Sunday, August 18, 2019

JINSI YA KUKABILIANA NA MABADILIKO MAKUBWA YA MAISHA KIAFYA.

Kuna wakati tunakutana na mabadiliko makubwa kimaisha kwenye afya zetu. mabadiliko haya yanaweza kutuyumbisha sana kama hatuna msingi sahihi tunaouishi. Mfano ni pale mtu anapopata ulemavu wa mwili ambao unaathiri maisha na hata kazi za mtu. Wengi huvurugwa sana na mabadiliko ya aina hii, kitu ambacho hupelekea maisha yao kudorora na hata kufa mapema.
Wastoa wanatupa njia sahihi ya kukabiliana na mabadiliko ya aina hii, kwa kutuambia tunapaswa kufikiria na kutumia kile tulichonacho na siyo kuangalia tumekosa nini. Kama umepata ulemavu wa miguu, kumbuka bado una mikono, macho, masikio, na viungo vingine, ambavyo kama utaweza kuvitumia vizuri maisha yako yatakuwa bora.
Mmoja wa wanafalsafa wa Ustoa, Epictetus, ambaye alikuwa mwalimu bora sana wa falsafa hii, alikuwa mtumwa. Katika maisha yake ya utumwa, aliumizwa na kupata ulemavu wa miguu. Hili lilimpa ulemavu wa maisha, lakini hakuruhusu ulemavu huo uathiri maisha yake, aliangalia mambo gani mengine anayoweza kufanya, kama kujifunza na kufundisha falsafa na siyo kuangalia alichokosa.
Somo muhimu la kuondoka nalo hapa ni usiweke nguvu zako kwenye yale uliyokosa au kupoteza, badala yake weka nguvu zako kwenye yale uliyonayo na jinsi unavyoweza kuyatumia kwa ubora zaidi.

No comments:

Post a Comment