Monday, October 22, 2018

KABLA HUJAINGIA BIASHARA YOYOTE JIULIZE MASWALI HAYA

Yapo maswali mawili muhimu sana kwa kila mtu kujiuliza kabla ya kuingia kwenye biashara yoyote ile. Kwa kujiuliza maswali haya, utaingia kwenye biashara ukiwa na uelewa sahihi, na ukijua ni hatua zipi sahihi kwako kuchukua ili kufanikiwa zaidi kwenye biashara unayofanya.

 (1). NI   NANI  MWENYE  FEDHA  ZANGU?

Nilishakuambia siku za nyuma kwamba hutafuti fedha bali unakusanya fedha. Fedha unayoitaka sasa, ipo kwenye mikono ya mtu mwingine. Hivyo hatua ya kwanza kabisa kwenye kufikiria biashara yako ni kujiuliza nani mwenye fedha zako.
Hapa unahitaji kuwajua wateja halisi wa biashara yako, watu ambao wana shida, wana changamoto, wana uhitaji ambao unaweza kuutimiza. Pia watu hao wana fedha ya kuweza kukulipa wewe kwa kile ambacho unawapa.
Kama hujawajua watu wenye fedha zako, ukianzisha biashara utakuwa unapoteza muda wako. Kwa sababu hata kama unaona wengine wanauza sana, utashangaa unakaa kwenye biashara na hupati mauzo makubwa kama wengine.
Kwa sababu unakua hujajua nani mwenye fedha zako na kumfuatilia huyo zaidi.
Kama uliingia kwenye biashara bila kujiuliza swali hili, kaa chini sasa hivi na jiulize nani mwenye fedha zako? Orodhesha sifa za watu ambao wanaweza kunufaika na aina ya biashara unayofanya, na wenye uwezo wa kulipia kile unachouza.
Ukishajua kwa hakika nani mwenye fedha zako, ni rahisi kumlenga huyo na ukaweza kumhudumia vizuri na wote mkanufaika sana.

(2).JUA  NI  KITU  GANI  UNABADILISHANA  NAO  ILI  WAKUPE  FEDHA.
Baada ya kuwajua wenye fedha zako, unahitaji kujua kitu gani unahitaji kuwapa ili nao wakupe fedha walizonazo. Kwa sababu kila mtu amepata fedha yake ka uchungu, na hivyo hataki kuipoteza. Lazima uwe na sababu kubwa ya kumshawishi mtu akupe fedha zako. Kumbuka akishakupa fedha wewe, hawezi tena kuitumia kwa mambo yake mengine.
Hapa unahitaji kujua kwa hakika ni thamani gani unatoa kwa wateja wa biashara yako. Hapa unahitaji kujua kwa hakika ni mahitaji gani waliyonayo wateja wako ambayo unayatimiza, ni maumivu gani ambayo unayatuliza.
Kama huna sababu ya kutosha, ya kumshawishi mteja akupe fedha yake aliyoipata kwa shida, hutaweza kufanikiwa kwenye biashara yako.
Kwa sababu kumbuka mteja hanunui kwa sababu wewe unauza, wala hanunui kwa sababu anakuonea huruma. Bali mteja ananunua kwa sababu ana uhitaji, ana maumivu ndani yake ambayo hawezi kuendelea nayo na kuna mtu amemshawishi kwamba ana kitu cha kutimiza mahitaji yake au kutuliza maumivu yake.
Hivyo baada ya wewe kujua ni nani mwenye fedha zako, jua maumivu yake ni yapi, kisha mweleze jinsi kile unachouza kinavyoweza kutuliza maumivu aliyonayo.

Sunday, October 21, 2018

KUFANIKWA HUHITAJI KUFANYA KILA KITU AU KUJUA KILA KITU.

Ili kufanikiwa huhitaji kufanya kila kitu au kujua kila kitu. Badala yake chagua eneo lako ambalo unaweza kufanya vizuri, kisha kazana kufanya vizuri, kuwa bora kuliko wengine wote na utaweza kufanikiwa zaidi. Kadiri unavyochagua vizuri eneo lako na kuweka juhudi kubwa, ndivyo unavyotumia nguvu zako na umakini wako vizuri.

NI ASILIMIA KUMI TU NDIO MUHIMU.

Jifunze kutofautisha kati ya mawazo na mawazo mazuri, bidhaa na bidhaa bora, uwekezaji na uwekezaji mzuri. Asilimia 90 ya vitu vyote unavyokutana navyo, siyo muhimu, yaani ukiachana navyo hutakosa chochote. Ni asilimia 10 tu ndiyo muhimu, jua hiyo asilimia kumi na ukazane nayo huku ukipuuza mengine yote.

ISHI MAISHA YAKO., USIJIONYESHE WEWE NI BORA KULIKO WENGINE.

Kuwa na kiasi, haijalishi umefanikiwa kiasi gani, miaka 200 ijayo, huenda hakuna atakayejua hata kama uliishi hapa duniani. Kila unapoanza kujiona wewe ni muhimu kuliko wengine, kumbuka kitakachotokea miaka 200 ijayo, dunia itakuwa imekusahau kabisa. Ishi maisha yenye maana kwako na siyo maisha ya kujionesha na kutaka wengine waone wewe ni muhimu kuliko wao.

MAFANIKIO YA KWELI NI MAFANIKIO YA NDANI .KAZANA KUWA BORA KILA SIKU.

Kuna orodha nyingi za watu waliofanikiwa, kuanzia ndani ya nchi mpaka dunia nzima. Lakini jinsi mafanikio hayo yanavyopimwa inaweza isiwe sahihi kwako. Mafanikio ya kweli kwako ni mafanikio ya ndani yako, ambayo siyo rahisi kupimwa kwa nje. Mafanikio ya ndani utayapata kwa kuweka juhudi kwenye yale maeneo uliyochagua, kuweka umakini wako kwenye mambo yaliyo ndani ya uwezo wako na kuachana na mengine yote. fedha, madaraka na umaarufu ni vitu vya nje, ambavyo huwezi kuvidhibiti, unachoweza kudhibiti ni hatua unazochukua. Kazana kuwa bora kila siku na weka juhudi zaidi kwenye kile ulichochagua kufanya.

Tuesday, October 16, 2018

WAZAZI HUKWAMISHA AU KUENDELEZA VIPAJI VYA WATOTO WAO.

9 Oktoba 2018
Mzazi ana nafasi kubwa sana katika kuendeleza kipaji cha mtoto

Kipaji ni uwezo wa kuzaliwa nao wa kufanya jambo fulani kwa ngazi ya juu bila kufundishwa au baada ya kufundishwa kidogo tu. Kipaji kinaweza kuwa cha kimwili au cha kiakili lakini pia kinaweza kuendelezwa au kudumazwa.
Mzazi ni mtu wa kwanza anayeweza kutambua uwezo ama kipaji cha mtoto wake. Hata hivyo ana fursa ya kuendeleza au kutokukiendeleza kipaji cha mtoto.

Baadhi ya wazazi hutambua vipaji vya watoto mapema na kuanza kuviendeleza kwa kuwapatia nyenzo mbali mbali ambazo huwasaidia katika kuboresha uwezo walio nao.

Lakini pia wapo wazazi ambao wanamalengo yao juu ya ni kitu gani wanapenda watoto wao wafanye. Ama yamkini hawana ufahamu wa nini cha kufanya ili kumwendeleza mtoto mwenye kipaji .Hata hivyo vipo baadhi ya vipaji ambavyo wazazi huona ni upotevu tu wa maadili mfano kuimba na kucheza mziki.

