Sunday, October 4, 2020

UCHAMBUZI WA KITABU , MINDSET ( SAIKOLOJIA MPYA YA MAFANIKIO )

Karibu kwenye uchambuzi wa kitabu Mindset: the new psychology of success kilichoandikwa na mwanasaikolojia Carol S. Dweck.

Hiki ni kitabu kinachoelezea mitazamo ambayo watu tunayo na jinsi inavyoathiri maisha na mafanikio yetu.

Kupitia kazi zake, tafiti mbalimbali na maisha ya wengine Carol anawagawa watu kwenye makundi makuu mawili;

Kundi la kwanza ni wale wenye MTAZAMO MGANDO ambao anauita FIXED MINDSET.

Huku kundi la pili wakiwa wale wenye MTAZAMO WA UKUAJI ambao anauita GROWTH MINDSET.

Tofauti hii moja na ndogo tu kwenye mtazamo, ndiyo inaleta tofauti kubwa kwenye maisha kati ya wale wanaofanikiwa sana na wale wanaokuwa na maisha ya kawaida.




Mtazamo ambao mtu unakuwa nao, uwe ni mgando au wa ukuaji, unatokana na imani ambazo umekuwa nazo kwa maisha yako yote. Imani hizo hujengeka mapema tangu ukiwa mdogo, kulingana na mazingira yanayokuzunguka.

Kile ambacho wengi tunaita haiba, ni mtazamo wa kuendesha maisha ambao mtu unakuwa umeuchukua na kwenda nao maisha yake yote. Na kitu ambacho kimekuwa kikwazo kwa wengi kufikia mafanikio makubwa kwenye maisha yao, ni aina ya mtazamo wanaokuwa nao.

Kwenye kitabu hiki, Carol anakwenda kutuonesha jinsi mitazamo tuliyonayo inavyojengwa, jinsi inavyokuwa kikwazo kwa mafanikio na pia jinsi ya kubadili mtazamo ambao mtu unao na kuwa na mtazamo bora zaidi.

Kitabu kimesheheni tafiti mbalimbali pamoja na mifano ya wale waliofanikiwa na kushindwa kwenye michezo, biashara na hata elimu, kutokana na aina ya mtazamo ambao mtu anakuwa nao.

Kitabu pia kinatusaidia jinsi ya kuwajenga watoto kwenye mtazamo sahihi ambao utawawezesha kufikia mafanikio makubwa kwenye maisha yao.




Tofauti kuu za mitazamo miwili kwa ufupi.

Mitazamo miwili ambayo watu wanayo, yaani mgando na ukuaji huwa inaleta tofauti nyingi kwa watu, lakini kubwa kabisa na zinazopelekea baadhi kufanikiwa na wengi kushindwa ni hizi;

1. UWEZO WA KIAKILI.

MGANDO; huona uwezo wa akili una ukomo na hivyo hawakazani kujiendeleza.

UKUAJI; huona uwezo wa akili hauna ukomo na hivyo hujiendeleza kwa kujifunza.

2. CHANGAMOTO.

MGANDO; huzikimbia changamoto.

UKUAJI; huzikaribisha changamoto.

3. VIKWAZO.

MGANDO; huona ndiyo mwisho wa safari yao na kukata tamaa.

UKUAJI; huona ni njia ya kufika wanakotaka na hivyo hung’ang’ana.

4. JUHUDI.

MGANDO; huona juhudi hazihitajiki, maana uwezo wao una ukomo.

UKUAJI; huweka juhudi kubwa wakijua zitabadili uwezo wao.

5. KUKOSOLEWA.

MGANDO; huepuka kila aina ya ukosoaji na hawajifunzi.

UKUAJI; hupokea ukosoaji na kujifunza.

6. MAFANIKIO YA WENGINE.

MGANDO; huona wivu pale wengine wanapofanikiwa na kuona ni hatari kwao.

UKUAJI; hufurahia mafanikio ya wengine na kujifunza kutoka kwao.

7. MAFANIKIO.

MGANDO; mafanikio yao hufikia kilele mapema na hawafanyi makubwa.

UKUAJI; wanafikia mafanikio makubwa na kuendelea kufanikiwa zaidi.


UTABIRI UTAKAOKUSAIDIA KWENYE MAISHA YAKO ?

Utabiri wa wataalamu ni wa uongo na umekuwa na upotoshaji mkubwa, je unawezaje kupanga mambo yako na kuchukua hatua zitakazokuwezesha kufanikiwa zaidi?

Kuna aina moja tu ya utabiri unaopaswa kuufanya mwenyewe na kuuishi kila siku. Utabiri huo ni huu kwamba kuna mabadiliko yanakuja, kwamba kila unachofanya sasa, kitaondoka na kupotea kabisa, hivyo kila mara uwe na maandalizi sahihi ya kuweza kukabiliana na mabadiliko hayo.

Kama umeajiriwa, kila siku ishi kwa kufikiri kesho unaweza kuamka na ajira yako isiwepo, kisha jiulize maisha yako yataendaje?

Kama unafanya biashara, kila siku ishi na utabiri kwamba kesho biashara hiyo haitakuwepo kabisa, halafu ona maisha yako yataendaje katika hali hiyo.

Utabiri huu unakufanya uwe na njia mbadala za kukabiliana na maisha yako ili chochote kinachotokea, isiwe mshangao kwako, badala yake iwe ni kitu ulichotegemea na kinachofuata ni kuchukua hatua ulizokuwa umepanga.

Kwa kuishi kwa namna hii, hutatikiswa na chochote, hutababaishwa na utabiri wa wengine na maisha yako yataendelea kwenda vizuri bila ya kutegemea nini kinaendelea.

Tuesday, September 29, 2020

USIWE MTU MWEPESI WA KUUDHIWA NA WATU , HATUA 09 ZA KUSHINDA DHIDI YA MAUDHI AU ADHA.

Habari mwanafalsafa, wadau  wangu  wa  MAISHA NA  MAFANIKIO  BLOG ,

Karibu katika mwendelezo wa safari ya kujifunza falsafa ya Ustoa. Falsafa hii imekuwa ni falsafa yenye msingi mzuri wa kuzalisha maisha matulivu na bora. Wiki hii nimejiwekea utaratibu wa kuendelea kujifunza falsafa hii ya ustoa kupitia mwandishi Dr. Chuck Chakrapani ambaye kaandika mfululizo wa kazi nyingi za kistoa kwa kukusanya nukuu na misemo ya wastoa kama Seneca, Epictetus na Marcus. Kitabu cha awali nilishirikisha kama mapendekezo katika moja ya mijadala ya kifalsafa kupitia substack kiitwacho “STOIC INSPIRATIONS”. Ni kitabu kizuri sana kukisoma

Mbali na hicho kitabu kuna kingine ambacho nimekipitia na ndio msingi wa kuandika makala hii unayoisoma. Kitabu hiki kinaitwa “UNSHAKABLE FREEDOM” kwa tafsiri iso rasmi inatafsiriwa kama “UHURU USOTIKISWA”. Uhuru ni hitaji mama la mtu yeyote yule sehemu yoyote Duniani. Uhuru unalindwa na uhuru wa maisha ni katika kujua mambo yapo makundi mawili; Mosi, ni yale yalo katika uwezo wako na pili yalo nje ya uwezo wako. Kitabu hiki kinagusa namna unavyoweza kuwa na uhuru usotikiswa. Kuudhiwa ni njia rahisi inayoweza kuharibu uhuru wetu katika maisha na usipokuwa na msingi wa falsafa utaishi kuamua ovyo.

Kuudhiwa kunaweza kukufanya ujisikie vibaya, upandwe na hasira na tatu unakupotezea utulivu wa akili na wakati mwingine mwili. Ila si vile ambavyo Marcus Aurelius anatushauri kuwa tuumie au tupandwe na hasira la hasha ila kutusaidia kuwa na utulivu pale tunapopitia hali ya kuudhiwa na watu wanaotuzunguka. Marcus Aurelius kaziweka kama hatua 09 za kufuata ili kwa lolote litakalojitokeza la kutuudhi basi tusipoteze utulivu wetu wa ndani.

Hatua hizi 09 zimegawanyika katika makundi mawili. Mosi ni hatua 04 za awali ambazo ni maswali 04 ya kujiuliza unapopitia hali ya kuudhiwa na pili ni hatua 05 za mwisho ambazo ni makumbusho/ tafakari kuhusu hali unayopitia ya kuudhiwa na mtu au matukio maishani.

