Tuesday, September 29, 2020

USIWE MTU MWEPESI WA KUUDHIWA NA WATU , HATUA 09 ZA KUSHINDA DHIDI YA MAUDHI AU ADHA.

Habari mwanafalsafa, wadau  wangu  wa  MAISHA NA  MAFANIKIO  BLOG ,

Karibu katika mwendelezo wa safari ya kujifunza falsafa ya Ustoa. Falsafa hii imekuwa ni falsafa yenye msingi mzuri wa kuzalisha maisha matulivu na bora. Wiki hii nimejiwekea utaratibu wa kuendelea kujifunza falsafa hii ya ustoa kupitia mwandishi Dr. Chuck Chakrapani ambaye kaandika mfululizo wa kazi nyingi za kistoa kwa kukusanya nukuu na misemo ya wastoa kama Seneca, Epictetus na Marcus. Kitabu cha awali nilishirikisha kama mapendekezo katika moja ya mijadala ya kifalsafa kupitia substack kiitwacho “STOIC INSPIRATIONS”. Ni kitabu kizuri sana kukisoma

Mbali na hicho kitabu kuna kingine ambacho nimekipitia na ndio msingi wa kuandika makala hii unayoisoma. Kitabu hiki kinaitwa “UNSHAKABLE FREEDOM” kwa tafsiri iso rasmi inatafsiriwa kama “UHURU USOTIKISWA”. Uhuru ni hitaji mama la mtu yeyote yule sehemu yoyote Duniani. Uhuru unalindwa na uhuru wa maisha ni katika kujua mambo yapo makundi mawili; Mosi, ni yale yalo katika uwezo wako na pili yalo nje ya uwezo wako. Kitabu hiki kinagusa namna unavyoweza kuwa na uhuru usotikiswa. Kuudhiwa ni njia rahisi inayoweza kuharibu uhuru wetu katika maisha na usipokuwa na msingi wa falsafa utaishi kuamua ovyo.

Kuudhiwa kunaweza kukufanya ujisikie vibaya, upandwe na hasira na tatu unakupotezea utulivu wa akili na wakati mwingine mwili. Ila si vile ambavyo Marcus Aurelius anatushauri kuwa tuumie au tupandwe na hasira la hasha ila kutusaidia kuwa na utulivu pale tunapopitia hali ya kuudhiwa na watu wanaotuzunguka. Marcus Aurelius kaziweka kama hatua 09 za kufuata ili kwa lolote litakalojitokeza la kutuudhi basi tusipoteze utulivu wetu wa ndani.

Hatua hizi 09 zimegawanyika katika makundi mawili. Mosi ni hatua 04 za awali ambazo ni maswali 04 ya kujiuliza unapopitia hali ya kuudhiwa na pili ni hatua 05 za mwisho ambazo ni makumbusho/ tafakari kuhusu hali unayopitia ya kuudhiwa na mtu au matukio maishani.

Jiulize haya; [ Haya ni maswali ambayo Marcus Aurelius anatupa mwongozo wa kujiuliza pale ambapo tunakuwa kati kati ya hali za kuudhiwa au dakika chache ya tendo la kuudhiwa limejitokeza ]

1.       Usizidishe ukali wa tatizo- Je ni mahusiano gani ninayo na huyu mtu?

mfano mtu aliyekukosea ni ndugu yako wa karibu, mfanyakazi wako, mke au mume wako. Ukiondoa upande wa kosa ambalo limejitokeza la kukufanya uudhike ila upande mwingine mzuri huyo mtu ni ndugu yako, mfanyakazi wako, mke au mume wako. Unaporuhusu kuona mahusiano ya mtu aliyekutendea kosa unakuwa katika nafasi ya kupunguza ukubwa wa tatizo au tukio lilojitokeza.

2.       Jitahidi kufahamu nini msukumo wa mtu kufanya hivyo;

Mtu anapotenda kitu usifanye haraka kutoa hukumu maana unazibwa na kutokujua kwa kina, je nini ni msukumo wa jambo alotenda. Ukiangalia kwa kina unaweza kuona msukumo wa kutenda jambo hilo. Huenda ni msukumo wa chuki, ujinga, wivu au wakati mwingine kutokukusudia.

