Sunday, May 12, 2019

SUKARI NI SUMU KWENYE MWILI WAKO , EPUKA VYAKULA VYA SUKARI.

Kama kuna kitu kimoja ambacho kila mtu anapaswa kuambiwa na kukielewa ni kwamba matatizo yetu mengi ya kiafya yanatokana na ulaji wa sukari. Kwa kifupi sukari ni sumu kubwa sana kwenye miili yetu. Japo tunaiona tamu na tunaipenda sana, lakini hakuna kinachotuua kama sukari.
Sukari ya kawaida tunayotumia inaitwa sucrose, ndani yake ina sukari rahisi za aina mbili, glucose na fructose. Glucose ndiyo sikari inayotumika kwa urahisi na mwili na hata ubongo katika kuzalisha nguvu. Fructose huwa haitumiki sana kuzalisha nishati, badala yake inageuzwa kuwa mafuta na kuhifadhiwa kwenye mwili. Na aina hii ya sukari rahisi ndiyo inachangia sana kwenye magonjwa ya moyo na mishipa ya damu kama kukomaa na kujaa mafuta kwenye mishipa hiyo kitu kinacholeta shinikizo la juu la damu (presha).
Ubaya zaidi wa sukari uko hapa, unapokula chakula cha sukari au wanga, sukari ni rahisi kumeng’enywa, hivyo muda mfupi baada ya kutumia sukari, kiwango cha sukari kwenye damu yako kinakuwa juu sana. Hali hii inachochea mwili kuzalisha homoni inayoitwa Insulin, ambayo kazi yake ni kuondoa sukari kwenye damu na kuihifadhi kwenye seli za mwili na nyingine kugeuzwa kuwa mafuta kwenye ini. Sasa kwa kuwa sukari imepanda kwa wingi kwenye damu, insulini inayozalishwa inakuwa nyingi pia, kitu ambacho kinapelekea sukari kwenye damu kushuka haraka. Hii inaleta hali ya mtu kujisikia uchovu na kutamani kula kitu cha sukari muda mfupi baada ya kula sukari.
Kama umekuwa unakunywa chai yenye sukari asubuhi, utakuwa unaliona hili mara kwa mara, saa moja baada ya kutumia sukari unajisikia kuchoka choka na unatamani kitu chochote chenye sukari. Hapa ndipo wengi wanakunywa soda au hata kula pipi, ili mradi tu kutuliza lile hitaji la mwili la kutaka sukari ya haraka.
Ndugu  yangu, kama kuna hatua moja ambayo unapasa kuichukua, hata kama utashindwa kuchukua hatua nyingine zozote kwenye ulaji wako, basi ni kuachana kabisa na sukari. Yaani acha kabisa kutumia sukari, na utaupumzisha mwili wako na hali hii ya kutengeneza sumu ambazo zinakuchosha, kukuletea magonjwa na hata kukuzeesha haraka.
Vyakula vya sukari vya kuepuka ni kama ifuatavyo, sukari yoyote unayoongeza kwenye chai au chakula, asali, miwa na juisi yake, matunda yoyote yenye utamu wa sukari, soda, juisi za matunda hata kama ni asili, bia, mvinyo, bidhaa zozote za kiwandani ambazo zimetengenezwa kwa kuongezwa sukari, kama mikate, maandazi na chochote ambacho kimeongezwa sukari.
Nyongeza; usidanganyike na vitu vitamu ambavyo unaambiwa havina sukari, mfano soda za dayati, hizi zina kemikali ambazo ni sumu kwenye mwili wako kama ilivyo sukari. Tofauti yake na soda nyingine ni kwamba hazipandishi sukari kwenye damu, lakini bado ni sumu.
Najua hili litakuwa limekustua sana, kwa sababu vyakula vingi hapo ndiyo unatumia kila siku. Lakini kutumia kila siku au kuzoea haifanyi kuwa sahihi. Tafiti za kisayansi na za lishe zinaonesha wazi kwamba mazoea yetu kwenye ulaji ndiyo kikwazo kwetu kuwa na afya bora. Hivyo tunapaswa kujifunza na kuchukua hatua sahihi ili tuwe na afya bora na maisha bora pia.

No comments:

Post a Comment