Sunday, June 30, 2019

KWA NINI WENYE UELEWA WA FEDHA SIYO WAZURI KWENYE BIASHARA.

Watu ambao wana uelewa mkubwa sana wa fedha, yaani wahasibu, wanahisabati, wachumi na hata washauri wa mambo ya fedha, huwa siyo wafanyabiashara wazuri. Yaani huwa wakiingia kwenye biashara hawafanikiwi ukilinganisha na wasiokuwa na uelewa mkubwa wa fedha.
Huku watu wasiokuwa na uelewa mkubwa wa fedha, ambao hawajui hata kuandika cheki vizuri, wakiingia kwenye biashara wanafanikiwa sana.
Katika maeneo mengi ya maisha, kadiri mtu anavyokuwa na uelewa mkubwa, ndivyo anavyochelewa kufanya maamuzi. Wale wenye uelewa mdogo, wanafanya maamuzi haraka, lakini wenye uelewa mkubwa wanahusisha mambo mengi kwenye maamuzi na hilo linawachelewesha kufikia maamuzi.
Inapokuja kwenye fedha, wasiokuwa na uelewa mkubwa kwenye fedha wanatumia hesabu za aina tano tu kwenye mambo ya kifedha, kujumlisha, kutoa, kugawanya, kuzidisha na asilimia. Ni hesabu hizo tu zinazotosha kuendesha biashara yenye mafanikio.
Wakati wale wenye uelewa mkubwa wa fedha wanakuwa na hesabu nyingi zaidi wanazotumia kwenye maamuzi, mfano, makadirio (projections), uwezekano (probaility), hatari (risk) na nyingine nyingi katika kufanya maamuzi, kitu ambacho kinawachelewesha na hata maamuzi wanayofanya yanakosa uhalisia.
Kama wewe una uelewa mkubwa wa kifedha na unataka kufanikiwa kwenye biashara, kubali kuweka sehemu ya uelewa wako pembeni na uendeshe biashara kwa  vitendo na siyo nadharia.
Unaposoma taarifa za kifedha, angalia zile hatua unazoweza kuchuka ili kukuza biashara yako sasa badala ya kuhangaika na vitu vya kufikirika.
Ukishajua MAGAZIJUTO basi una maarifa ya kifedha ya kukutosha kufanikiwa kwenye biashara yako. Muhimu ni kuzijua namba zako muhimu kwenye biashara kama masoko, mauzo, gharama za kuendesha biashara, faida na mtaji ili uweze kuendesha biashara yenye mafanikio makubwa.

No comments:

Post a Comment