Saturday, February 27, 2021

HASIRA HASARA , UNAPOKUWA NA HASIRA , JIFUNZE KUTULIA , TUMIA NAFASI VIZURI.

Tumeona namna matokeo ya hasira katika jamii zetu yalivyo makubwa. Tumeona namna watu hupigana, kutengana, kuuana sababu tu walikosa kujidhibiti hasira zao wakaamua kuchukua hatua za hatari ambazo zilihatarisha maisha ya watu wengine au kukatisha kabisa maisha ya watu wengine. Matokeo ya hasira ni mabaya mno na yameleta maumivu makali kwa maisha ya watu

Nakumbuka moja ya tukio maarufu lilitangazwa hata katika magazeti nilowahi kulisikia katika udogo wangu ni tukio la watu walokuwa wanapiga debe kupishana kidogo katika kauli na kuanzisha ugomvi maeneo ya Sokomatola mkoani Mbeya kipindi hicho kabla ya kuwa Jiji. Ugomvi huu ulipelekea mmoja kumchoma mwenzake kisu kifuani. Matokeo ya kuchomwa kwa huyu mtu aliyekuwa ni rasta yalipelekea kuvuja damu nyingi kiasi cha kufika hospitali “Mbeya Rufaa” akiwa katika hali mbaya ilopelekea kukatisha maisha yake. Mgomvi mwenzake hakujua tukio la kudhibiti hasira zake kungaliepusha kifo cha kuzuilika kabisa. Je ni wangapi wanakufa au kujeruhiana sababu ya kukosa udhibiti wa hasira ?

Mtu unapokuwa na hasira ni sawa na mtu aliyepoteza utimamu kwa muda. Akili unayokuwa nayo wakati ukiwa na hasira huwa inakuwa na maamuzi ya haraka bila kufikiri ambayo mtu hujutia baadaye baada ya kufanya kitu. Unapokuwa na hasira uwezo wa kufikiri hushuka na hisia hupanda na kuzalisha kujihami. Kujihami huku kiasili kunaweza mtu kutaka kupigana, kutukana au kujeruhi kabisa. Wengine wakiwa na hasira huvunja hadi vitu, hupiga mtu na wengine kuharibu mali zao. Matokeo ya hasara huleta maharibifu mengi maana anayefanya ni sawa na mtu aliyerukwa akili.

Mtu anaingia na hasira pale ambapo anaruhusu kujenga picha akilini juu ya kile kilichomtokea. Mfano mtu anapotukanwa lile tusi analitafsiri na kuona huenda anadhauriwa na hilo linaanzisha ugomvi na hatimaye kuzalisha matokeo mabaya. Mbona mtu huwa hajisumbui endapo mtu aliyemtusi mtu asiye mtimamu. Mtu asiye na utimamu huachwa kwa sababu mtu hutambua kuwa huenda huyo mtu ana matatizo tu ya akili basi asihangaike kushughulika naye. Vile vile tafsiri unayoitoa unapotukanwa au kukutana na tukio ndio inayoathiri kufanya maamuzi na udhibiti wa hasira ndani ya watu.

Jifunze kutulia unapokutana na hali ukakasirishwa ili uepuke madhara yatakayojitokeza endapo utaanzisha ugomvi au kutukana mtu. Vuta pumzi yako pindi unapokuta hasira imekupanda na jicheleweshe kuchukua hatua yoyote ile dhidi ya tukio au mtu aliyechochea upandwe na hasira. Hali ya mihemko ya hasira hupita kama vile upitavyo upepo. Ukingoja basi baada ya muda hasira inakuwa imeisha na unarudi hali ya kawaida ya kufikiri na kuamua mambo. Jifunze kutulia na si lazima kila unalokasirishwa useme au uchukue hatua fulani. Hili litakuepusha na mengi katika maisha.

Kwa wale ambao wanapenda zaidi kujifunza falsafa na kuishi hatua hadi hatua za kifalsafa. Nimeshirikisha hapa hiki kiungo pia cha mwandishi mstoa Ryan Holiday akigusia misemo mifupi mifupi ya Kistoa kwa ajili ya kuishi maisha bora na imara. Ipitie na kuisoma kwa kina utapata mengi zaidi ya kujifunza 


KOCHA MWL.  JAPHET    MASATU

WhatsApp  +255 716924136  / + 255  755  400  128 




 

1 comment:

  1. Jifunze kutulia na si lazima kila unalokasirishwa useme au uchukue hatua fulani. Hili litakuepusha na mengi katika maisha.

    ReplyDelete