Jiulize haya; [ Haya ni maswali ambayo Marcus Aurelius anatupa mwongozo wa kujiuliza pale ambapo tunakuwa kati kati ya hali za kuudhiwa au dakika chache ya tendo la kuudhiwa limejitokeza ]

1.       Usizidishe ukali wa tatizo- Je ni mahusiano gani ninayo na huyu mtu?

mfano mtu aliyekukosea ni ndugu yako wa karibu, mfanyakazi wako, mke au mume wako. Ukiondoa upande wa kosa ambalo limejitokeza la kukufanya uudhike ila upande mwingine mzuri huyo mtu ni ndugu yako, mfanyakazi wako, mke au mume wako. Unaporuhusu kuona mahusiano ya mtu aliyekutendea kosa unakuwa katika nafasi ya kupunguza ukubwa wa tatizo au tukio lilojitokeza.

2.       Jitahidi kufahamu nini msukumo wa mtu kufanya hivyo;

Mtu anapotenda kitu usifanye haraka kutoa hukumu maana unazibwa na kutokujua kwa kina, je nini ni msukumo wa jambo alotenda. Ukiangalia kwa kina unaweza kuona msukumo wa kutenda jambo hilo. Huenda ni msukumo wa chuki, ujinga, wivu au wakati mwingine kutokukusudia.

3.       Itafakari hali ilojitokeza

Usiwe na haraka ya kilichotokea kukipa tafsiri. Vuta ukimya na kuwa tayari kuona hali ilojitokeza imechangiwa na nini. Utaona pengine kuna nafasi ya ujinga kuwepo ndo maana tukio hilo limejitokeza. Usitoe mwitikio haraka tukio linapojitokeza.

4.       Hebu jiangalie hujawahi watendea wengine ulofanyiwa ?

Ni rahisi sana kuona watu wanaotuudhi wanamakosa zaidi na tukasahau hata sisi kuna watu wengi tunawaudhi kwa mambo yetu. Mimi na Wewe ni bado wanadamu na tuna mapungufu mengi kama wengine. Wanapokosea wengine tuwe waelewa kama ambavyo nasi tunavyotaka watu wengine watuelewe.

Jikumbushe haya; [Haya ni mambo ya kujikumbusha ambayo Marcus Aurelius anatupa mwongozo wa kujikumbusha pale ambapo tunakuwa kati kati ya hali za kuudhiwa au dakika chache ya tendo la kuudhiwa limejitokeza]

5.       Jua kuwa huna picha kamili ya jambo lilivyo

Wakati mwingine tunaona vitu kwa picha ndogo kuliko uhalisia ulivyo. Huwezi jua mtu aliyekukosea kwa wakati huo ni mambo gani anayoyapitia, au ni mambo yepi yalochangia yeye kufanya hivyo. Utaona mambo mengi ya watu walokosea ukichimba kwa kina kuna baadhi ya taarifa hatukuweza kuzijua kwanini hilo limejitokeza. Kila tukio linapotokea jua kuwa huna picha kamili ya mambo yalivyo. Usifanye haraka kutoa hukumu.

6.       Kumbuka Maisha ni mafupi

Miaka 200 toka sasa na kuifikiria ijayo hatutakuwepo; hii ikiwa ina maana wewe unayesoma hii makala miaka 200 ijayo sote hatutakuwepo. Hili linadhihirisha maisha yalivyo mafupi na hatupaswi kuhifadhi hasira au chuki na mtu yeyote yule. Kwa kujua hili unakazana kuishi katika kuchagua furaha kuliko kitu kingine chochote.

7.       Jua maoni ya mtu mwingine hayana nguvu dhidi yako endapo utapuuza au kuzuia kuyapa tafsiri

Kinachotuumiza sana siku zote kwa watu wanaotuudhi, wanaotutukana ni juu ya kuyapa tafsiri yale ambayo wamesema. Kuyapa tafsiri ni kuruhusu waloyasema yawe na nguvu dhidi yetu. Kwa kuona hilo Marcus anatushauri kutoyapa tafsiri au tukiweza tuyapuuze.

8.       Jua hasira ukiijenga itakuumiza zaidi ndani yako

Hasira inaunguza kama mtu aliye na kaa la moto katika kiganja. Ukiudhiwa na ukajenga hasira ndani yako, hasira inaanza kukuumiza wewe na pengine aliyekuudhi hana mpango wowote wa kukuwazia wewe. Hasira isiruhusiwe idumu ndani yako.

9.       Ukiweza tabasamu

Hakuna kitu kinachomfanya mtu aliyekuudhi au kukutukana pale unapotabasamu na wakati mwingine kucheka kwa kile alichokifanya. Inaonesha kwako kuwa alichokifanya hujakipa nguvu na pengine kukidharau. Lengo la mtu wakati mwingine kukutusi ni kutegemea kuona umekasirika, sasa unapokuwa unacheka unampa aumie zaidi kuona alichotegemea hakijafanikiwa.

Hizi hatua 09 ni mwongozo mzuri unaoweza kuutumia kila inapoitwa leo unapoendelea kukutana na watu mbalimbali. Maisha ya kila siku hatutaacha kukutana na watu ambao kwa namna moja wataleta adha dhidi yetu. Tutumie huu msingi kulinda utulivu wetu wa ndani maana tukumbushe maisha yetu ni mafupi.

 

KILA SIKU NI YA PEKEE SANA , ISHI KAMA LEO NA USIIPOTEZE.

Wanasema unaweza kulalamika huna viatu, ila ni mpaka siku utakayokutana na mtu asiye na miguu ndiyo utakumbuka kushukuru kwamba angalau wewe una miguu na hivyo viatu haviwi tatizo tena kwako.

Ni kawaida kwetu binadamu kuzoea vitu tulivyonavyo na kuvichukulia kawaida, kwa sababu tumekuwa tunaviona kila siku. Lakini vitu hivyo hivyo tunavyovichukulia pia, kuna wengine wanavitamani kweli ila hawawezi kuvipata.

Moja ya vitu hivyo ni hizi siku tunazokuwa nazo kila siku, tangu umezaliwa mpaka hapo ulipofika sasa, umekua unaanza na kumaliza siku zako na hivyo umeshazoea, asubuhi unaamka, unaenda na shughuli zako na siku inaisha, unalala na kuamka tena siku inayofuata.

Kwa kuwa umeshazoea sana siku zako, umekuwa unajiaminisha kabisa kwamba kesho ipo na huchelewi kuacha kufanya kitu leo kwa kujiambia utafanya kesho. Ni kitu gani kinakupa uhakika kiasi hicho?

Unapopata habari za misiba ya watu wa karibu, wale ambao uliwajua na walikuwa na mipango mikubwa ila wamefariki ghafla, huwa unapata mshtuko, unaona kweli maisha ni mafupi. Lakini haikuchukui siku nyingi unarudi kwenye mazoea yako, unazichukulia siku zako poa na kuahirisha mambo.

Tunawezaje kuondokana na hali hii ili tuweze kuzipa siku zetu uzito unaostahili na kuishi kwa ukamilifu?

Mwanafalsafa Seneca ana mengi ya kutueleza kwenye hili. Kwenye moja ya barua alizoandika kwa rafiki yake Lucilius akimweleza kuhusu wengi wanavyokihofia kifo, aligusia hili la kuishi kila siku kwa mazoea.

Seneca anasema wengi wamekuwa wakijiuliza maisha yao yataenda hivyo mpaka lini, kila siku kulala na kuamka, kuwa na njaa na kushiba, majira ya masika na kiangazi. Kwa kuyatazama maisha hivyo unaona kama ni mzunguko, hakuna kipya, kila kitu kinajirudia.

We slip into this condition, while philosophy itself pushes us on, and we say; "How long must I endure the same things? Shall I continue to wake and sleep, be hungry and be cloyed, shiver and perspire?  There is an end to nothing; all things are connected in a sort of circle; they flee and they are pursued.  – Seneca

Seneca anatutahadharisha kwamba tukiyaangalia maisha kwa mtazamo huo, tutayaona maisha ni maumivu yasiyo na mwisho, unaimaliza leo ukijua kesho inakwenda kuanza na kuisha kama leo. Majira ya masika yanaisha ukijua kiangazi kinakuja. Una njaa na kutafuta chakula kizuri kula, ila ukishashiba unajua kuna njaa itakuja tena. Kwa namna hii, maisha yanakuwa kama gereza la mateso, kusukuma siku usubiri kufa.

Lakini ipo namna nyingine ya kuyaangalia maisha kwa namna ambayo yatatunufaisha, mtazamo wa tofauti unaotusukuma kuyaishi maisha yetu kwa ukamilifu. Mtazamo huo ni kuyaona maisha kama zawadi, kila siku mpya unayoipata inakuwa kama nyongoza na hivyo unaitumia vizuri zaidi.

