Saturday, September 22, 2018

KILA MTU APAMBANE NA HALI YAKE,USINUNUE MATATAIZO YA WATU.

Chukua mfano una ndugu wa karibu au mtoto ambaye bado hajaweza kutengeneza maisha yake vizuri, lakini wewe maisha yako yameshakaa vizuri. Yeye hana kazi na ni mlevi. Hivyo unaamua kumsaidia awe na kipato, kwa sababu maisha yake siyo mazuri. Unampa mtaji wa kuanzisha biashara, anatumia vibaya na biashara inakufa. Unaona kwa kuwa una uwezo, basi unaweza kuwa unampa fedha ya kujikimu, lakini ukimpa fedha anaenda kulewa. Unakwama, usipompa fedha maisha yake yanakuwa magumu na unaonekana umemtenga ndugu yako, ukimpa anaenda kulewa na kuzitumia vibaya.

Wawezeshe watu kutatua matatizo yao wenyewe, na usisukumwe kufanya vitu kwa sababu unataka kuonekana una roho nzuri. Wale utakaowawezesha kutatua matatizo yao, utawasaidia hata wakati wewe haupo. Ila wale unaobeba matatizo yao, utawaandaa kuanguka vibaya pale ambapo wewe hutakuwepo. Na nikukumbushe tu, haijalishi unampenda mtu kiasi gani, hutakuwa naye kwa maisha yako yote, hivyo mpende kwa kumfanya aweze kutatua matatizo yake mwenyewe.

Katika kukazana kwetu kuwasaidia wengine, hasa wale wa karibu kwetu, watoto, wenza, ndugu tuliozaliwa nao, tumekuwa tunakazana kuwaibia matatizo yao. Tunayachukua kabisa matatizo yao na kuyafanyia kazi na wao wanabaki hawana cha kufanya.



Hii ni njia mbovu sana ya kutaka kumsaidia mtu, kwa sababu unakuwa humsaidii, badala yake unamsababishia matatizo zaidi. Kwa sababu unapomchukulia matatizo yake, anabaki hana cha kufanya, hivyo anaenda kutengeneza matatizo zaidi.

Kwa sababu ukikimbilia kuyabeba ili uonekane una roho nzuri, utaishia kumharibu zaidi yule mwenye matatizo. Kwa sababu maisha yetu yanatoa maana kwenye matatizo na changamoto tunazokutana nazo mara kwa mara na kuzitatua.

Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

Friday, September 21, 2018

JE, WAIJUA AKAUNTI YA FEDHA YA SAIKOLOJIA ?

Unahitaji kujizoesha kifikra na kisaikolojia kuwa na fedha nyingi, hata kama bado hujazishika kwenye mikono yako au kuwa nazo kwenye akaunti yako ya benki. Na unaweza kuanza kwa kufikiria mara kumi ya kipato unachopata sasa, kisha kufikiria kipato hicho mara kwa mara, kukiwekea mipango na kuweka lengo lako la kipato liwe ni kukua kufikia mara kumi ya kipato chako cha sasa. Kwa njia hii utaongeza kiwango chako cha fedha kisaikolojia.

 Watu wengi wanajua aina moja ya akaunti ya kifedha, ambayo ni akaunti ya benki, au akiba na uwekezaji ambao wamekuwa wamefanya. Hivyo ukitaka kuangalia utajiri wa mtu, unaangalia ni kiasi gani cha fedha anacho kwenye akaunti zake za benki na uwekezaji kiasi gani amefanya.

 Aina ya pili ya akaunti ya kifedha, ukiacha akaunti ya benki, ni akaunti ya fedha ya kisaikolojia. Kila mmoja wetu, ana kiwango chake cha kifedha kwenye fikra zake, ambacho ndiyo ameshajiambia anapaswa kupata kiwango hicho. Yaani kila mmoja wetu, kuna kiwango chake cha fedha, ambacho ameshakiweka kwenye fikra na mawazo yake, na akishapata kiwango hicho basi akili yake inatulia na hakazani tena kupata fedha zaidi.

Waangalie watu wote ambao wamepata fedha nyingi kwa mkupuo, kiasi kikubwa cha fedha ambacho hawajawahi kukishika kwenye maisha yao. Waangalie watu ambao wameshinda bahati nasibu, waangalie watu ambao wamerithi mali, waangalie watu ambao wamepokea mafao. Wengi haiwachukui muda wanakuwa wameshapoteza fedha nyingi walizopata na kurudi kwenye maisha yao ya kawaida.
Wanakuwa wamepata fedha nyingi kwenye akaunti ya benki, lakini akaunti yao ya kisaikolojia inasoma kiwango cha chini. Hivyo wanaacha kufikiria kabisa kuhusu fedha, wanaanza kupoteza fedha, mpaka zinapofika kwenye kile kiwango chao cha kisaikolojia ndiyo wanastuka na kuanza kufikiria kuhusu fedha.