BBC imezungumza na mama Ritha, mama mwenye watoto wanne. Anasema kwa kiasi kikubwa baadhi ya wazazi na hata yeye mwenyewe kipindi cha nyuma walikwamisha sana watoto sababu walikuwa hawatambui kama kipaji pia ni njia salama ya kumwezesha mtoto kimaisha.
"Wazazi wengi huwa hawajuagi tena zamani tulikuwa tunaona watoto wanapotea kabisa. Mi binti yangu wa kike alikua anapenda kuandika nyimbo za wasanii wa marekani na hata za kwake mwenyewe kwenye daftari lake afu kukiwa na sherehe yeye ndo mwimbaji. Nikaona anapotea nlikua na mchapa na nlimwambia akifika chuo kikuu ndo afanye uo mziki lakini si nyumbani kwangu maana hata baba yake alikuwa hapendi kabisa," Mama Ritha anaiambia BBC
Hata hivyo ameongeza kuwa wazazi pia huwanyima fursa za kujifunza watoto kwani kila akishika kitu mzazi hupiga kelele mtoto aache kwa madai kwamba ataumia.
Hata hivyo wapo baadhi ya watoto ambao wamepewa msaada mkubwa na wazazi wao katika kuboresha na kuendeleza vipaji vyao.

BBC imezungumza na mwanadada mpambaji Plaxeder Jumanne au baby precious kama anavyojulikana katika kazi zake za upambaji, anasema mama yake ndio mtu wa kwanza kumshauri ageuze kipaji chake kuwa biashara huku akimnunulia vifaa orijino vya urembo.

"Mie nlikuwa nawachukua watoto wenzangu nawapamba nlikua napenda sana urembo kama mama yangu. Hata nilipo kuwa nikaanza kuwapamba watu. Nilikuwa natumia vifaa feki hivi vya bei rahisi lakini mama yangu alianza kwa kuninunulia vifaa orijino kabisa. Na huwezi amini nilikua nampamba yeye na kumfuta kabla sijapata wateja tena nimejifunza kufunga maremba ya kinaijeria kichwani kwa mama na alikuwa ananisaidia sana, sasa hivi nasafiri hadi mikoani na kupamba watu mbali mbali hadi watu maarufu na nimepata pesa nikanunua vifaa vingi sana Orijino," Plaxeda anaiambia BBC.

Hata hivyo manadada huyo anasema kwa sasa mama yake ametangulia mbele za haki tangu mwaka jana ila bado anamshukuru kwa sababu hivi sasa kazi ya upambaji inampa pesa kuliko ajira yake na imemwezesha kufungua biashara zingine.

"Mimi sijajitangaza sana ila kupitia vifaa alivyonianzishia navyo mama yangu nikawa napamba hadi maharusi na wasimamizi wao. Na kipaji hiki kimenipa pesa ninafanya biashara ya kutengeneza nywele hasa mawigi na pia kufungua biashara ya nguo. Mama yangu angekuwepo angefurahi sana ila naamini anaona. Nimewaremba baadhi ya wasanii wa Tanzania. Safari ndo inaanza," Plaxeder anaiambia BBC.


Mwanaharakati wa masuala mbali mbali ya kibinadamu Shahista Alidina maarufu kama Shaykaa, anasema baadhi ya wazazi hupenda kutimiza ndoto zao kupitia watoto na mwishowe huwakwamisha.

"Unakuta mzazi kama alishindwa kuwa mwanasheria au daktari kama alivyotaka huko nyuma atataka mtoto wake afuate ndoto hiyo. Hawataki kuwapa uhuru watoto wafuate wanavyopenda. Unakuta kipaji cha mtoto kinaweza mletea kipato cha kutosha tu ila mzazi anampa mtoto shinikizo la kufaulu tu shule awe namba moja, mbili au tatu na ndiomaana unaona watoto wengine hadi wanajiua. Wanawanyima fursa watoto kufanya vitu wanavyovipenda," Shaykaa anaiambia BBC.

Hata hivyo anaongeza kuwa kunachangamoto nyingine kwa wazazi kupangia kazi watoto kuwa hii ni ya wanawake au hii ni ya wanaumena kujenga uoga kwa watoto na kuwanyima fursa ya kujituma zaidi.

"Kusoma kwa mtoto ni muhimu ila kuna muda wa ziada na kuna maisha nje ya darasa. Unakuta mtoto wa kike anapenda kucheza mpira, lakini mzazi atapinga kuwa huu ni mchezo wa wanaume mwanamke hatakiwi, sasa hapo moja kwa moja mzazi atakuwa ameua kabisa kipaji cha mtoto kama mtoto atakosa fursa ya kujiendeleza huko mbele," anasema Shaykaa
Mwanaharakati huyo pia amewaasa wazazi kuhakikisha wanawasaidia watoto kujiendeleza kijamii.

"Mtoto ni muhimu awe na maisha yake pia, na tutambue kuwa na wao ni binadamu wala si wafungwa. Ni muhimu ndio kufuata dini na misingi bora ya maisha pamoja na mila na desturi lakini tusisahau kuwa mtoto anapofikia umri wa kujielewa anahaki ya kufanya maamuzi kuwa anapenda nini ilimradi ni jambo jema kisheria, kidini, kiafya na kijamii. Tuwe marafiki kwao lakini tusiwapotoshe watoto wetu, Shaykaa anaiambia BBC.

JE, TUWAPE WATOTO WETU SIMU ZETU ZA MKONONI WACHEZEE ??

14 Oktoba 2018, BBC  SWAHILI

  Simu yaweza kumsaidia mtoto kujifunza lakini bado nimuhimu kwa mzazi kuwa makini
Hivi karibuni imekuwa kawaida sana kumkuta mtoto anatumia simu ya mkononi ya mzazi wake na mara nyingine wanatumia bila hata kupata ridhaa ya mzazi mwenyewe.
Baadhi ya watoto huonyesha utaalamu wa hali ya juu katika kufungua kurasa mbalimbali za simu hizo.

Na inadaiwa kuwa kuna watoto ambao huwa wanajifunza mambo mengi kupitia simu za mkononi.
Hata hivyo si wazazi wote ambao hukubali simu zao zitumiwe na watoto, baadhi huwa wakali na kuweka kila aina ya nywila ingawa wengine huwa hawaoni shida kuwapatia watoto wao simu punde tu wanaporejea kutoka kwenye majukumu yao ya kila siku.

Baadhi ya wazazi huwa wanaona kuwa simu ndio njia pekee inayoweza kuwafanya watoto wao watulie na wao wapate muda wa kupumzika ama hata kufanya shughuli zao za nyumbani. 

Je,kuna faida yeyote endapo mtoto atatumia simu?
BBC imezungumza na baadhi ya wazazi ili kufahamu ni kwa kiasi gani watoto wao hutumia simu zao na wanawadhibiti vipi vitu anavyoangalia mtoto?

"Kwa kweli simu yangu hata sina uhuru nayo huwa nikifika tu nyumbani wanangu huwa wananipokea kwa mbwembwe zote na cha kwanza kubeba ni simu na nikihitaji lazima niwaombe wao.
Simu ikiita utakuta wao ndio wanapokea,mara nyingi wanaangalia video za kartoon au za watoto wenzao zilizopo you tube," Mama Brian anaeleza

Baadhi ya watoto hutambua hadi nywila za simu za wazazi wao
Alex Kayetta ambaye ni baba wa mtoto mmoja, anasema simu yake huwa haimiliki punde tu anapofika nyumbani ,
"Mwanangu akishashika simu yangu yani kuipata lazima nimbembeleze, na akichukua mara nyingine huwa lazima nimtafute alipo ,kuna siku nilimkuta amejificha ndani ya beseni akicheza michezo ya kwenye simu'game' nikampiga picha".

Freddie Kyara ni mwanasaikolojia kutoka nchini Tanzania ambaye anaeleza kuwa hali hii huwa inafanana na jinsi mzazi anapokua kwenye simu muda mrefu na hupoteza fursa ya kuwa karibu jamii na ndivyo hivyo inavyotokea kwa mtoto.

Na kwa upande wa mtoto kutumia simu huwa kuna madhara pia "Kukua kwa mtoto kunahitaji awe na mbinu za kijamii, kama vile kucheza na watoto wenzake na kujifunza mambo mbalimbali kutoka kwa wenzake, lakini siku hizi unaweza kukuta mtoto anashindwa kucheza na watoto wengine kwa sababu amezoea yeye rafiki yake ni simu tu.

