Tuesday, July 23, 2019

PIMA KILA KITU.

Kila hatua unayochukua kwenye biashara yako, unapaswa kuipima, la sivyo hutaweza kujua kama inaleta matokeo sahihi au la. Usiendeshe biashara yako kwa kubahatisha, badala yake iendeshe kwa kupima kila unachofanya na kisha kufanya maamuzi sahihi kutokana na matokeo unayoyapata baada ya kupima.
Kwenye biashara, mara nyingi unachotaka wewe siyo ambacho soko linataka, unachopenda wewe siyo ambacho soko linapenda. Hivyo acha kujifikiria wewe na angalia soko linapenda nini kisha lipe.
Kama unaendesha matangazo, pima matangazo hayo kwa kutumia njia mbalimbali kama kutumia vichwa vya habari tofauti, kutumia vyombo vya habari tofauti, kutoa ofa tofauti, kutumia bei tofauti na hata kutoa ofa tofauti. Kisha pima matokeo unayopata kwa kila njia unayotumia na ile inayoleta matokeo mazuri ndiyo inakuwa njia kuu.
Kila unachofanya kwenye biashara yako, unapaswa kukipima na kujua matokeo yake. Na hata baada ya kupata matokeo bora kabisa na kuchagua njia kuu, bado unapaswa kuendelea kupima kadiri unavyokwenda ili uweze kujua matokeo unayopata na kama kuna njia bora zaidi basi itumike hiyo.
Unapokuwa unapima, unapaswa kuanza kwa hatua ndogo na ukishapata matokeo basi unakwenda kwenye hatua kubwa. Kwa mfano kama unajaribu tangazo, anza kwa kuwafikia watu wachache kisha ukishaona njia bora ndiyo unapeleka tangazo hilo kwa watu wengi zaidi.

No comments:

Post a Comment