 Pia unaweza kufikiria mara 100, mara 1000 na hata zaidi ya kipato unachopata sasa. Fikra zote hizo zitaiandaa akili yako kupokea fedha zaidi na kuweza kutulia na fedha zaidi unazopata. Unapofikiria mara elfu moja ya kipato unachopata sasa, ongezeko kidogo halitakusumbua kama linavyokusumbua sasa.


Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

Sunday, September 16, 2018

JE, WAJUA NJIA ZA KUONGEZA THAMANI YA MAISHA YA WATEJA WAKO ?? JIFUNZE HAPA .

Wateja wako wanapokaa na wewe kwa muda mrefu ndivyo unavyonufaika zaidi. Hivyo unahitaji kuweka juhudi kuhakikisha wateja wanabaki na wewe kwa muda mrefu. Yafuatayo ni mambo muhimu ya kuzingatia ili wateja wakae na wewe kwa muda mrefu.

  1. Toa huduma bora sana kwa wateja wako, ambazo hawawezi kuzipata sehemu nyingine yoyote ila kwako tu.
  2. Kutengeneza mahusiano mazuri na wateja wako, wafanye wateja kuwa rafiki kwako na kwa biashara yako, waone siyo tu wanakuja kununua, bali wanakuja kwa rafiki yao, anayewajali na kuwapa kile kilicho sahihi kwao.
  3. Weka mbele maslahi ya wateja wako na siyo faida unayotaka kupata.
  4. Waelimishe wateja wako, washauri vizuri, hata kama utapoteza mauzo, lakini hilo litawajengea imani zaidi na hivyo kuendelea kununua zaidi.
  5. Wafanye wateja wako kuwa mashabiki wa biashara yako.
Zipo hatua saba ambazo wateja wanapitia mpaka kufikia ngazi ya ushabiki.

Hatua ya kwanza ni wapitaji tu, wanaisikia au kiona biashara yako lakini hawajawahi kuuliza chochote.

Hatua ya pili ni wateja tarajiwa, wamesikia na wamefuatilia kutaka kujua zaidi kuhusu biashara yako.

Hatua ya tatu ni wanunuaji, hapa wamejua, wakafuatilia na wakajaribu kununua kile unachouza.

Hatua ya nne ni wateja, hapa mtu amejaribu kununua kwa mara ya kwanza, na amerudi tena kununua. Mtu kununua mara moja haimfanyi kuwa mteja, na wala haikufanyi wewe kuwa mjanja. Ni mpaka mtu atakaporudi tena kununua ndiyo utajua umefanya kazi nzuri.

Hatua ya tano ni mwanachama, hapa mteja anakuwa mnunuaji wa mara kwa mara na unaweza kumpa manufaa ya kadiri anavyonunua. Labda akifika kiwango fulani anapata zawadi, au akinunua mara tano, ya sita anapata bure. Hapa mwanachama anakuwa na kielelezo cha kuonesha idadi ya manunuzi yake.

Hatua ya sita ni mtetezi wa biashara yako, hapa mteja anakuwa tayari kuwaambia watu wengine kuhusu biashara yako, anatoa shuhuda kwa wengine na hasiti kuwaalika wengi waje kununua.
Hatua ya saba ni shabiki kindakindaki, hawa ni wale wateja ambao hawaambiwi chochote kuhusu biashara yako, yaani wao wameshachukulia biashara yako kama sehemu ya maisha yako. Hawa ni wateja ambao wanaiongelea biashara yako muda wote, na wakikutana na mtu ambaye hanunui kwako wanaona anakosa kitu kikubwa sana.
Katika kuboresha thamani ya maisha ya wateja wako, kazana kuwapandisha wateja wako ngazi mpaka wafikie kiwango cha watetezi na mashabiki wa biashara yako.
 
Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

JE, WAJUA AINA ZA GHARAMA ZA KUWAPATA WATEJA WA BIASHARA YAKO ?? JIFUNZE HAPA.

Kuna aina mbili za gharama ya kupata wateja wa biashara yako.

Aina ya kwanza ni GHARAMA ZINAZORUHUSIWA za kupata mteja. Hapa unatumia gharama ambazo mteja akinunua mara moja basi gharama ile inarudi. Chukua mfano umetengeneza tangazo ambalo limekugharimu tsh 100,000/= na tangazo hilo limewafikia watu 1000. Katika hao 1000 ndiyo wamenunua. Na kwa kila unayenunua unapata faida ya shilingi elfu moja. Inamaana kwa watu 100, faida unayopata ni tsh 100,000/= sawa sawa na gharama ulizoingia kutoa tangazo. Hivyo hiyo ni gharama inayoruhusiwa ya kupata mteja. Kama utaandaa tangazo kwa gharama kubwa kuliko faida unayopata, hiyo sasa siyo GHARAMA INAYORUHUSIWA kupata wateja.