3.       Itafakari hali ilojitokeza

Usiwe na haraka ya kilichotokea kukipa tafsiri. Vuta ukimya na kuwa tayari kuona hali ilojitokeza imechangiwa na nini. Utaona pengine kuna nafasi ya ujinga kuwepo ndo maana tukio hilo limejitokeza. Usitoe mwitikio haraka tukio linapojitokeza.

4.       Hebu jiangalie hujawahi watendea wengine ulofanyiwa ?

Ni rahisi sana kuona watu wanaotuudhi wanamakosa zaidi na tukasahau hata sisi kuna watu wengi tunawaudhi kwa mambo yetu. Mimi na Wewe ni bado wanadamu na tuna mapungufu mengi kama wengine. Wanapokosea wengine tuwe waelewa kama ambavyo nasi tunavyotaka watu wengine watuelewe.

Jikumbushe haya; [Haya ni mambo ya kujikumbusha ambayo Marcus Aurelius anatupa mwongozo wa kujikumbusha pale ambapo tunakuwa kati kati ya hali za kuudhiwa au dakika chache ya tendo la kuudhiwa limejitokeza]

5.       Jua kuwa huna picha kamili ya jambo lilivyo

Wakati mwingine tunaona vitu kwa picha ndogo kuliko uhalisia ulivyo. Huwezi jua mtu aliyekukosea kwa wakati huo ni mambo gani anayoyapitia, au ni mambo yepi yalochangia yeye kufanya hivyo. Utaona mambo mengi ya watu walokosea ukichimba kwa kina kuna baadhi ya taarifa hatukuweza kuzijua kwanini hilo limejitokeza. Kila tukio linapotokea jua kuwa huna picha kamili ya mambo yalivyo. Usifanye haraka kutoa hukumu.

6.       Kumbuka Maisha ni mafupi

Miaka 200 toka sasa na kuifikiria ijayo hatutakuwepo; hii ikiwa ina maana wewe unayesoma hii makala miaka 200 ijayo sote hatutakuwepo. Hili linadhihirisha maisha yalivyo mafupi na hatupaswi kuhifadhi hasira au chuki na mtu yeyote yule. Kwa kujua hili unakazana kuishi katika kuchagua furaha kuliko kitu kingine chochote.

7.       Jua maoni ya mtu mwingine hayana nguvu dhidi yako endapo utapuuza au kuzuia kuyapa tafsiri

Kinachotuumiza sana siku zote kwa watu wanaotuudhi, wanaotutukana ni juu ya kuyapa tafsiri yale ambayo wamesema. Kuyapa tafsiri ni kuruhusu waloyasema yawe na nguvu dhidi yetu. Kwa kuona hilo Marcus anatushauri kutoyapa tafsiri au tukiweza tuyapuuze.

8.       Jua hasira ukiijenga itakuumiza zaidi ndani yako

Hasira inaunguza kama mtu aliye na kaa la moto katika kiganja. Ukiudhiwa na ukajenga hasira ndani yako, hasira inaanza kukuumiza wewe na pengine aliyekuudhi hana mpango wowote wa kukuwazia wewe. Hasira isiruhusiwe idumu ndani yako.

9.       Ukiweza tabasamu

Hakuna kitu kinachomfanya mtu aliyekuudhi au kukutukana pale unapotabasamu na wakati mwingine kucheka kwa kile alichokifanya. Inaonesha kwako kuwa alichokifanya hujakipa nguvu na pengine kukidharau. Lengo la mtu wakati mwingine kukutusi ni kutegemea kuona umekasirika, sasa unapokuwa unacheka unampa aumie zaidi kuona alichotegemea hakijafanikiwa.

Hizi hatua 09 ni mwongozo mzuri unaoweza kuutumia kila inapoitwa leo unapoendelea kukutana na watu mbalimbali. Maisha ya kila siku hatutaacha kukutana na watu ambao kwa namna moja wataleta adha dhidi yetu. Tutumie huu msingi kulinda utulivu wetu wa ndani maana tukumbushe maisha yetu ni mafupi.

