Saturday, February 27, 2021

VYOTE TUNAVYOFIKIRI TUNAMILIKI , HATUVIMILIKI.

Maisha tunayoishi na vyote tunavyopata maishani hudumu nasi kwa muda tu na mwisho huwa tunavipoteza, vinaharibika, vinapoteza thamani na wakati mwingine hufa. Hakuna kitu ambacho kitadumu nasi maisha yote. Hili ni suala la uhalisia na huwa tunaliona ni kweli pale ambapo tunapopoteza zaidi watu wetu wa karibu kwa njia ya kifo. Si kifo pekee kinatufundisha hili kuwa hatutaishi na wanaotuzunguka milele ipo siku watakuwa mbali nasi siku moja ikiwa bado haijatokea.

Umiliki wetu wa watu au vitu ndio chanzo kikubwa cha maumivu ambayo hutokea pindi tunapokuwa tumepoteza hivyo vitu. Utaumia zaidi pale utakapopoteza mtu au vitu ulivyokuwa navyo karibu au kuvitegemea au kufikiri ulikuwa unamiliki maisha yote kumbe si kweli huwa vina ukomo wake kwako na huondoka mbali na wewe. Chochote ulichonacho sasa kitapotea au utakikosa kwa baadaye. Kuanzia uhai wako utafika ukomo, mwili wako utazeeka, wanaokuzunguka watakufa, ajira ulonayo utafika utastaafu, ujana wako utaisha na kupotea. Wakati wa kukoma kwa kila kitu husogea taratibu kama ilivyo muda unapovyoondoka kwa kuanza na dakika, saa, masaa, wiki, mwezi, miezi, mwaka, miaka hadi karne.

Jiondoe katika kuamini kuwa ulichonacho utaweza kukimiliki milele maana kadri muda uendavyo ndivyo nafasi ya kuvipoteza inapokaribia. Una mke, mume au watoto au wazazi unaweza kuishi kama umewamiliki ni wa kwako ila hufika ukomo usimiliki chochote toka kwao. Wanaweza kukimbia, wanaweza kufa wakati wowote ule na wasiwe wako tena. Wewe ni mzazi unaweza fikiria kuwa unamiliki mtoto wako ila kadri muda unavyoenda umiliki wako unapungua kwake. Mtoto anaweza kuwa mbali na wewe akaanzisha familia yake, anaweza kuondoka na kuishi ng’ambo asikumbuke nyumbani tena au akapoteza maisha kabisa. Umiliki wa chochote unaweza kutengeneza manung’uniko au maumivu pale ambapo vitakapopotea na hukuwa unajua kuwa vitapotea.

Kama falsafa ya Ustoa inavyotufundisha kuwa imara na kuwa tayari kwa chochote kitakachojitokeza tusishangazwe nacho maana tayari tunajua hakuna kitakachodumu milele, chochote kinaweza kukutwa na mabadiliko na hakuna namna au uwezo wa kuzuia mambo yaliyo nje ya uwezo wetu. Tunajua kuwa kila ambacho tunacho sasa kina nafasi kubwa ya kupotea na hili linatukumbusha kuvipa uzito vitu hivyo vinapokuwepo nasi. Hili linatuamsha namna ya kuthamini muda wa kuwa navyo hivyo vitu ili vinapopotea tusiumizwe na mabadiliko hayo.

Unapofanya chochote jikumbushe kuwa huenda kitu hicho unakifanya mara ya mwisho sasa na hutakipata nafasi ya kukiona au kukitumia tena. Ondoa yale mazoea kuwa vitu vitaendelea kuwepo namna unavyovichukulia kila siku. Mabadiliko hutokea na vile vyote ulivyokuwa unafikiria vitaendelea kuwepo vinaweza kusitishwa, kuharibika, kufungwa, kuanguka au kufa kabisa. Vitu vingi vilikuwepo miaka 100 ilopita ila sasa havipo, vimeanguka, vimesahaulika na vimekufa. Hili pia lina nafasi ya kuleta mabadiliko miaka 100 ijayo kuwa chochote ambacho kipo sasa hakitakuwepo au kitakuwa kimeharibika au kubadilika. Tumia nafasi ulizonazo sasa kwa chochote kile ulichopewa au kukiona kama ni nafasi adhimu mno ya kutochukulia kirahisi ukijua kuna siku hutapata hiyo nafasi.

KOCHA  MWL.  JAPHET  MASATU

WhatsApp + 255 716   924  136 ) /  + 255 755  400   128

 

No comments:

Post a Comment