Aina ya pili ni GHARAMA UWEKEZAJI KWA WATEJA. Hapa unatumia gharama kubwa, ambayo inakuletea wateja, lakini manunuzi ya mwanzo ya mteja hayalipi gharama hiyo. Lakini kwa kuwa mteja ataendelea kununua, basi huko mbeleni ile gharama inarudi. Hivyo hapa unakuwa umewekeza kwa mteja, ukijua kwamba atafanya biashara na wewe kwa muda mrefu na gharama zako zitarudi.
Kwa biashara ndogo, ni vyema kutumia gharama zinazoruhusiwa, kwa biashara kubwa, ambazo zina rasilimali nyingi, zinaweza kuwekeza kwa wateja na baadaye zikanufaika zaidi. Usikimbilie kununua wateja kabla hujajua ni gharama kiasi gani unaingia na kama zinalipwa na idadi ya wateja watakaonunua.

Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

JE, WAJUA JINSI YA KUNUNUA WATEJA WA BIASHARA YAKO ??? JIFUNZE HAPA !!

Kazi kubwa ya kila biashara ni kununua wateja wa biashara hiyo. Sasa ili biashara iweze kufanikiwa, lazima iweze kununua wateja bora kwa gharama ambazo siyo kubwa. Kitu ambacho wafanyabiashara wengi siyo tu hawakifanyii kazi, ila hata hawakijui.
Inawezekana upo kwenye biashara, lakini hujui kama biashara yako inanunua wateja. Sasa nikuambie tu, kila biashara huwa inatumia fedha kununua wateja, na biashara yako pia inatumia fedha kununua wateja.
Labda nikuulize swali, biashara yako inatumia gharama kiasi gani kununua wateja? Na je gharama ambazo biashara yako inatumia kununua wateja zinarudi? Najua maswali haya yanaweza kukuacha ukiwa umeduwaa kwa sababu hujawahi kufikiria kuhusu kununua wateja.
Sasa kwenye kitabu nilichosoma ; BUYING CUSTOMERS, kilichoandikwa na kocha wa biashara Bradley Sugars, mwandishi ametushirikisha njia sahihi za kununua wateja bora wa biashara zetu na kwa gharama nafuu ambazo biashara inaweza kumudu.
Kwa kuanza, kila biashara huwa inanunua wateja. Kila hatua unayotumia kuwafanya wateja wajue kuhusu uwepo wa biashara yako, ni kununua wateja. Kama umewahi kutangaza biashara yako, umewahi kuandaa vipeperushi, kama umetengeneza bango, au kuuza vitu kwa pamoja kwa bei ya punguzo, kama umewahi kupunguza bei ili mteja anunue, au kutoa zawadi kwa mteja anayenunua. Kama umewahi kutoa usafiri kwa mteja, au kumpelekea alichonunua, au kumwomba mteja wako akuletee wateja zaidi. Zote hizo ni harakati za kununua wateja unazotumia kwenye biashara yako.
Sasa kuna ambazo zinakuletea wateja bora, nyingine hazikuletei wateja wazuri. Nyingine ni za gharama kubwa kwako, nyingine ni za gharama ndogo.
Kupitia kitabu cha BUYING CUSTOMERS, tunakwenda kujifunza jinsi ya kununua wateja bora kwa gharama nafuu kwenye biashara zetu.

 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

JE, WAJUA NJIA ZA KUTENGEHEZA FAIDA KATIKA BIASHARA YAKO ? JIFUNZE HAPA ,

 Njia hizi zinategemeana na zinaenda kama ngazi, hivyo ili kunufaika lazima uzifanyie kazi kwa pamoja.

Njia ya kwanza ni kuongeza idadi ya watu wanaoijua biashara yako. Na hapa ndipo zoezi zima la kununua wateja linapofanya kazi. Kadiri watu wengi wanavyojua kuhusu biashara yako, ndivyo inakuwa rahisi kwako kuwageuza watu hao kuwa wateja. Kama watu 1000 ndiyo wanaojua kuhusu uwepo wako, ukiongeza watu 100 unakuwa umeenda mbele zaidi.

Njia ya pili ni kuwageuza wanaojua kuhusu biashara yako kuwa wateja halisi. Mtu kujua biashara yako haimaanishi ndiyo mteja wa biashara hiyo. Mteja ni yule ambaye ametoa fedha na kununua kitu kwenye biashara yako. ili kuongeza wateja wa biashara yako, unahitaji kuwashawishi wale wanaojua kuhusu biashara yako wanunue kile unachouza.

Njia ya tatu ni kuwafanya wateja warudi kununua tena na tena. Kama umetumia gharama kumfikisha mteja kwenye biashara yako, jua kabisa akinunua mara moja ni hasara kwako. Unapata faida pale mteja anaponunua tena na tena na tena. Na unachopaswa kujua ni kwamba, ni rahisi kumuuzia mteja ambaye alishanunua kwako kuliko kumuuzia mteja mpya kabisa. Hivyo weka juhudi katika kuwafanya wateja waendelee kununua kwako zaidi na zaidi.

Njia ya nne; kuongeza kiwango cha manunuzi. Kama mteja akija kwako ananunua kitu kimoja, unahitaji kumshawishi anunue kitu kingine ambacho kinaendana na kile alichonunua. Hapo unaongeza mauzo na kuongeza faida pia. Kwa mfano kama unauza vifaa vya ujenzi, akaja mteja kununua rangi, unahitaji kumshawishi anunue na brashi za kupakia rangi na vitu vingine vinavyoendana na hili. Kadhalika kwenye mavazi na hata vifaa vya kielektroniki, mpe mteja wigo wa kununua vitu vinavyoendana na kile anachotaka.

