Tuesday, June 25, 2019

SABABU TANO ( 5 ) ZINAZOUA BIASHARA NYINGI KUKUA

(1). MMILIKI  WA  BIASHARA.
Mmiliki wa biashara ni kikwazo cha kwanza kabisa kwenye ukuaji wa biashara. Pale ambapo biashara inamtegemea mmiliki wa biashara hiyo kwenye kila kitu haiwezi kukua. Kama mwanzilishi wa biashara ndiye anayetegemewa kufanya kila kitu kwenye biashara, biashara haiwezi kukua.
Ili biashara kukua lazima mmiliki aweze kujitofautisha na kujitenganisha na biashara hiyo. Ajenge biashara ambayo inaweza kujiendesha yenyewe bila ya uwepo wake.

(2). KUKOSA  WATEJA  WAPYA.
Biashara inakua kwa kutengeneza wateja wapya kila wakati. Biashara nyingi zimekuwa hazina mfumo mzuri wa kutengeneza wateja wapya kila wakati. Hivyo wanaendelea kuwa na wateja wale wale na hilo linakuwa kikwazo kikubwa kwenye ukuaji.
Ili biashara ikue lazima iwe inatengeneza wateja wapya kila wakati. Wateja wapya ndiyo wanaoleta ukuaji wa biashara.

 ( 3 ). KUKOSA   WAFANYAKAZI  BORA.
Wafanyakazi wa biashara ndiyo wanaoweza kuikuza au kuiangusha. Biashara nyingi hazina wafanyakazi sahihi na hilo limekuwa linazizuia biashara hizo kukua.
Wafanyabiashara wengi hawana mfumo mzuri wa kuajiri watu sahihi kwenye biashara zao na hilo limekuwa linawagharimu kwenye ukuaji. Ili biashara ikue, inahitaji kuwa na wafanyakazi bora ambao wanaweza kutekeleza majukumu yao vizuri.

 ( 4 ). MZUNGUKO  HASI  WA   FEDHA.
Fedha ndiyo damu ya biashara, mzunguko wa fedha ukiwa vizuri biashara inakua, ukiwa vibaya biashara inakufa.
Biashara nyingi zinazokufa zina mzunguko hasi wa fedha, ikiwa na maana kwamba matumizi ya biashara ni makubwa kuliko mapato.
Ili biashara ikue, inahitaji kuwa na mfumo bora wa kudhibiti mzunguko wa fedha ili uwe chanya. Mapato yawe makubwa kuliko matumizi.

 ( 5 ). MAUZO  YASIYOTOSHELEZA.
Mauzo ndiyo injini au moyo wa biashara. Mauzo ndiyo yanayosukuma mzunguko wa fedha kwenye biashara. Bila ya mauzo hakuna biashara.
Biashara nyingi zimekuwa hazina mauzo ya kutosheleza kuzalisha mapato yanayoiwezesha biashara hiyo kujiendesha kwa faida.
Biashara hizo hazina mfumo bora wa masoko ambao unawezesha mauzo kuwa mazuri na yanayoiwezesha biashara kujiendesha yenyewe.
Rafiki, hizi ndizo sababu tano kubwa zinazozuia biashara nyingi kukua, ukizikabili sababu hizi tano, biashara yako itaweza kukua sana.

No comments:

Post a Comment