There are many who think that living is not painful, but superfluous. – Seneca.

Unapoiona siku mpya unayoianza kama nyongeza, unaitumia vizuri kwa sababu unajua huna uhakika kama utaiona siku nyingine kama hiyo. Huangalii jana ulifanya nini maana imeshapita, na wala huangalii kesho itakuwaje maana haipo, unachoangalia ni zawadi iliyo mbele yako.

Tukiweza kuziishi siku zetu kwa mtazamo huu, tutaacha kuona marudio yanayotuumiza na tutaanza kuona vitu vizuri vya kufanyia kazi.

Mahali pengine Seneca amewahi kutuasa jinsi ya kuziishi siku zetu kwa ukamilifu, mfano ni nukuu hizi;

“Anza kuishi mara moja na ichukulie kila siku mpya kama maisha tofauti.”

“Nitaendelea kuyaangalia maisha yangu na muhimu zaidi nitaitathmini kila siku yangu kwa kufunga vitabu vya maisha kila siku.”

Kama kauli za Seneca zinavyosisitiza, usichukulie poa hii siku uliyonayo leo, kuna wengine wangetamani sana kuwa nayo lakini haijawezekana. Iishi kwa upekee wake, ipangilie vizuri na fanya mambo ambayo mwisho wa siku ukiyaangalia unajiambia kweli umeiishi siku hii.

Kila unapoimaliza siku yako, jifanyie tathmini, pitia kila ulichofanya tangu kuamka mpaka unaporudi kulala na kisha jiulize maswali haya matatu;

Moja; Ni yapi mazuri nimefanya leo na ambayo nitaendelea kuyafanya nikipata zawadi ya siku nyingine?

Mbili; Ni yapi mabaya nimefanya leo ambayo sitarudia tena kufanya kama nitazawadiwa siku nyingine?

Tatu; Yapi ambayo sijayafanya kwa ubora unaostahili na ambayo nitayaboresha zaidi nitakapopata zawadi ya siku nyingine?

Ukijiuliza maswali hayo matatu kila siku na kujipa majibu sahihi, kisha kuyafanyia kazi, maisha yako yatakuwa bora, hutazichoka siku zako, hutaahirisha chochote na utayazuia matatizo mengi kabla hayajawa makubwa.

Wenye hekima wanajua, maisha siyo mateso bali zawadi, ichukulie hivyo na utakuwa na maisha bora na tulivu.

 

Saturday, September 5, 2020

JINSI YA KUKUZA BIASHARA KUTOKA WATU 10 MPAKA WATU 10,000 KATIKA KAMPUNI.

Jukumu La Mtendaji Mkuu (CEO)

Kwenye vitabu vingi vya biashara, majukumu ya CEO yamekuwa yanaainishwa kuwa;

1. Kuweka mwelekeo na mkakati wa kampuni na kuuwasilisha kwa wafanyakazi, wateja na wawekezaji.

2. Kuajiri, kufundisha na kutengeneza utamaduni sahihi kwenye kampuni.

3. Kukusanya mtaji na kuugawa kwa usahihi kwenye shughuli za kampuni.

4. Kuwa mwanasaikolojia mkuu wa kampuni, kwa kuwapa wengine moyo pale mambo yanapokuwa magumu.

Kutafuta, Kuajiri Na Kusimamia Vipaji.

Ukuaji na mafanikio ya kampuni unategemea sana watu unaowaajiri kwenye kampuni yako. Ni muhimu uajiri watu sahihi, wenye uwezo wa kutekeleza majukumu yao na hamasa ya kufanya hivyo.

Kujenga Timu Ya Watendaji.

Wakurugenzi wa vitengo mbalimbali vya biashara yako ndiyo watendaji kwenye kampuni. Hawa wanahusika kusimamia vitengo vyao ili viweze kuisaidia kampuni kufikia maono yake. Kama mkurugenzi mkuu, utaweza kukuza kampuni yako unapokuwa na timu nzuri ya watendaji.

Kujenga timu bora ya watendaji ni zoezi gumu kwa waanzilishi wachanga, kwa sababu mwanzoni walikuwa wanafanya kila kitu peke yao. Lakini sasa kampuni inakua kwa kasi, hawawezi tena kufanya hivyo. Na hapo bado wengi wanakuwa hawajawa tayari kugatua majukumu yao.

Lakini inafika hatua ambapo kama mwanzilishi huwezi tena kusimamia kila kitu peke yako, kwa sababu majukumu yanayotaka muda wako ni mengi kuliko muda ulionao. Hivyo unakuwa huna budi kujenga timu ya watendaji.

Changamoto kubwa kwenye kuajiri watendaji ni kwamba unapaswa kutafuta watu wenye uzoefu zaidi yako, kitu ambacho siyo rahisi. Lakini unapofanikiwa kuajiri mtendaji wa kwanza vizuri, wanaofuata haitakuwa changamoto kwenye kuwaajiri.

Unapokuwa na watendaji wazuri, mambo mengi kwenye kampuni yanaenda bila ya wewe mwenyewe kuhusika moja kwa moja. Unaona kama ni miujiza maana mambo yaliyokuwa yanakusumbua awali hayakusumbui tena kwa sababu wapo wanaoyafanyia kazi.

Lakini pia kuna wakati makosa yanafanyika kwenye uajiri na mtendaji anayeajiriwa anakuwa siyo sahihi. Hapo msongo unakuwa mara mbili, kwa majukumu yanayokutegemea na mtendaji asiyefaa. Mtendaji wa aina hiyo huwa chanzo cha wafanyakazi wazuri kuikimbia kampuni yako.

Muundo Wa Kampuni Na Ukuaji Wa Kasi.

Muundo wa kampuni kwenye kipindi cha ukuaji wa kasi ni jambo lenye changamoto kwa waanzilishi wasio na uzoefu. Hii ni kwa sababu inakuwa vigumu kuwa na muundo mmoja, kadiri kampuni inavyokua, ndiyo mabadiliko yanayohitajika kwenye muundo.

Masoko Na Mahusiano Ya Umma.

Masoko na mahusiano ya umma (marketing and PR) ni eneo muhimu kwenye ukuaji wa kampuni yoyote ile. Ila kwa kampuni zilizo kwenye hatua ya ukuaji wa kasi, eneo hilo ni muhimu na linapaswa kufanya kwa usahihi.

Mchango wa masoko na mahusiano ya umma ni kujenga jina la kampuni (brand), kutengeneza taswira nzuri kwa umma, kupata kutunza wateja wa kampuni.

Kwenye uchambuzi kamili utajifunza njia bora za kufanya masoko na mahusiano kwa umma ili kampuni iweze kunufaika.

Usimamizi Wa Bidhaa.

Usimamizi wa bidhaa ni eneo muhimu wakati wa ukuaji wa kasi wa kampuni. Hii ni kwa sababu uhitaji unakuwa mkubwa na hivyo kusipokuwa na usimamizi mzuri, bidhaa inaweza isiwe bora au mahitaji ya wateja yasifikiwe.

Usimamizi mzuri wa bidhaa unaiwezesha kampuni kuweka maono makubwa ya bidhaa, mipango ya kufikia maono hayo, mikakati ya kufanyia kazi na hatua za kuchukua.

Usimamizi mbaya wa bidhaa unakuwa fujo kwa kampuni nzima kwani hakuna maono, na mambo hayafanyiki kwa wakati.

Ili kuwa na usimamizi mzuri wa bidhaa, unapaswa kuwa na kitengo mahususi kwa ajili ya bidhaa, kinachosimamiwa na meneja wa bidhaa ambaye anakuwa na ujuzi wa juu kwenye bidhaa husika. Pia unapaswa kutengeneza mchakato sahihi unaofuatwa kwenye kuandaa bidhaa husika.

Fedha Na Uthaminishaji.

Fedha na uthaminishaji ni eneo muhimu kwenye ukuaji wa kasi wa kampuni. Katika kipindi cha ukuaji wa kasi, japo kampuni inaweza kuwa na wateja wengi, lakini inaweza isiwe inazalisha faida. Hivyo kama CEO utahitaji kupata fedha za kuendelea kuendesha kampuni. Huu ndiyo wakati utakaohitajika kuithaminisha kampuni na kisha kukaribisha wawekezaji kuwekeza mitaji yao. Pia unaweza kuiuza kampuni au kuipeleka kwa umma.

Kuungana Na Kununua.