Njia ya tano ni kuongeza bei, hii ndiyo wengi huwa wanaikimbilia, lakini ukitumia hizo nne na hii kwa pamoja, utanufaika sana. kwenye njia ya tano, unaongeza bei ya kitu ili upate faida zaidi. Kama utafanyia kazi hatua hizi tano kwa pamoja, ongezeko dogo, kama la asilimia 10 kwenye kila hatua, litaleta ongezeko la asilimia 61 kwenye faida. KAZI  KWAKO  NDUGU .

 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

WEKA MKAZO KATIKA THAMANI YA MAISHA YA MTEJA , GHARAMA YA KUMPATA MTEJA NA KIWANGO CHA WATEJA WANAOPATIKANA KWENYE BIASHARA YAKO UTAFANIKWA SANA.

Ili biashara yako ifanikiwe, inahitaji kuweka mkazo kwenye maeneo haya matatu muhimu sana.

(1). THAMANI YA MAISHA YA MTEJA. Wafanyabiashara wengi huwa wanamwangalia mteja kwa wakati ule anaokuja kununua tu. Huwa hawaangalii thamani yake ya maisha. Kwa mfano kama mteja akija kununua kwako mara moja, unapata faida ya shilingi elfu moja, ni rahisi kuona elfu moja inakuja. Lakini chukua mfano kwamba mteja huyo ananunua kila wiki, na anaweza kununua kwako kwa miaka mitano ijayo. Hii ina maana kwa mwaka, anakuingizia faida ya 1000 x 52(idadi ya wiki za mwaka) ambayo ni tsh 52,000/= na kwa miaka mitano; 5 x 52,000/= ambayo ni sawa na 260,000/=. Thamani ya maisha ya mteja wako huyo ni shilingi laki mbili na elfu sitini, na siyo ile elfu moja unayoiona anapokuja. Je kwa kujua hilo hutaongeza umakini zaidi kwa mteja huyu ili aendelee kuwa na wewe kwa miaka hiyo mitano na hata zaidi?

(2).GHARAMA YA KUMPATA MTEJA. Hapa ndipo gharama za kununua wateja wa biashara yako zinapoingia. Kabla hujachukua hatua yoyote ya kuongeza wateja zaidi kwenye biashara yako, lazima ujiulize gharama unayotumia inaleta wateja wangapi na kama gharama hizo zinarudi kupitia mauzo. Upo usemi kwenye utangazaji wa biashara kwamba nusu ya bajeti ya matangazo huwa inapotea, ila mtu hawezi kujua ni nusu ipi. Hii ina maana kwamba, gharama nyingi watu wanazotumia kutangaza biashara zao zinapotea, hazirudi kabisa kwenye biashara. Lazima ujue gharama zako na zinarudije.

(3). KIWANGO CHA WATEJA WAPYA WANAOPATIKANA. Unapotangaza biashara yako, watu wengi wanajua kuhusu uwepo wako. Lakini watu kujua kuhusu biashara yako hakukunufaishi chochote. Ni mpaka pale watu hao watakapochukua hatua ya kununua ndiyo biashara inanufaika, kama gharama zimepigwa vizuri. Hivyo eneo la kuweka mkazo ni kuongeza kiwango cha wanaojua biashara kuwa wateja wa biashara hiyo. kadiri watu wengi wanaofikiwa na tangazo wanakua wateja, ndivyo gharama za kupata wateja zinakuwa ndogo na faida inakuwa kubwa baadaye.


 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

JINSI YA KUONGEZA WATEJA WAPYA WENGI ZAIDI KATIKA BIASHARA.

Baada ya kutangaza biashara yako, utakuwa na watu wengi wanaojua kuhusu biashara yako, hawa ni wateja tarajiwa. Sasa unahitaji kuwabadili hawa na kuwa wateja halisi wa biashara yako. Kadiri unavyowageuza wengi kuwa wateja halisi, ndivyo gharama ya kuwapata inakuwa ndogo na ndivyo faida inakuwa kubwa kwako.
Kuongeza kiwango cha wateja wapya, fanya yafuatayo;

  1. Toa uhakika wa kile unachouza, mpe mteja uhakika kwamba kama anachonunua hakitafanya kazi basi anaweza kurudisha na akapata kitu kingine au akarudishiwa fedha zake.
  2. Tumia shuhuda za wateja walionunua kwako siku za nyuma na wakanufaika sana. shuhuda zina nguvu kubwa ya ushawishi.
  3. Kuwa na kitu cha tofauti ambacho kinapatikana kwako tu na mteja hawezi kukipata kwa wafanyabiashara wengine, na mweleze wazi kwamba atakipata kwako tu.
  4. Uza viti vya thamani kubwa, ambavyo upatikanaji wake siyo rahisi.
  5. Tengeneza mwonekano mzuri wa kile unachouza, ikiwa ni pamoja na unavyopakia kile unachouza. Mwonekano mzuri unaongeza mauzo.
  6. Weka majaribio ambapo mteja anaweza kujaribu kitu kabla hajakinunua.
Njia ambazo unapaswa kuziepuka sana kuwashawishi watu kununua ni kupunguza bei au kutoa zawadi zenye thamani kubwa. Kwa kufanya hivi utapunguza faida na pia utavutia wateja ambao baadaye watakuwa wasumbufu sana kwako.
 
