Sunday, August 18, 2019

FALSAFA YA USTOA NA UTAJIRI.

Kwenye Falsafa ya Ustoa, vitu vimegawanyika katika makundi matatu;
Kundi la kwanza ni vitu vizuri kufanya au kuwa navyo (virtues), ambavyo ni vinne; hekima, ujasiri, haki na kiasi.
Kundi la pili ni vitu vibaya kufanya au kuwa navyo (vices), ambavyo ni kinyume na hivyo vizuri, yaani, upumbavu, woga, udhalimu na tamaa.
Kundi la tatu ni vitu ambavyo siyo vizuri na wala siyo vibaya (indifferent), ambavyo hakuna ubaya kuwa navyo, lakini pia hupaswi kujitesa ili kuwa navyo. Hapa vitu vingine vyote kwenye maisha vinaingia hapo, kuanzia afya, kazi, biashara, fedha na kadhalika.
Sasa kwa misingi ya ustoa, wengi hufikiri inawataka wawe masikini, watu wasiojali fedha wala utajiri. Lakini katika historia, moja ya wanafalsafa waliokuwa na maisha mazuri basi ni wastoa. Seneca alikuwa tajiri mkubwa enzi zake na mwanasiasa, Marcus Aurelius alikuwa mtawala wa Roma. Kwa kifupi wastoa walijihusisha na maisha ya kila siku na ya kawaida, wakifanya yale ambayo kila mtu anafanya.
Na hii ni sababu nyingine nzuri kwa nini tunapaswa kuwa wastoa, kwa sababu ni falsafa ambayo haipingi mtu kuwa na fedha, au kujihusisha na mambo mengine, kama tu hayavunji msingi wa wema.
Zipo baadhi ya dini na falsafa ambazo zinawafundisha wafuasi wake kuachana kabisa na mambo ya dunia, kutoa maisha yao kwa ajili ya falsafa au Mungu pekee. Lakini wote tunajua maisha yana mahitaji yake, hutaenda kulipa ada za watoto kwa falsafa, na wala hutaenda dukani kupata chakula kwa kusema wewe ni mwanafalsafa.
Hivyo kwa kuishi kwa falsafa ya ustoa, unakuwa huru kufanya upendacho, ila tu kiwe sahihi kwako na kwa wengine, na pia unakuwa huru kujikusanyia fedha utakavyo, ila tu ufanye hivyo kwa usahihi na kwa manufaa ya wengine pia.
Na kikubwa nilichojifunza ni kwamba ukiishi misingi ya falsafa ya ustoa, una nafasi kubwa ya kuwa tajiri, lakini pia utakuwa huru na utajiri huo. Kwa sababu kwanza utakuwa unafanya kilicho sahihi na kuachana na yasiyo sahihi, pia utaepuka kufanya mambo ambayo yatakupotezea fedha, kwa kudhibiti vizuri hisia zako. Lakini kilicho muhimu zaidi ni kwamba hutafungwa na utajiri wako, hata kama utapoteza kila kitu, bado utabaki imara na maisha yako yataendelea.
Naweza kuhitimisha kwa kusema, Ustoa ni falsafa ya watu wakuu na matajiri, najua unapenda kuwa mkuu, unapenda kuwa tajiri na kuwa huru na maisha yako, hivyo basi, ijue na kuiishi misingi ya ustoa.

No comments:

Post a Comment