Njia nyingine ya kukuza zaidi kampuni yako ni kuungana na kampuni nyingine ambayo ni kubwa zaidi au kununua kampuni ambayo ni ndogo.

Kuungana na kununua (Mergers & acquisitions) kunaiwezesha kampuni kupata bidhaa, teknolojia, timu na hata kuondoa ushindani kwenye soko.

 

Monday, August 31, 2020

NGUVU YAKO YA UBUNIFU ILIYOKO NDANI YAKO NDIYO HAZINA YAKO YA PESA ULIYONAYO,

Pesa ni kitu gani mpaka karibu kila mtu anaitafuta? Kama pesa inatafutwa na kila mtu, lazima kujiuliza wapi hasa inapatikana. Je? Ni kweli wote tunafahamu sehemu au mahali inapopatikana? Kama mahali pesa ilipo hapajulikani tutawezaje kuipata? Maswali yote haya yanahitaji majibu kwanza kutoka kwa kila mmoja wetu ambaye anazitaka pesa kwa dhati.

Maswali yote haya pia ndiyo yanatoatafsiri halisi ya kwanini kila mmoja anakwambia kuwa anahangaika kutafuta pesa, wengine wanakwambia siku hizi kuwa wanapambana. Yote haya yanaonyesha dhahiri kuwa kuna vita ndani kwa ndani katika fikra, akili na nafsi zetu juu ya wapi pesa itapatikana. 

Uzoefu unaonyesha kwamba mahali pesa ilipo bado hapajulikani kwa waliowengi. Kutokana na hali hii, wengi suala la kutafuta pesa linabaki kuwa suala la kubahatisha na kubangaiza. Kutafuta pesa kwa kubangaiza kumekuwa ndiyo hali ya maisha ya kila siku kwa waliowengi. 

Wakati ukiendelea kutafuta majibu ya maswali hapo juu, ni vizuri kutambua mambo makuu muhimu juu ya pesa; Moja ni kwamba, pesa halisi inapatikana ndani yetu; Pili, pesa yote unayoiona ni ISHARA tu ya kitu fulani kilichofanyika. 

Pesa inakuwaje ISHARA na kupatikana ndani yako? 

Nguvu ya hisia ikichanganyika na matamanio ndani ya akili, inaachia nguvu ya ubunifu wa vitu na huduma mbalimbali. 

Baada ya hapo akili yako inakusukuma ili ukamilishe kazi ya kubadilisha huo ubunifu uliopo katika hali ya wazo kuwa vitu halisi ambavyo mwisho wake hukuletea pesa. 

Ndiyo maana tunasema PESA ni ishara ya nguvu ya ubunifu ulionao katika hali ya kuonekana kwa macho. Kwahiyo, pesa tunatembea nazo mawazoni mwetu, tunalala nazo usingizini, tunakuwa nazo kila mahali tunapokua. 

Kazi tunayo moja tu nayo ni kuzitoa huko ndani yetu. Ili tuweze kuzitoa pesa ndani yetu tunahitaji kuendelea kujifunza namna bora ya kuzitoa nje, maana zikikaa tutakufanazo. 

Binadamu ukishapata kile unachohitaji na ukawa na uhuru wa kuchagua upate nini na uache nini ndiyo unapata kuishi maisha ya furaha na kuridhika pia. 

Unachotakiwa kufahamu ni kwamba wewe umejaliwa nguvu ya ubunifu ndani yako na hiyo ndiyo hazina ya pesa uliyonayo. Kwahiyo, unatakiwa kuwa mtu mwenye matumaini na kuhakikisha hofu na mashaka havina nafasi kwako. 

Habari njema ni kwamba leo hii kuna idadi ya watu wengi sana ambao tunakaribia kuwa watu bilioni tisa hivi. 

Watu wote hawa wako tayari kulipa pesa ili kukidhi mahitaji yao. Unachotakiwa kufanya kama wewe ni kukidhi mahitaji ya asilimia ndogo sana ya watu wote walioko hapa duniani. 

Kwahiyo, ukiona umepata pesa ujue kuwa hiyo ni ishara inayoonyesha nguvu ya ubunifu ndani yako. 

Wengi wanaofikiri hawana pesa siyo kwamba hawana nguvu ya ubunifu tunayosema BALI ni kwamba hawajachukua muda wao kutambua kuwa nguvu hiyo ipo lakini pia hawajachukua hatua ya kuibadilisha nguvu hiyo kuwa vitu halisi vyenye thamani na ambavyo vinaweza kuuzika kwa watu wengine tukapata pesa. 

Kila wakati tuzame zaidi katika kutafiti na kufuatilia hitaji hasa la jamii tunayoweza kuifikia na katika hitaji lao hilo tuone pesa kwa macho yetu ya rohoni. 

Tukishaona kwa macho ya ndani tuanze kufanyakazi ya kuitoa ndani kwa maana ya kufanyakazi kwa vitendo ili kukidhi hitaji lililopo kwenye jamii husika. 

Kazi ya nguvu ya ubunifu ikishakamilika, watu wenye uhitaji wataleta pesa kwako na utaanza kuikusanya kwenye kapu, hapo ndio itaanza kuonekana kwa watu wengine. 

Baadae, utaanza kusikia watu mtaani wakisema fulani amezipata pesa, sijui amezitoa wapi wakati wao ndio wamezileta kwako….hivyo ndivyo maisha yanavyokwenda. 

Mpendwa msomaji wa makala hii litafakari sana suala hili la kuitoa nje pesa iliyoko ndani kwani ni rahisi kuutokomeza umaskini moja kwa moja. 

Najua unapenda kufuata njia za mkato lakini ukweli ni kwamba ukae ukijua kuwa pesa inayopatikana kwa njia za mkato inadumu kwako muda mfupi sana na wakati mwingine njia inayotumika siyo rahisi kuitumia wakati mwingine. 

Kwahiyo, wakati ukiendelea na njia zako za mkato anza taratibu kufuata kidogo kidogo njia hii ya nguvu ya ubunifu ili kutengeneza mfereji wa pesa zitiririkazo kuja kwako bila kikomo.

 

KUJIJENGEA NIDHAMU NA UDHIBITI WA MIPANGO UNAYOJIWEKEA.

Kupanga ni rahisi, ila kuchukua hatua kwenye kupanga ndipo wengi wanapokwama. Ni rahisi sana kupanga halafu wakati wa kufanya unapofika unaahirisha.

Hata haya uliyojifunza hapa, utafurahia kweli na kujiambia utayafanya, lakini inapofika wakati wa utekelezaji, unaona huwezi kuanza sasa, au unahitaji maandalizi zaidi na sababu nyingine lukuki.

Iko hivi rafiki, mazoea ni rahisi, kufanya kitu kipya kunaumiza, unakimbia kufanya kwa sababu hutaki maumivu.

Hakuna namna utaweza kufanya makubwa wewe peke yako, lazima utaishia kuahirisha na kujiambia haujawa tayari.

Hivyo ili kujijengea nidhamu na udhibiti kwenye kutekeleza mipango yako, unahitaji nguvu ya nje. Unahitaji mtu ambaye atakusimamia kwa karibu, ambayo hatakuachia kirahisi pale unapojipa sababu.

Unaweza kufanya hivyo kwa njia kuu tatu;

Njia ya kwanza ni kujiunga na kikundi cha watu wanaofanya kitu fulani, ukiwa ndani ya kikundi unasukumwa zaidi kufanya kwa sababu hutaki kuwaangusha wengine.

Njia ya pili ni kuwatumia watu wako wa karibu kukusukuma kufanya, hapo unaweza kumwambia mtu kwamba utafanya kitu fulani, na usipofanya basi utapaswa kumlipa kiasi fulani. Unapojua kwamba usipofanya utalipa gharama basi utapata msukumo wa kufanya.

Njia ya tatu ni kuwa na kocha ambaye anakusimamia kwa karibu. Kwa kuwa na kocha, mnaweka mipango na hatua za kuchukua, kisha kocha anakufuatilia kwa karibu kwenye utekelezaji na kuendelea kukupa mwongozo zaidi.

Tumia moja ya njia hizo au zote kwa pamoja kwenye yale unayopanga kufanya na utapata msukumo mkubwa wa kufanya kila unachopanga kufanya.


Kujijengea nidhamu na udhibiti ni hitaji muhimu sana kwa mafanikio yako, huwezi kufanikiwa kama unayaendesha maisha yako kikawaida. Lazima ujue pia kwamba kujijengea nidhamu na udhibiti kutakuja na maumivu, utakosa baadhi ya uliyoyazoea, lakini utapata yaliyo bora kabisa.