 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

JE, UMEAJIRIWA ? AU WEWE NI MFANYABIASHARA ? ONGEZA KIPATO CHAKO KILA MWEZI KWA KUFANYA HIKI.

Rafiki, kwenye eneo la fedha, ukuaji unapimwa kwa ongezeko lako la kipato. Na ongezeko siyo la mwaka, bali la mwezi. Kila mwezi, inabidi kipato chako kiwe kinaongezeka.
Kama kipato chako kinabaki pale pale kila mwezi, kama ilivyo kwa waajiriwa na hata wafanyabiashara wengi, siyo kwamba unabaki pale pale, bali unarudi nyuma kwa upande wa kipato.
Kwa sababu kila siku gharama za maisha zinaongezeka, hivyo kipato kisipoongezeka, unazidi kurudi nyuma.
Njia pekee ya kuongeza kipato chako kila mwezi ni kutoa thamani zaidi kwa wengine. Kama upo kwenye biashara hilo ni rahisi, uzia wateja wengi zaidi kila mwezi, hata kupata mteja mmoja wa ziada kila mwezi ni hatua nzuri. Wauzie wateja ulionao zaidi kila mwezi, na pia ongeza bidhaa na huduma ambazo wateja wako wanahitaji pia.
Kwa walioajiriwa, pia unaweza kuongeza thamani zaidi kwenye kazi yako au nje ya kazi yako na ukaongeza kipato chako. Kama una utaalamu fulani, tumia utaalamu huo nje ya kazi yako kwa kutoa huduma za utaalamu huo. Unaweza kutoa huduma za ushauri kulingana na utaalamu ulionao na watu wakalipia msaada ambao unakuwa umewapatia.
Chochote unachofanya, hakikisha kila mwezi kipato chako kinaongezeka zaidi. Na hivyo ni muhimu kila mwezi ukapiga hesabu za kujua kipato chako ni kiasi gani.


 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

USITAFUTE MCHAWI WA MAISHA YAKO , MCHAWI NI WEWE MWENYEWE !!

‘Be miserable. Or motivate yourself. Whatever has to be done, it’s always
your choice.’ – Wayne Dyer
kama unajisikia vibaya, hilo ni tatizo lako ninafsi. Wala usitafute mtu wa kumlaumu, hakuna anayeharibu siku yako ila wewe mwenyewe. Hakuna anayeharibu maisha yako ila wewe mwenyewe. Wewe ndiye unayechagua ufikirie nini, usikilize nini, uangalie nini, uambatane na nani na ufanye nini.
Sasa kama unachagua kufikiria vitu vinavyokufanya ujisikie vibaya, unataka kumlaumu nani? Kama umechagua mwenyewe kusikiliza na kuangalia habari hasi, halafu unajisikia kukata tamaa na maisha, unataka kumlaumu nani? Kama umechagua kukaa na watu ambao hawana wanakoelekea, watu waliokata tamaa na maisha yao, na wewe unaanza kuona maisha yako hayana maana, unafikiri nani wa kulaumiwa?
Kama unajisikia vibaya, umekata tamaa na maisha au unakosa hamasa ya kuchukua hatua, anza kuangalia maamuzi uliyofanya kwenye maisha yako, na utaona jinsi yale uliyochagua wewe mwenyewe yanakuweka kwenye hali hiyo.
Na uzuri ni kwamba wewe ndiye unayechagua, hivyo usijaribu kumlaumu yeyote. Kama hupendi pale ulipo sasa badili kitu, wewe siyo mti kwamba lazima uendelee kuwa hapo ulipo sasa.



