Sunday, August 18, 2019

MATAWI MATATU YA FALSAFA YA USTOA.

Falsafa ya ustoa inafananishwa na mti ambao una vitu vitatu ili uweze kuwa mti. Mti una mizizi ambayo inaupa uimara na virutubisho, shina ambalo linahifadhi chakula na kutoa umbo na matawi ambayo yanatengeneza chakula na kuvuta hewa.
Falsafa ya ustoa ina matawi matatu;
Moja ni fizikia (physics), hili ni tawi linalojihusisha na sayansi ya asili, jinsi dunia ilivyo na inavyojiendesha. Hii ndiyo mizizi ya falsafa hii.
Mbili ni maadili (ethics), hili ni tawi ambalo linaipa falsafa hii msimamo, jinsi ya kuishi na kujihusisha na wengine. Hili ndiyo shina la falsafa hii.
Tatu ni mantiki (logic), hili ni tawi ambalo linahusika na kufikiri pamoja na kufanya maamuzi sahihi. Haya ndiyo matawi ya falsafa hii.
Ili maisha yetu yakamilike, lazima tuwe vizuri kwenye maeneo hayo matatu, kuijua dunia na hapa tunapaswa kuwa na ujasiri na kiasi, kuwa na maadili tunayoyaishi ambapo tunapaswa kuwa watu wa haki na mwisho kutumia akili zetu kufikiri, ambapo tutaweza kuwa na hekima.
Ukiona hapo, matawi matatu ya ustoa ambayo ni FIZIKIA, MAADILI NA MANTIKI, ndiyo yanazalisha misingi mikuu minne ya ustoa ambayo ni HEKIMA, UJASIRI, HAKI NA KIASI. Kwa kifupi, falsafa nzima ya Ustoa imejumuishwa kwenye sentensi hiyo.

No comments:

Post a Comment