Fanyia kazi haya uliyoifunza hapa na hutaweza kubaki pale ulipo sasa.

Nakutakia utekelezaji mwema wa yale ambayo umejifunza,


 

KUJIJENGEA NIDHAMU NA UDHIBITI WA MUDA.

Tambua muda ndiyo rasilimali yenye uhaba, ambayo ukishapoteza hairudi tena. Katika kujijengea nidhamu na udhibiti wa muda, fanya yafuatayo;

1. Chukua kalamu na karatasi, gawa karatasi yako katika pande mbili, A na B.

2. Upande A orodhesha mambo yote ambayo umefanya kwenye wiki moja iliyopita, kila ulichofanya kiorodheshe, uliingia mtandaoni, orodhesha, uliangalia mpira, weka, ulibishana na watu weka.

3. Upande B orodhesha malengo na mipango uliyonayo, kile unachotaka kufikia ndani ya mwaka mmoja, miaka 5, 10 na mpaka 20 ijayo.

4. Linganisha orodha A na B, piga mstari kile ulichofanya upande A ambacho kinakusaidia kufikia upande B.

5. Baada ya hapo, chukua yale ya upande A ambayo yana mchango kwenye upande B na hayo tu ndiyo utakayoanza kuyafanya kuanzia sasa. Yale mengine uliyokuwa unafanya na hayana mchango kwenye kufikia malengo na mipango yako, achana nayo mara moja.

Yaani jiambie tu kuanzia leo sifanyi tena haya, na acha mara moja. Vitu kama kufuatilia habari, kubishana, mitandao ya kijamii na mengine utapaswa kuachana nayo mara moja.

Manufaa ya zoezi hili ni wewe kupata muda mwingi zaidi wa kufanya yale ambayo ni muhimu zaidi kwako. Na hapo hutakuwa tena na tatizo la muda.


 

Sunday, August 30, 2020

JINSI YA KUJIJENGEA NIDHAMU NA UDHIBITI WA FEDHA.

Kila pesa inayopita kwenye mikono yako ni mbegu, ambayo ukiitumia vizuri itakuwa na manufaa kwako. Lakini wengi wamekuwa hawana nidhamu na udhibiti mzuri wa fedha zao. Hapa kuna hatua za kuchukua kwenye kujijengea nidhamu na udhibiti wa fedha zako.

1. Nenda kwenye benki unayotumia sasa na fungua akaunti maalumu ambayo unaweza kuweka fedha lakini kutoa siyo rahisi au kuna ukomo. Karibu kila benki ina akaunti ya aina hii.

2. Omba huduma ya fedha kuhamishwa kwenye akaunti yako ya sasa ambayo ndiyo inaingiza kipato chako kikuu, iwe ni mshahara au fedha unazoweka akiba. Kwamba kila mwezi kuna kiasi watakikata kwenye akaunti yako ya akiba kwenda kwenye akaunti yako maalumu.

3. Weka akiba kwenye akaunti hiyo maalumu kila mwezi, bila kuigusa kwa angalau mwaka mmoja. Jiwekee kiwango cha kipato chako ambacho kitaenda kwenye akaunti yako, unaweza kuanza na asilimia 10 au nyingine itakayokufaa wewe.

4. Hakikisha kipato chako kinakatwa kabla ya matumizi, kama unafanya shughuli zako binafsi basi unapolipwa, kabla hujaanza kutumia weka kwanza pembeni kiasi cha akiba na kiweke kwenye akaunti hiyo.

5. Pesa iliyo kwenye akaunti hiyo maalumu isahau kabisa, chukulia kama ulinunua kitu fulani na hivyo usiiweke kwenye mahesabu. Ni mpaka mwaka uishe ndiyo utarudi kwenye fedha hiyo na kuchagua ufanye nayo kitu gani cha kuzalisha zaidi.

Zoezi hili linakulazimisha kujiwekea akiba na baadaye kuiwekeza, kitu ambacho kitakuweka vizuri kwenye eneo la fedha.



 

Saturday, August 22, 2020

KWANINI UNAPITIA CHANGAMOTO NYINGI ? JIFUNZE SABABU TANO ( 05 ) NA JINSI YA KUKABILIANA NA CHANGAMOTO HIZO.

Kitu pekee tunachojifunza kwenye historia ni kwamba hakuna tunachojifunza kwenye historia, hiyo ni kauli aliyowahi kuitoa mwanafalsafa Hegel.

Ni kauli nzito na inayopaswa kutufundisha mengi, lakini kama Hegel alivyoeleza, haitufundishi chochote.

Iko hivi rafiki, hakuna kitu kipya kinachotokea hapa duniani kwa sasa. Kila kinachotokea sasa kimewahi kutokea huko nyuma, kwa sasa kimetokea tu kwa namna tofauti, labda kutokana na teknolojia kuwa ya juu.

Kuanzia matatizo yanayoikumba dunia, nchi na hata mtu mmoja mmoja, yote yamewahi kutokea tena huko nyuma. Maisha tunayoishi sasa ni marudio tu.


Lakini cha kushangaza, tunarudia makosa yale yale ambayo waliotutangulia waliyafanya walipokuwa wanapitia hali kama tunazopitia sasa. Kama tungechukua muda kujifunza kupitia waliotutangulia, tungepunguza makosa ambayo tunafanya.


Lakini hatufanyi hivyo, kwa sababu ambazo nakwenda kukushirikisha hapa. Kwa kila sababu nitakushirikisha hatua ya kuchukua ili maisha yako yaweze kuwa bora na uweza kukabiliana na kila changamoto unayopitia sasa.

( 01 ). WATU   KUACHA  KUSOMA  VITABU.

Uandishi ndiyo uvumbuzi mkubwa kuwahi kutokea duniani, alinukuliwa Abraham Lincolin. Hebu fikiria, leo hii unaweza kusoma vitabu vilivyoandikwa zaidi ya miaka elfu 2 iliyopita. Ni kwa sababu uandishi umeruhusu maarifa hayo kuweza kutunzwa na kurithishwa vizazi na vizazi.


Uzuri ni kwamba, kila unachopitia sasa, kuna mtu alishapitia miaka mingi iliyopita na akaandika kitabu kuhusu uzoefu wake kwenye hilo alilopitia. Kama mtu alipambana na kitu kwa miaka kumi na kukiandika kitabu, unaweza kukisoma kwa siku chache na ukaokoa kupoteza miaka 10 kwa kurudia makosa waliyofanya wengine.


Lakini cha kusikitisha ni kwamba watu wameamua kuacha kusoma vitabu. Wana kila sababu kwa nini hawasomi vitabu, lakini hakuna sababu yenye mashiko. Ni sawa na kukutana na mtu ambaye yuko mbio na unajaribu kumsimamisha anakuambia anachelewa. Ukimuuliza kwani unawahi wapi, hajui, lakini yuko kasi.

Ondoka mara moja kwenye tabia hiyo ya kutokusoma vitabu, chagua eneo unalotaka kubobea, amua wapi unataka kufika, kisha tafuta vitabu bora kwenye hayo na visome.


Ukitenga saa moja kila siku ya kusoma, au ukaweka utaratibu wa kusoma kurasa 10 za kitabu kila siku, kila mwezi utamaliza angalau kitabu kimoja na kwa mwaka angalau vitabu kumi.


Kama utatafakari yale uliyojifunza kwa kina, kisha ukachukua hatua kwenye maisha yako, huwezi kubaki pale ulipo sasa. Lazima utapiga hatua kubwa, utaepuka kurudia makosa ya wengine na kujifunza njia bora zaidi za kufanya unachofanya. 

( 02 ). WATU  KUPENDA    KUSOMA   VITU  VIFUPI.

Vitabu ni njia moja ya kujifunza, lakini pia zipo njia nyingine za kujifunza, kama kupitia makala, tafiti, ripoti mbalimbali na hata insha.


Uzuri ni kwamba, tunaishi kwenye zama ambazo mtandao wa intaneti unarahisisha kusoma maarifa hayo mbalimbali, tena bure kabisa.


Lakini cha kushangaza, watu hawapendi kusoma vitu virefu. Makala kama hii, wengi walioanza kusoma wameishia aya ya tatu, na wengine wanapita wakiangalia vichwa au maneno yaliyokolezwa tu.

Watu hawana tena umakini na utulivu wa kuweza kutenda dakika kumi za kusoma kitu kwa kina na kuondoka na maarifa ya kwenda kufanya kazi.