 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

ILI UFANIKIWE KIBIASHARA KUNA WATEJA NI LAZIMA UACHANE NAO,

Ili biashara yako ikue vizuri na uweze kupata faida, lazima ufukuze baadhi ya wateja.
Kwanza kabisa unahitaji kuwapanga wateja wako kwenye makundi A, B, C, na D.
Kundi A ni wale wateja ambao wanalipa fedha nyingi na siyo wasumbufu.
Kundi B ni wale wateja ambao wapo tayari kulipia, lakini siyo walipaji wa fedha nyingi, ila ni wateja wenye msimamo, ambao unaweza kwenda nao muda mrefu, na hawana usumbufu mkishakubaliana.
Kundi C ni wale wateja ambao wanataka punguzo kwenye kila kitu, na watakusumbua sana, wanaweza kununua kwa bei ya punguzo na bado wakarudi tena kulalamika kwamba haikuwa sawa kwao.
Kundi D ni wale wateja ambao ni matatizo kwa biashara yako, kwanza hawalipi kwa wakati, na kwenye kila kitu wanatafuta njia ya kubishana au kugombana. Hawa ni wateja ambao wanakuja wakiwa wamejipanga kukusumbua, ili wanufaike zaidi wao.
Ukishawagawa wateja wako kwenye makundi hayo manne, wahudumie vizuri wateja wa kundi A na B, na fukuza wateja wa kundi C na D, kwa sababu hawa ni wateja mabao hawana faida, na pia wanakuzuia usiwahudumie vizuri wateja wa kundi A na B.
Swali ni unawafukuzaje wateja hao?
Zipo njia mbili;
Ya kwanza ni kuwapa utaratibu mpya wa kufanya biashara na wewe, kwamba yale waliyozoea hayapo tena. Bei ni moja na haipungui na malipo ni kwanza na siyo baadaye. Kama hawawezi hilo wanaweza kwenda kwenye biashara nyingine.
Njia ya pili ni kuongeza bei ya bidhaa au huduma unayouza, na moja kwa moja watakimbia wenyewe.
Ukishaachana na wateja hao wasumbufu, nguvu zako peleka kwa wale wateja wazuri wa biashara yako.
Pia unapotangaza biashara yako, hakikisha unatumia lugha inayowavutia wateja wa kundi A na B, badala ya kundi C na D. Kwa mfano kama tangazo lako linasema kuna punguzo la bei au zawadi ya bure, utajikuta unavutia C na D wengi, maana ndiyo wanaopenda rahisi na bure.

 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com
MAARIFA SAHIHI + KUCHUKUA HATUA KUBWA = MAFANIKIO MAKUBWA.

JIFUNZE KUJITHIBITI, KUWA HALISIA , KUJITAMBUA ,KUJIENDELEZA UTAFANIKIWA SANA KIMAISHA.

(1).  KUJIDHIBITI
Eneo la kwanza kabisa unalohitaji kulifanyia kazi kila siku ili kuwa na maisha bora ni kwenye udhibiti. Unahitaji kujidhibiti wewe mwenyewe, la sivyo utawapa wengine nafasi ya kukudhibiti wewe. Unahitaji kujipangia nini utafanya na kipi hutafanya na kufuata mpango huo.
Muda ulionao kila siku ni mfupi sana, ni muda ambao kama ukiweza kujidhibiti utaweza kufanya makubwa. Lakini ukishindwa kujidhibiti, utashangaa muda unaisha na hakuna ulichofanya. Lazima uweze kujiambia HAPANA wewe mwenyewe, pale unapojiona unakosa udhibiti. Pia lazima uweze kujiadhibu wewe mwenyewe pale unapokwenda kinyume na mipango uliyojiwekea wewe mwenyewe.
Jidhibiti wewe mwenyewe na kila siku yako itakuwa siku ya ushindi, kwa sababu utafanya yale ambayo ni muhimu zaidi kwako.

(2). KUWA  HALISIA / ACHA MAIGIZO
Kitu kimoja ambacho dunia inakazana sana kufanya kwako ni wewe uwe kama wengine. Kwa sababu dunia inajua ukiwa wewe, utakuwa msumbufu, hutafaa kutawaliwa na hivyo inakazana sana uwe kama wengine, uwe ndani ya kundi ili uweze kutawaliwa na kutumiwa vizuri na wengine.
Hivyo eneo la pili la kufanyia kazi kila siku ili kuwa na maisha bora ni uhalisi. Unapaswa kukazana kuwa halisi kila siku, kuishi maisha yako kwa uhalisia, kuacha kuigiza na kuacha kufanya vitu ili kuwaridhisha wengine au uonekane na wewe unafanya.
Hutaweza kufanikiwa kama huishi maisha halisi kwako, hata kama utapata vitu vingi kiasi gani, kama maisha unayoishi siyo halisi kwako, kila mara utasikia sauti inakuambia wewe bado sana. Na hapa ndipo wengi husema wamefanikiwa lakini hawana furaha.
Shida yao ni moja tu, maisha wanayoishi siyo halisi kwao, ni maisha feki na hivyo mafanikio yoyote wanayopata yanakuwa yanaonekana na wengine lakini siyo ndani yao binafsi.
Kuwa halisi kwako, jua uimara wako, jua madhaifu yako, jua yapi yenye maana kwako na jua kusudi la maisha yako ni lipi. Kisha tumia kila dakika ya siku yako kuishi maisha ambayo ni halisi kwako. Utafanikiwa kariri unavyoishi maisha halisi kwako.

