Friday, June 7, 2019

NJIA ZA KUONDOKANA NA MSONGO NA KUWA NA MAISHA TULIVU.

  1. Acha tamaa.

Chanzo kikuu cha msongo ni tamaa. Pale tunapotamani kuwa na vitu ambavyo vipo nje ya uwezo wetu kwa wakati huo, tunazalisha msongo kwenye miili yetu.

Maisha ya sasa yamejengwa kwenye mashindano ya kijinga. Mashindano ya kutaka kitu kwa sababu kila mtu anacho. Mashindano haya yamepelekea wengi kuingia kwenye madeni ili kupata wanachotaka. Wanaweza kupata wanachotaka, lakini madeni wanayobaki nayo yanakuwa chanzo cha msongo mkubwa kwao.

Acha tamaa, acha kushindana na wengine na ishi maisha yako kwa ukamilifu, fanya kile unachoweza kufanya kwa pale ulipo sasa, na kama kuna kitu kipo nje ya uwezo wako usijilazimishe nacho.

  1. Dhibiti taarifa zinazoingia kwenye akili yako.

Taarifa tunazoruhusu ziingie kwenye akili zetu zina madhara makubwa kwenye miili yetu. Pale ambapo taarifa zinazoingia ni hasi na za kukatisha tamaa, tunaingiwa na hofu na hapo mwili unaingia kwenye msongo.

Tumezungukwa na taarifa nyingi hasi na za kutisha na hata wale waliotuzunguka wana kila njia ya kutukatisha tamaa. Unapaswa kuwa makini ni aina gani ya taarifa unaruhusu ziingie kwenye akili yako na aina gani ya watu unaowasikiliza ili kuepusha kuingia kwenye msongo usio na umuhimu.

Epuka sana kufuatilia habari na pia waepuke sana watu ambao ni wakatishaji wa tamaa na wanaoona magumu mara zote.

  1. Ishi wakati uliopo.

Sababu nyingine kubwa ya msongo ni pale ambapo mtu anashinda kuishi wakati uliopo. Kuna nyakati tatu kwenye maisha yako, wakati uliopita, wakati uliopo na wakati ujao.

Unapojikuta kwenye msongo, kwa hakika utakuwa unaishi wakati uliopita ambapo mambo yameshapita na huwezi kuyabadili au utakuwa unaishi wakati ujao, ambao bado hujaufikia na hivyo huwezi kubadili chochote.

Huwezi kuwa na msongo kama unaishi wakati uliopo, kama mawazo yako yote yapo kwenye kile kitu unachofanya sasa, msongo hauwezi kupata nafasi kabisa. Jifunze kuweka akili yako yote kwenye kitu unachofanya kwa wakati huo, linapokuja wazo la kitu cha nyuma au kijacho liandike pembeni na jilazimishe kurudisha akili kwenye kile unachofanya. Kwa njia hii utaondokana kabisa na msongo.

  1. Ondokana na vilevi.

Wengi wamekuwa wanatumia vilevi kama njia ya kuondokana na msongo, lakini wote tunajua vilevi vinasogeza msongo mbele, unajisahaulisha kwa muda lakini ulevi unapoisha msongo unarudi pale pale.

Vilevi vinazidi kuuchosha mwili na kutengeneza msongo mpya. Hivyo epuka kutumia njia ya vilevi kama sehemu ya kukabiliana na msongo.

Epuka matumizi ya kahawa au sigara, vitu viwili ambavyo watu hutumia sana wanapokuwa na msongo. Kemikali zilizopo kwenye vitu hivi vinauweka mwili kwenye hali ya msongo zaidi.

  1. Fanya mazoezi.

Mazoezi ni njia bora ya asili ya kukabiliana na msongo. Mwili unapokuwa kwenye mazoezi, unazalisha homoni tofauti na za msongo, homoni ambazo zinafanya mtu ajisikie vizuri.

