Saturday, June 22, 2019

ELIMU YA FEDHA : CHANGAMOTO YA FEDHA

Fedha imekuwa changamoto kubwa sana kwenye zama tunazoishi sasa. Tunapoteza muda na maisha yetu kwenye kufanya kazi ngumu, lakini fedha tunazozipata tunazipoteza kwa kununua vitu ambavyo siyo mahitaji ya msingi.
Makampuni makubwa yanatumia mbinu za kisaikolojia kututangazia bidhaa na huduma zao kwa namna ambayo tunajisikia vibaya kama hatuna wanachouza.
Pia taasisi za fedha zimerahisisha sana matumizi yetu, hata kama mtu huna fedha za kununua kitu, basi ni rahisi kukopa fedha ili kununua unachotaka. Na hapo sasa mtu analipa mkopo pamoja na riba kubwa.
Yote haya ni matatizo ya kujitakia, kwa kushindwa kudhibiti tamaa zetu na kujilinganisha na wengine.
Ili kuondokana na changamoto hii ya fedha, fanya yafuatayo;
  1. Jua mahitaji yako ya msingi ambayo utayagharamia na yale ya anasa ambayo utaachana nayo. Mahitaji ya msingi ni manne, maji, chakula, moto na malazi. Mengine yoyote nje ya hapo ni anasa, yanaweza kusubiri.
  2. Kuwa na bajeti ya matumizi yako ya fedha, usitumie tu fedha kwa sababu unazo, bali weka bajeti na ifuate hiyo.
  3. Usikope fedha kwa ajili ya matumizi, ni kuchagua kupoteza fedha.
  4. Kwenye kila kipato unachoingiza, sehemu ya kumi hupaswi kuitumia kabisa, hivyo ni fedha unayojilipa kwa ajili ya uwekezaji wako wa baadaye.
  5. Usishindane na watu wengine wala kujilinganisha na yeyote kwenye mali, mavazi na hata maisha.
  6. Fanya tahajudi rahisi kabla hujanunua kitu. Kabla hujalipia jiulize je unachotaka kulipia ni hitaji la msingi au anasa. Hii itakuepusha kufanya manunuzi yasiyo muhimu.
  7. Fanya mfungo wa matumizi. Kwa mwezi mmoja, usinunue kabisa kitu ambacho siyo cha msingi. Jizuie kabisa kununua chochote ambacho siyo lazima kwa kipindi cha mwezi mzima, kisha ona jinsi maisha yako yatakuwa bora zaidi.
  8. Wekeza akiba yako kwenye maeneo ambayo yanazalisha zaidi baadaye.
  9. Usinunue vitu ambavyo thamani yake inashuka kadiri muda unavyokwenda.
  10. Ongeza kipato chako kwa kuwa bora zaidi kwenye kile unachofanya, toa huduma bora zaidi, wahudumie wengi zaidi na utaweza kuongeza kipato zaidi.

No comments:

Post a Comment