Sunday, August 18, 2019

HAKUNA ANAYEKOSEA KWA MAKUSUDI.

Upo msingi wa ustoa ambao utakuwezesha kuishi maisha yako kwa utulivu bila ya kujali wengine wanasema au kufanya nini. Moja ya vitu ambavyo vinatusumbua sana zama hizi ni mambo ambayo wengine wanasema au wanafanya. Huwa tunayaruhusu yatuumize, tukiamini kwamba watu hao wanafanya mambo hayo kwa makusudi ili kutuumiza.
Lakini wastoa wanatuambia kwamba, watu wanaofanya mambo ambayo yanatuumiza, hawafanyi hivyo kwa makusudi, bali wanafanya hivyo kwa sababu hawajui kulicho sahihi kufanya. Hivyo hupaswi kuumia kwa sababu yao, badala yake unapaswa kuwaonea huruma na kuona kama kuna namna unaweza kumsaidia ili asiendelee kukosea.
Mfano mzuri ni pale mtoto mdogo anapokupiga kofi, je utarejesha kwa kumpiga kofi pia? Je utakasirika? Je utamnunia? Je utasema amekudharau? Majibu hapo ni hapana. Lakini vipi mtu mzima mwenzako akikupiga kofi? Hapo mambo yanabadilika, unaona amekudharau, utataka kulipiza, utakasirika na hata kumnunia. Lakini kama utachukulia mtu huyo amekupiga kofi kwa kutokujua au kwa bahati mbaya, hutapata hisia hizo.
Hivyo cha kujifunza hapa, tusikimbilie kuhukumu pale watu wanapofanya vitu kwamba ni vibaya au wamedhamiria kutuumiza. Badala yake tuchukulie kwamba watu hao hawajui wanachofanya au wamefanya kwa bahati mbaya, na hilo litatuzuia sisi kuumia.
Mfano mzuri ni kwenye wizi au utapeli, mtu akikuibia, badala ya kuumia, unapaswa kumwonea huruma, kwa sababu kwanza hajui njia sahihi ya kutengeneza kipato ambayo itampa maisha ya utulivu na pili, kwa tabia yake hiyo, ataishia jela au kaburini, maana ataiba akamatwe na wananchi wenye hasira kali hadi kufa, au apelekwe polisi na baadaye kufungwa. Unaona jinsi ambavyo unaondoka kwenye upande wa lawama na kuwa upande wa utulivu!

No comments:

Post a Comment