Ubunifu wa mtoto unaweza kupungua. Sisi wakati tunakuwa hatukuwa tunajua habari za simu, ilikuwa ni kucheza mpira na kujishughulisha na shughuli mbalimbali za nyumbani na hali hiyo ilitufanya tuweze kujenga urafiki na watu na kujua tabia za watu tofautitofauti. 

Mtoto anaweza kujifunza pia kwenye simu lakini lazima uthibiti uwepo kwa sababu sio kila kilichopo kwenye simu kina maudhui mazuri kwa watoto na wanapaswa kutengewa muda" Kyara ,mtaalamu wa saikolojia alieleza.

Hata hivyo jumbe mbalimbali zimekuwa zikisambaa kuonya madhara ya mionzi ya simu kwa watoto wadogo na kudai kuwa umri sahihi wa kupewa simu ni kuanzia miaka kumi na sita.
Jambo ambalo Daktari Fredrick Mashili anasema madhara ya namna hiyo huwa inategemeana zaidi na umri wa mtoto japo kwa upande mwingine macho yanaweza kupata shida ingawa hakuna ushahidi wa kutosha kuthibitisha madhara hayo ya mionzi.

"Kuna wasiwasi kwamba mtu akianza kutumia simu mapema anaongeza muda wa kuyashughulisha macho yake katika mionzi kwa muda mrefu zaidi kitu ambacho si kizuri kwa afya ya macho," Dkt.Mashili alieleza.


Friday, October 12, 2018

KILA MTU ANA NAMBA NA VIWANGO VYAKE KIFEDHA. HATUWEZI KULINGANA.

Linapokuja swala la fedha, kila mtu ana namba na viwango vyake. Kwa sababu tunatofautiana ndoto, kazi/biashara, kipato, mitindo ya maisha na hata mazingira, matokeo yetu ya kifedha hayawezi kulingana.

Hivyo kujipima hatua ulizopiga kifedha kwa kuwatumia wengine ni kujiumiza na hata kujirudisha nyuma, kwa sababu kuna namba nyingi ambazo utakuwa huzijui kuhusu wengine. Kwa mfano unaweza kumwona mtu kwa nje anaonekana kuwa na vitu vinavyoashiria ana fedha nyingi, lakini kumbe vitu vyote hivyo amepata kwa mkopo ambao ataulipa maisha yake yote.
Pia unaweza kumwona mtu ukafikiri hayupo vizuri kifedha kwa mwonekano wake wa nje, kumbe anafanya uwekezaji ambao baadaye utamwezesha kufikia uhuru wa kifedha.

Kwa kuwa ni vigumu kupima hatua ulizopiga kifedha kwa kuwatumia watu wengine, unahitaji kujitumia wewe mwenyewe.

UTOAJI WA FEDHA KWA WENGINE BILA KUTEGEMEA KUPATA CHOCHOTE NI MUHIMU SANA.

Kiasi cha fedha unachotoa kwa wengine bila ya kutegemea kupata chochote ni kiwango kingine muhimu sana cha kupima afya yako kifedha na kujua hatua ulizopiga. Kwa kadiri unavyotoa zaidi ndivyo unavyoonesha kwamba unaitumia fedha na siyo fedha inakutumia wewe.

Unahitaji kuwa na utaratibu wa kutoa fedha kuwasaidia wengine bila ya kutegemea kulipwa fedha hizo. Kwa sababu tunatoshelezwa zaidi na utoaji kuliko upokeaji.

Pia unapotoa fedha kwa wengine, unatengeneza pengo ambalo itabidi lizibwe, hivyo unakuwa umejiweka kwenye nafasi ya kuongeza kipato chako zaidi.

WEKA AKIBA ILI USIINGIE KWENYE MADENI MABAYA NA CHANGAMOTO ZA MAISHA.


Hichi ni kiwango kinachoonesha maandalizi yako uliyonayo sasa kwa upande wa fedha. Kadiri unavyokuwa na akiba kubwa kifedha, ndivyo unavyoweza kujilinda na dharura mbalimbali zinazoweza kukutokea. Akiba unayokuwa nayo ndiyo itakukinga usiingie kwenye madeni mabaya pale unapokutana na changamoto ambazo hukuzitegemea.

Kiwango sahihi cha akiba unayopaswa kuwa nayo ni ile inayoweza kutosheleza kuendesha maisha yako kwa miezi 6 mpaka mwaka mmoja hata kama utakuwa huna kipato kabisa katika kipindi hicho.

Kuza kiwango chako cha akiba na hili litakupa pumziko na kukuondolea wasiwasi kuhusu fedha kitu ambacho kitakuwezesha kufanya mambo yako kwa utulivu na ufanisi mkubwa.

EPUKA MADENI ILI KUEPUKA KUJIWEKA KWENYE WAKATI MGUMU KIFEDHA.

Kiasi cha fedha unachodaiwa na wengine kutokana na vitu ulivyonunua bila ya kuwa na fedha ni kipimo cha maamuzi yako ya kifedha kwa siku za nyuma. Kadiri madeni yako yanavyokuwa makubwa, ndivyo sehemu kubwa ya kipato chako inavyoelekea kwenye kulipa madeni hayo na wewe kubaki na kiasi kidogo ambacho hakiwezi kukutosheleza.

Unahitaji kutokuwa na deni binafsi kabisa, na madeni mazuri unayopaswa kuwa nayo ni yale yanayojilipa yenyewe. Madeni yanayojilipa yenyewe ni yale ambayo yanazalisha faida na faida hiyo unatumia kulipa deni. Haya ni madeni ambayo hayakuumizi.

Lakini madeni ambayo unalipa kwa fedha zako unazopata kwenye shughuli zako binafsi, ni utumwa ambao utakutesa kwa muda mrefu. Kama upo kwenye madeni ya aina hii kazana kuondoka na usiingie tena ili kuepuka kujiweka kwenye wakati mgumu kifedha.

WEKEZA SASA KWA AJILI YA BAADAYE , WAKATI UNA NGUVU ZA KUFANYA KAZI.

Kiwango ambacho umekiwekeza kwenye maeneo ambayo yanazalisha riba au faida ni kipimo muhimu kwa maandalizi yako ya kifedha ya baadaye. Kama hapo ulipo hujafanya uwekezaji wote kwa ajili ya baadaye, kama hujawa na maandalizi ya kukuwezesha kuingiza kipato bila ya wewe kufanya kazi moja kwa moja, huna maandalizi ya kifedha ya baadaye, na haupo eneo zuri kifedha.

Unahitaji kufanya uwekezaji kwa ajili ya baadaye, kwa sababu utakuja wakati ambapo huna uwezo wa kufanya kazi kama unavyofanya sasa, lakini una mahitaji muhimu kwa maisha yako. Unapokuwa umewekeza na uwekezaji unazalisha, maisha yako yanakwenda vizuri.

Kiwango sahihi cha uwekezaji unachopaswa kuwa nacho ni kile ambacho kinazalisha faida au riba ambayo inakuwezesha wewe kuendesha maisha yako kwa kadiri ya mahitaji yako.

Wednesday, October 10, 2018

TATIZO NI TAFSIRI YA MATUKIO YANAYOTUTOKEA.

Watu wawili wanaweza kushindwa kwenye kitu kimoja, mmoja akachukulia kushindwa huko kama kichocheo cha kufanya zaidi na akafanikiwa. Mwingine anaweza kuchukulia kushindwa huko kama sababu ya kukata tamaa na kushindwa kabisa.

Tukio ni moja, tafsiri tofauti na matokeo tofauti kabisa.
Siyo kinachotokea, bali namna unavyotafsiri kinachotokea ndiyo inaleta madhara kwako.
Kwenye Falsafa ya Ustoa pia kuna dhana inayoitwa upili wa udhibiti. Dhana hii inaeleza kwamba vitu vyote vinavyotokea kwenye maisha yako, vinagawanyika katika makundi mawili, kundi la kwanza ni vitu unavyoweza kuviathiri, hivi vipo ndani ya uwezo wako. Kundi la pili ni vitu usivyoweza kuviathiri, hivi vipo nje ya uwezo wako.

