Tuesday, July 23, 2019

PATA HASARA MWANZONI KUPATA FAIDA MBELENI.

Kikwazo kikubwa cha ukuaji wa biashara imekuwa kushindwa kumshawishi mteja kununua kwa mara ya kwanza. Hivyo hapa ndipo unapaswa kuweka nguvu zako kubwa.
Kwa sababu tayari una mkakati bora wa kutoa thamani kubwa kwa wateja wako, hawataweza kuona hilo mpaka pale watakaponunua kwako kwa mara ya kwanza.
Swali ni je utawezaje kumshawishi mteja kununua kwako kwa mara ya kwanza, mteja ambaye hajawahi kununua kabisa kwako?
Jibu ni kwa kuondoa vizingiti au vikwazo vyote ambavyo vinamzuia mteja kwa sasa. Kikwazo kikubwa kabisa kimekuwa ni hatari ambayo mteja anaona iko mbele yake, ya kupoteza fedha zake iwapo anachonunua hakitamfaa.
Hatua za kuchukua ni kuwa na mkakati wa kupata hasara mara ya kwanza mteja anaponunua kwako, lakini kwa kuwa utamhudumia vizuri na atarudi tena na tena, basi utaweza kutengeneza faida siku za mbeleni.
Hapa unaweza kutoa zawadi kwa mteja anaponunua kwa mara ya kwanza au kuwa na punguzo fulani. Vyote ni kumfanya achukue hatua ya kununua kwako kama kukujaribu, na akishanunua kwako mara moja, ataendelea kununua.
Zawadi au punguzo unalompa mwanzo linaondoa kabisa ile faida ambayo ungeweza kuipata, lakini anapokuja kununua tena, unatengeneza faida.
Chukua mfano unauza kitu ambacho bei yake ni elfu 10 na faida unayopata ni elfu 3. Mteja ananunua kitu hicho kila mwezi mara moja na unaweza kwenda naye kwa angalau miaka mitatu. Sasa unaweza kumpa mteja wako zawadi au punguzo la hiyo elfu tatu na hata zaidi anaponunua kwa mara ya kwanza. Lakini atakapoendelea kununua, utarudisha faida hiyo na zaidi.
Kabla ya kuchukua hatua hii unapaswa kukokotoa kiasi cha faida unachopata na muda ambao mteja atanunua ili uweze kupata matokeo mazuri.

No comments:

Post a Comment