 

KILA SIKU NI YA PEKEE SANA , ISHI KAMA LEO NA USIIPOTEZE.

Wanasema unaweza kulalamika huna viatu, ila ni mpaka siku utakayokutana na mtu asiye na miguu ndiyo utakumbuka kushukuru kwamba angalau wewe una miguu na hivyo viatu haviwi tatizo tena kwako.

Ni kawaida kwetu binadamu kuzoea vitu tulivyonavyo na kuvichukulia kawaida, kwa sababu tumekuwa tunaviona kila siku. Lakini vitu hivyo hivyo tunavyovichukulia pia, kuna wengine wanavitamani kweli ila hawawezi kuvipata.

Moja ya vitu hivyo ni hizi siku tunazokuwa nazo kila siku, tangu umezaliwa mpaka hapo ulipofika sasa, umekua unaanza na kumaliza siku zako na hivyo umeshazoea, asubuhi unaamka, unaenda na shughuli zako na siku inaisha, unalala na kuamka tena siku inayofuata.

Kwa kuwa umeshazoea sana siku zako, umekuwa unajiaminisha kabisa kwamba kesho ipo na huchelewi kuacha kufanya kitu leo kwa kujiambia utafanya kesho. Ni kitu gani kinakupa uhakika kiasi hicho?

Unapopata habari za misiba ya watu wa karibu, wale ambao uliwajua na walikuwa na mipango mikubwa ila wamefariki ghafla, huwa unapata mshtuko, unaona kweli maisha ni mafupi. Lakini haikuchukui siku nyingi unarudi kwenye mazoea yako, unazichukulia siku zako poa na kuahirisha mambo.

Tunawezaje kuondokana na hali hii ili tuweze kuzipa siku zetu uzito unaostahili na kuishi kwa ukamilifu?

Mwanafalsafa Seneca ana mengi ya kutueleza kwenye hili. Kwenye moja ya barua alizoandika kwa rafiki yake Lucilius akimweleza kuhusu wengi wanavyokihofia kifo, aligusia hili la kuishi kila siku kwa mazoea.

Seneca anasema wengi wamekuwa wakijiuliza maisha yao yataenda hivyo mpaka lini, kila siku kulala na kuamka, kuwa na njaa na kushiba, majira ya masika na kiangazi. Kwa kuyatazama maisha hivyo unaona kama ni mzunguko, hakuna kipya, kila kitu kinajirudia.

We slip into this condition, while philosophy itself pushes us on, and we say; "How long must I endure the same things? Shall I continue to wake and sleep, be hungry and be cloyed, shiver and perspire?  There is an end to nothing; all things are connected in a sort of circle; they flee and they are pursued.  – Seneca

Seneca anatutahadharisha kwamba tukiyaangalia maisha kwa mtazamo huo, tutayaona maisha ni maumivu yasiyo na mwisho, unaimaliza leo ukijua kesho inakwenda kuanza na kuisha kama leo. Majira ya masika yanaisha ukijua kiangazi kinakuja. Una njaa na kutafuta chakula kizuri kula, ila ukishashiba unajua kuna njaa itakuja tena. Kwa namna hii, maisha yanakuwa kama gereza la mateso, kusukuma siku usubiri kufa.

Lakini ipo namna nyingine ya kuyaangalia maisha kwa namna ambayo yatatunufaisha, mtazamo wa tofauti unaotusukuma kuyaishi maisha yetu kwa ukamilifu. Mtazamo huo ni kuyaona maisha kama zawadi, kila siku mpya unayoipata inakuwa kama nyongoza na hivyo unaitumia vizuri zaidi.

There are many who think that living is not painful, but superfluous. – Seneca.

Unapoiona siku mpya unayoianza kama nyongeza, unaitumia vizuri kwa sababu unajua huna uhakika kama utaiona siku nyingine kama hiyo. Huangalii jana ulifanya nini maana imeshapita, na wala huangalii kesho itakuwaje maana haipo, unachoangalia ni zawadi iliyo mbele yako.

Tukiweza kuziishi siku zetu kwa mtazamo huu, tutaacha kuona marudio yanayotuumiza na tutaanza kuona vitu vizuri vya kufanyia kazi.