Hivyo unapokutana na chochote na ukajiambia ni kigumu au kinakushinda, huna haja ya kusumbuka, badala yake jiulize je kipo ndani ya uwezo wako au nje ya uwezo wako. Kama kipo ndani ya uwezo wako chukua hatua sahihi, kama kipo nje ya uwezo wako kikubali kama kilivyo au kipuuze. Hakuna namna bora ya kuendesha maisha yako kama hii, kwa sababu hakuna chochote kitakachotokea, ambacho kitakuvuruga kabisa.

Ndugu  yangu , nikukumbushe tena ya kwamba kama unataka kuitawala dunia, kuna mtu mmoja unayepaswa kumtawala, na mtu huyo ni wewe mwenyewe. Hutaweza kujitawala wewe mwenyewe kwa mabavu au nguvu, badala yake utajitawala kwa kudhibiti mawazo yako na hisia zako.

JINSI YA KUJENGA IMANI KWA WATEJA WAKO KWENYE KILE UNACHOUZA.KUWA MUUZAJI MZURI.


Moja; penda kile unachofanya, usifanye kwa sababu ya fedha pekee, fanya kwa sababu unapenda kufanya, fanya kwa sababu unajali, fanya kwa sababu kuna mchango unaotoa kwa wengine.

Mbili; kuwa mtumiaji wa kwanza wa kile unachouza, hakikisha wewe mwenyewe unaweza kutumia, au unaweza kumshauri mtu wako wa karibu kabisa, unayempenda sana atumie. Kwa maneno mengine usiuze kitu ambacho wewe mwenyewe huwezi kutumia au huwezi kumpa mtu wako wa karibu atumie.

Tatu; toa uhakika wa unachouza na mpe mteja nafasi ya kurudisha iwapo alichonunua hakitamfaa au hakitafanya kazi kama alivyotegemea. Mfanye mteja aone hana cha kupoteza anaponunua kwako.
Nne; jua tatizo la mteja unalotatua na elezea kile unachouza kwa namna kinavyotatua tatizo hilo. Usieleze sifa za kitu pekee, bali eleza namna zinatatua tatizo la mteja wako.

Tano; usiwaseme vibaya washindani wako, usihangaike kuwashinda wengine, kama unachouza ni kizuri kweli, huna haja ya kuhangaika na wengine wanauza au kusema nini. Lakini kama huamini kwenye unachouza, itabidi uanze kuwakosoa na kuwasema vibaya wengine, ili kumfanya mteja wako aone wewe upo sahihi, lakini hata unapowasema vibaya wengine, mteja anajua kuna shida kwenye biashara yako.

Monday, October 8, 2018

KWANINI UISHIE KUPATA PESA YA KULA TUU ??? UHA HAKI YA KUPATA PESA YA KUTOSHA.


“Pesa ya kula ni sumu ya maendeleo na utajiri” – Cypridion Mushongi 

Kila mmoja anajitahidi kutafuta pesa popote anakojua. Habari njema ni kwamba kila anayetafuta pesa hii ya KULA anapata. Lakini.. pamoja na kuipata, wengi wamekuwa wakilalamika kuwa ni ndogo na kwamba inatosha kula tu! Wengi wanatamani kupata pesa nyingi zaidi ya hiyo wanayoipata kwasasa. Kwaujumla, wengi wanashangaa ni kwanini hawapati pesa ya kutosha kuweza kufanya mambo makubwa zaidi ya KULA na kulipa ADA za watoto. 

Sababu mojawapo ya kushindwa kupata pesa ya kutosha ni malengo mahususi tunayojiwekea kabla ya kutafuta pesa. Watu wengi wakiamka asubuhi, malengo yao makubwa kabisa ni kutafuta pesa ya KULA, ADA na kujenga NYUMBA ya makazi. Wengine akijikakamua kidogo analenga kununua GARI la kutembelea. Malengo ya watu yanabainishwa kwenye maongezi yao ya kawaida. Pindi ukiwasikiliza watu, utasikia wakiambizana kuwa “mimi natafuta pesa ya kula basi! Wengine utawasikia wakisema “natafuta pesa kwaajili ya watoto” wengine wamekwenda mbali na kusema kuwa wanatafuta pesa, “ili watoto wao angalau waweze kwenda choo” Ni wazi kuwa maongezi ya namna hii, yanakupa jibu la moja kwa moja kuwa watu wengi wana malengo ya kutafuta kiasi kinachotosha KULA, kulipa KARO na kujenga NYUMBA ya makazi basi! kwamba zaidi ya hapo ni bahati tu. 

Wengi wa wale wanaolalamika kupata pesa kidogo ni wale walioweka malengo ya kutafuta pesa ya KULA. Ukiweka malengo ya KULA, ujue malengo hayo ni madogo sana na kwa vyovyote vile yatavutia pesa kidogo sana kwako. Mtu yeyote mwenye malengo ya kupata pesa ya KULA, hawezi kuweka utajiri kama kipaumbele chake. Na mwisho wake ujikuta hana ndoto yoyote ya kutajirika maisha yake yote. 

Ukweli ni kwamba, pesa ya KULA siku zote huwa ni ndogo japokuwa inapatikana kila ikitafutwa. Pamoja na kupatikana kila siku, tatizo lake ni moja; kwamba, ikishapatikana muhusika anakuwa tayari ana njaa na hivyo kuitumia mara moja. Ikishaisha muhusika uenda kutafuta tena, na huo ndio unakuwa mzunguko na mtindo mzima wa maisha ya kila siku. 

Kujiwekea malengo ya kutafuta pesa ya KULA na ADA siyo jambo baya! Ubaya unakuja pale utakapofanya suala la kutafuta pesa ya KULA kama lengo lako kuu. Mara nyingi watu waliofanikiwa wanatushauri kuyaweka malengo ya KULA na ADA ndani ya malengo makubwa zaidi (Utajiri). Tunahimizwa kuachana na utamaduni wa kuweka KULA na ADA kama malengo makuu katika maisha, kwasababu, kwa kufanya hivyo tutazidi kupoteza muda mwingi na matokeo yake hututakaa tupate muda wa kufanya mambo makubwa. 

Kwa mfano: “Ikiwa wewe unaishi DAR-ES-SALAAM na lengo lako kuu ni kwenda KARAGWE, maana yake, inabidi ujipange kutafuta jinsi ya kupata pesa itakayokuwezesha kufika KARAGWE. Pesa ya kufika KARAGWE ikishapatikana, maana yake ni kwamba sehemu zote za njiani kabla ya kufika mwisho wa safari yako kwa vyovyote vile, utafika sehemu zote za njiani japo hilo halikuwa lengo lako kuu. Sehemu za njiani ambazo kwa vyovyote vile lazima upite ni pamoja na Morogoro, Dodoma, singida, Tabora, Kahama n.k. Sehemu zote hizi utaweza kufika kwa kutumia nauli ile ile ya DAR-ES-SALAAM hadi KARAGWE” 

Mfano huo hapo juu, unatufundisha kwamba tunahitaji kuweka juhudi na maarifa yetu kwenye vitu vikubwa kama vile miradi ya maendeleo (majumba ya kupangisha, kilimo biashara, viwanda, biashara kubwa n.k). Tukiwekeza akiri zetu kwenye mambo kama hayo ni wazi kwamba pesa ya KULA na ADA za watoto zitapatikana humo humo ndani ya miradi hiyo. Kitu cha msingi hapa ni kuhakikisha tunajizuia kufanya kazi ya kutafuta pesa ya KULA na ADA kama malengo yetu makuu. Tusifanye KULA na ADA kuwa mwisho wa safari yetu BALI suala la pesa ya kula na ADA liwe ni sehemu za njiani kuelekea Kwenye ndoto kubwa (Utajiri). 

