Sunday, August 18, 2019

UNAHITAJI FALSAFA YA MAISHA.

Zamani za kale, wakati binadamu wanajifunza kuwa na makazi ya kudumu, watu walijenga nyumba zao bila ya misingi. Lakini walijifunza somo moja kubwa sana, kwamba kipindi cha dhoruba mbalimbali kama mvua, kimbunga na tetemeko, nyumba hizo zilibomoka haraka sana. Hivyo wakajifunza kwamba ili nyumba iwe imara na idumu, basi inapaswa kuanza kujengwa kwa msingi imara. Na mpaka sasa wahandisi wote wanajua kwamba nyumba imara inaanza na msingi imara. Na kadiri nyumba inavyopaswa kuwa kubwa, ndivyo msingi unavyopaswa kuwa imara zaidi. Mfano, msingi wa nyumba ya kawaida hauwezi kufanana na msingi wa nyumba ya ghorofa.
Hivi pia ndivyo ilivyo kwenye maisha yetu. Kwenye maisha tunakutana na dhoruba mbalimbali. Kuna kuugua, kuvunjika kwa mahusiano, kufukuzwa kazi, kufilisika kibiashara, kufa kwa watu wetu wa karibu na hata sisi wenyewe kufa. Dhoruba hizi huwa zina madhara tofauti kwa watu tofauti. Kuna watu wanapokutana na dhoruba za maisha zinawayumbisha sana na kuvuruga kabisa maisha yao. Lakini wapo wengine ambao wanakutana na dhoruba kali za maisha lakini maisha yao hayayumbi.
Kinachowatofautisha watu hao wa aina mbili ni msingi ambao wamejijengea. Kwenye nyumba tumeona msingi wa kuanza, kwenye maisha yetu, msingi muhimu sana ni falsafa ambayo mtu anakuwa nayo juu ya maisha. Falsafa unayokuwa nayo, ndiyo inapima kiasi gani dhoruba unazokutana nazo kwenye maisha. Kama huna falsafa unayoiishi na kuisimamia, dhoruba ndogo kama biashara kufilisika inatosha kukuvuruga kabisa. Lakini kama una falsafa unayoiishi, dhoruba kubwa kama kuhukumiwa kifo, inakufanya uwe imara na kuyafurahia maisha yako mpaka dakika ya mwisho.
Hii ni kukuambia wewe rafiki yangu kwamba unapaswa kuwa na falsafa ya maisha yako, falsafa ambayo unaitumia kama msingi wako wa kufanya maamuzi na kuendesha maisha yako. Falsafa ambayo itakuwezesha kukabiliana na dhoruba za maisha, ambazo kadiri siku zinavyokwenda zinazidi kuwa kali zaidi.
Dini zilipaswa kuwa msingi wetu kwenye changamoto hizi za maisha, lakini dini nyingi zimesahau jukumu hilo, na badala yake zimekuwa sehemu ya kuwapa watu hofu zaidi ya maisha kuliko matumaini. Dini zimekuwa zinaweka nguvu kubwa kwenye kuwaandaa watu kwa maisha yajayo (baada ya kifo) kuliko maisha waliyonayo sasa. Japokuwa unahitaji maandalizi ya maisha yajayo (kulingana na imani yako), lakini kitu muhimu sana unachohitaji ni maandalizi ya maisha unayoishi sasa, maana hayo ndiyo yanayokujenga au kukubomoa.
Kwa kuwa dini zimeshindwa kufanya kazi ambayo tulitegemea zifanye, kutujenga na kutuandaa kwa maisha ya sasa na kuweza kukabiliana na dhoruba tunazokutana nazo kwenye maisha yetu ya kila siku, basi linabaki kuwa jukumu la kila mmoja wetu kuwa na falsafa ya maisha, ambayo ataitumia kuendesha maisha yake.
Kukaa chini na kutengeneza falsafa yako mwenyewe ni kazi kubwa, inakuhitaji ujaribu na kukosea vitu vingi, kitu ambacho huna muda wala nguvu za kufanya, maana changamoto zinazokukabili ni nyingi.
Hivyo suluhisho ni wewe kujifunza falsafa zilizopo, na kisha kuchagua ile ambayo itakufaa wewe katika kuendesha maisha yako.
Zipo falsafa nyingi ambazo zinatokana na wanafalsafa mbalimbali kama Socrates, Plato, Aristotle, Epicurus, Zeno na wengineo.

No comments:

Post a Comment