(4). JITAMBUE.
Kujitambua ni eneo muhimu sana la kufanyia kazi, na linatangulia uhalisia. Kwa sababu bila ya kujitambua, hutaweza kuishi uhalisia wako. Na changamoto ya kujitambua ni kwamba ni zoezi endelevu.
Watu wengi wamekuwa wakifikiri wakishajua wanataka nini kwenye maisha yao, wakishaweka malengo makubwa basi wamemaliza. Hiyo siyo sahihi, unachojua leo kuhusu wewe, kinaweza kuwa tofauti kabisa na utakachotambua kesho kuhusu wewe.
Kubadili mazingira, kukutana na changamoto, kote huko kutakufunulia kwa undani kuhusu wewe. Mara nyingi huwezi kujua una uwezo wa kufanya makubwa kiasi gani mpaka pale unapokutana na changamoto kubwa kwenye maisha yako.
Hivyo zoezi la kujitambua ni endelevu, kila siku, kwa kila unachopitia, jiulize ni kipi kipya umejua kuhusu wewe. Na wakati mzuri wa kujipima ni pale unapopitia mambo magumu. Utaweza kupima uwezo wako wa kudhibiti hasira pale unapokasirishwa hasa. Unaweza kujua unaweza kuvumilia ugumu kiasi gani pale unapokutana na ugumu zaidi.
Kila siku mpya ya maisha yako ni siku ya kujitambua zaidi, ishi kila siku kwa kutaka kujitambua na maisha yako yatakuwa bora sana.


(4).KUJIENDELEZA.
Eneo la nne ambalo unapaswa kulifanyia kazi kila siku ni kujiendeleza wewe binafsi. Kila siku lazima ukazane kuwa bora zaidi kuliko siku iliyopita. Kila siku unapaswa kujifunza kitu kipya. Usikubali siku iishe ukiwa kama siku ya jana ilivyoisha.
Weka kipaumbele kwenye kujifunza. Jifunze kupitia kusoma, kusikiliza, kuangalia na hata kufanya. Soma vitabu, sikiliza mafundisho mbalimbali, waangalie wengine kwa namna wanavyofanya na jaribu vitu vipya kwa ajili ya kujifunza kwa kufanya.
Jinsi unavyojifunza kila siku, unazidi kuwa bora na kuyafanya maisha yako kuwa bora zaidi.
Rafiki yangu mpendwa, maeneo haya manne ni muhimu sana kwako kuyafanyia kazi kila siku. Ninaposema kila siku, namaanisha kila siku ya maisha yako. Na usiache hata siku moja, mpaka siku unaondoka hapa duniani.
Kama unajiambia huwezi kila siku, kama unajiambia utajisahau au kupitiwa na maisha mengine, ninayo nafasi ya kukumbusha hili kila siku, na kukushirikisha fursa za kujifunza na kujitambua kila siku. Karibu kwenye KISIMA CHA MAARIFA, ambapo utapata nafasi ya kuingia kwenye kundi la wasap, na kila siku utajifunza kwenye maeneo hayo manne na mengine mengi.


 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker(MC), Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

Saturday, September 15, 2018

UKIFANYA KWA MSUKUMO WA NDANI , UTAPATA PESA SANA.

Kwa chochote ambacho unafanya kwenye maisha yako, kuna misukumo au hamasa za aina mbili.
(2):-
         Aina ya kwanza ni msukumo au hamasa inayotoka ndani yako. Hapa ni pale unapofanya kitu kwa sababu umechagua kufanya, kwa sababu unajua ni kitu muhimu kwako kufanya na kwa sababu unajua kuna thamani unaongeza kwenye maisha ya wengine.

        Aina ya pili ni msukumo au hamasa inayotoka nje. Hapa ni pale unapofanya kitu ili kuonekana unafanya, au kwa sababu wengine wanafanya, au kwa sababu watu wanakutegemea ufanye hivyo. Pia unaweza kuwa unafanya ili upate kitu fulani unachotaka.(BENDERA  FUATA  UPEPO ).

(1) .MSUKUMO  AU   HAMASA KUTOKA  NDANI

Msukumo wa ndani yako ndiyo wenye nguvu sana, kwa sababu utafanya licha ya kinachoendelea nje yako. Lakini msukumo wa nje hauna nguvu kubwa, kwa sababu mazingira ya nje yakibadilika, basi na msukumo unabadilika.
Sasa kama unataka kupata fedha zaidi, tafiti zinaonesha kwa kutumia msukumo wa ndani unaweza kutengeneza fedha mara tatu zaidi ya unavyotumia msukumo wa nje.
Pale unapofanya kitu kwa sababu umechagua kufanya, kwa sababu unataka kuwasaidia wenye uhitaji au unataka kutoa mchango wako, utatengeneza kipato kikubwa kuliko pale unapofanya ili tu upate fedha ya kulipa gharama za maisha yako.
 
Unapofanya kitu kwa sababu tu unataka fedha, unapata fedha kidogo, kuliko kama utafanya kitu hicho hicho kwa msukumo kutoka ndani yako.
Na pale unapofanya kitu kwa msukumo wa ndani, haimaanishi kwamba hujali fedha, unajali sana, ila msukumo wa wewe kufanya ni mkubwa kuliko fedha, hivyo unakuwa umejiweka juu ya fedha, kitu ambacho kinakuwezesha kupata fedha kama unavyotaka.



