kozi za kufundisha mtandaoni na mtu kulipia kujifunza. Kuwa na blog au kundi ambalo ili mtu aingie lazima alipe. Njia ni nyingi, angalia hadhira yako inataka nini zaidi, kuwa na viwango vya juu vya maarifa hayo na kiasi cha ada ambacho hadhira yako itamudu na weka mpango huo.

Rafiki yangu mpendwa, umejifunza mengi hapa kuhusu uendeshaji wa biashara ya maarifa, nihitimishe kwa kukuambia kitu kimoja, unaweza kuona kama soko la biashara hii limejaa na watu ni wengi, lakini mimi nimekuwa kwenye biashara hii kwa muda nakuambia kitu kimoja, soko halijajaa, fursa bado ni nyingi mno. Wengi wanaofanya biashara hii hawaifanyi kibiashara bali wanafanya kwa hobi. Watu wana changamoto nyingi ambazo wanakosa maarifa sahihi kuzitatua. Ukichagua unaowalenga na kujua changamoto zao kisha kuwaandalia maarifa bora ya kuzitatua huku ukijipa muda wa kujenga hadhira yako, kuna fursa kubwa.

Nikutakie kila la kheri kama tayari upo kwenye tasnia hii na nikukaribishe kama ndani yako una ujumbe ambao unasukumwa kuutoa na uko tayari kuweka kazi. Maana kingine kinachowaangusha wengi ni kufikiri ni njia ya haraka ya kupata fedha. Kwa uzoefu wangu binafsi, ndiyo watu watakuwa tayari kukulipa kiasi kikubwa ili wajifunze, lakini haitakuja haraka, imenichukua zaidi ya miaka mitano mpaka kuweza kuwatoza watu ada za juu kwenye mafunzo mbalimbali. Na hiyo yote ni kwa sababu nimekuwa naisaidia hadhira yangu kupiga hatua na kadiri wanavyopiga hatua wanaweza kumudu gharama zaidi.

Nakutakia utekelezaji mwema wa yale ambayo umejifunza,

Rafiki na Kocha wako

MWL   JAPHET   MASATU

 

CHANGAMOTO HAZIEPUKIKI KATIKA MAISHA.

 Tunaishi katika zama ambazo watu wanakumbana na matukio mbalimbali na kupitia matukio hayo wanapoteza utulivu mkubwa wa ndani. Utulivu unapopotea ndani ya mtu maisha nayo huanza kuvurugika kabisa. Kufukuzwa kazi, mahusiano yamevunjika, biashara imeanguka, soko limeshuka, magonjwa yamejitokeza matukio kama haya yanapotokea kwa mtu, basi wengi hupata masumbuko ya moyo na wanapoteza ustahimilivu ndani yao.

Falsafa ya Ustoa si kuwa inakuandaa usiwe mtu wa hisia la hasha bali kukusaidia kuwa mtu ambaye hata katika lolote litakalojitokeza uwe imara ndani yako. Ukikosa uimara ndani yako umekosa kitu kikubwa maishani. Maisha hayataacha kutupa changamoto, magumu, matatizo si kutuharibu ndani yetu ila kutupa ukweli wa maisha kuwa maisha hayatakosa magumu toka kuzaliwa kwetu hadi kufa kwetu.

Magumu ni vikwazo ambavyo unaona vinatokea njiani au katika safari ya maisha. Kinapojitokeza kikwazo tu basi eneo moja linalojeruhika haraka ni hisia zetu kuhusu yale yalotokea. Kinachotuumiza wakati wote kwa matukio yoyote ambayo hujitokeza ni tafsiri ambazo huwa tunazitoa kuhusu yalotutokea. Tafsiri yako kuhusu mambo ndio inayokuumiza siku zote na inakutengenezea ugumu katika mambo.

Marcus Aurelius anasema “The first rule is to keep an untroubled spirit. The second is to look things in the face and know them for what they are.” Hii ikiwa na maana “Sheria ya Kwanza ni Kutoruhusu Roho Kusumbuliwa. Pili ni Kuangalia Mambo Jinsi yenyewe Yalivyo – Sheria ya kwanza ni kuzuia roho kusumbuliwa na pili kuyaacha mambo jinsi yenyewe yalivyo. Hizi sheria mbili zinaweza kukusaidia kukabiliana na magumu ambayo utayapitia katika safari ya maisha.

Chochote kile ambacho kitakutokea uwe umetarajia au hujatarajia kitakupima juu ya uimara wako ndani. Ikiwa jambo litajitokeza na huna uwezo wa kuhimili ndani basi litakuharibu na kukuyumbisha. Watu wote ambao tunawaita hodari si kuwa mambo wanayokutana nayo ni mepesi hapana ila wana nguvu ya kustahimili toka ndani wakijua lilijitokeza limekuwa hivyo na wanabadili namna la kuliona.

