Saturday, June 22, 2019

ELIMU YA FEDHA : MUDA WAKO NI PESA YAKO

Ndugu  yangu mpendwa, nimekuwa napenda kukuambia sana kauli hii, HAKUNA KITU CHA BURE. Ukiona mtu anakupa kitu bure, jua kuna namna unalipia ambayo wewe hujui au kuna mtu ameshalipa kwa ajili yako. Huu ni msingi ambao ukiweza kuuishi na kuusimamia kwenye maisha yako, utajiepusha na matatizo mengi mno. Mfano huwezi kutapeliwa kama utaishi kwa msingi kwamba hakuna kitu cha bure. 

Sasa tuje kwenye mitandao ya kijamii, orodhesha mitandao yote ya kijamii ambayo unaitumia. Je ni Instagram? Facebook? Whattsapp? Twitter? Snapchat? Na mingine zaidi. Swali ni je umekuwa unalipa kiasi gani ili kutumia mitandao hii ya kijamii?
Ukiacha bando (data) unazonunua ili kuweza kuingia mtandaoni, hulipi hata senti moja kutumia mitandao hii. Lakini unaweza kuitumia muda wowote, masaa 24 kwa siku, siku 7 za wiki.
Swali jingine unalopaswa kujiuliza ni je mitandao hii inapataje fedha za kujiendesha. Maana mitandao hii ina wafanyakazi wengi, na ambao ni wasomi kweli kweli, ina rasilimali nyingi na wamiliki wake ni matajiri wakubwa sana duniani. Ukichukua mfano wa mmiliki wa Facebook na Instagram, ambaye ni bilionea mkubwa duniani, ambaye yupo kwenye watu 10 matajiri zaidi duniani. Hizo fedha wanazitoa wapi?

Kama hujawahi kujiuliza swali hili basi leo unakwenda kupata mwanga, na utakufanya uangalie kwa mtazamo tofauti kabisa mitandao hii ya kijamii.
Mitandao ya kijamii inaingiza kipato kupitia MATANGAZO. Mfumo wao wa biashara uko hivi, kusanya watu wengi watumie huduma yako ya mtandao wa kijamii, kisha nenda kwa mtu mwenye biashara na mwambie unaweza kutangaza biashara yako kwenye mtandao wangu ambao una watumiaji wengi, na wanaotumia huduma hiyo kwa muda wao mwingi wa siku.
Sasa kama unavyojua tabia yetu binadamu, huwa tunafanya zaidi kile tunacholipwa ili kufanya. Kwa kuwa makampuni haya yanapata fedha kwa watu kutangaza kupitia mitandao yao, na kwa sababu wingi wa fedha unaamuliwa na wingi wa watembeleaji na muda ambao watembeleaji wanatumia kwenye mitandao hiyo, basi mitandao hii imekuwa inahakikisha inatumiwa na wengi, na ukishaitumia huachi, kila muda unataka kuitembelea. Kama nilivyokuambia kwenye kipengele namba moja, hujavutiwa kutembelea mitandao hii, umesukumwa kuitembelea kila wakati, kwa sababu unavyoitembelea zaidi, ndivyo wenye mtandao wanatengeneza kipato zaidi.
Hivyo basi, MUDA WAKO = PESA ZAO. Muda unaotumia kwenye mitandao ya kijamii ndiyo fedha ambazo zinawafanya wamiliki wa mitandao hiyo kuwa mabilionea wakubwa.
Swali jingine muhimu sana ni je, kwa matumizi yako makubwa ya mitandao ya kijamii, ni manufaa gani unayapata? Najua wengi mnajiambia naungana na marafiki na kujua yanayoendelea. Kama jibu hilo ni kweli, swali jingine litakuwa je unahitaji zaidi ya masaa mawili kwa siku kutembelea mitandao hii? Je kweli unahitaji kila baada ya nusu saa au saa moja kutembelea tena mitandao hii?
Rafiki, nafikiri unapata picha ni jinsi gani tumechagua kuharibu na kupoteza maisha yetu, kuwafaidisha wengine, huku sisi wenyewe tukibaki hatuna kitu.
Nikuache na mbinu moja ya kupima matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii kwako. Chukulia hili, kama kila dakika unayotumia kwenye mitandao ya kijamii ulikuwa unailipia shilingi elfu moja, je ungekuwa tayari kulipa shilingi ngapi kwa siku kutembelea mitandao hii?
Je ungekuwa tayari kulipa tsh 120,000/= kila siku ili tu utumie mitandao ya kijamii? (kwa wastani mtumiaji wa mitandao ya kijamii anatumia masaa mawili kila siku). Kama jibu ni hapana basi jua muda unaoweka kwenye mitandao hiyo unaupoteza. Kama kweli unatumia mitandao ya kijamii kuungana na marafiki na kujua yanayoendelea, utahitaji dakika 10 tu kwa siku kwa ajili ya hilo. Muda mwingine utakuwa na manufaa kwako kama utatumia kwenye mambo yenye tija.
Kila unapoingia kwenye mitandao ya kijamii jikumbushe hili, MUDA WAKO = PESA KWAO na jiulize kama kweli unataka kuendelea kuwa bidhaa inayouzwa.
Na mwisho kabisa, pima umuhimu wa mitandao hii kwa kujiuliza kama ungekuwa tayari kulipia ili kuitumia, maana bure inakudanganya na kukupotezea muda wako.

No comments:

Post a Comment