(2).MSUKUMO  AU   HAMASA  KUTOKA  NJE

Lakini unapofanya kwa ajili ya fedha pekee, utapata fedha, lakini utakuwa umeweka fedha juu yako, hivyo unakuwa umejiwekea ukomo wewe mwenyewe, ukishafika kiwango fulani cha fedha utaacha kufanya kwa sababu hamasa yako ilikuwa fedha pekee.

Kuwa na msukumo wa ndani kwenye kila unachofanya, penda fedha na ihitaji, lakini isiwe msukumo pekee wa wewe kufanya kitu. Fanya unachofanya kwa msukumo wa ndani na utaweza kupata fedha kadiri utakavyo, na hutakuwa na ukomo wowote kwenye kipato unachoweza kutengeneza.


 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki ---Mwl  wa  Maisha Na  Mafanikio, Mshauri, Public Speaker, MC,Mwandishi, Mjasiriamali /
Tuwasiliane kwa :+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com


Sunday, September 2, 2018

JINSI YA KUDHIBITI TABIA YA KUNUNUA VITU OVYO ! KWA KUTUMIA SHERIA YA SIKU 30 KWENYE FEDHA.

Moja ya tatizo kubwa ambalo watu wanalo kwenye fedha ni kushindwa kudhibiti matumizi. Watu wanapokuwa na fedha, na wakakutana na kitu kizuri, wanajikuta wameshanunua.
Ndiyo maana watu wanaishia kuwa na nguo ambazo hawazivai, vitu ambavyo hawavitumii, lakini wamenunua. Ukiwauliza kwa nini walinunua hata hawawezi kukupa jibu la wazi. Wengine watakuambia ilikuwa rahisi na wasingeweza kupata kwa bei rahisi vile. Wengine watakuambia wanajua watakuja kuhitaji kitu hicho siku moja.
Haijalishi unajifariji kwa maneno gani, kama umenunua kitu ambacho hukitumii sana, umepoteza fedha. Au kama umenunua kitu, lakini inakulazimu ukitumie ili usijione umepoteza fedha, jua umeshapoteza fedha.
Sasa, ipo sheria inayoweza kukusaidia usirudie tena makosa uliyofanya huko nyuma ya kununua kitu ambacho hukitumii. Sheria hiyo ni sheria ya siku 30.
Sheria hii inasema kwamba, kama umekutana na kitu na ukajishawishi unahitaji kukinunua, usikinunue hapo hapo. Badala yake andika mahali kwamba unataka kununua kitu hicho, kisha subiri kwa siku 30 kabla hujakinunua. Sasa kama siku 30 zitaisha na bado ukawa unauhitaji mkubwa wa kitu hicho, au hata siku 30 hazijaisha uhitaji unakuwa mkubwa mno la sivyo maisha hayawezi kwenda, nunua kitu hicho.
Rafiki, kwa sheria hii, usijidanganye kwamba hii ni bei rahisi na hutapata tena, au kitu hicho ni cha mwisho na hakitapatikana tena. Sheria ni moja, subiri siku 30 zipite na utanunua.
Kitu ambacho utanufaika nacho kwenye sheria hii ni kwamba baada ya siku tatu kupita, wala hata hutakumbuka kama ulipanga kununua kitu hicho.

 Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki  /+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

USIOGOPE KUACHA KITU KAMA HAKINA TIJA.


Usiogope kuacha kitu pale unapoona hakikupi matokeo uliyotaka. Watu wengi huwa wanafikiria kuacha ni kushindwa. Siyo sahihi, unaweza kuacha kitu ambacho hakifanyi vizuri na kufanya kingine ambacho kitakuwezesha kufanikiwa zaidi.


Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki  /+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

FANYA MAAMUZI KWA WAKATI.

Fanya maamuzi wakati unapokutana na hitaji la kufanya maamuzi. Usijiambie wacha nifikiri nitaamua baadaye. Kama kitu ni muhimu fanya maamuzi sasa, au hutayafanya kabisa. Maamuzi yanayosogezwa mbele ni maamuzi ambayo yamekuwa hayafanywi.

Usiogope kukosea pale unapochagua kufanya maamuzi. Ni bora ufanye maamuzi ukosee, kwa sababu utarekebisha makosa yako, kuliko kutokufanya maamuzi kabisa.


Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki  /+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com

USIKIMBIZANE NA VITU VYA KUPITA . WEWE KAZANA NA AMBAVYO SIYO VYA KUPITA.

Weka nguvu zako kwenye vitu ambavyo havitabadilika. Watu wengi huwa wanakazana kukimbizana na vitu vinavyopita, fursa mpya, fasheni na habari mpya ya mjini. Wewe kazana na vile ambavyo siyo vya kupita, na biashara yako itakuwa imara. Achana na vitu ambavyo watu wanataka sasa, kazana na vitu ambavyo watu wataendelea kuhitaji miaka kumi ijayo.



Na  Mwl  Japhet  Masatu , Dar  es  salaam , Tanzania,  Afrika Ya  Mashariki  /+ 255 755 400 128 / + 255 716 924136(WhatsApp ).  EMAIL: japhetmasatu@gmail.com