Saturday, February 27, 2021

KAMA HUNA HABARI ZA KUTOSHA KUHUSU WATU EPUKA KUWAZUNGUMZIA.

Kwa asili yetu sisi binadamu huwa tunapenda kuzijua habari za watu wengine. Inaweza kuwa hujioneshi ila kwa namna fulani unavutiwa kusikia maisha ya watu wengine yalivyo. Mtu asipoweza kujidhibiti basi ataangukia katika kufuatilia maisha ya watu. Tena kwa siku hizi ilivyo watu wanaonesha maisha yao kupitia mitandao basi mitandao yenye habari za maisha ya watu “udaku” hupata wafuasi wengi wakijua ni asili ya watu kupenda kujua maisha ya watu wengine.

Wengi tunaangukia katika mtego wa kutamani sana kuzungumzia watu wengine na pengine mazungumzo hayo yanajaa kuwazungumzia ubaya au mambo ambayo hatujaona kwa macho bali tumepokezana tu kusikia sikia kuhusu wao. Tumeishia kuhukumu watu na kuwaona kwa ubaya kumbe tungejua ukweli kuhusu wao baadaye tunakuja kujilaumu kuwa tumesambaza habari zao ambazo si kweli kuhusu wao. Mtego huu unapokosa kuuvuka unawaletea watu wengi matatizo na wanajishushia heshima walowekewa na wengine. Maisha ya watu wengine huenda si jambo unalopaswa kuliweka kipaumbele ikiwa unataka kuimarisha maisha yako ya kila siku.

Kufuatilia watu wengine na kuanza kuchambua maisha yao ni chanzo cha watu wengi kupatwa na wivu, chuki, hasira na kujichelewesha kufanikiwa kwa mambo yao. Si kwa ubaya kujifunza kupitia maisha ya watu wengine ila jambo la kuzungumza mambo usio na uhakika nayo ni kukosa kufikiri na kuhoji kama mwanafalsafa. Vipi ulichosambaza si kweli kumhusu mtu na ukajulikana ni wewe uliyezungumza. Utajisikiaje na watu watakupa tafsiri gani ?, je ni lazima kuzungumzia maisha ya watu unapokuwa huna ufafanuzi wa kutosha?. Ni muhimu sana kujiuliza mara kwa mara pale unapotaka kuzungumza maisha ya watu wengine.

Usinase katika mtego wa kubeba uliyoyasikia na kuwaambia wengine kama ni jambo toshelevu kuhusu habari au taarifa za mtu. Isitoshe sisi ni binadamu na tu watu wa viungo katika mwili mmoja. Kutamani maisha ya watu wengine yasambazwe kwa habari za uongo ni kukosa kukomaa kifalsafa. Mtu aliye na njia ya maisha hafanyi kitu bila kufikiri au kuongozwa na mihemko ya mkumbo. Hujiuliza na kupima ulazima wa jambo kufanya. Muda ambao tunaishi ni mfupi usotosha kupoteza maisha yetu kuwa watumwa wa maisha ya watu wengine kuchambua maisha yao na yale yote wanayoyapitia.

Wavumilie wengine na jiepushe na mazungumzo ya kuwafuatilia watu ukiwa huna ufafanuzi wa kutosha wa maisha yao. Hata ikitokea upo katika mazungumzo jaribu kuwa msikilizaji na kujifunza namna watu wasivyoweza kujidhibiti na kufikiri katika kuyaangalia mambo. Kuwa kimya ni bora kuliko kuongea kitu kisicho na uthibitisho. Usisukumwe kusambaza chochote au tetesi tu bila kushuhudia au kitu hicho kuthibitishwa. Ila ongozwa na fikara za kujiuliza hivi je hiki nachotaka kuzungumza au kusambaza ni lazima ?

KOCHA  MWL.  JAPHET   MASATU

 ( WhatsApp +255 716 924136 ) /  + 255  755 400128


 

No comments:

Post a Comment