Usumbufu ni mwingi, kila mtu anapitia vitu juu juu, kinachotokea ni maarifa mazuri yanaelea huko mtandaoni huku wanaoyahitaji wakiteseka. Ni sawa na mtu ambaye anaogelea kwenye ziwa, lakini anakufa kwa kiu.

Kuondokana na hili, kwenye siku yako tenga muda ambao utasoma vitu kwa kina, ni bora usome vitu vichache kwa kina kuliko usome vitu vingi kwa juu juu. Kwa kila unachosoma, usikiache mpaka umeorodhesha nini umejifunza na namna gani unaenda kuboresha maisha yako.

Chagua mitandao au waandishi ambao utakuwa unajifunza kwao na weka umakini wako wakati unasoma kitu chochote kile. Usiwe na haraka wala kukimbilia popote, hakuna mashindano wala tuzo za aliyesoma vitu vingi zaidi. Tuzo pekee ni maisha yako kuwa bora, hivyo kazana na hilo.

( 03 ).  WATU  KUTUMIA   MUDA  MWINGI  KWENYE   MITANDAO  YA  KIJAMII.

Mitandao ya kijamii imepata umaarufu mkubwa na karibu kila mtu anaitumia kwa sasa. Mitandao hii imetuhadaa kwamba inatupa nafasi ya kuwasiliana na wengine na kutengeneza marafiki wengi.

Lakini ukweli wa mitandao huu umekuwa unafichwa. Mitandao hii imetengeneza mabilioni ya pesa, kwa kukuuza wewe. Angalia, hii mitandao haina bidhaa yoyote inayouza, na wewe unaitumia bure. Unajua inapataje pesa? Kwa kuuza umakini wako kwa watu wanaotaka kutangaza biashara zao mbalimbali.

Mitandao hii pia imechangia watu kukosa muda na umakini wa kusoma vitabu na mafunzo mengine mazuri.


Mtandao wa instagram umepata umaarufu mkubwa kwa sababu huhitaji kufikiria chochote, wewe piga picha yako na weka, halafu subiri wa kukusifia na kukupa likes.

Mtandao wa twitter umepata umaarufu mkubwa kwa sababu ukomo wa unayoweza kuandika, ambao ni herufi 280 tu, huwezi kuandika zaidi ya hapo. Hivyo ni vitu vifupi vifupi tu vinaandikwa huko, na kwa sababu watu hawataki vitu virefu, wanafurahia sana mtandao huo.

Rafiki, kama hutumii mitandao hiyo ya kijamii kibiashara, yaani kama huingizi fedha moja kwa moja kutoka kwenye mitandao hiyo, basi acha kuitumia mara moja. Hakuna manufaa yoyote unayoyapata kwenye mitandao hiyo, zaidi ya usumbufu, msongo na kupunguza umakini wako.

Jitoe kabisa kwenye mitandao yote ya kijamii, na ghafla utaona jinsi ulivyo na muda mwingi wa kufanya yale muhimu kwako. Nilichukua hatua hii mwaka 2018 baada ya kukaa kwenye mitandao hiyo kwa miaka 9 na sijawahi kujutia maamuzi hayo.

(04 ). WATU  KUISHI  KWA   MAZOEA  NA  KUFUATA  MKUMBO.

Hivi umewahi kukaa chini na kujiuliza kwa nini unafanya kila unalofanya? Umefanya kazi au biashara uliyonayo sasa kwa muda, lakini je unajua kwa nini uliingia kwenye kazi au biashara hiyo? Unajua wapi unapotaka kufika?


Hata mengine unayofanya kwenye maisha, labda umechukua mkopo, umejenga nyumba, umeoa au kuolewa, umewahi kujiuliza kwa nini ulifanya maamuzi hayo?


Kwa bahati mbaya sana, maamuzi mengi ambayo watu wanafanya ni kwa mazoea au kufuata mkumbo. Mtu anaambiwa wenzako wameshaoa au kuolewa, na yeye anafanya hivyo. Mtu anaona wenzake wanachukua mkopo na yeye anachukua. 

Maisha ya aina hii yamekuwa hayakosi changamoto, kwa sababu mtu anahangaika na mengi lakini hayana maana kwake. Hivyo mwisho wa siku anayaona maisha yake yakiwa tupu, anaweza kuwa na kila anachoambiwa anapaswa kuwa nacho, lakini hana furaha.

Huwezi kuwa na furaha kwenye maisha kama hujayaishi maisha yako, kama hujajijua wewe mwenyewe na kuishi kwa uhalisia wako. Unaweza kupata kila ambacho wengine wanacho, tena wengine wakakuonea wivu kwa nafasi uliyonayo, lakini ndani yako ukajiona ni mtupu.

Acha sasa kuishi maisha ya mazoea au kufuata mkumbo, kwa kila jambo unalofanya, jua kwa nini unafanya. Kwanza kabisa jitambue wewe mwenyewe, jua uimara na udhaifu wako, jua wapi unataka kufika na maisha yako. Kisha hoji kila unalotaka kufanya linaendanaje na wewe na linakufikishaje kule unakotaka kufika.


Usiogope kufanya kitu peke yako, usiogope kupingwa, kukosolewa na kuchukiwa na wengine. Wewe pekee ndiye unayejijua kuliko wengine wanavyokujua, chagua kuyaishi maisha yako na siyo kuwafurahisha wengine.


( 05 ). KUTEGEMEA  FURAHA  KUTOKA  KWNEYE  VITU  VYA   NJE.

Kama unajiambia ukishafika hatua fulani au kuwa na kitu fulani ndiyo utakuwa na furaha basi jua unatembea na laana. Hiyo ni kwa sababu hakuna furaha ya kudumu utakayoipata kwa kitu chochote cha nje yako. Unaweza kupata raha ya muda mfupi, lakini siyo furaha ya kudumu.

Kutegemea furaha kutoka kwenye vitu vya nje imekuwa ndiyo chanzo cha matatizo ambayo wengi wanakutana nayo kwenye maisha. Ulevi ambao wengi wanaangukia ni kutafuta furaha za nje na za haraka, kitu ambacho kimekuwa hakidumu.

Tambua kwamba furaha ya kweli na idumuyo inaanzia ndani yako, inaanza na wewe mwenyewe na haitegemei chochote cha nje. Kama huna furaha kabla hujapata unachotaka, hata ukikipata huwezi kuwa na furaha.

Mafanikio hayaleti furaha, bali furaha ndiyo inaleta mafanikio. Hivyo anza na furaha, jitambue, jua wapi unakwenda, jipende, penda unachofanya na kila siku piga hatua kuwa bora zaidi. Kwa njia hizi, utakuwa na furaha bila kujali uko kwenye ngazi ipi.

Rafiki yangu mpendwa, hizo ndizo sababu kubwa tano za changamoto nyingi tunazopitia kwenye maisha ya zama hizi. Tukiweza kutatua hizi kwa kuzingatia yale tuliyojifunza, hakuna kitakachokukwamisha, utakuwa na maisha tulivu, yenye furaha na mafanikio makubwa.

 

Rafiki, kama ungependa kuendelea kupokea makala na mafunzo mengine mazuri 

ENDELEA  KUSOMA   HAPA " MAISHA   NA  MAFANIKIO( LIFE  AND  YOU )  BLOG  " KARIBU   PIA    UJIUNGE  KATIKA   " DARASA  LETU--ONLINE  " KWA   KUWA   MWANACHAMA.

Makala Hii Imeandikwa Na MWL.  JAPHET   MASATU , Ambaye Ni MWALIMU   KITAALUMA , KOCHA   WA  MAISHA   NA   MAFANIKIO , MSHAURI , MWANDISHI NA MJASIRIAMALI,  PUBLIC  SPEAKER


Tuwasiliane  kwa  WhatsApp + 255 716924136   /    + 255 755  400128  / + 255 688361539

 

Wednesday, August 19, 2020

WATEJA WA ZAMANI NI LULU ?? WEKA KUMBUKUMBU ZAO . !!!

 Nguzo muhimu katika biashara yoyote duniani ni wateja. Ninaweza kusema kwamba biashara inafanikishwa na watu wawili; yaani mfanyabiashara ambaye ndiye anauza bidhaa au huduma na wa pili ni mteja ambaye ananunua bidhaa. Kama unafanya biashara ambayo wateja wapo, tunasema biashara hiyo inalipa lakini kama wateja hawapo tunasema biashara yako hailipi. Kwahiyo, kuendelea kwa biashara yako ni
wateja. Kwenye biashara kuna aina mbili za wateja, ambao ni wateja wa zamani na wateja wapya. 