Mazoezi pia ni njia ya kuurudisha mwili kwenye asili yake, kwa sababu sisi binadamu hatukuumbwa kukaa kwa muda mrefu, shughuli za watangulizi wetu zilikuwa za kuhusisha viungo vyote vya mwili. Lakini hali ya sasa tunajikuta tunakaa kwa muda mrefu, kitu ambacho kinachochea msongo zaidi. Unapofanya mazoezi unauondoa mwili kwenye hali ya msongo.

  1. Ongeza ukomavu wako kwenye msongo.

Sababu nyingine kubwa ya msongo kuwa tatizo kwa wengi zama hizi ni kwamba miili yetu haijazoea kabisa mazingira magumu. Tumeishi kwenye kipindi ambacho ni rahisi kupata kila tunachotaka, na hivyo mwili unabweteka na kuwa laini, usioweza kupambana hata na vitu vidogo.

Ondokana na hali hii kwa kuukomaza mwili wako. Unaweza kufanya hivi kwa kuupa mwili msongo wa muda mfupi ambao unakukomaza zaidi. Njia za kufanya hivyo ni kama kufanya mazoezi makali sana ambayo yanakuletea maumivu, lakini unayafanya kwa muda mfupi. Kuoga maji ya baridi kali sana wakati wa asubuhi pia ni njia nyingine ya kukomaza mwili kwenye msongo. Na pia kufunga ni njia ya kuufanya mwili kutokutegemea chakula muda wote.

  1. Tahajudi ya kuondoa msongo.

Njia bora kabisa ya kuondokana na msongo ni kufanya tahajudi (meditation) ya kuondoa msongo. Kwa sababu msongo unaendelea kuwa na sisi kila wakati, ni muhimu kujua jinsi ya kufanya na kuifanya tahajudi hii kila mara na tutaweza kuwa na maisha tulivu sana.

Maandalizi ya kufanya tahajudi ya kuondoa msongo.

Katika kufanya tahajudi hii, unapaswa kutenga sehemu tulivu ambapo unaweza kukaa na kufanya tahajudi bila ya kusumbuliwa. Unapaswa kutenga dakika 5 mpaka kumi za kufanya tahajudi hii. Pia unapaswa kuzima simu yako au kuiweka kwenye utulivu wakati ambao unafanya tahajudi.

Jinsi ya kufanya tahajudi ya kuondoa msongo.

Kaa wima, mgongo ukiwa umenyooka na macho ukiwa umeyafunga.

Pumua kwa kina kwa kuingiza na kutoa hewa kupitia pua, vuta pumzi kwa kuielekeza tumboni, chini kidogo ya kitovu.

Weka mkono wako wa kushoto kwenye goti la kushoto, kiganja kikiangalia juu na kidole gumba kugusana na kidole kidogo.

Tumia mkono wako wa kulia kufunga matundu ya pua yako, tundu moja kwa wakati.

Ingiza pumzi ndani kwa kutumia tundu la pua la kushoto huku ukiwa umeziba tundu la kulia. Toa hewa nje kwa kutumia tundu hilo hilo la kushoto.

Rudia kuingiza pumzi na kutoa kwa kutumia tundu la kulia, huku ukiwa umeziba tundu la kushoto.

Endelea kurudia zoezi hili, tundu la kushoto na tundu la kulia mpaka muda uliotenga wa kufanya tahajudi kuisha (hapo unakuwa umeweka alamu itakayoita baada ya muda uliotenga kuisha).

Muda unapoisha, maliza kwa kupumua kwa kina kawaida kwa matundu yote mawili ya pua na mdomo na hapo unarudi kwenye hali yako ya kawaida.

Hii ni tahajudi rahisi sana kufanya, ambayo itaweza kukusaidia kuondokana na msongo wowote unaokuwa nao. Lakini pia unaweza kuifanya ukiwa popote na kwa muda mfupi na ukapata manufaa makubwa.

No comments:

Post a Comment