Saturday, February 27, 2021

USITOE MAJIBU MEPESI KAMA HUJAWAHI KUPITIA HALI WALIZOPITIA WENGINE.

Chochote kile ambacho hujawahi kukipitia unaweza kutoa maoni mepesi au kuwaona wanaofanya kuna sehemu wanakosea usijue kuwa ingekuwa zamu yako kupitia hiyo hali huenda ungeharibu zaidi. Kitu chepesi ambacho huwa tunawaambia watu wanapopitia magumu ni kusema hilo litapita tu usijali. Au mtu kafiwa ni rahisi kusema pole sana na Mungu akuvushe unalopitia na pengine ukasahau kabisa kufikiri ni kwa vipi huyo mtu hali anayopitia. Ila hiyo hali inapokuja kugusa maisha yako unaweza kuona namna huenda ulichokuwa ukikifikiri ni tofauti kabisa.

Unapokuwa nje ya uwanja na kuangalia wachezaji wanavyocheza unaweza kuona namna wanavyokosea na walivyo wazembe katika mchezo huo wa mpira. Huenda ukiingia katika mchezo isitoshe ukafanya kama wao au kukosea kabisa zaidi. Ndivyo maisha yetu ya kila siku tunavyoyafanya kwa kuwa watazamaji na watoa maoni kuhusu maisha ya watu wengine wanapopitia hali mbalimbali katika maisha. Huenda watu wanapopitia mambo tunawachukulia kuwa ni watu wasio imara, wazembe, wavivu na wasiojitambua kwa sababu sio sisi tunaopitia hizo hali na kuchukulia kiwepesi tu kusema.

Wakati naanza safari ya kujifunza kuchambua vitabu mwaka 2017 mwishoni mwishoni nilikuwa naona wanaofanya kazi ya uchambuzi wa kitabu ni kazi nyepesi mpaka nilipokuja kuanza mwenyewe kuchambua na kujua ukweli kuwa si vile nilivyokuwa nafikiria. Si hilo tu bali kuna wale watu ambao nimewahi kukutana nao wanaosubiri mtu achambue kitabu au afanye kazi fulani ya uandishi na yeye abadili jina na kujimilikisha kuwa ni jasho la kazi alofanya. Ila unapokutana naye na kujua kazi imeibiwa na kumsaidia kama kapenda hizo kazi ajifunze hachukui siku nyingi anakimbia katika mafunzo hayo. Sababu ya kukimbia mafunzo hayo ni kuujua ukweli kuwa kazi hiyo sio rahisi kama alivyokuwa akidhani na kuanzia hapo hutambua kuwa kuandika au kuchambua kitabu si kazi ya kubeza wanaofanya hilo.

Tunaishi katika jamii ambayo inarahisisha mambo na kuchukulia vitu rahisi rahisi tu. Watu wengi hawathamini yale wanayofanya wengine kwa sababu hawajui namna hao watu wanavyopitia. Ni rahisi siku hizi kuona watu wanaomba bidhaa za vitabu zilizo katika nakala laini “softcopy” hata kwa kazi za wazawa wakiona ni jambo la waandishi hao kuwajibika kutoa bidhaa hizo kwa kila mtu. Si vibaya kushirikisha maarifa katika jamii ila jamii inayopuuza jasho la mtu ni jamii inayokosa kutambua hali wanazopitia watu wengine. Mfano uandishi wa kitabu ni mgumu sana na walio waandishi wanajua. Utatumia muda kuandika, kusoma sana na pengine kutumia pesa kukamilisha kitabu hicho. Ni maumivu makubwa ambayo mtu anayapitia ila wale wanaotaka kazi hiyo hiyo kwa urahisi hawajali wala kuweka uzito.

Tukianza kujifunza kuwa katika viatu vya watu wanapopitia hali mbalimbali katika maisha hatutakuwa watu wepesi kuongea ongea au kulaumu watu hao. Tunapojua kuwa hata sisi tungekuwa katika hali kama zao huenda tungeumia zaidi kuliko wao au tungeishia njiani kabisa. Tusiwe wepesi kusema mambo au kuyaona mambo kiwepesi wepesi hasa yanapotokea kwa watu wengine. Inapotokea watu wengine wanapitia hizo hali tuvae viatu vyao na kuona namna si mambo rahisi bali tunahitaji tuwatie moyo katika hilo waweze kuvuka.

Unaposikia jambo lolote lile kuhusu watu basi kabla ya kufanya chochote kile au kuiga mkumbo wa maoni ya watu wengine basi jifunze kutulia na kuwaza vipi kama ingekuwa ni wewe umepata hiyo hali ungefanyaje ?. Ukiwa unajiuliza hivi mara kwa mara maishani utajifunza kuwa kimya na kujua hali wanazopitia hao watu zikoje.

KOCHA   MWL.  JAPHET   MASATU ,

 ( WhatsApp +255 716 924136  ) , +  255  755  400128


 

No comments:

Post a Comment