Kwa jinsi hali ilivyo huku mitaani kwetu, ni kwamba wafanyabiashara wengi wanajali zaidi wateja mpya. 

Mteja mpya anaonyeshwa kila aina ya upendo kiasi cha kumkatishatamaa mteja wa zamani endapo ikitokea wote wawili wakawepo pamoja eneo la biashara. 

Hali hii ya kutengwa kama mteja wa zamani imenitokea mara nyingi na kunifanya niamini kwamba kadiri unavyozidi kununua bidhaa mara nyingi kutoka kwa mfanyabiashara fulani ndivyo anavyoacha kukujali. 

Kiashiria mojawapo ni wakati mwingine mteja wa zamani anapouziwa vitu kwa bei tofauti na Yule mteja mpya. Yaani ni ajabu wateja wapya wanapunguziwa wakati wale wa zamani wanaonunua vitu mara kwa mara wanapandishiwa bei. 

Wakati mwingine baadhi ya wafanyabiashara wanakupunja wewe mteja wao wa zamani kupitia vipimo hasa kwa bidhaa kama sukari, nyama, mchele n.k. 

Ukweli ni kwamba, mteja wa zamani ni LULU. Unapashwa kumtengenezea mazingira rafiki kwa kuhakikisha unampatia unafuu kadiri mtakavyozidi kukaa pamoja kibiashara. Ikiwa utazidi kumjali na yeye atazidi kuwa na sababu ya kuendelea kuwa mteja wako daima. 

Kwanini mteja wa zamani? 

Ukizidi kuwajali wateja wa zamani inakusaidia wewe kupata wateja wapya kwa gharama kidogo sana; kuliko ambavyo ungewatafuta wewe mwenyewe moja kwa moja. 

Mteja wa zamani ni mtaji mkubwa” endapo utakaanaye vizuri, na hii nikutokana na ukweli kwamba, anaouwezo wa kukuletea wateja wapya kila mara. 

Mteja wa zamani ni rahisi kumtunza kuliko kupata mteja mpya. 

Sisi wataalamu wa masuala ya masoko tunasema kuwa gharama za kumpata mteja mpya ni mara saba zaidi ya gharama za kukaa na mteja wako wa zamani. 

Mteja wa zamani tayari anakufahamu kwahiyo, akiambiwa juu ya mali mpya hana mud sana wa kuhoji kwasababu tayari anakuamini na hivyo ataweza kuitikia haraka. 

Uzoefu wangu unaonyesha kuwa inachukua muda na nguvu nyingi kumshawishi mteja mpya kukubali bidhaa yako kuliko wa mteja zamani. 

Tayari wewe unafahamu vizuri tabia na mahitaji ya wateja wako wa zamani, kwahiyo inakuwa rahisi kujua namna nzuri ya kutengeneza mkakati wa kuongeza mauzo yako bila kusahau kuwapa kilicho bora. 

Nifanye nini kukuza uhusiano na wateja wangu wa zamani? 
Unachotakiwa kufanya ni kujifunza jinsi ya kujenga na kuimalisha mahusiano na watu hasa wale wanaokuja kununua bidhaa na huduma mbalimbali kutoka kwako. 

Ni muhimu sana kujenga mahusiano ya karibu na kila mteja mpya wakiwemo wale walioletwa na mteja wako wa zamani, lakini jenga uhusiano na kila mmoja peke yake siyo kama kikundi. 

Katika mchakato wa kujenga uhusiano na wateja fanya yafuatayo; 

Badili tabia yako juu ya mahusiano: Tabia yako ya mahusiano na watu wengine ni muhimu sana. Usidhani suala zima la kujali watu litatokea tu siku moja, lazima uzame ndani kwenye tabia yako kwanza. 

Andaa orodha ya majina na namba za simu: Jiwekee utaratibu wa kuwa na orodha ya majina pamoja na namba zao za simu. Ukiwa na orodha ya majina ni rahisi kuwa na kumbukumbu ya nani kanunua nini na kiasi gani mwaka mwezi au mwaka huu. 

Inapofika sikukuu maalum kama Krismas hawa ndio wa kuwapa kipaumbele unapotuma salam za pongezi. Sijui wewe kama uliwahi kumtumia mtu heri ya krismas kwasababu tu ni mteja wako mzuri..kama hujafanya hivyo basi jitafakari na uchukue hatua. 

Toa elimu juu ya bidhaa/huduma: Hakikisha wateja wako wanapata elimu bora juu ya matumizi sahihi ya bidhaa zako, ili waweze siyo tu kununua bali kueneza habari njema kwa wateja wengine. Kadiri utakavyozidi kuwaelimisha ndivyo utakavyozidi kuzalisha wateja wengi ambao ni waaminifu. 

Shirikiana nao shughuli za kijamii: Jaribu kuwa nao karibu kwenye shughuli za kijamii; kama ni kuchangia harusi fanya hivyo, hawa ndio unatakiwa kuwachangia, kama ni misiba hawa unalazimika kuwatembelea na kuwafariji. 

Kwahiyo, kupitia mahusiano yako na wateja, unajikuta umejenga kundi kubwa la marafiki na ndugu mlioshibana. 

Bahati mbaya sana wengi tunashiriki zaidi shughuli za kijamii kwa watu ambao hawana uhusiano wowote na biashara zetu. 

Unahitaji kuwaongeza kwenye orodha wateja wako, ili linapofika suala zima la kushirikiana katika shughuli za kijamii, nao wawe ni sehemu ya watu unaowakumbuka. 

Toa tuzo kwa wateja: Kama unachukua kumbukumbu za wateja vizuri ni rahisi kwako kuona nani amechukua pesa zake kwa wingi kwa katika kipindi cha mwezi, robo, nusu mwaka au mwaka mzima. 

Hapa utakuwa na nafasi ya kujua ni nani umpe tuzo. Tuzo hiyo siyo lazima uwambie, unaweza ukatafuta utaratibu wa kumpongeza au kumpa tuzo. 

Mafano; kutoa mwaliko wa chakula cha jioni au kinywaji nyumbani au hoterini; unaweza kutuma salam za pongezi mfano kupata mtoto, kumaliza shule kwa watoto n.k. 

Wewe uliye na biashara yoyote tambua kuwa unahitaji kuendelea kujifunza mpaka ufike sehemu uone kwamba wateja ndio ndugu namba moja. 
 
KWA   KUJIFUNZA   KWA  MAPANA  NA   MAREFU    JIUNGE  NA   "  DARASA   ONLINE "   KWA  KUWA  MWANACHAMA.
Tuwasiliane  kwa  WhatsApp  + 255 716924136  /   + 255 755  400128  + 255  688  361  539

Ndimi  RAFIKI   NA   KOCHA   MWL.  JAPHET  MASATU , 
DAR  ES  SALAAM , TANZANIA.

 

MAMBO 03 UNAYOHITAJI ILI UNUFAIKE NA USOMAJI WA VITABU

 



Wengi wa wanaosoma vitabu wanapoteza tu muda wao, wanakazana kusoma ili waweze kuwaambia wengine wamesoma vitabu vingapi, huku maisha yao yakiwa hayabadiliki kwa namna yoyote ile.

Huu siyo tu upotevu wa muda, bali pia kuchafua akili, maana kama ambavyo Alexander Pope amewahi kusema, “Maarifa kidogo ni kitu hatari, unapaswa kunywa kwa kina au usionje kabisa maji ya chemchem ya maarifa. Maarifa ya juu juu ni sumu kwa akili.”

Hili tumekuwa tunaliona wazi, mtu anapata maarifa kidogo ambayo hata hajayaelewa kwa kina na kuanza kuona anajua kila kitu, kuanza kuwadharau wengine ambao hawana maarifa hayo, lakini cha kushangaza, maisha yao yanabaki vile vile.




Mtu anaweza kusoma kitabu kimoja au vichache na kujifunza juu juu kwamba elimu rasmi ni upotevu wa muda na ajira ni utumwa. Akatoka hapo na moto wa kwenda kuacha shule au kuacha kazi, lakini anakuwa hajaiva kwenye nini aende kufanya, kinachotokea ni majuto baadaye.

Wapo wanaokuja kukiri wazi kwamba waliponzwa na vitabu na wapo ambao hawataki kuona kosa ni lao, bali hutafuta wengine wa kuwalaumu. Na siku hizi limepatikana kundi rahisi la kulaumu kwenye kupotezwa na maarifa ambalo ni la wahamasishaji au kama wanavyojulikana ‘motivational speakers’.