Pili kubali mambo yanavyotokea kuwa imekuwa hivyo yametokea. Ondoa tafsiri yako kuhusu chochote kinachotokea maana kuweka tafsiri yako ni kuandaa mazingira ya kujiumiza na huo ndo mwanzo wa masumbuko makubwa katika maisha. Usisumbuke na mambo yanavyotokea ila imarishwa katika kuwa na utulivu kwa lolote ambalo litatokea. Usiyumbishwe na chochote au kushangazwa na chochote maana maisha yatakutana na ugumu ambao hautakoma hadi tunahitimisha ukomo wa maisha yetu.

Ili utunze utulivu ndani yako basi tambua kuwa njia ya maisha itakumbana na mfululizo wa magumu yasokoma. Ukweli huu unapokubali unakusaidia kuwa hodari na shujaa kuwa hili ambalo limejitokeza au litakalojitokeza limepaswa kuwepo na si kulaumu ila kuwa na ustahimilivu na nguvu ya kufurahia maisha. Maisha licha yatabakia na ugumu ila namna unavyoona mambo na kuyatafsiri itakupa wepesi wa mambo mengi na matukio ya kimaisha yanayoendelea kutokea. Tunayoyapitia zama hizi walowahi kuishi nao walipitia na njia ya maisha imeendelea kuwa na magumu tofauti tofauti kulingana na nyakati.

USIWAHUKUMU WATU HARAKA HUJUI KILICHOWASUKUMA KUFANYA HIVYO.

Kuna namna umewahi kuwahukumu watu katika maisha yako bila kujua ulihukumu haraka kabla ya kujua ukweli wa mambo ulikuaje. Mfano unaweza kumpigia mtu simu na isipokelewe ukaanza kuhukumu ndani yako kuwa huyu mtu mbona hapokei simu, kanidharau, hajali au si mtu makini. Ila huwezi jua ni kwanini hajapokea simu yako. Je huenda yupo mbali na simu utajuaje ?, huenda simu ipo katika chaji, huenda anafanya kitu ambacho kitamzuia kupokea simu kama kusali au kuswali ?. Ila wengi huwa tunahukumu mapema pale ambapo tulotegemea halijafanyika hivyo.

Mahusiano mengi ya watu hasa ya kimapenzi yamevunjika na mengine yakiwa katika misuguano isokoma kwa watu kuhukumu haraka bila kujua kwanini hali hiyo imejitokeza kwa watu wengine. Mfano mdogo ni ule ambao mpenzi mmoja anapiga simu na anakuta simu ya mwenza wake ikitumika “The number you are calling is on another call” ikiwa na maana namba unayopiga inatumika. Wengi huanza kuhukumu mapema kuwa huenda wenzi wao si waaminifu wanazungumza na michepuko yao. Ila je mtu amewahi fikiria vipi anayezungumza naye akiwa mzazi wake, mfanyakazi mwenzake, wateja na kadhalika.

Tumekuwa wepesi sana kuwa na hisia hasi juu ya watu pale ambapo mambo hayaendi vile ambavyo tulitaka iwe. Umepita sehemu na kumsalimia mtu hajakujibu basi unatoka na tafsiri yako kuwa huyu mtu anajiona siku hizi, anadharau au hathamini watu wengine. Huwezi jua kwanini hajaitikia salamu yako. Vipi ikiwa hakusikia, vipi ikiwa ana mawazo mengi katika akili yake au vipi huenda amepokea taarifa mbaya hajatulia. Ila kwa kuwa huwa tunategemea mambo na yasipotokea tunaumia au kuhukumu mapema. Mambo si hivyo huwa wakati wote tutegemeavyo.

Mfano mwingine ni pale ambapo mtu anakutusi. Kutukanwa ni kitu kinachoumiza sana hasa kuumiza hisia endapo utaendelea kufikiria ulichotukanwa. Mtu anayekutukana ukihukumu haraka haraka utaona amekudharau au kukushusha ila ukitulia na usipojibu kuhusu tusi lake na ukatafakari unaweza kujifunza mengi. Unaweza kujiuliza kwanini kaamua kunitukana, je nini kilichomsukuma kunitukana ?. Hapo unaweza kugundua mengi juu ya mtu huyo kuwa huenda ni matokeo ya malezi mabovu aloyapata hivyo ni maisha anayoishi, huenda mtu anayekutusi anatumia njia hiyo kujilinda au kujihami na tatu huenda ni mtu asiyejitambua. Unapoona kitu kwa mfumo huo hutakuwa unahukumu watu haraka bila kujua kwanini wamefanya ulichokiona.

Falsafa inatufundisha kuwa watu wenye kufikiri na kuamua vizuri na si kuongozwa na hisia. Mtu anayehukumu haraka jua kuwa bado hajakomaa katika kufikiri bali anateswa na hisia zake. Unahukumu mara nyingi katika kutofika kwa matarajio yako na mategemeo. Mtu aliyekomaa kifikara na kifalsafa huongozwa na kudadisi na kujiuliza maswali katika yote ambayo hujitokeza na kuja na njia nzuri ya kukabiliana na kitu au hali ilojitokeza.

