Sunday, August 18, 2019

KUHUSU KIFO NA KUJIUA.

Moja ya vitu ambavyo vimekuwa vinawasumbua watu wengi n kifo. Wote tunajua kuna siku tutakufa, lakini hatutaki kufikiria wala kupata picha ya kifo chetu. Kadhalika tunajua wale watu wa karibu kwetu, ambao tunawapenda sana kuna siku watakufa. Lakini huwa hatufikirii wala kupata picha ya vifo vyao. Kinachotokea ni tunakutana na vifo ghafla na vinatuumiza sana.
Wastoa wana maeneo matatu ya kuzingatia kuhusu kifo.
Kwanza ni kifo chako mwenyewe, ambapo wastoa wanasema hakuna sababu ya kukiogopa kifo, kwa sababu ni sehemu ya maisha yako na kinaweza kutokea muda wowote. Hivyo wakati wowote unapaswa kuwa tayari kukikabili kifo. Inapofanya jambo lolote, lifanye kama ndiyo mara ya mwisho kwako kulifanya, kama vile kifo kinakusubiri. Kwa njia hii hutaahirisha jambo lolote muhimu na utafanya mambo kwa usahihi. Wastoa wanasema kama unaogopa kifo, maana yake bado hujaanza kuishi. Lakini kama utachagua kuishi maisha yako, kifo hakitakusumbua, kwa sababu wakati wowote utakuwa tayari.
Mbili ni vifo vya watu wa karibu kwetu. Wazazi wetu, watoto wengu, wenzi wetu na ndugu wengine ni watu tunaowapenda na kuwajali sana. Inapotokea wamefariki dunia, huwa tunaumia, tunalia na kuhuzunika sana. Kwa wengine vifo vya watu wao wa karibu huwa vinawavuruga sana, vinaishia kuwapa magonjwa ya akili. Wastoa wanatuambia vifo vya watu wa karibu kwetu vinatuumiza kwa sababu vinatukuta hatujajiandaa. Wanatuambia kila unapoongea au kukutana na mtu wako wa karibu, jiambie kimoyomoyo kwamba hiyo ni mara ya mwisho kukutana naye. Epictetus anatuambia kila unapombusu mtoto wako, jiambie unambusu mtu ambaye anaweza kufa muda wowote. Kwa kuchukulia hivi, utajali sana, kwa sababu unajua mtu anaweza kupotea muda wowote, na hilo linapotokea utaumia, lakini halitakuvuruga, kwa sababu ni kitu ambacho ulijua kitatokea, a pia ulishatumia fursa ulizokuwa nazo kabla mtu huyo hajafariki.
Tatu ni kujiua. Wastoa wa zamani, wengi waliishia kujiua wenyewe au kupewa adhabu ya kifo. Hii ilitokana na tawala za kidhalimu zilizokuwepo enzi hizo na wastoa hawakuogopa kuzisema na kuzipinga. Hilo liliwafanya wawekwe vizuizini, kufukuzwa au kuhukumiwa kufa. Wastoa walikuwa wakipokea adhabu hizo bila ya kuruhusu ziharibu utulivu wao wa ndani. Mfano mstoa alipohukumiwa kifo, alikipokea kama sehemu ya maisha na kusimamia misingi yake. Lakini pia wapo wastoa ambao walipofika mwisho wa maisha yao, yaani uzee na kuona wameshakamilisha jukumu lao la maisha, basi walijiua. Hii ni dhana ambayo ilikuja kupotea, lakini zama hizi imeanza kurudi. Wapo watu ambao wanachagua kuyakatisha maisha yao kwa sababu mbalimbali. Hapa hatuzungumzii wale wanaojiua kukimbia majukumu au matatizo waliyosababisha, bali wale ambao wanaona imetosha sasa na wanataka kupumzika. Hilo pia ni zoezi la kistoa.

No comments:

Post a Comment