Wito wangu kwako msomaji ni wewe kuiambia akili yako na nafsi yako mwisho wa safari yako, yaani safari ya kuelekea kwenye maisha unayotamani kuishi. Naamini ukiweza kuiambia ukweli akili na nafsi yako, basi ujue hapo utakuwa umefikia hatua ya kutafuta pesa nyingi zaidi ya hiyo ya KULA na kulipa ADA. Ili linawezekana, limewezekana kwangu, limewezekana kwa wengine na hakuna sababu yoyote ya kutowezekana kwako.

ACHA KUWA KARANI WA FEDHA ZAKO, JILIPE WEWE KWANZA

 Wapo watu wengi ambao wanakuwa na mipango mizuri sana kabla hawajawa na fedha, wanajua kabisa wakipata fedha watafanya nini na nini. Na tena watawashangaa sana wale wanaopata fedha na kuzitumia vibaya. Lakini subiri watu hao hao wazipate fedha, mipango yote inayeyuka, fedha zinatumika hovyo na mpaka zinapoisha ndiyo akili zinawarudia.

Kitu kimoja ambacho nataka kushauri leo kwa wale wote wenye shida ya kukaa na fedha, ni hiki; ACHA KUWA KARANI WA FEDHA ZAKO.
Watu wengi linapokuja swala la fedha, hawana tofauti na makarani, ambao wanapokea fedha na kuzipelekeka zinapopaswa kwenda. Ukienda benki kuweka fedha na ukamkabidhi karani wa benki fedha zako, utaona kama anashika fedha nyingi, lakini mwisho wa siku fedha hizo habaki nazo yeye, bali anakabidhi zinapohusika.

Sasa watu wengi wamekuwa wanayaishi maisha yao kama makarani wa fedha zao. Kinachotokea ni hiki, mtu anafanya kazi au biashara na analipwa mshahara au kupata faida kama kipato chake. Anachukua kipato hicho na kwenda kulipia vitu na kununua vitu mbalimbali. Mwisho anabaki hana fedha kabisa.

Alichokifanya mtu huyu ni kuchukua fedha kwenye kazi au biashara na kwenda kuitoa kwa wale wanaomdai au wanaouza vitu mbalimbali. Mwisho wa siku anabaki hana hata senti moja.

Acha mara moja kuwa karani wa fedha zako, kwa kuzihamisha kutoka unakozipata na kuzipeleka kwenye matumizi na wewe kubaki huna kitu.
Na ipo njia moja rahisi kwako kuacha kuwa karani wa fedha zako, njia hiyo ni KUJILIPA WEWE MWENYEWE KWANZA.

Kwa kila kipato unachoingiza kwenye maisha yako, kabla hujapeleka kwenye matumizi yoyote, toa sehemu ya kipato hicho na iweke pembeni. Sehemu hiyo ya kipato uliyoitoa ndiyo malipo yako kwako na hupaswi kuitumia kwa shughuli nyingine yoyote ya matumizi. Hichi ni kipato ambacho utakiwekeza zaidi ili uweze kufanikiwa zaidi.

Sasa najua ni vigumu kukaa na fedha, kwa sababu kama wanavyosema watu, fedha huwa hazikosi matumizi. Ukishakua na fedha, dunia itahakikisha unazitumia kwa namna yoyote ile. Hivyo vitu vitaharibika, watu wataumwa utashangaa unapokuwa na fedha ndiyo unapokea simu nyingi zikitaka utoe msaada fulani.

Hivyo kuna njia nyingine bora kabisa ya kuhakikisha kile unachojilipa hakipati matumizi na ukakipoteza. Njia hiyo ni KUJENGA GEREZA LA AKIBA YAKO. Kile kiasi ambacho unajilipa wewe mwenyewe, kitengenezee gereza, ambapo ukishaingiza, huwezi kutoa tena, hata itokee nini. Hata uwe na dharura kiasi gani, gereza hilo halikuruhusu uondoe fedha ulizoweka.

Gereza la fedha zako ni mfumo wowote unaokuruhusu kuweka fedha lakini kutoa inakuwa siyo rahisi. Na unaweza kufanya hivyo kwa kuwa na akaunti maalumu ya benki ambayo inakuruhusu kuweka lakini siyo kutoa. Unaweza pia kufanya uwekezaji wa moja kwa moja ambao utafanya kupata fedha yako kuchukue muda. Lakini pia unaweza kuweka mpango na mtu au watu wengine, na mkawa mnaweka fedha lakini hamtoi.
Angalia njia inayokufaa wewe, ambapo ukiweka fedha, inakuwa vigumu sana kwako kuitoa, na hilo litakusaidia kujiwekea fedha zako kulingana na mipango uliyonayo.

Hivyo nimalize kwa kukumbusha mambo muhimu sana tuliyojadili hapa;
ACHA KUWA KARANI WA FEDHA ZAKO.
JILIPE WEWE MWENYEWE KWANZA.
TENGENEZA GEREZA LA FEDHA ZAKO.
Fanya hayo matatu na fedha yako itaweza kutulia, na utaweza kufanya makubwa. Ukishaweza kuituliza fedha yako, utaweza kuiwekeza na kupitia uwekezaji ndiyo utaweza kufikia utajiri na uhuru wa kifedha.

USIRUHUSU HISIA ZAKO ZIKUTAWALE , THIBITI HISIA ZAKO, USITAFSIRI TUKIO.

Moja ya changamoto kubwa zinazowapelekea wengi kushindwa kwenye maisha ni kuendeshwa na hisia badala ya wao kuendesha hisia zao. Wote tunajua kwamba pale tunaporuhusu hisia zitutawale, tunakuwa tumeondoa kabisa uwezo wetu wa kufikiri. Kwa sababu hisia kali na fikra haviwezi kukaa pamoja.

Kupitia falsafa ya ustoa, tunajifunza kwamba hisia ni kitu ambacho tunakitengeneza sisi wenyewe na hakuna anayetupa, hivyo tunaweza kuchagua kutoruhusu hisia zitawale maamuzi yetu.
Epictetus ana maneno mazuri ya kutuambia kuhusu hisia;
It isn’t the things themselves that disturb people, but the judgements that they form about them. Death, for instance, is nothing terrible, or else it would have seemed so to Socrates too; no, it is in the judgement that death is terrible that the terror lies. Accordingly, whenever we are impeded, disturbed or distressed, we should never blame anyone else but only ourselves, that is, our judgements. It is an act of a poorly educated person to blame others when things are going badly for him; one who has taken the first step towards being properly educated blames himself, while one who is fully educated blames neither anyone else nor himself. – Epictetus, Handbook, 5
Kinachotusumbua siyo kile kinachotokea, bali tafsiri yetu kwa kile kinachotokea. Kwa mfano kifo, siyo kitu cha kutisha, kama ingekuwa hivyo wanafalsafa kama Socrates wangekiogopa. Ni tafsiri yetu kwamba kifo ni kitu kibaya ndiyo inatusumbua. Hivyo hivyo, tunapokuwa tumekwazika, tumesumbuka au kupata msongo, hatupaswi kumlaumu mtu yeyote bali sisi wenyewe, kwa sababu hivyo vinatokana na tafsiri zetu wenyewe. Kwa asiyekuwa na elimu, huwalaumu wengine pale mambo mabaya yanapomtokea, anayeanza kujifunza hujilaumu mwenyewe wakati yule aliyeelimika hamlaumu yeyote wala hajilaumu yeye mwenyewe.

TARAJIA MABAYA NA MAGUMU, KUWA MSTAHIMILIVU.

Maisha siyo rahisi, hakuna chochote kwenye maisha yako kitaenda kama ulivyopanga. Utakutana na magumu na changamoto ambazo zitakuangusha na kujaribu kukukatisha tamaa. Ili uweze kufanikiwa, ili uweze kupata chochote unachotaka, unapaswa kuwa mstahimilivu, unapaswa kuwa mgumu, unapaswa kuwa kinga’ang’anizi na unapaswa kutokujua kabisa msamiati unaoitwa kushindwa au kukata tamaa.
Falsafa ya ustoa inatujenga tuwe wastahimilivu kwa kutuandaa kukutana na magumu na hata kuweza kuyavuka bila ya kukata tamaa.

