Sunday, February 17, 2019

TENGENEZA FURAHA KILA HATUA UNAYOPIGA KILA SIKU, USISUBIRI MPAKA UFIKE MWISHO

Miaka 2300 iliyopita, mwanafalsafa Aristotle alijumuisha kwamba watu wanatafuta furaha kuliko kitu kingine chochote. Kwamba lengo kuu la kila ambacho tunafanya kwenye maisha yetu, ni kutegemea kupata furaha mwishoni.

Na hili ndiyo linawasukuma watu kuchukua hatua mbalimbali, kuanzia kuboresha afya zetu, kuboresha mwonekano wetu, kupata fedha na hata madaraka ni kwa lengo la kutengeneza furaha kwenye maisha.
 
Lakini sasa tunapofanya furaha kuwa lengo la mwisho, hapo ndipo tunapojiangusha. Kwa sababu wengi wanafika mwisho wa kile walichofikiri kitawapa furaha, lakini hawapati furaha ambayo walifikiria wangeipata.
 
Hivyo njia bora ya kuipata furaha, siyo kusubiri mpaka mwisho wa kile tunachofanya, bali kutengeneza furaha wakati unakifanya.
 
Kama unataka furaha ya kweli kwenye maisha, basi usisubiri mpaka mwisho wa kile kitu unachofanya ndiyo uwe na furaha, badala yake tengeneza furaha kwenye kila hatua unayopiga. Furaha inapaswa kuwa matokeo ya kile unachofanya kila siku, na siyo kusubiri mpaka ufike mwisho.
 
Na hili ndiyo tunakwenda kujifunza kwa kina kwenye kitabu cha juma hili.
 
Tafiti zinaonesha kwamba furaha siyo kitu kinachotokea kwa bahati na wala siyo kitu ambacho fedha inaweza kununua au madaraka kulazimisha. Furaha haitegemei matokeo ya nje badala yake inategemea jini tunavyotafsiri yale yanayotokea.
 
Furaha ni hali ambayo inapaswa kuandaliwa, kutengenezwa na kulindwa na kila mtu, kwa kuwa na tafsiri sahihi ya kila kinachoendelea kwenye maisha yako.
 
Ni kwa kujihusisha moja kwa moja na kila kinachoendelea kwenye maisha yako, kiwe kizuri au kibaya ndiyo tunapata furaha. Siyo kwa kukimbia au kutoroka yale yanayotokea au kujaribu kuikimbiza furaha, bali kuyaishi maisha yako kwa namna yalivyo, ndiko kunakokuletea furaha.
 
Hivyo jibu fupi la kuwa na furaha kwenye maisha yako ni kujihusisha moja kwa moja na maisha yako na kupokea kila kinachokuja kwako, iwe kizuri au kibaya.

No comments:

Post a Comment