Tutaendelea kuishi na watu wa kila aina na usiwe mwepesi kuhukumu bila kujua kwanini watu wamefanya hivyo. Utakapojua sababu za wao kufanya hivyo utajikuta ulihukumu haraka kabla ya kujua ukweli wa mambo ulivyo. Tumewahukumu watu wengi bila kujua kilichokuwa nyuma ya pazia kilikuwa kitu gani. Kila litakalotokea usiongozwe na hisia bali fikiri kwanini au ni msukumo gani ulofanya watu au mtu kufanya alichokifanya.

Tunapojua kwa undani kwanini watu wamefanya hicho walichokifanya bila kuwahukumu ni njia rahisi ya kuweza kuwasaidia zaidi.

 

KOCHA  MWL.  JAPHET  MASATU

WhatsApp  + 

 

MUDA WA KUTIMIZA NDOTO ZAKO NI SASA . ISHI UKIWA TAYARI KUAGA KILA DAKIKA INAYOPITA.

Muda wa sasa ni wa thamani kubwa mno ila watu wengi hawatalii maanani. Thamani ya maisha yetu hufungamanishwa na muda. Unaweza kupima maisha ya mtu kupitia muda na yale ambayo amejitoa kufanya. Mtu anapokufa huandika siku ya kuzaliwa na mwaka na siku ambayo alokufa. Utaona inaitwa RIP fulani xxxx alizaliwa 9/02/2021- kufa 9/7/2067 kinachopimwa hapa ni muda na mchango wa mtu katika siku za kuishi kwake.

Kuna watu ambao wameishi muda mrefu ila mchango wao unaweza kuwa mdogo na wengine wameishi muda mfupi ila mchango wao ukadumu miaka mingi. Utofauti ni namna kila dakika moja yao walivyoweza kuipa uzito na kuishi kitoshelevu kila siku. Ingekuwa kila mtu anajua siku atakayokufa na iko wazi kwake atakufa siku fulani, mwezi fulani au mwaka fulani sidhani kama mtu angekuwa yu tayari kupoteza hata dakika moja ya kuishi.

Tafiti zinaonesha wazi duniani kote kuwa watu ambao wanapokea taarifa za kuwa maisha yao hayatadumu bali watakufa katika kipindi kijacho cha muda. Jambo moja kubwa huambatana na watu hawa huanza kuishi kitoshelevu na kujali kila nafasi ya pumzi yao maana wanajua hawana muda mrefu wataendelea kuwepo. Watu wenye hatua mbaya za saratani ni moja ya makundi ambayo wakati mwingine hupokea taarifa toka kwa wataalamu wa afya kuwa kutokana na namna saratani ilivyoenea au kukua kiasi cha kuyatoa maisha hawana siku nyingi watakufa tu. Je unajisikiaje unapojua ndani ya miezi sita ijayo utakufa ?

Si hilo tu hutokea kwa wale wanaojua watakufa siku sio nyingi pia kuna kundi la watu ambao hunusurika na ajali, walowahi kuwa mahututi na walonusurika vifo mbali na ajali au umahututi. Watu hawa hujenga mtizamo mpya kabisa kuhusu maisha kuwa nafasi ambayo wanayo sasa walipaswa wasiwepo kutokana na kupona katika ajali ambazo watu hawakutegemea endapo wangepona au namna walivyokuwa mahututi watu hawakutegemea endapo wangeinuka tena. Ikitokea wamepona na kuishi tena ile hali ya kujali nafasi ya pumzi huthaminiwa sana.

Je tungoje kuwa tuna nafasi ndogo ya kuishi ?, ndipo tuanze kuishi ndoto zetu?, au kuanza kuihudumia jamii zetu kwa vipaji, uzoefu, hekima au maarifa. Je tungoje tupone katika mambo mazito tutambue thamani ya kila dakika moja ya maisha yetu. Kama wanafalsafa hatungoji kufika hizo hali bali tunaanza sasa kuthamini kila dakika ya maisha yetu tukijua hii dakika moja tunaweza tusiirudie tena au kuipata kwa siku za baadaye.

Weka uzito wa kila dakika ambayo unaipata maishani ukijua kuna watu ambao ndani ya dakika moja wapo wanaokufa, wapo wanaopata ajali, wapo wanaokata pumzi mahospitalini. Hivyo ukiwa na mtizamo wa juu wa kuyaona mambo hivi basi unasukumwa kila siku kuhakikisha unatumia nafasi ya pumzi na muda kuchangia mambo chanya kwa jamii, kuisaidia jamii kimaarifa na kiutambuzi na kuliishi kusudi la uwepo wako.

