Friday, April 26, 2019

JIWEKE KWENYE VIATU VYA MWINGINE HUTAKUWA NA SABABU YA KUUMIZWA NA CHOCHOTE TOKA KWA WENGINE


Njia ya kuondokana na msongo na kupata utulivu kwenye maisha yako ni kujiweka kwenye viatu vya wengine, kukaa kwenye nafasi ya mwingine ili kuweza kuelewa kwa nini mtu amefanya kile ambacho amefanya.

Chanzo kikubwa cha hasira, msongo na hata migogoro kwenye maisha yetu ni mahusiano yetu na wengine. Pale wengine wanapofanya vitu ambavyo hatukutegemea wafanye, tunapatwa na hasira na msongo. Tunaona kama wamefanya kwa makusudi au wamepanga kutuumiza kwa namna fulani.

Lakini mara nyingi sana watu wanafanya vitu kwa nia njema, hasa kwa upande wao. Ni wachache sana ambao wanafanya kitu kwa makusudi ili kumuumiza mtu mwingine. Ukitaka kuelewa kwa nini mtu amefanya kile alichofanya, jaribu kwanza kujiweka kwenye nafasi yake.

Kila mtu huwa ana sababu nzuri ya kufanya kile ambacho amefanya, iwe ni kizuri au kibaya kwako. Ukichukua nafasi ya kuelewa sababu hiyo, hasa kwa kujiweka kwenye nafasi yako, utagundua huna sababu ya kuwa na hasira au msongo. Kwa sababu huenda na wewe ungekuwa kwenye nafasi kama yake ungefanya kama alivyofanya yeye.

Tambua kwamba watu wana mitazamo tofauti, vipaumbele tofauti, uelewa tofauti na hata imani tofauti. Ukichukua nafasi ya kuelewa hayo kuhusu wengine, utaona huna sababu ya kuumizwa na chochote ambacho wengine wanafanya.

No comments:

Post a Comment