Monday, July 15, 2019

USIOGOPE KUWAAMBIA WATU WAKULIPE.

Watu wengi wanaofanya biashara za huduma, hasa za ushauri au mafunzo, huwa wanaanza kutoa huduma hizo bure ili watu wawajue. Ni vigumu sana kuanza kwa kuwachaji watu fedha ndiyo uwashauri au kuwafundisha mambo mbalimbali.
Hivyo mtu anapoanza kutoa huduma zake bure, watu wengi wanamfuatilia na kujifunza au kunufaika na huduma hizo kama ni za ushauri au nyinginezo.
Sasa mtu anaweka juhudi kubwa kutengeneza wafuasi wengi, akiwa na lengo kwamba watu wanaomfuatilia wanapokuwa wengi na wengi zaidi kuhitaji huduma zake, basi anaweza kuwatoza ada na kutengeneza kipato.
Lakini unapofika wakati wa kuwaambia watu wakulipe ili kuendelea kupata huduma ambazo umekuwa unawapa bure, wengi huwa wanaogopa. Wengi wanajenga hofu hii pale wanapoanza kuwaambia watu kuhusu malipo na watu hao wakawaambia hawakutegemea kulipia ushauri au mafunzo yanayotolewa.
Watu wengi ambao wamekuwa wananufaika na mafunzo hayo ya bure watapinga sana pale mtu aliyekua anatoa mafunzo hayo bure anapoanza kutoza ada. Na hili limekuwa linawafanya wengi kushindwa kuendelea na huduma zao na hivyo huduma hizo zinakufa.
Nikuambie leo rafiki yangu, kama unaendesha huduma yoyote ile, iwe ni ushauri, uandishi, ukocha, au huduma ya kiimani, lazima ujue kwamba ili huduma hiyo iendelee unahitaji njia ya kukuingizia kipato. Hivyo basi usiogope kuwatoza watu fedha pale wanapohitaji huduma zaidi kutoka kwako.

No comments:

Post a Comment