Hofu kubwa ambazo hutokea pindi maisha yetu yanapokaribia kuisha na tunapopata fursa ya kujua tuna muda mfupi wa kuishi ni hofu mbili kubwa. Hofu ya kwanza ni majuto ya kuwa tulikuwa na muda mwingi ila hatukuishi kitoshelevu au kutumia vipaji au mawazo kwa ukubwa. Pili ni hofu juu ya ulimwengu ujao kuwa je baada ya mwili wetu kuharibika na pumzi kutoweka nini kitakachofuatia. Hilo ni fumbo kubwa la kiimani ambalo mifumo mbalimbali ya dini inaelezea mengi. Fumbo hili gumu kwa kuwa hakuna aliyekufa na akaenda kutafiti na kurejea kusema maisha baada ya kifo yakoje

Ishi maisha kitoshelevu ukiwa unathamini kila dakika unayopata kuwa huenda ndio nafasi ya mwisho kuishi au kutenda jambo fulani. Umeonana na mtu fanya kitu ambacho unajua usipofanya leo basi huenda usipate nafasi hiyo tena katika maisha yako. Unaandika kitu au kitabu kama ndo kitabu unachoandika na hutaandika tena. Kujenga mtizamo huu ni kazi kwa kuanza ila kadri unavyojituma na kuishi hivi utaona siku zako za kushiba hata kifo kitakapokuja hutakuwa na kitu ulichobakiza kuihudumia Dunia. 

KOCHA  MWL   JAPHET   MASATU

 ( WhatsApp  + 255 716 924  136  )

 

JIULIZE MWENYEWE : JE, HIKI NACHOTAKA KUFANYA KINA ULAZIMA ?? NI MUHIMU SANA ?

Tumeingia katika matatizo mengi maishani kwa kujaribu kuona kila tunachokiona au kuambiwa na watu lazima tufanye. Maumivu na masumbuko mengi kumbe yangeepukika kwa kutoyaona ni mambo ya lazima kufanya. Watu wameingia katika shida hizo mf. Kutuma picha za kila unachokifanya kiwe mtandaoni na baadaye kimewagharimu watu wengi. Je hiki nachotaka kukifanya kina ulazima inaweza kuwa njia ya kwenda kuepusha matatizo mengi ya mtu kujitakia.

Mtu amekutukana, tulia na jiulize swali hili je kumtukana ni lazima ?, je kulipa kisasi na mimi kwake ni lazima?, kama utajiuliza swali hili mara nyingi basi utaona hakuna ulazima wa kumtusi mtu wala ulazima wa kulipiza kisasi. Kutofanya ulivyopanga kufanya kama wengine ambavyo wangefanya kunakuepusha na mambo mengi. Vipi mtu amekutana na wewe umtusi, je wajua athari zinazoweza kujitokeza hapo ?. Jiulize usichoke swali la je hiki nachotaka kufanya kina ulazima nifanye ?.

Umepata fedha nyingi, na tunavyojua unapokuwa na fedha nayo inakufungua akili ya matumizi ambayo hayakuwepo kabla ya kuwa na pesa. Jiulize je hiki nachotaka kufanya kina ulazima?. Je starehe, pombe, sigara na aina zote za starehe una ulazima kufanya kwa sababu unazo pesa ?. Ukitulia utaona mambo mengi unayotaka kufanya si lazima uyafanye na hili linakusaidia kuepuka matokeo ambayo kwa baadaye unayajutia kwanini ulifanya.

Zama tuishizo sasa hatuwezi kusahau namna fursa mpya mpya kila siku zinaibuka na watu wanakimbizana na kila fursa na mwisho hakuna wanachoambulia kizuri zaidi ya kupoteza muda, nguvu na fedha. Jiulize wakati wote je hii fursa ambayo imekuja kwangu ni lazima niiendee au ni lazima nijiunge nayo?. Utaona fursa nyingi si lazima ujiunge nazo au kukimbizana nazo kila kukicha. Jiulize wakati wote swali hili utajiepusha na matatizo mengi yakuepukika kabisa.

Usije kusahau kuwa marafiki wana nguvu kubwa katika maamuzi ya mambo yetu katika maisha. Mahusiano yao kwetu yanaweza kutuathiri kirahisi zaidi. Na kuna nyakati ambazo unakuwa na msimamo wako wa jambo ila marafiki wanakulainisha unasahau ulichopanga unawafuata wao. Jiulize kila wakati je hiki nachotaka kukubali au kufanya kutokana na hawa rafiki zangu ni lazima?. Najua unaweza kutengwa na watu unapokuwa umesimamia msimamo wako kuachana na mambo ambayo si lazima uyaunge mkono au kuyafanya.

Kadri unavyotumia hii kauli kwa kila muda unapokutana na hali au tukio lolote maishani inakusaidia kuwa na utulivu na kutokuwa mtu unayetumikishwa na hisia. KUANZIA   SASA  kwa kila utakalokuwa unakutana nalo basi jiulize, Je hiki nachotaka kufanya kina ulazima ? Muhimu sana ??

KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU

+ 255 716924136 ( WhatsApp ) /  + 255 755 400128  /  + 255 688 361 539 /   + 255 629  748 937

EMAIL :  japhetmasatu@gmail.com

 

Saturday, January 23, 2021

TUNATEGEMEANA NA TUNAHITAJIANA KILA SIKU ILI MAISHA YAENDE.


Hakuna mtu anayeweza kusimama kwa ujasiri na kujipiga kifua mara nyingi nakusema nimeyaweza haya yote kama jeshi la mtu mmoja. Mtu huyu anayesema haya basi hajui maisha ni muunganiko na hakuna mtu awezaye kujisifu na kusema kafanya yote mwenyewe bila kuhitaji watu wengine. Utasema umefanikiwa kibiashara lakini je bila wateja kuja katika biashara yako ungefanikiwa ?

Kila kitu unachokifanya na kufanikiwa jua kuna pahala umehitaji msaada au umetegemea watu wengine. Mf umenunua gari na kuweza kujisifu kuwa unamiliki gari lakini ukiangalia kwa ndani si wewe uliyefanya ubunifu huo wa gari bali pana watu ambao wametengeneza na wewe umepata matokeo tu ya ubunifu wao. Huwezi jidai hapa kusema unaweza kila kitu mwenyewe bila kuhitaji wengine au kutegemea wengine.

Maisha yetu ni muunganiko wa vitu na vyote vyakaa katika umoja siku zote. Kuna msemo rahisi na huwa tunausikia sana “Umoja ni Nguvu”. Umoja ni nguvu kwa maana ya maisha unahitaji nguvu kutoka kwa watu wengine, utawahitaji wengine na utawategemea wengine ili katika umoja huo upate matokeo makubwa. Watu ambao wanaona ni wao wamefanikiwa kwa nguvu zao basi husahau mchango wa watu wengine ambao walijitoa kwa ajili yake.

Huwezi kusimama mwenyewe katika safari ya maisha. Ikiwa hata maiti husaidiwa basi ni zaidi ya mtu aliye hai ambaye kila hatua ya maisha yake inahitaji watu na kutegemea watu. Hili lilionwa toka zamani katika maisha ya wastoa kama Marcus Aurelius ambaye katika maandiko ya notibuku yake anaonesha namna ya kutambua mchango wa kila mtu katika maisha yake kuanzia utoto hadi utu uzima ikihusisha vipindi mbalimbali vya maisha. Hili linamshawishi kuandika kuwa tumeumbwa kwa ajili ya wengine.

Marcus Aurelius anasema “Meditate often on the interconnectedness and mutual interdependence of all things in the universe. For in a sense, all things are mutually woven together and therefore have an affinity for each other – Marcus Aurelius. Hii ikiwa na tafsiri iso rasmi “Tafakari nyakati zote juu ya muunganiko wetu sisi binadamu na mategemeano ya kila kitu katika asili. Jua kuwa kwa namna moja tunaunganishwa na kutegemeana kwa ukaribu kati ya mtu mmoja na mwingine”. Ni maneno mazito na fikirishi sana.

Ubinafsi wa watu na kuona wanaweza kufanya kila kitu ndiko kunachelewesha watu wengi kufanikiwa. Watu ambao wanakuwa wazito kuhitaji msaada au kutegemea watu wengine hawajajua maisha kwa upana. Kwa kuwa hakuna ambaye kapewa kila kitu ndani yake isipokuwa vingine vingi vipo kwa watu wengine. Hili ndilo ambalo linatualika kutegemeana na kuhitajiana maisha yetu ya kila siku ili yaende.

Ishi siku zote katika kuwa sehemu ya muunganiko wa kutegemeana na kuhitajiana. Kuna vitu vingine utavipata kwa wengine ukiwa tayari kujitoa na kujua maisha ni mategemeano na kuhitajiana. Tumeumbwa kuhitajiana kama ulivyo mwili na viungo vyake vinavyofanya kazi katika kusaidiana na kushirikiana.

Saturday, January 2, 2021

JINSI UMASKINI UNAVYOHARIBU AKILI NA JINSI YA KUEPUKA MTEGO WA UMASKINI.

Umasikini siyo tu ni mzigo na kikwazo kwa mtu kuwa na maisha bora na yenye uhuru, bali pia ni laana ambayo inamfanya anase kwenye maisha ambayo hawezi kujinasua.

Utafiti ambao umewahi kufanywa nchini Marekani na India unaonesha kwamba umasikini huwa unaharibu akili ya mtu.

Utafiti huo ulionesha kwamba wale wanaoishi kwa umasikini, wana upungufu wa alama 13 za kipimo cha akili (IQ) ukilinganisha na wale ambao hawaishi kwenye umasikini.

Kwa lugha rahisi na ya kueleweka vizuri ni kwamba umasikini unawafanya watu kuzidi kuwa wajinga.




Swali unaloweza kujiuliza ni kwa namna gani umasikini unaharibu akili za watu na kuwafanya kuwa wajinga?