Mahali pengine Seneca amewahi kutuasa jinsi ya kuziishi siku zetu kwa ukamilifu, mfano ni nukuu hizi;

“Anza kuishi mara moja na ichukulie kila siku mpya kama maisha tofauti.”

“Nitaendelea kuyaangalia maisha yangu na muhimu zaidi nitaitathmini kila siku yangu kwa kufunga vitabu vya maisha kila siku.”

Kama kauli za Seneca zinavyosisitiza, usichukulie poa hii siku uliyonayo leo, kuna wengine wangetamani sana kuwa nayo lakini haijawezekana. Iishi kwa upekee wake, ipangilie vizuri na fanya mambo ambayo mwisho wa siku ukiyaangalia unajiambia kweli umeiishi siku hii.

Kila unapoimaliza siku yako, jifanyie tathmini, pitia kila ulichofanya tangu kuamka mpaka unaporudi kulala na kisha jiulize maswali haya matatu;

Moja; Ni yapi mazuri nimefanya leo na ambayo nitaendelea kuyafanya nikipata zawadi ya siku nyingine?

Mbili; Ni yapi mabaya nimefanya leo ambayo sitarudia tena kufanya kama nitazawadiwa siku nyingine?

Tatu; Yapi ambayo sijayafanya kwa ubora unaostahili na ambayo nitayaboresha zaidi nitakapopata zawadi ya siku nyingine?

Ukijiuliza maswali hayo matatu kila siku na kujipa majibu sahihi, kisha kuyafanyia kazi, maisha yako yatakuwa bora, hutazichoka siku zako, hutaahirisha chochote na utayazuia matatizo mengi kabla hayajawa makubwa.

Wenye hekima wanajua, maisha siyo mateso bali zawadi, ichukulie hivyo na utakuwa na maisha bora na tulivu.

 

Saturday, September 5, 2020

JINSI YA KUKUZA BIASHARA KUTOKA WATU 10 MPAKA WATU 10,000 KATIKA KAMPUNI.

Jukumu La Mtendaji Mkuu (CEO)

Kwenye vitabu vingi vya biashara, majukumu ya CEO yamekuwa yanaainishwa kuwa;

1. Kuweka mwelekeo na mkakati wa kampuni na kuuwasilisha kwa wafanyakazi, wateja na wawekezaji.

2. Kuajiri, kufundisha na kutengeneza utamaduni sahihi kwenye kampuni.

3. Kukusanya mtaji na kuugawa kwa usahihi kwenye shughuli za kampuni.

4. Kuwa mwanasaikolojia mkuu wa kampuni, kwa kuwapa wengine moyo pale mambo yanapokuwa magumu.

Kutafuta, Kuajiri Na Kusimamia Vipaji.

Ukuaji na mafanikio ya kampuni unategemea sana watu unaowaajiri kwenye kampuni yako. Ni muhimu uajiri watu sahihi, wenye uwezo wa kutekeleza majukumu yao na hamasa ya kufanya hivyo.

Kujenga Timu Ya Watendaji.

Wakurugenzi wa vitengo mbalimbali vya biashara yako ndiyo watendaji kwenye kampuni. Hawa wanahusika kusimamia vitengo vyao ili viweze kuisaidia kampuni kufikia maono yake. Kama mkurugenzi mkuu, utaweza kukuza kampuni yako unapokuwa na timu nzuri ya watendaji.

Kujenga timu bora ya watendaji ni zoezi gumu kwa waanzilishi wachanga, kwa sababu mwanzoni walikuwa wanafanya kila kitu peke yao. Lakini sasa kampuni inakua kwa kasi, hawawezi tena kufanya hivyo. Na hapo bado wengi wanakuwa hawajawa tayari kugatua majukumu yao.

Lakini inafika hatua ambapo kama mwanzilishi huwezi tena kusimamia kila kitu peke yako, kwa sababu majukumu yanayotaka muda wako ni mengi kuliko muda ulionao. Hivyo unakuwa huna budi kujenga timu ya watendaji.

