Sunday, May 5, 2019

FANYA KAZI NJE YA BIASHARA YAKO.

Kama unataka kufurahia biashara yako, basi unapaswa kufanya kazi nje ya biashara na siyo ndani ya biashara. Kufanya kazi ndani ya biashara ni pale ambapo unakuwa bize na shughuli za kila siku za biashara hiyo, kuuza, kuwahudumia wateja na kuzalisha au kuandaa bidhaa na huduma unazouza. Japokuwa unaweza kuona hilo ni muhimu na hata kupenda sana kulifanya, linakuzuia kuikuza zaidi biashara yako, maana unapofanya kazi ndani ya biashara, unachoka sana na hupati nafasi ya kuona mbali zaidi ya kile unachofanyia kazi kwenye biashara hiyo.
 
Kufanya kazi nje ya biashara yako ni pale ambapo unaiangalia biashara yako kama mtu baki, kuangalia kila kitu kinavyofanyika na kuona uimara na udhaifu wako. Ni sawa na kupanda juu angani kisha kuangalia biashara yako kwa chini, na kutathmini kila kinapofanyika. Unapofanya kazi nje ya biashara, hufikirii yale majukumu ya kila siku ya biashara, bali unaangalia kule ambako biashara inakwenda na uwezo wa kufika huko.
 
Kama unataka biashara yako ikue, lazima uweze kufanya kazi nje ya biashara yako, uweze kuiangalia biashara kama mtu wa pembeni na kupata picha ya pale ilipo sasa na inapoweza kufika.
 

No comments:

Post a Comment