Jibu liko wazi, masikini anakuwa ametingwa zaidi na mawazo ya hali ngumu anayokuwa anapitia, hivyo akili yake inakuwa imechoka muda wote. Inapokuja kwenye uhitaji wa kufikiri mambo makubwa na magumu, masikini hawezi kufikiri kwa usahihi, kwa kuwa akili yake tayari imeshachoka.

Chukua mfano wa watu wawili, wana elimu sana na wanafanya kazi ya aina moja. Mtu A ni tajiri na B ni masikini. Mtu A ameamka asubuhi, kapata kifungua kinywa kizuri, kaingia kwenye gari yake binafsi na kwenda kazini. Mtu B ameamka hana hata kifungua kinywa, anaenda kazini kwa kutumia usafiri wa umma ambao ni wa shida na hajui siku hiyo atakula nini, wakati huo huo kuna watu wanamdai na wanamtafuta sana. Watu hao wawili wanapewa jukumu moja la kukamilisha, ambalo linahitaji utulivu wa akili ili kulikamilisha, unafikiri yupi atalikamilisha kwa umakini?

Unajionea mwenyewe hapo, jinsi ambavyo umasikini unakuwa mzigo ambao unaharibu akili ya mtu na kumfanya awe mjinga.

Umasikini unapunguza uwezo wa mtu kufikiri na kufanya maamuzi kwa sababu muda mwingi akili yake inakuwa imetingwa na fikra na hofu mbalimbali.

Mbaya zaidi sasa, na hapa ndipo ilipo laana ya umasikini, ni pale uwezo mdogo wa kufikiri unapomfanya mtu afanye maamuzi mabovu zaidi na yanayomfanya abaki kwenye umasikini.

Tuendelee na mfano wa mtu B, ambaye anafikiria siku yake inaishaje, maana mshahara umeshaisha na mwezi ndiyo kwanza uko katikati. Anasikia kuna mtu anatoa mkopo wa haraka ila una riba kubwa. Kwa sababu anachohofia zaidi ni fedha na hawezi kufikiri kwa usahihi, anajikuta anachukua mkopo huo. Anakuja kulipa mkopo kwa riba kubwa, kitu kinachopunguza kipato chake zaidi.

Maamuzi mengi ambayo mtu anasukumwa kuyafanya akiwa masikini huishia kuwa maamuzi ya kumuumiza zaidi na kumfanya abaki kwenye umasikini.

Unaondokaje kwenye mtego na laana hii ya umasikini?

Umejionea hapo jinsi umasikini unavyoharibu akili na kumnasa mtu kwenye umasikini zaidi.

Kama bado hujafikia uhuru wa kifedha, kama bado unategemea kipato unacholipwa kwa kufanya kazi au biashara ndiyo uendeshe maisha yako, haijalishi kipato hicho ni kikubwa kiasi gani, upo kwenye hii hatari.

Hivyo hatua muhimu kwako kuchukua ni kujijengea uhuru wa kifedha. Na hapa kuna maeneo sita muhimu ya kufanyia kazi ili kuondoka kwenye mtego na laana ya umasikini.

Eneo la kwanza ni kuongeza kipato chako. Kipato chochote unachoingiza sasa hakiwezi kukutosha, gharama za maisha zinachukua sehemu kubwa ya kipato chako. Hivyo pambana kuongeza kipato chako. Kama umeajiriwa anzisha biashara ya pembeni. Kama upo kwenye biashara ongeza huduma na bidhaa zaidi na wafikie wateja wengi zaidi. Kwa kipato chochote unachoingiza sasa, pambana kukikuza zaidi.

Eneo la pili ni kudhibiti matumizi yako. Matumizi huwa yana tabia ya kukua kadiri kipato kinavyokua. Usipoyadhibiti, ongezeko la kipato ulilopambana nalo halitaleta tofauti kwenye maisha yako, badala yake litakuwa limekuchimbia kwenye umasikini zaidi. Dhibiti matumizi yako kwa kuhangaika na yale ya msingi pekee, hasa kama unaanzia kwenye umasikini wa chini kabisa.

Eneo la tatu ni kuwa na akiba ya dharura ya miezi 6 mpaka 12. Kama unaishi maisha ya mkono kwenda kinywani, yaani unafanya kazi, unaingiza kipato na unakitumia chote, basi upo kwenye hatari ya umasikini kuharibu akili yako zaidi. ukipata dharura yoyote ile, iwe ni kazi kusimama au biashara kuyumba, utaanguka vibaya mno. Hakikisha unakuwa na akiba ya kukuwezesha kuendesha maisha yako kwa miezi sita mpaka 12 hata kama hutakuwa na kipato kabisa. Unapokuwa na akiba ya aina hii, unapata utulivu mkubwa ndani yako na kuweza kufanya maamuzi sahihi kwako. Mfano kama umefukuzwa kazi na huna akiba, utalazimika kufanya kazi yoyote hata kama haikulipi, kwa sababu unataka kipato cha kuendesha maisha. Lakini kama umefukuzwa kazi na una akiba ya miezi 12 ya kuendesha maisha, unaweza kusubiri kwa muda mpaka upate kazi nzuri, maana akiba ya kuendesha maisha ipo.

