Tuesday, July 23, 2019

HATUA MBILI ZA KUONGEZA KIPATO CHAKO -----------"Elimu Ya Msingi Ya Fedha "

Rafiki yangu mpendwa, moja ya vitu ambavyo nimekuwa nakusisitizia sana wewe rafiki yangu ni kuwa na vyanzo mbadala vya kukuingizia kipato. Hii ndiyo njia pekee kwako kuweza kupata uhuru kamili wa maisha yako.
Kama kipato chako kinategemea mtu mmoja au wachache basi haupo huru, utalazimika kufanya kile ambacho anayedhibiti kipato chako anakutaka ufanye, hata kama hutaki kukifanya au unaona siyo sahihi kufanya.
Mfano unapokuwa umeajiriwa na chanzo pekee cha kipato chako ni mshahara unaopata kwenye ajira hiyo, unajikuta unakuwa chini ya mwajiri wako, kufanya chochote anachotaka hata kama kwa upande wako siyo kitu sahihi au muhimu kufanya.
Hivyo ili kupata uhuru kamili, ili kupata mafanikio makubwa kwenye maisha yako, unapaswa kuwa na vyanzo tofauti, kipato chako kusitegemee mtu mmoja au watu wachache.
Zipo njia nyingi sana za kuongeza njia za kuingiza kipato na hatimaye kuongeza kipato chako. Lakini njia zote hizi tunaweza kuzigawa kwenye hatua mbili, ambayo inarahisisha sana uchukuaji hatua wa mtu katika kuongeza kipato.
Hatua ya kwanza; ongeza thamani zaidi pale ulipo sasa.
Hatua ya kwanza ya kuongeza kipato chako ni kuongeza thamani zaidi pale ulipo sasa. Hapa huhitaji kuanza kufanya kitu kipya, bali unaendelea kufanya kile unachofanya sasa, lakini kwa viwango vya juu zaidi ambavyo vinakuwezesha kutengeneza kipato zaidi.
Kama una biashara hapa unakazana kuwahudumia vizuri zaidi wateja ambao tayari unao, kuongeza wateja wapya na kuwapa vitu vipya ambavyo wateja wanahitaji lakini kwako havipatikani.
Kama upo kwenye ajira ni kuongeza thamani unayotoa kwenye ajira hiyo, kwa kuchukua majukumu mengi na makubwa, kufanya kazi kwa muda mrefu zaidi na kufanya kazi yako kwa viwango vya juu zaidi. Japokuwa kwenye ajira kuna ukomo, bado ni sehemu ya kuanzia ili kuondoka kwenye utumwa huo.
Hatua hii ni muhimu sana kwa kila mtu kuitumia kwa sababu haihitaji uwe na rasilimali za ziada. Mfano watu wengi wamekuwa wanasema wangekuwa na fedha wangeanzisha au kukuza zaidi biashara walizonazo. Kwa kuwa hawapati fedha wanazotaka, basi wanabaki vile walivyo. Kama kila mtu angefanyia kazi hatua hii ya kwanza na kufanya zaidi pale alipo sasa, wangeweza kutengeneza kipato zaidi na kwenda kufanya kile hasa wanachotaka kufanya.
Hatua ya pili; fanya kitu cha tofauti.
Hatua ya pili kwenye kuongeza kipato chako ni kufanya kitu cha tofauti na unachofanya sasa. Hapa ndipo unakwenda kuanza biashara mpya kama huna biashara au kuanza biashara ya tofauti na ile unayofanya sasa au kwenye eneo tofauti na unalofanyia biashara sasa.
Hii ni hatua muhimu na unayopaswa kuichukua kwa umakini, kwa sababu inahitaji maamuzi unayokwenda kuyasimamia kwa muda mrefu. Wengi wamekuwa wanachukua hatua hii bila ya kujitathmini vizuri na kujikuta wametengeneza gereza zaidi kwa kile kipya wanachokwenda kufanya.
Mfano mtu anakwenda kuanzisha biashara mpya wakati biashara anayofanya sasa bado hajaweza kuiendesha vizuri, kinachotokea ni biashara zote mbili kufa. Au mtu anatoka kwenye ajira moja na kwenda kwenye ajira nyingine, kitu ambacho hakibadilishi sana hali yake ya maisha.
Kama unataka kuongeza kipato chako, anzia hapo ulipo sasa na chagua kitu cha kufanya zaidi. Kama ni biashara fikiria wateja wapya unaoweza kuafikia, huduma na bidhaa mpya unazoweza kuwapatia na ubora wa huduma unazotoa. Kama ni kwenye ajira angalia majukumu makubwa zaidi unayoweza kufanyia kazi, muda zaidi unaoweza kuweka kwenye kazi zako na thamani kubwa zaidi unayoweza kuzalisha. Ukishaweka juhudi kubwa kwenye kile unachofanya sasa, ndipo sasa unaweza kufanya kitu cha tofauti.
Kila mtu ana fursa nyingi za kufanya zaidi kwenye kile anachofanya sasa, hebu anza kutumia fursa hizi ili kuongeza kipato chako zaidi.

No comments:

Post a Comment