Wednesday, May 15, 2019

KWA NINI SUKARI NI MADAWA YA KULEVYA YALIYOHALALISHWA.

Pamoja na madhara makubwa ya kiafya ya utumiaji wa sukari tutakayojifunza hapo chini, sukari haina tofauti kubwa sana na madawa ya kulevya kama kokeini au heroine.
Hii ni kwa sababu matumizi ya sukari yamedhibitishwa kusisimua sehemu za ubongo ambazo zinasisimuliwa na madawa hayo. Pale mtu anapotumia sukari, ubongo unasisimka na kuzalisha homoni inayoitwa dopamine, hii ni homoni ambayo huwa inaleta raha na kumsukuma mtu kurudia tena kile alichofanya.
Hivyo unapotumia sukari, ubongo unazalisha dopamine, ambayo inakufanya ujisikie vizuri na upate utamu wa sukari. Lakini baada ya hapo unasukumwa kutumia tena sukari ili upate utamu zaidi na kujisikia vizuri zaidi.
Hii ndiyo sababu watu wamekuwa wanapata msukumo mkubwa sana wa kutumia kitu chenye sukari, na wakishatumia mara moja hawawezi kuacha, wanatumia tena na tena na tena.
Matumizi haya ya sukari yanaleta hali ya uteja au uraibu ambao ni mgumu sana kuuvunja. Kila mtu anapoona kitu cha sukari akili yake haifikirii kitu kingine chochote bali jinsi ya kupata sukari hiyo. Na anapoonja mara moja, hawezi kujizuia bali atataka tena na tena.
Tafiti zinaonesha pia ya kwamba matumizi ya sukari yamekuwa yanabadili tabia za watu. Muda mfupi baada ya kutumia sukari watu wengi huwa wakorofi, wenye hasira na wasio na subira. Sukari inawapa nguvu za ziada ambazo zinawasukuma kuzitumia kwa njia ambazo siyo sahihi. Mtu anapokuwa na sukari nyingi kwenye mwili huwa kwenye hali ya msongo kama mtu ambaye ametumia kilevi.
Hivyo kwa uwezo wa sukari kusisimua ubongo kama madawa mengine, kitendo cha watu kuwa tegemezi kwenye sukari na kuadilika kwa tabia baada ya mtu kutumia sukari, kunaifanya sukari kuwa kwenye kundi moja na madawa ya kulevya.

No comments:

Post a Comment