Eneo la nne ni uwekezaji. Huwezi kufanya kazi muda wote na kila muda ambao hufanyi kazi hunufaiki. Unapaswa kuwa na njia ya kuingiza kipato hata kama hufanyi kazi moja kwa moja. Na njia ya kufanya hivyo ni kuwa na uwekezaji ambao unazalisha faida na kukua thamani kadiri muda unavyokwenda. Unapokuwa na uwekezaji unaozalisha faida kubwa ya kukuwezesha kuendesha maisha yako hata kama hufanyi kazi moja kwa moja, unakuwa umefikia uhuru wa kifedha.

Eneo la tano ni kulipa madeni ambayo unayo. Kama umekopa, pambana kulipa madeni yako kwa kutumia ongezeko la kipato ulilofanyia kazi.

Eneo la sita ni kuacha kukopa. Usikope tena, rahisisha maisha yako, punguza yasiyo muhimu na kama kitu huwezi kukimudu jipe muda. Vitu vingi unavyoingia kwenye madeni ili kuwa navyo ni vitu ambavyo siyo muhimu sana kwako. Ukiacha kuiga maisha ya wengine na kuchagua kuishi maisha yako, hutahangaika na mikopo inayokusumbua.

Zingatia maeneo hayo sita ili kuweza kuondokana na mtego na laana ya umasikini.

Ndimi   KOCHA  MWL.  JAPHET  MASATU ,  DAR  ES  SALAAM

 ( WhatsApp + 255 716 924 136 ) /  + 255 755400128 /  + 255 688361539

EMAIL : japhetmasatu@gmail.com

 

Friday, January 1, 2021

JINSI YA KUINUKA BAADA YA KUANGUKA KAMA UMEJAJAIRI.

Karibu kwenye makala ya ushauri wa changamoto mbalimbali zinazotuzuia kufikia mafanikio makubwa tunayotaka.

Kwenye makala ya leo tunakwenda kupata ushauri wa jinsi ya kuinuka na kuendelea na safari baada ya kuanguka kwenye kujiajiri.

Kabla ya kupata ushauri huo, tupate maoni ya msomaji mwenzetu ambaye ametuandikia kuomba ushauri kwenye hilo.

Niliacha kazi nilioajiriwa ili niweze kujiajiri kwenye Kilimo na Ufugaji, toka 2017 lakini mambo mwanzo yalienda sawa ila ,kwa sasa 2020 Nimeanguka kwenye kilimo na mtaji kwa ujumla. Naomba ushauri nifanyeje? - Mdachi K. J.

Msomaji mwenzetu ametushirikisha changamoto yake ya kuanguka kwenye kujiajiri baada ya kuachana na ajira, ambapo mwanzoni mambo yalikwenda vizuri ila baadaye yakabadilika.

Hii ni changamoto ambayo kila ambaye amewahi kupambana kufanikiwa ameshaipitia na ni sehemu ya kupikwa ili uweze kupokea mafanikio makubwa zaidi baadaye.

Anguko ambalo mwenzetu amepata ni darasa kubwa sana kwake kwenye safari ya mafanikio na hasara aliyopata ni ada ya kupata darasa hilo.

Kwa sasa anajua mambo gani akifanya ataanguka na hivyo anapaswa kuepuka kufanya mambo hayo.




Hivyo ushauri wa kwanza na muhimu kabisa kwa yeyote ambaye anapitia magumu au kuanguka ni kutokukata tamaa wala kuangalia kama kitu kibaya. Badala yake ona ni darasa umepitia na kukomazwa ili kuyapokea mafanikio makubwa zaidi baadaye.

Waswahili wanasema kufanya kosa siyo kosa, bali kurudia kosa. Kuna mengi ambayo mtu unakuwa umefanya mpaka ukaanguka. Pia ipo kauli inayosema ujinga ni kufanya jambo lile lile kwa namna ile ile kisha kutegemea matokeo tofauti.

Kwa kuwa hujakata tamaa, unaendelea na kile ambacho ulikuwa umechagua kufanya. Kwa sababu ukilipa ada, lazima uendelee na masomo. Lakini usiendelee kwa kurudia makosa ambayo umeyafanya, ukifanya hivyo utakuwa umepoteza ada yako.

Ushauri wa pili kwenye hili ni kukaa chini na kutafakari kila ulichofanya kwenye mradi wako ulioshindwa. Anza na yale uliyokuwa unafanya wakati mambo yanakwenda vizuri. Kisha nenda kwenye yale ambayo ulikuwa unafanya na mambo yakaenda vibaya. Kisha jua ni mambo gani ambayo hutarudia tena kuyafanya unapoanza mradi wako upya.

Kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja huwa ni chanzo cha kushindwa kwenye yote. Kila kitu kipya unachoanzisha kinakuhitaji mno hasa mwanzoni. Sasa kama unafanya mambo mengi, unatawanya sana nguvu zako na hivyo kila jambo halipati umakini wa kutosha kitu kinachopelekea kushindwa.

Ushauri wa tatu hapa ni kuchagua kitu kimoja tu ambacho utaanza nacho na kuweka umakini wako wote kwenye kitu hicho. Achana na mengine yote, acha kuhangaika na kila fursa inayokuja kwako na kushawishiwa ni bora zaidi. Sikiliza rafiki yangu, fursa bora kwako ni ile uliyoichagua na uko tayari kuifanyia kazi kwa moyo wako wote.

Kama umeamua kulima kitunguu, lima hicho, achana na hadithi kwamba nyanya zinalipa zaidi na kufanya kitunguu na nyanya kwa wakati mmoja. Kama umeamua kufuga kuku fanya hivyo, achana na kelele kwamba sungura au bata mzinga wanalipa zaidi.

Unapokuwa chini, hiyo ndiyo sehemu pekee unayoweza kuanzia. Na uzuri ukiwa chini huna tena pa kuangukia.

Ushauri wa nne hapa ni kuanzia pale ulipo, kuanzia chini kabisa, kuanza kwa hatua ndogo kabisa unayoweza. Kwa kuwa umeshapoteza kila kitu na kwa kuwa umeamua kuanza na kitu kimoja, anza na chochote kilicho ndani ya uwezo wako kwa sasa. Hata kama ni kidogo kiasi gani, wewe anza na pambana kukua kwa kuanzia hapo. Usisubiri mpaka upate uwezo mkubwa wa kuanza, anzia popote pale ulipo sasa. Kama utaanza na sehemu ndogo ya kulima fanya hivyo, kama utaanza na ufugaji kidogo fanya hivyo. Anza kidogo na utazidi kuona fursa za kukua zaidi.

Maisha lazima yaendelee na kama umeanguka kabisa, kuna machaguo mawili, kurudi kwenye ajira itakayokupa msingi wa kuanza tena au kuishi kama mtawa ili kuweza kupambana hapa mwanzoni.

Ushauri wa tano ni kuamua maisha yako yataendeleaje, kwa kuwa umepoteza kila kitu, ina maana hata gharama za kuyaendesha maisha yako huwezi kuzimudu. Hapa unaweza kuchagua kurudi tena kwenye ajira ili upate fedha ya kuendesha maisha yako huku ukijijengea msingi imara zaidi. Au unaweza kuchagua kuishi kama mtawa, kwa kipindi cha mwanzo ambacho unaanza upya, punguza kabisa gharama zako za maisha. Yaani gharamia yale ya msingi tu, mfano chakula na cha kawaida kabisa. Hapa hununui kitu chochote kile cha anasa, yaani ambacho siyo muhimu kabisa. Kwa kufanya hivi unapunguza sana gharama za maisha yako huku pia ukipata muda mwingi wa kuweka kwenye kile unachofanya.

Usimamizi wa uhakika na wa karibu kwenye kitu chochote kile ni muhimu ili kiweze kukua. Kitu chochote kinachoshindwa huwa kinakosa usimamizi na udhibiti mzuri.

Ushauri wa sita ni kuhakikisha unakuwa na usimamizi na udhibiti wa karibu wa kile unachofanya. Yaani hakikisha upo kila wakati na kwa kila hatua inayochukuliwa. Usimuamini yeyote, hata kama anakushawishi na kukuridhisha kiasi gani. Jua kwenye jambo lolote lile, mhusika ana uchungu zaidi na hivyo atafanya maamuzi sahihi zaidi kuliko ambaye ni mjumbe tu. Kama utakuwa na wasaidizi ni vizuri, ila hapa mwanzoni, hakikisha upo mwenyewe kwa kila hatua. Baadaye utaweza kuweka mfumo mzuri, lakini mwanzoni, kila kitu ni wewe.

Maarifa sahihi kwenye kile unachofanya ni muhimu, kuna makosa mtu unaweza kuwa unafanya bila ya kujua na yanakukwamisha na kukuangusha. Wengi huwa wanafanya kwa mazoea kitu kinachokuwa kikwazo kwao.

Ushauri wa saba ni kupata maarifa sahihi juu ya kile unachofanya, chagua vitabu sahihi kusoma kwenye kile ulichochagua kufanya. Kama ni kilimo soma vitabu vya kilimo hicho, kadhalika kwenye ufugaji. Epuka sana maarifa ya kusisimua yanayoshirikisha mitandaoni, wewe nenda kwenye vitabu, jifunze kwa kina na jua hatua sahihi za kuchukua. Pia soma vitabu vinavyokupa maarifa ya jumla na hamasa ili upate nguvu ya kuendelea na safari yako, kwa sababu haitakuwa rahisi kwako.

 

Ndimi  KOCHA   MWL.  JAPHET    MASATU

(WhatsApp + 255 716924136 ) /   0755400128 /  0688361539