Ili kuzuia mabaya yanayotokea yasituvuruge, tunapaswa kuwa na maandalizi ya mabaya na magumu yanayoweza kutokea.

Kama wastoa tunaweza kujiandaa na magumu kwa njia mbili. Njia ya kwanza ni kuishi magumu yenyewe, kujiweka katika nyakati ngumu hata kama hujafikia ugumu huo. Kufanya kama vile huna kitu fulani, hata kama tayari unacho. Kwa njia hii, hutashtushwa pale kile ulichokuwa unategemea kitakapokuwa hakipatikani.
Njia ya pili ni kujijengea taswira ya magumu kabla hayajatokea. Unapopanga chochote, usiangalie tu yale mazuri unayotegemea yatokee, bali pia jenga taswira ya mabaya yanayoweza kutokea. Jiulize kipi kibaya kabisa kinachoweza kutokea, kisha pata picha kwamba kitu hicho kimetokea na ona utawezaje kukabiliana nacho. Zoezi hili la kujijengea taswira ya mabaya linakufanya usipatwe na mshangao pale unapokutana na magumu, kwa sababu ulishapata picha ya magumu hayo. Pia kwa sababu  hutapata magumu makubwa kabisa, utajiambia ulishaona magumu zaidi ya uliyokutana nayo, hivyo hayakusumbui.
Marcus anatuambia;
Be like the headland, on which the waves break constantly, which still stands firm, while the foaming waters are put to rest around it. ‘It is my bad luck that this has happened to me.’ On the contrary, say, ‘It is my good luck that, although this has happened to me, I can bear it without getting upset, neither crushed by the present nor afraid of the future.’ This kind of event could have happened to anyone, but not everyone would have borne it without getting upset. – Marcus Aurelius, Meditations, 4.49
Kuwa kama ukingo wa mto au bahari ambao unapigwa na mawimbi ya maji kila mara lakini unaendelea kusimama imara na kuyatuliza mawimbi ya maji. Chochote kibaya kinapotokea, usijiambie nina bahati mbaya hiki kimetokea kwangu, badala yake jiambie nina bahati nzuri hiki kimetokea kwangu kwa sababu nitaweza kukikabili bila ya kukasirika au kuumizwa nacho kwa sasa au wakati ujao. Kitu kama hicho kingeweza kutokea kwa yeyote, lakini siyo kila mtu anaweza kukipokea kwa utulivu.

Pia Seneca anatukumbusha kuishi kila siku yetu kama ndiyo siku ya mwisho kwenye maisha yetu;
Glad and cheerful, let us say, as we go to our rest: ‘I have finished living; I have run the course that fortune set for me’. If God gives us another day, let us receive it with joy. The happiest person, who owns himself more fully, is the one who waits for the next day without anxiety. Anyone who can say, ‘I have had my life’ rises with a bonus, receiving one more day. – Seneca, Letters, 12.9.

Kila unapoimaliza siku yako jiambie kwa furaha na uchangamfu nimemaliza kuishi, nimemaliza mwendo ambao asili imenitengenezea. Kama Mungu atanipa tena siku nyingine, nitaipokea kwa furaha. mtu mwenye furaha anajimiliki yeye kwa ujumla, anaisubiri siku nyingine bila ya wasiwasi. Yeyote anayejiambia nimeyamaliza maisha yangu, anapata zawadi ya siku nyingine tena ya kuishi.

USISINGIZIE HAUNA MUDA WA KUTOSHA KUFANYA YALE MUHIMU.

Moja ya kisingizio cha watu wengi kwenye kushindwa kufanya yale wanayotaka kufanya kimekua ni muda. Muda unaonekana kuwa mfupi sana na mambo ya kufanya yakiwa mengi. Hivyo tumekuwa tunatamani kama masaa ya siku yangeongezwa ili tuweze kufanya zaidi.
Lakini ukweli ni kwamba, masaa ya siku hayataongezeka, ni yale yale 24. Na wale wanaofanikiwa sawa sawa na wanaoshindwa, wana masaa hayo hayo kwa siku. Sasa kwa nini wachache wafanikiwe kwenye muda huo, wakati wengi wanashindwa na kuona hawana muda?
Seneca analo jibu zuri sana kwetu kuhusu muda;
Life is long enough, and a sufficiently generous amount has been given to us for the highest achievements if it were all well invested. But when it is wasted in heedless luxury and spent on no good activity, we are forced at last by death’s final constraint to realize that it has passed away before we knew it was passing. So it is: we are not given a short life but we make it short, and we are not ill-supplied but wasteful of it. Just as when ample and princely wealth falls to a bad owner it is squandered in a moment, but wealth however modest, if entrusted to a good custodian, increases with use, so our lifetime extends amply if you manage it properly. – Seneca, On The Shortness Of Life.
Maisha ni marefu vya kutosha na muda wa kutosha tumepewa kwa kufikia yale makubwa kama tutauwekeza muda huo vizuri. Lakini tunapopoteza muda huo kwa anasa zisizo na maana na kushindwa kufanya yale mazuri, tunakuja kustuka tumepoteza muda na maisha yetu pale tunapofikia kifo. Hivyo basi, siyo kwamba tuna maisha mafupi, bali tunayafanya kuwa mafupi, siyo kwamba muda ni mdogo, bali tunao mwingi mpaka tunaupoteza. Kama ambavyo utajiri ukiwa kwenye mikono ya mtu asiye makini unapotea na ukiwa kwenye mikono ya mtu makini unakua, ndivyo maisha yetu yalivyo, yanakua kama yataendeshwa vizuri.

TENGENEZA NJIA , USIFUATE NJIA

”Do not go where the path may lead, go instead where there is no path and leave a trail.” – Ralph Waldo Emerson

Watu wengi wamekuwa wanashindwa kwenye maisha kwa sababu hawathubutu kufanya vitu vipya, badala yake wanaangalia kile ambacho tayari kimeshafanya na wao wanafanya. Hii ni kufuata njia, sasa unapochagua kufuata njia fulani, jua utafika kule ambapo njia hiyo imeelekea. Kama utafanya kile ambacho wengine wanafanya, utapata matokeo ambayo wanayapata.

Njia pekee ya kufanikiwa zaidi, ni kufanya mambo mapya, kufanya yale ambayo hakuna mwingine anayefanya, kutengeneza njia mpya, pale ambapo hakuna njia. Hili linatisha, kwa sababu unakuwa huna uhakika, nafasi ya kushindwa ni kubwa, lakini pia nafasi ya kufanikiwa ni kubwa zaidi.
Kwenye chochote unachochagua kufanya, acha kuangalia wengine wanafanya nini ili uige, badala yake angalia kipi muhimu kinachopaswa kufanya kisha kifanye kwa njia ambayo ni sahihi kwako kufanya na kwa wale unaowahudumia. Kwa namna hii utatengeneza njia mpya na wewe kama kiongozi wa njia hiyo utanufaika zaidi.
Rafiki, sindano za leo zimekuwa ndefu na kali, lakini kama utazifanyia kazi, hutabaki hapo ulipo. Sina kingine cha kuongeza zaidi ya kukukumbusha kanuni yetu muhimu ambayo ni MAARIFA SAHIHI + KUCHUKUA HATUA KUBWA = MAFANIKIO MAKUBWA. Maarifa ni hayo, kazi kwako kuchukua hatua ili ufanikiwe.

Sunday, October 7, 2018

FANYA YALIYO NDANI YA UWEZO WAKO, USISUMBUKE NA YALIYO NJE YA UWEZO WAKO

Sisi binadamu huwa tunasumbuka na mambo mengi sana, lakini tukianza kuyaangalia mambo hayo, mengi tunajisumbua nayo bure, kwa sababu yapo nje ya uwezo wetu, hakuna chochote tunachoweza kufanya tukayabadili au kuyaathiri.
Mambo yote yanayotokea kwenye maisha yetu tunaweza kuyagawa kwenye makundi mawili, yaliyo ndani ya uwezo wetu, haya ni yale ambayo tunaweza kuyaathiri, tunaweza kuyafanya kuwa bora zaidi. Na kuna yale ambayo yapo nje ya uwezo wetu, ambapo hatuna cha kufanya.