Changamoto kubwa kwenye kuajiri watendaji ni kwamba unapaswa kutafuta watu wenye uzoefu zaidi yako, kitu ambacho siyo rahisi. Lakini unapofanikiwa kuajiri mtendaji wa kwanza vizuri, wanaofuata haitakuwa changamoto kwenye kuwaajiri.

Unapokuwa na watendaji wazuri, mambo mengi kwenye kampuni yanaenda bila ya wewe mwenyewe kuhusika moja kwa moja. Unaona kama ni miujiza maana mambo yaliyokuwa yanakusumbua awali hayakusumbui tena kwa sababu wapo wanaoyafanyia kazi.

Lakini pia kuna wakati makosa yanafanyika kwenye uajiri na mtendaji anayeajiriwa anakuwa siyo sahihi. Hapo msongo unakuwa mara mbili, kwa majukumu yanayokutegemea na mtendaji asiyefaa. Mtendaji wa aina hiyo huwa chanzo cha wafanyakazi wazuri kuikimbia kampuni yako.

Muundo Wa Kampuni Na Ukuaji Wa Kasi.

Muundo wa kampuni kwenye kipindi cha ukuaji wa kasi ni jambo lenye changamoto kwa waanzilishi wasio na uzoefu. Hii ni kwa sababu inakuwa vigumu kuwa na muundo mmoja, kadiri kampuni inavyokua, ndiyo mabadiliko yanayohitajika kwenye muundo.

Masoko Na Mahusiano Ya Umma.

Masoko na mahusiano ya umma (marketing and PR) ni eneo muhimu kwenye ukuaji wa kampuni yoyote ile. Ila kwa kampuni zilizo kwenye hatua ya ukuaji wa kasi, eneo hilo ni muhimu na linapaswa kufanya kwa usahihi.

Mchango wa masoko na mahusiano ya umma ni kujenga jina la kampuni (brand), kutengeneza taswira nzuri kwa umma, kupata kutunza wateja wa kampuni.

Kwenye uchambuzi kamili utajifunza njia bora za kufanya masoko na mahusiano kwa umma ili kampuni iweze kunufaika.

Usimamizi Wa Bidhaa.

Usimamizi wa bidhaa ni eneo muhimu wakati wa ukuaji wa kasi wa kampuni. Hii ni kwa sababu uhitaji unakuwa mkubwa na hivyo kusipokuwa na usimamizi mzuri, bidhaa inaweza isiwe bora au mahitaji ya wateja yasifikiwe.

Usimamizi mzuri wa bidhaa unaiwezesha kampuni kuweka maono makubwa ya bidhaa, mipango ya kufikia maono hayo, mikakati ya kufanyia kazi na hatua za kuchukua.

Usimamizi mbaya wa bidhaa unakuwa fujo kwa kampuni nzima kwani hakuna maono, na mambo hayafanyiki kwa wakati.

Ili kuwa na usimamizi mzuri wa bidhaa, unapaswa kuwa na kitengo mahususi kwa ajili ya bidhaa, kinachosimamiwa na meneja wa bidhaa ambaye anakuwa na ujuzi wa juu kwenye bidhaa husika. Pia unapaswa kutengeneza mchakato sahihi unaofuatwa kwenye kuandaa bidhaa husika.

Fedha Na Uthaminishaji.

Fedha na uthaminishaji ni eneo muhimu kwenye ukuaji wa kasi wa kampuni. Katika kipindi cha ukuaji wa kasi, japo kampuni inaweza kuwa na wateja wengi, lakini inaweza isiwe inazalisha faida. Hivyo kama CEO utahitaji kupata fedha za kuendelea kuendesha kampuni. Huu ndiyo wakati utakaohitajika kuithaminisha kampuni na kisha kukaribisha wawekezaji kuwekeza mitaji yao. Pia unaweza kuiuza kampuni au kuipeleka kwa umma.

Kuungana Na Kununua.

Njia nyingine ya kukuza zaidi kampuni yako ni kuungana na kampuni nyingine ambayo ni kubwa zaidi au kununua kampuni ambayo ni ndogo.

Kuungana na kununua (Mergers & acquisitions) kunaiwezesha kampuni kupata bidhaa, teknolojia, timu na hata kuondoa ushindani kwenye soko.