Tuesday, July 23, 2019

TATIZO HUJUI UNACHOTAKA.

Pata picha, unataka kuwa na safari, unaondoka nyumbani umebeba mizigo yako na kuelekea kituo cha mabasi. Unakaribishwa na kuulizwa unaenda wapi, unasema popote basi linapokwenda. Je unafikiri basi hilo litakupeleka wapi?
Unaweza kushangaa na kujiuliza inawezekanaje mtu mwenye akili timamu aende kituo cha basi kwa ajili ya safari halafu hajui anakokwenda!
Kabla hujaendelea kushangaa, hebu jiulize kwanza maswali haya muhimu; unakwenda wapi na maisha yako? unakwenda wapi na biashara unayofanya? Unakwenda wapi na kazi uliyonayo? Unakwenda wapi na mahusiano uliyonayo?
Kwa maneno mengine, miaka 5, 10, 20 na zaidi ijayo unajiona wapi? Kama huwezi kutoa jibu moja kwamba unajiona wapi katika vipindi hivyo, kwa hakika huna tofauti na anayeenda kwenye kituo cha mabasi huku akiwa hajui anakwenda wapi.
Na hivi ndivyo watu wengi wanavyoendesha maisha yao, wanakazana sana kufanya chochote wanachofanya, lakini hawajui wanakwenda wapi, hivyo wanafanya leo kama walivyofanya jana, huku kesho ikiwa haipo kwenye mawazo yao kabisa.
Kama mpaka sasa maisha yako huyaelewi, kama umeshajaribu kazi na biashara nyingi lakini bado huoni matokeo mazuri, tatizo lako ni moja, hujui nini hasa unachotaka, hujui wapi hata unakotaka kufika.
Na kama hutachukua hatua ya kwanza muhimu ya kujua kwanza nini unachotaka na wapi unapotaka kufika, hutaweza kuwa na maisha bora. Kila siku utaishia kuyumbishwa kama bendera inayopeperushwa na upepo. Watu watakuja kwako na kila aina ya fursa mpya na utahangaika nazo, na hakuna hata moja itakayokusaidia kufanikiwa.
Jua kwanza ni nini hasa unachotaka, jua ni wapi unakotaka kufika, kisha weka juhudi zako zote katika kufika kule unakotaka kufika. Kuwa kiziwi na kipofu kwa vitu vingine vyote visivyohusiana na kile unachotaka. Usiwe mtu wa kukimbizana na kila aina ya fursa mpya, badala yake weka nguvu kubwa kufika kule unakotaka kufika.
Kujua unachotaka na kuweza kukipata, anza kwa kujiuliza maswali haya muhimu sana;
  1. Mimi ni nani?
  2. Ni nini ninachotaka?
  3. Ni nini kinanipa furaha?
  4. Nini hakinipi furaha?
  5. Uimara wangu uko wapi?
  6. Udhaifu wangu uko wapi?
  7. Ni mchango gani mkubwa naweza kutoa kwa wengine kupitia maisha yangu, kazi yangu, biashara yangu na mahusiano yangu?
Ukijiuliza na kujipa majibu sahihi kwenye maswali hayo saba, na kufanyia kazi majibu hayo, utaweza kupata chochote unachotaka kwenye maisha yako.

No comments:

Post a Comment