 Baadhi ya vitu vipo ndani ya uwezo wetu na vingine vipo nje ya uwezo wetu. Vilivyo ndani ya uwezo wetu ni maoni yetu, fikra zetu, maamuzi yetu na matendo yetu, kwa kifupi yale yote ambayo sisi tunayafanya. Vitu vilivyo nje ya uwezo wetu ni miili yetu, mali zetu, sifa zetu na nafasi nyingine tunazopewa, kwa kifupi chochote ambacho hatufanyi sisi moja kwa moja, kipo nje ya uwezo wetu. Vitu vilivyo ndani ya uwezo wetu ni bure, huru na visivyo na ukomo, vilivyo nje ya uwezo wetu ni dhaifu, visivyo huru, vyenye ukomo na visivyo vyetu.

Kwa vyovyote vile, hupaswi kusumbuliwa na chochote, kwa sababu kama kitu kipo ndani ya uwezo wako basi unahitaji kuchukua hatua, na kama kipo ndani ya uwezo wako huna hatua ya kuchukua hivyo kubaliana nacho kama kilivyo au kipuuze.

ISHI KULINGANA NA MISINGI YA ASILI

Huwa tunayaona maisha yetu ni magumu na tuna mengi ya kukabiliana nayo, lakini hebu fikiria jinsi ulimwengu unavyojiendesha. Fikiria jinsi ambavyo sayari yetu ya dunia inalizunguka jua mwaka mzima, na kutupatia majira ya mwaka. Fikiria jinsi sayari hii inajizungusha kwenye mhimili wake kila siku na kutupatia usiku na mchana. Asili imeyapangilia mambo yake ambayo yanajiendesha vizuri.

Sisi pia tunapaswa kuishi kwa msingi wa asili, kujua kile ambacho tunapaswa kufanya, kujipanga kukifanya na kukifanya kwa ubora na msimamo kama ambavyo asili inafanya mambo yake. Kwa kuishi kulingana na asili, hata matatizo yetu yanayotusumbua yanaonekana ni madogo sana ukilinganisha na jinsi ulimwengu mzima unavyojiendesha.

 Kazi za Mungu ndiyo zinatupa sisi riziki, na kazi za asili hazitofautiani na asili yenyewe. Kila kitu kinatokana na asili. Kila kitu ambacho ni muhimu na kinachohitajika na ulimwengu mzima kinatokana na asili. Kila kinachotokana na asili na kila kinachoitunza asili ni kizuri kwa kila sehemu ya asili. Mabadiliko ya kipengele chochote kwenye asili, ndiyo yanaufanya ulimwengu kuwa kama ulivyo.

JENGA MAHUSIANO BORA KATIKA MAISHA YAKO

Sisi binadamu ni viumbe wa kijamii, hatuwezi kuishi kwa kujitegemea wenyewe kwa kila kitu. Hivyo mahusiano yetu na wengine ni moja ya vitu muhimu sana kwetu ili kuweza kuwa na maisha bora.
Falsafa ya ustoa inatufundisha jinsi ya kutengeneza mahusiano bora na wale wanaotuzunguka kwa kuimarisha mahusiano yetu na ushirikiano kwenye mambo mbalimbali.
Njia bora ya kuimarisha mahusiano na ushirikiano ni kuangalia tabia nzuri zilizopo ndani ya wengine badala ya kuangalia mabaya pekee. Pia kuangalia namna ya kushirikiana na siyo kupingana.
Marcus ana maneno mazuri ya kutuambia kuhusu mahusiano;
Say to yourself first thing in the morning: I shall meet with people who are meddling, ungrateful, violent, treacherous, envious, and unsociable. They are subject to these faults because of their ignorance of what is good and bad. But I have recognised the nature of the good and seen that it is the right, and the nature of the bad and seen that it is the wrong, and the nature of the wrongdoer himself, and seen that he is related to me, not because he has the same blood or seed, but because he shares in the same mind and portion of divinity. So I cannot be harmed by any of them, as no one will involve me in what is wrong. Nor can I be angry with my relative or hate him. We were born for cooperation, like feet, like hands, like eyelids, like the rows of upper and lower teeth. So to work against each other is contrary to nature; and resentment and rejection count as working against someone. – Marcus Aurelius, Meditations, 2.1
Jiambie hili kitu cha kwanza asubuhi: Leo nakwenda kukutana na watu ambao ni waovu, wasio na shukrani, wenye fujo, wasaliti, wenye wivu na wasiojali. Watu hao wako hivyo kwa sababu hawajui kipi kizuri na kipi kibaya. Lakini mimi natambua asili ya uzuri na nimeona kipi sahihi na asili ya ubaya na kuona kipi kisicho sahihi na asili ya wanaofanya ubaya na kuona wana uhusiano na mimi, kwa sababu wana damu sawa na yangu na tunashirikiana mawazo yetu. Siwezi kuumizwa na yeyote kwa sababu hakuna anayeweza kunihusisha kwenye ubaya wake. Pia siwezi kuwa na hasira au kumchukia ndugu yangu. Sote tumezaliwa kwa ushirikiano, kama miguu, mikono, kope za macho, meno ya juu na ya chini. Hivyo kufanya kazi kwa kupingana ni kinyume na asili na chuki na kukataana ni kufanya kazi kinyume na wengine.

JIJENGEE TABIA NJEMA KATIKA MAISHA YAKO

Tabia njema ni moja ya misingi muhimu sana kwenye falsafa ya ustoa. Kadiri unavyojijengea na kuishi kwa tabia njema, ndivyo unavyojitengenezea maisha bora na yenye furaha wakati wote. Tabia njema ndiyo zao la furaha. Kwenye ustoa, tabia njema ni pale unapoishi na kusimamia yale yenye maana kwako na kwa wengine, na kuachana na yale yasiyo na maana.
Kwenye ustoa kuna tabia njema kuu nne;
HEKIMA; Ubora katika kufikiri na kufanya maamuzi.
UJASIRI; Uwezo wa kukabiliana na hatari kwa usahihi.
HAKI; Ubora katika mahusiano yetu na wengine.
KIASI; Uwezo wa kudhibiti hisia na tamaa.
Marcus ana haya ya kutuambia kuhusu tabia njema;

If you can find anything in human life better than justice, truthfulness, selfcontrol, courage […] turn to it with all your heart and enjoy the supreme good that you have found […] but if you find all other things to be trivial and valueless in comparison with virtue, give no room to anything else, since, once you turn towards that and divert from your proper path, you will no longer be able without inner conflict to give the highest honour to what is properly good. It is not right to set up as a rival to the rational and social good anything alien to its nature, such as the praise of the many, or positions of power, wealth, or enjoyment of pleasures. – Marcus Aurelius, Meditations, 3.6
Kama unaweza kupata kitu bora kwenye maisha ya mtu zaidi ya haki, ukweli, kujidhibiti na ujasiri, kishikilie sana kitu hicho. Lakini kama utakuta vitu vingine ni visivyo na maana ukilinganisha na tabia njema, usitoe nafasi kwa kitu kingine bali tabia hizo njema. Kwa sababu utakapoacha njia yako sahihi hutaweza tena kuzingatia yale ambayo ni mazuri kwako. Siyo sahihi kuleta upinzani kati ya fikra sahihi na vitu vya nje kama sifa kutoka kwa wengine, nafasi za madaraka, utajiri na kufurahia raha.

FANYA KILICHO SAHIHI, LAKINI USITEGEMEE CHOCHOTE.