Mtu anapata maarifa ya juu juu, anatoka akiwa amejaa upepo na kwenda kuchukua hatua, ambazo zinamwangusha vibaya. Badala ya kuangalia tatizo liko wapi, ambalo ni yeye, anatupa lawama kwa mwingine.

Leo tunakwenda kujifunza vitu vitatu unavyohitaji ili uweze kunufaika na usomaji wa vitabu. Ukizingatia vitu hivi vitatu, hutakuja kulaumu usomaji wa vitabu, maana utakuwa na manufaa makubwa kwako.

Kwenye kitabu cha Fahrenheit 451, mhusika mkuu, Guy Montag ni mzima moto (Fireman), ambaye kwenye jamii yao kazi yao siyo tena kuzima moto, bali kuchoma vitabu moto. Ni jamii ya watu ambao wameacha kusoma vitabu na kuendekeza starehe na burudani mbalimbali kama kuangalia tv na michezo mingine.

Guy amefanya kazi hiyo kwa miaka kumi, lakini hajawahi kupata nafasi ya kutafakari kama kazi hiyo ina maana kwake au inampa furaha. Kwa udadisi, amekuwa akiiba vitabu kwenye nyumba wanazokwenda kuchoma, ila hajawahi kuvisoma, amekuwa anavificha ndani.

Siku moja Guy anakutana na binti ambaye anamhoji maswali yanayomfanya aanze kuyatafakari maisha yake na hapo anagundua kwamba maisha anayoishi siyo sahihi.

Anaamua aanze kusoma vitabu, lakini tatizo linakuja kwamba haelewi chochote anachosoma. Siku nzima anakazana kufungua vitabu na kusoma, lakini haelewi chochote.

Anakumbuka aliwahi kukutana na mzee mmoja ambaye alikuwa profesa aliyepoteza kazi yake baada ya watu kuacha kusoma. Anamtafuta ili amsaidie jinsi anavyoweza kusoma vitabu na kuelewa.

Profesa huyo anampa vitu vitatu anavyopaswa kuzingatia ili aweze kusoma vitabu, kuvielewa na maisha yake yabadilike. Hapa nakwenda kukushirikisha vitu hivyo vitatu ili na wewe uweze kupiga hatua kubwa kwenye maisha yako kupitia usomaji wa vitabu.

Kitu cha kwanza; jua jinsi ya kuchagua vitabu vyenye maarifa bora.

Vitabu havifanani, ubora wa maarifa unaopatikana kwenye vitabu haulingani. Kuna vitabu ambavyo ni bora, vyenye maarifa mazuri na unayoweza kutumia kupiga hatua.

Halafu kuna vitabu ambavyo ni vya hivyo, vyenye maarifa ambayo hayana manufaa kwako.

Kitu cha kwanza kuzingatia ni ubora wa maarifa yaliyo kwenye kitabu. Unapaswa kujua jinsi ya kuchagua vitabu bora kwako kusoma ili uweze kupata maarifa ambayo ni bora.

Kwa zama tunazoishi sasa, mitandaoni kunapatikana kila aina ya vitabu, na vingi sana ni vya hovyo. Ikiwa unataka kuanza kusoma vitabu kwa sasa, utajikuta njia panda usijue ni vitabu gani vya kuanza navyo.

Njia rahisi kwako kujua vitabu vya kuanza navyo, ni kuchagua watu ambao wamepiga hatua kwenye eneo unalotaka kupiga hatua, kisha waulize ni vitabu gani wamesoma.

Kama kuna mtu amefanikiwa zaidi yako, kwenye eneo lolote la maisha, kuna vitu anajua ambavyo wewe hujui. Badala ya kumwonea wivu au kumwogopa, mwombe akushirikishe ni aina gani ya vitabu anasoma, hapo utapata vya kuanzia.

Uzuri wa zama hizi ni mitandaoni kuna orodha za vitabu ambavyo wale waliofanikiwa wamekuwa wanashauri watu wavisome.

Hicho ni kitu cha kwanza, kuweza kuchagua vitabu ambavyo ni bora kwa maarifa yaliyo ndani yake.

Kitu cha pili; muda wa kutafakari yale uliyoyasoma.

Kusoma pekee, hata kama ni kitabu chenye maarifa bora kabisa hakutakuwa na manufaa kwako. Kwanza kabisa hutaweza kukumbuka kila ulichosoma na pili siyo kila maarifa yaliyo kwenye kitabu yatakuwa na manufaa kwako.

Hivyo unapaswa kupata muda wa kutafakari kile ulichosoma. Na hapa ndipo wengi wanapofeli na kuja kulaumu wengine. Wanasoma au kusikia kitu na kukimbilia kuchukua hatua kabla hawajatafakari kwa kina.

Kila maarifa unayoyapata, yatafakari kwa kina. Angalia maisha yako yalipotoka, yalipo sasa na kule yanakokwenda. Angalia ni jinsi gani maarifa uliyoyapata unaweza kuyaingiza kwenye maisha yako.

Kwa bahati mbaya sana, kutafakari ni kitu unachopaswa kukifanya mwenyewe, kwa sababu ni wewe pekee unayeyajua maisha yako kwa undani. Watu wawili mnaweza kusoma kitabu kimoja na wote mkakielewa, lakini hatua za kuchukua zikawa tofauti, kwa sababu maisha yenu ni tofauti.

Ambacho nimekuwa nashauri watu kwenye usomaji wa vitabu ni hiki, anza kwa kujua unataka nini kwenye maisha yako, kisha kila kitabu unachosoma jiulize kinakusaidiaje kupata au kufika pale unapotaka kufika.

Ikiwa hujafanya maamuzi unataka nini, kwenye kila kitabu unachosoma utakuja na vitu vipya. Utasoma kitabu cha kilimo cha tikiti na kuona ndiyo kitu bora, unaenda kufanya, unasoma kitabu cha ufugaji wa kuku unaona huo ndiyo wenyewe, unaenda kufuga. Unasoma kitabu cha forex na kusema siwezi kupitwa na hii, unaenda kufanya. Mwisho unajikuta umejaribu mengi lakini hakuna hatua uliyopiga.

Anza na unachotaka, kisha kwa kila kitabu unachosoma, tafakari kinakusaidiaje kufika kule unakotaka kufika.

Kitu cha tatu; kuchukua hatua kwenye yale uliyojifunza na kutafakari.

Kusoma maarifa ambayo ni bora na kuyatafakari jinsi unavyoweza kuyatumia kwenye maisha yako ili kupata unachotaka ni asilimia 10 ya manufaa ya kitabu.

Asilimia 90 inapatikana kwenye kuchukua hatua. Usikubali usome kitabu halafu maisha yako yabaki kama yalivyokuwa kabla hujasoma kitabu hicho. Chukua hatua, hata kama ni ndogo kabisa, kuhakikisha unakuwa bora kuliko ulivyokuwa kabla ya kusoma kitabu hicho.

Hivyo kwa tafakari unayoifanya, weka hatua utakazochukua na anza kuzichukua mara moja. Hazihitaji kuwa hatua kubwa sana, bali zinapaswa kuwa hatua zenye tija kwako, kiasi kwamba ukijiangalia unaona kitabu ulichosoma kimekuwa na manufaa kwako.

Siyo maarifa yote unayoyapata kwenye kitabu utaweza kuyatumia kwa mara moja, kuna mengine utayahifadhi kwa ajili ya baadaye. Lakini hupaswi kusoma kitabu na ukamaliza kisha ukarudi kwenye maisha yako ya awali kama yalivyokuwa. Badili kitu kwenye maisha yako, hata kama ni mtazamo wako au jinsi unavyotumia muda wako na kuendesha siku zako.

Kuna mengi ya kufanya pale unapopata maarifa bora na kuyatafakari yanakufaaje kwenye maisha yako.

Soma vitabu kwa tija na viwe na manufaa kwenye maisha yako, chagua vitabu vilivyo bora, pata muda wa kutafakari ulichojifunza na chukua hatua kuyafanya maisha yako kuwa bora zaidi. Ukizingatia hayo matatu, usomaji wa vitabu utayafanya maisha yako kuwa bora zaidi.

Rafiki, kama ungependa kuendelea kupokea makala na mafunzo mengine mazuri , JIUNGE  NA   DARASA  ONLINE---NA  ENDELEA   KUSOMA  KILA   SIKU  HAPA   "MAISHA  NA   MAFANIKIO   BLOG "  LIFE   AND   YOU  

Tuwasiliane  kwa  + 255 716 924136 /   + 255  755 400128 /  + 255 688 361 539  

Ndimi  KOCHA   MWL    JAPHET   MASATU