Sunday, August 18, 2019

FALSAFA YA USTOA

Falsafa ya Ustoa ilianza miaka 300 kabla ya Kristo ambapo Zeno, mwanzilishi wa falsafa ambaye kwa wakati huo alikuwa mfanya biashara alikuwa safarini na chombo chake kikaharibika akiwa Athens Ugiriki. Akiwa hapo Athens, alitembelea maktaba na kuperuzi maandiko yaliyokuwepo, alikutana na mafunzo ya Socrates na yakamvutia sana. Akamuuliza mhusika wa maktaba ile, ni wapi anaweza kuwapata watu ambapo atajifunza zaidi kuhusu falsafa, na hapo akaoneshwa mwanafalsafa Crates na akamfuata, hapo ndipo safari yake ya kujifunza na kuwa mwanafalsafa ilipoanzia.
Zeno alijifunza kupitia Crates ambaye alikuwa kwenye shule ya falsafa inayoitwa Cynics, ambao ni watu ambao hawakujali kuhusu chochote, waliishi maisha kwa wakati waliokuwa nao na walihoji na kutilia mashaka kila kitu.
Baada ya kujifunza kwenye falsafa hii kwa muda, Zeno aliona falsafa ya Cynics ilikuwa na mapungufu, kwa sababu huwezi kupuuza kila kitu kuhusu maisha na ukawa na maisha bora. Hivyo alianzisha shule yake ya falsafa, ambapo alikuwa akifundisha chini ya mti ulioitwa stoa. Na hapo ndipo jina la Ustoa (Stoicism) lilipoanzia.
Tangu kipindi cha Zeno, pamekuwepo wanafalsafa ambao wameiendeleza na kuikuza zaidi falsafa hii ya zeno. Wanafalsafa kama Cato, Musonius Rufus, Seneca, Epictetus na Marcus Aurelius kwa nyakati tofauti waliishi na kufundisha falsafa hii.

No comments:

Post a Comment