Moja ya sababu zinazopelekea wengi kukosa furaha ni kufanya vitu ambavyo wanajua siyo sahihi, lakini kwa sababu wengine wanafanya au wanawategemea wafanye, basi wanafanya ili kuwaridhisha wengine. Hatari nyingine kubwa ni watu kufanya kitu wakitegemea matokeo fulani yatokee. Yaani unachukua hatua, ukitegemea matokeo fulani ili uwe na furaha. Hii ni njia ya kujitengenezea kushindwa na kujinyima furaha.
Cicero ana haya ya kutuambia kuhusu kufanya na kutegemea;
The wise person does nothing that he could regret, nothing against his will, but does everything honourably, consistently, seriously, and rightly; he anticipates nothing as if it is bound to happen, but is shocked by nothing when it does happen …. and refers everything to his own judgement, and stands by his own decisions. I can conceive of nothing which is happier that this. – Cicero, Tusculan Disputations 5.81
Mtu mwenye hekima hafanyi chochote atakachoweza kujutia, hafanyi chochote kinyume na matakwa yake bali anafanya kila kitu kwa heshima, msimamo, umakini na usahihi; hategemei chochote kitatokea kwa yeye kufanya, lakini pia hashangazwi na chochote kinachotokea, na anarejea kila kitu kwa maamuzi yake mwenyewe na kusimamia maamuzi hayo. Hakuna kitu chenye furaha kama kuishi kwa namna hii.
Kama ambavyo Cicero anatuambia, furaha siyo kitu unachokipata kutokana na kupata vitu fulani au kuwa kwenye hali fulani kama wengi wanavyofikiri.
Bali furaha ni matokeo ya maisha unayoishi na namna unavyofanya mambo yako. Kama unafanya kile kilicho sahihi mara zote, ukawa na msimamo na kufanya kwa umakini na usahihi, utapata matokeo mazuri. Na kama hufanyi ukitegemea matokeo mazuri, matokeo yoyote yatakayotokea hayatabadili chochote kwenye furaha yako, kusudi lako wewe ni kufanya kwa usahihi na siyo kulazimisha matokeo unayotaka wewe. Fanya maamuzi yako na yasimamie kwenye maisha yako, hili litakupa furaha kuliko kuhangaika na kukosa msimamo.

KABLA YA KULALA IPIME SIKU YAKO

Kila siku tunayoishi ni nafasi nzuri kwetu kuwa bora zaidi, kwa sababu kuna mengi tunakutana nayo ya kujifunza, kuna makosa tunayoyafanya na yapo mazuri tunayafanya pia. Wengi wamekuwa wanakosa nafasi ya kuzitumia siku zao kuwa bora zaidi kwa sababu hawapati muda wa kutafakari kila siku yao.
Kupitia Ustoa, tunashauriwa kuipima na kutafakari kila siku yetu kabla ya kulala. Na hapa ndipo tunapata nafasi ya kujifunza na kujiandaa kuwa bora zaidi kwenye siku inayofuata.
Jioni unapoimaliza siku yako, usikimbilie tu kulala na kuona siku imeisha, badala yake unahitaji kuwa na tahajudi ambayo utaipitia siku yako yote.
Kwenye tahajudi hii, pitia siku yako nzima, kwa kufikiria kila ulichofanya kwenye siku yako, kila uliyekutana naye na mawazo na hisia ulizokuwa nazo siku nzima.
Kisha jiulize na kujijibu maswali haya matatu;
Moja; vitu gani umefanya vibaya? Katika yale uliyofanya kwa siku nzima, je vitu gani umefanya kwa ubaya au kwa njia ambazo siyo sahihi?
Mbili; vitu gani umefanya vizuri? Katika vitu vyote ulivyofanya kwa siku nzima, vipi ambavyo umevifanya kwa uzuri, ni kwa namna gani umeishi misingi na tabia za ustoa?
Tatu; Vitu gani utakwenda kufanya tofauti? Ni vitu gani unahitaji kuvifanya kwa utofauti ili kuweza kuishi kulingana na msingi na tabia za ustoa?
Kwa kujiuliza na kujipa majibu ya maswali hayo matatu, utaweza kujipima kwa kila siku yako, na pia kujiandaa vyema kwa siku inayofuata. Pia utaepuka kurudia makosa uliyofanya kwa siku husika.
Kauli ya Epictetus kwenye tahajudi ya jioni;
“Allow not sleep to close your wearied eyes, Until you have reckoned up each daytime deed: “Where did I go wrong? What did I do? And what duty’s left undone?” From first to last review your acts and then Reprove yourself for wretched [or cowardly] acts, but rejoice in those done well.”
(Discourses, 3.10.2–3)
Anasema usikubali usingizi ufumbe macho yako kabla hujahesabu kila tendo ulilofanya kwenye siku yako. kipi umekosea, kipi umefanya vizuri na kipi ambacho hujakamilisha. Kuanzia tendo la kwanza mpaka la mwisho, jikaripie kwa yale uliyofanya vibaya na jisifie kwa yale uliyofanya vizuri.

TEGEMEA KUKUTANA NA WATU WABAYA KATIKA MAISHA YAKO YA KILA SIKU

Huwa tunazianza siku zetu tukitegemea kutekeleza yale tuliyopanga na kufanya mambo makubwa sana. Lakini siku zetu zimekuwa haziendi kama ambayo tumepanga, yamekuwa yanatokea mambo ambayo hatukutegemea yatokee, hasa kwa wale ambao tulitegemea wafanye vitu fulani na wasifanye.

Hili limekuwa linawanyima wengi furaha, lakini kwa falsafa ya ustoa, hupaswi kukosa furaha kwa mambo kama hayo, kwa sababu unapaswa kuyategemea yakitokea kabla hata hayajatokea.
Mstoa Marcus Aurelius ana hili la kutuambia pale tunapoianza siku yetu;
“Say to yourself first thing in the morning: I shall meet with people who are meddling, ungrateful, violent, treacherous, envious, and unsociable. They are subject to these faults because of their ignorance of what is good and bad.” (Meditations, 2.1)
Jiambie unakwenda kuianza siku ambayo utakutana na watu wachafu, wasio na shukrani, wenye fujo, wasaliti, wenye wivu na wasiojali mambo ya wengine. Na wanafanya mambo hayo kwa sababu hawajui mazuri na mabaya.
Kwa kuianza asubuhi yako kwa tafakari yenye nguvu namna hii, hakuna chochote kitakachokutokea ambacho kitakushangaza, maana ulishakitegemea.

WHAT IS A HAPPY LIFE ??

Kauli ya Seneca kuhusu kuishi kwa furaha;

“What is a happy life? It is peacefulness and lasting tranquillity, the sources of which are a great spirit and a steady determination to hold fast to good decisions. How does one arrive at these things? By recognizing the truth in all its completeness, by maintaining order, moderation and appropriateness in one’s actions, by having a will which is always well-intentioned and generous, focused on reason and never deviating from it, as lovable as it is admirable.” – Seneca, Letters, 92.3

Seneca anauliza maisha ya furaha maana yake nini? Ni maisha ambayo yana amani na utulivu, ambayo chanzo chake ni imani kuu na maamuzi ya kushikilia maamuzi sahihi. Na je mtu anawezaje kufikia hili? Ni kwa kugundua ukweli kamili, kwa kuenda kulingana na mipango, kuwa na kiasi katika matendo na kuwa na nia njema na ukarimu, kuongozwa na fikra sahihi na kutokupotoka.

FALSAFA YA USTOA NI NINI ???

USTOA ni falsafa ya matendo, ni falsafa ambayo imelenga kumwezesha mtu kuwa na maisha bora, kwa kufikiri sahihi na kuchukua hatua sahihi kwenye maisha yake. Falsafa ya ustoa siyo kama falsafa nyingine za kubishana na kutaka kuonekana unajua zaidi, badala yake ni falsafa ya kufikiri sahihi na kuchukua hatua sahihi. Falsafa ya ustoa inalenga kudhibiti hisia zetu na kuishi kulingana na asili. Kwa njia hiyo, tunakuwa na maisha bora wakati wote.

Falsafa ya ustoa ilianzishwa na Zeno wa Citium miaka ya 301 K.K na baadaye kupokelewa na kukuzwa na wanafalsafa Cato, Seneca, Epictetus na Marcus Aurelius. Hawa wote ni wanafalsafa walioishi zaidi ya miaka 2000 iliyopita, wakati wa utawala wa Roma.