Monday, July 1, 2019

VIPANDE VIKUU VINNE VYA BIASHARA YENYE MAFANIKIO.

(1). WATEJA.
Wateja ndiyo kipande cha kwanza muhimu sana cha biashara yako. Kama hakuna wateja basi hakuna biashara. Lazima uchague biashara yako inakwenda kuwahudumia watu gani, wanaopatikana wapi na unawafikiaje. Biashara lazima ijenge wateja ambao wanaotegemea kwa kile inachofanya.

Unapoingia kwenye biashara anza na kitu ambacho tayari watu wanajihitaji, hivyo wewe unakuja na suluhisho na kuhakikisha watu wanajua uwepo wako kwenye biashara hiyo. Hivi ndivyo unavyoweza kutengeneza wateja wa biashara yako.

(2).  MAHITAJI  YA  WATEJA.

Ukishachagua aina ya wateja ambao biashara yako inawahudumia, unapaswa kujua yale mahitaji yao ya msingi. Yale mahitaji yanayowasukuma kununua kile ambacho wewe unauza. Ukishayajua mahitaji hayo, jipange kuyatimiza kwa namna ambayo hakuna mfanyabiashara mwingine anayeweza kuyatimiza hivyo.

Kuna vitu viwili muhimu sana unapaswa kujua kuhusu mahitaji ya wateja wako, hofu na tamaa. Wateja wa biashara yako wanafanya maamuzi kwa kutumia hisia hizo mbili, labda wana tamaa ya kupata kitu fulani au wana hofu ya kupoteza kitu fulani. Jua hisia hizo mbili za wateja na zitumie katika mauzo.

(3). NAFASI  YAKO  KATIKA  SOKO.

Biashara yoyote unayofanya, kuna nafasi ambayo upo kwenye soko, unaweza kuwa ndiyo namba moja yaani wateja wanakufikiria wewe kwanza au ukawa haupo kwenye namba za juu, yaani wateja hawakufikirii kabisa. Ili kukuza biashara yako, unapaswa kuwa kwenye nafasi ya juu kwenye soko lako. Unapaswa kuwafanya wateja wako wakufikirie wewe kwanza inapokuja kwenye mahitaji yao.

Matangazo, alama za kibiashara, rangi za kibiashara, kauli mbiu na hata utamaduni wa tofauti wa biashara yako ni vitu vinavyowafanya wateja wakukumbuke na kukufikiria muda mrefu. Tengeneza picha ya tofauti ya biashara yako ambayo inawafanya wateja wakufikirie wewe mara zote.

(4). UBOBEZI  WA   BIASHARA   YAKO.

Je biashara yako imebobea kwenye nini? Biashara yako inajulikana kwa kipi? Je ni kitu gani wateja wanapata kwako ambacho hawawezi kupata kwa wafanyabiashara wengine?

Hayo ni maswali muhimu ya kupima ubobezi wa biashara yako. Biashara iliyobobea kwenye kile inachofanya ndiyo biashara ambayo inapata mafanikio makubwa sana.

Jua ni aina gani ya biashara unayofanya, na kipi cha tofauti unachotoa kwa wateja wako kisha kazana kutoa kitu hicho kwa namna ambayo wateja hawawezi kupata sehemu nyingine na utaweza kufanikiwa sana kwenye biashara unayofanya. Bobea kwenye vitu vichache na hilo litakufanya kinara kuliko kung’ang’ana kufanya vitu vingi.

No comments:

Post a Comment